Hamia kwenye habari

Hamia kwenye yaliyomo

HADITHI YA 107

Stefano Anapigwa kwa Mawe

Stefano Anapigwa kwa Mawe

MWANAMUME huyu anayepiga magoti ni Stefano. Ni mwanafunzi mwaminifu wa Yesu. Lakini tazama yanayompata sasa! Watu hawa wanamtupia mawe makubwa. Acha tuone sababu ya kumfanyia hivyo Stefano.

Mungu amekuwa akimsaidia Stefano afanye miujiza. Watu hawapendi hivyo, basi wanaanza kubishana naye juu ya kufundisha watu kweli. Lakini Mungu anampa Stefano hekima kubwa, naye Stefano anawaonyesha watu hawa kwamba wamekuwa wakifundisha mambo ya uongo. Hili linawakasirisha zaidi. Basi wanamkamata, na kuita watu waseme uongo juu yake.

Kuhani mkuu anamwuliza Stefano hivi: ‘Hiyo ni kweli?’ Stefano ajibu kwa kutoa hotuba nzuri ya Biblia. Kwa kumalizia, anasimulia namna watu wabaya walivyochukia manabii wa Yehova zamani. Ndipo anasema: ‘Ninyi ni kama watu hao. Mlimwua Yesu mtumishi wa Mungu, nanyi hamkuzitii sheria za Mungu.’

Hayo yanawakasirisha sana viongozi hawa wa dini! Wanasaga meno yao kwa hasira. Ndipo Stefano anainua kichwa chake, na kusema: ‘Tazama! Namwona Yesu akisimama upande wa kuume wa Mungu mbinguni.’ Kwa sababu hiyo, wanamkamata Stefano kwa nguvu na kumvuta nje ya mji.

Wakiwa huko wanavua mavazi yao ya nje na kumpa kijana Sauli ayaangalie. Unamwona Sauli? Ndipo wengine wao wanaanza kumtupia Stefano mawe. Stefano anapiga magoti, kama unavyoona hapa, akimwomba Mungu hivi: ‘Yehova, usiwaadhibu kwa ubaya huu.’ Anajua wengine wao wamefanywa wajinga na viongozi wa dini. Kisha Stefano anakufa.

Mtu akikutendea vibaya, je! unajaribu kulipa kisasi, au kumwomba Mungu amwumize? Stefano na Yesu hawakuwa hivyo. Walihurumia hata wale waliowatenda vibaya. Na tufuate mfano wao.