Hamia kwenye habari

Hamia kwenye yaliyomo

HADITHI YA 94

Anapenda Watoto Wadogo

Anapenda Watoto Wadogo

MTAZAME Yesu hapa akimkumbatia mtoto. Unaweza kujua kwamba Yesu anapenda sana watoto. Wanaume wanaotazama ni mitume wake. Yesu anawaambia nini? Acha tuone.

Sasa ndiyo Yesu na mitume wake wamerudi katika safari ndefu. Njiani mitume hao waligombana. Basi baada ya safari hiyo Yesu anawauliza: ‘Mlikuwa mkigombana njiani juu ya nini?’ Yesu anajua walichogombania. Lakini anauliza maulizo aone kama mitume watamwambia.

Mitume hawajibu, kwa sababu njiani waligombana juu ya nani kati yao aliye mkubwa zaidi. Mitume fulani wanataka kuwa wakubwa kuliko wenzao. Yesu atawaambia namna gani kwamba haifai kutaka kuwa mkubwa zaidi?

Amwita mvulana mdogo na kumsimamisha mbele yao wote. Kisha anawaambia wanafunzi wake hivi: ‘Nataka mjue hakika ya hili, kama hamgeuki mwe kama watoto wadogo, hamtaingia katika ufalme wa Mungu. Aliye mkubwa zaidi katika ufalme huo ni mtu anayekuwa kama mtoto huyu.’ Unajua sababu Yesu alisema hivyo?

Watoto wadogo sana hawataki kuwa wakubwa kuliko wenzao. Inawapasa mitume wawe kama watoto kwa njia hiyo, wasigombane juu ya ukubwa.

Nyakati nyingine pia, Yesu anaonyesha namna anavyopenda sana watoto wadogo. Miezi michache baadaye watu fulani wanaleta watoto wamwone Yesu. Mitume wanajaribu kuwazuia. Lakini Yesu anawaambia mitume wake hivi: ‘Acheni watoto waje kwangu, msiwazuie, kwa sababu ufalme wa Mungu ni wa watu kama hao.’ Ndipo Yesu anachukua watoto mikononi mwake, anawabariki. Ni vizuri kujua kwamba Yesu anawapenda watoto wadogo, sivyo?