Hamia kwenye habari

Hamia kwenye yaliyomo

HADITHI YA 116

Tunavyoweza Kuishi Milele

Tunavyoweza Kuishi Milele

UNAJUA msichana huyu mdogo na rafiki zake wanasoma nini? Ni kitabu hiki unachosoma wewe—Kitabu Changu cha Hadithi za Biblia. Wanasoma hadithi hii unayosoma—“Tunavyoweza Kuishi Milele.”

Unajua wanajifunza nini? Kwanza, kwamba yatupasa tujue habari za Yehova na Mwanawe Yesu ikiwa tutaishi milele. Biblia yasema: ‘Hii ndiyo njia ya kuishi milele. Jifunzeni habari za Mungu mmoja wa kweli, na Mwanawe ambaye alituma duniani, Yesu Kristo.’

Tunaweza kujifunza habari za Yehova Mungu na Mwanawe Yesu namna gani? Njia moja ni kwa kusoma Kitabu Changu cha Hadithi za Biblia mwanzo mpaka mwisho. Kinasema mambo mengi juu ya Yehova na Yesu, sivyo? Tena kinasema mambo mengi ambayo wamefanya na mambo watakayofanya. Lakini lazima tufanye zaidi ya kusoma tu kitabu hiki.

Unakiona kitabu kingine chini? Ni Biblia. Mwombe mtu fulani akusomee sehemu za Biblia ambazo ndizo msingi wa hadithi za kitabu hiki. Biblia inatujulisha yote tunayotaka ili sote tuweze kumtumikia Yehova kwa kufaa na kupata uzima wa milele. Basi inatupasa tuzoee kuisoma Biblia mara nyingi.

Lakini hatupaswi kujifunza tu juu ya Yehova Mungu na Yesu Kristo. Twaweza kujua mambo mengi sana juu yao na juu ya mafundisho yao, na bado tusipate uzima wa milele. Unajua nini zaidi linatakiwa?

Yatupasa pia tufuate mambo tunayojifunza. Unamkumbuka Yuda Iskariote? Alikuwa mmoja wa wale 12 ambao Yesu alichagua wawe mitume wake. Yuda alijua mambo mengi juu ya Yehova na Yesu. Lakini ikawaje kwake? Baada ya muda mfupi akawa na choyo, alimshtaki Yesu kwa adui zake ili apewe vipande 30 vya fedha. Hivyo Yuda hatapata uzima wa milele.

Unamkumbuka Gehazi, yule mwanamume tuliyejifunza habari zake katika Hadithi ya 69? Alitaka mavazi na fedha ambazo si zake. Akasema uongo ili apate vitu hivyo. Lakini Yehvoa alimwadhibu. Atatuadhibu sisi pia kama hatutii sheria zake.

Lakini kuna watu wazuri wengi waliomtumikia Yehova sikuzote kwa uaminifu. Twataka tuwe kama hao, sivyo? Samweli mdogo ni mfano mzuri wa kufuata. Kumbuka, kama tulivyoona katika Hadithi ya 55, alikuwa na miaka minne au mitano tu alipoanza kumtumikia Yehova katika hema yake. Basi hata uwe mchanga namna gani, unaweza kumtumikia Yehova.

Bila shaka, mtu ambaye sote twataka tufuate ni Yesu Kristo. Hata alipokuwa mvulana, kama Hadithi ya 87 inavyoonyesha, alikuwa hekaluni akizungumza na wengine mambo ya Baba yake wa mbinguni. Na tufuate mfano wake. Na tuwaambie watu wengi mambo ya Mungu wetu wa ajabu Yehova, na Mwanawe Yesu Kristo. Tukifanya hivyo, tutaweza kuishi milele katika paradiso mpya ya Mungu hapa duniani.