Hamia kwenye habari

Hamia kwenye yaliyomo

HADITHI YA 105

Kungojea Yerusalemu

Kungojea Yerusalemu

WATU walio hapa ni wafuasi wa Yesu. Wametii wakakaa Yerusalemu. Wote wanapongojea pamoja, kelele kubwa inajaa nyumba yote. Ni kama upepo wenye nguvu unaopita mbio. Ndipo ndimi za moto zinaanza kuonekana juu ya kichwa cha kila mmoja wa wanafunzi hao. Unaona moto juu ya kila mmoja wao? Maana yake nini?

Ni mwujiza! Yesu amerudi mbinguni akiwapo na Baba yake. Anawamwagia wafuasi wake roho takatifu ya Mungu. Unajua roho inawaongoza wafanye nini? Wote wanaanza kusema lugha mbalimbali.

Watu wengi Yerusalemu wanasikia kelele hiyo iliyo kama ya upepo wenye nguvu, wanakuja kuona kama kuna nini. Wengine ni watu wa kutoka mataifa mengine waliokuja kuhudhuria sikukuu ya Pentekoste ya Waisraeli. Lo! wageni hao wanashangazwa! Wanasikia wanafunzi wakiyasema kwa lugha zao wenyewe maajabu ambayo Mungu amefanya.

‘Watu hawa wote wanatoka Galilaya,’ wageni wanasema. ‘Basi, wamewezaje kusema lugha hizo mbalimbali za nchi zetu?’

Sasa Petro anasimama na kuwaeleza. Anapaza sauti yake na kuwaambia watu namna Yesu alivyouawa na kwamba Yehova alimfufua katika wafu. ‘Sasa Yesu yuko mbinguni mkono wa kuume wa Mungu,’ Petro asema. ‘Naye amemwaga roho takatifu. Ndiyo sababu mmeona na kusikia miujiza hii.’

Basi, Petro anaposema hayo, watu wengi wanasikitikia sana waliyomfanyia Yesu. ‘Tufanye nini?’ wanauliza. Petro awaambia: ‘Inawapasa mgeuze maisha zenu mbatizwe.’ Basi siku hiyo watu karibu 3,000 wanabatizwa na kuwa wafuasi wa Yesu.