Hamia kwenye habari

Hamia kwenye yaliyomo

HADITHI YA 106

Wanafunguliwa Katika Gereza

Wanafunguliwa Katika Gereza

MTAZAME malaika huyu hapa akifungua mlango wa gereza. Anafungulia mitume wa Yesu. Na tuone kilichofanya watiwe gerezani.

Ni muda mfupi tu tangu roho takatifu ilipomwagwa juu ya wanafunzi wa Yesu. Na hili linatokea: Petro na Yohana wanaingia katika hekalu Yerusalemu alasiri moja. Hapo, karibu na mlango, pana mwanamume kilema maisha yake yote. Watu humbeba kumleta hapa kila siku ili aweze kuwaomba fedha wale wanaoingia hekaluni. Anapoona Petro na Yohana, anaomba wampe kitu. Mitume hao watafanya nini?

Wanasimama na kumtazama maskini huyo. ‘Sina fedha,’ Petro anasema, ‘lakini nitakupa nilicho nacho. Katika jina la Yesu, simama utembee!’ Ndipo Petro anamchukua mtu huyo kwa mkono wa kuume, na mara hiyo anaruka na kuanza kutembea. Watu wanapoona hilo, wanastaajabu na kufurahia mwujiza huo.

‘Tulifanya mwujiza huu kwa nguvu za Mungu, aliyemfufua Yesu kutoka kwa wafu,’ Petro anasema. Wakati yeye na Yohana wangali wakisema, viongozi fulani wa dini wanafika. Wamekasirika kwa sababu Petro na Yohana wanawaambia watu habari za kufufuliwa kwa Yesu. Basi wanawakamata na kuwatia gerezani.

Kesho yake viongozi wa dini wanafanya mkutano mkubwa. Petro na Yohana, pamoja na yule mtu waliyeponya, wanaletwa. ‘Mlifanya mwujiza huu kwa uwezo gani?’ viongozi wa dini wauliza. Petro anawaambia kwamba ni kwa uwezo wa Mungu, aliyemfufua Yesu katika wafu. Makuhani hao hawajui la kufanya, maana hawawezi kusema mwujiza huo haukutokea. Basi wanawaonya mitume wasiseme tena juu ya Yesu, na kuwaachilia.

Siku zinapopita mitume wanazidi kuhubiri juu ya Yesu na kuponya wagonjwa. Habari za miujiza hiyo zaenea pote. Hata watu wengi kutoka miji inayozunguka Yerusalemu wanaleta mitume wagonjwa ili wawaponye. Jambo hilo lafanya viongozi wa dini wawe na wivu, wanawakamata mitume na kuwatia gerezani.

Usiku malaika wa Mungu anaufungua mlango, kama unavyooweza kuona hapa. Malaika huyo anasema: ‘Nendeni mkasimame hekaluni, mzidi kuwaambia watu.’ Kesho yake, viongozi wa dini wanatuma watu wakawachukue mitume, hawako. Baadaye watu hao wanawakuta wakifundisha hekaluni kisha wanawapeleka kwenye Baraza Kuu.

‘Tuliwaamuru kabisa msifundishe tena juu ya Yesu,’ viongozi wa dini wanasema. ‘Lakini ninyi mmejaza Yerusalemu mafundisho yenu.’ Ndipo mitume wanajibu hivi: ‘Imetupasa kumtii Mungu kama mtawala kuliko wanadamu.’ Hivyo wanazidi kufundisha ‘habari njema.” Je! huo si mfano mzuri kwetu kufuata?