Hamia kwenye habari

Hamia kwenye yaliyomo

HADITHI YA 95

Namna Yesu Anavyofundisha

Namna Yesu Anavyofundisha

SIKU moja Yesu anamwambia mtu fulani kwamba yampasa ampende jirani yake. Mtu huyo anamwuliza Yesu hivi: ‘Jirani yangu ni nani?’ Yesu anajua fikira za mtu huyo. Mtu huyo anadhani jirani zake ni watu wa kabila lake na dini yake. Basi na tuone Yesu anavyomwambia.

Mara nyingine Yesu anafundisha kwa kusimulia hadithi. Ndivyo anafanya sasa. Anasimulia hadithi juu ya Myahudi na Msamaria. Tumekwisha jifunza kwamba Wayahudi wengi hawapendi Wasamaria. Basi, hadithi ya Yesu ndiyo hii:

Palikuwa na Myahudi aliyekuwa akitembea katika njia ya mlima kwenda Yeriko. Lakini wevi wakamshambulia. Wakachukua fedha zake na kumpiga sana karibu kufa.

Baadaye, kuhani Myahudi akapita njia hiyo. Akamwona mtu huyo aliyepigwa sana. Unadhani alifanya nini? Alipita upande mwingine wa njia akaendelea na safari yake. Kisha mwana-dini mwingine akaja. Alikuwa Mlawi. Alisimama? Wala hakusimama amsaidie mtu huyo. Unaweza kuona kuhani na Mlawi mbali kule wakitelemka njiani.

Lakini mwone aliye hapa pamoja na mtu aliyepigwa. Ni Msamaria. Anatia dawa kwenye vidonda vyake. Kisha anampeleka Myahudi huyo mahali pa kupumzika na kupona.

Akiisha kumaliza hadithi yake, Yesu anamwambia mtu yule aliyemwuliza ulizo: ‘Unadhani ni nani kati ya hao watatu aliyekuwa jirani ya mtu aliyepigwa? Je! ni kuhani, Mlawi au Msamaria?’

Mtu huyo anajibu: ‘Ni Msamaria. Alihurumia mtu aliyepigwa.’

Yesu anamwambia: ‘Wasema kweli. Basi nenda ukatendee wengine namna iyo hiyo.’

Je! hupendi namna Yesu anavyofundisha? Twaweza kujifunza mengi ya maana tukisikiliza anayosema Yesu katika Biblia, sivyo?