Hamia kwenye habari

Hamia kwenye yaliyomo

Uasi Katika Makao ya Roho

Uasi Katika Makao ya Roho

Shetani alipotumia nyoka kuzungumza na Hawa, Hawa alijiunga naye kumwasi Mungu

Viumbe wote wa roho ambao Yehova aliwaumba walikuwa wema. Halafu malaika mmoja akabadilika na kuwa mbaya. Malaika huyo ni Shetani Ibilisi. Shetani alitaka watu duniani wamwabudu yeye badala ya kumwabudu Yehova. Hivi ndivyo mambo yalivyokuwa:

Katika bustani ya Edeni, kulikuwa na miti mingi yenye matunda matamu. Yehova alimwambia Adamu na Hawa, mke wake, kwamba wangeweza kula matunda hayo wapendavyo. Hata hivyo, kulikuwa na mti mmoja ambao Mungu alisema hawapaswi kula matunda yake. Ikiwa wangekula, hakika wangekufa.—Mwanzo 2:9, 16, 17.

Siku moja Hawa alikuwa peke yake nyoka aliposema naye. Bila shaka, si nyoka aliyeongea; ni Shetani Iblisi aliyefanya ionekane kama kwamba ni nyoka aliyekuwa akizungumza. Shetani alimwambia Hawa kwamba kama angekula tunda lililokatazwa, angekuwa na hekima kama Mungu. Pia alimwambia kwamba hakika hangekufa. Taarifa zote mbili zilikuwa uwongo. Hata hivyo, Hawa alimwamini Shetani, akala tunda lililokatazwa. Baadaye, akampa Adamu, naye pia akala.—Mwanzo 3:1-6.

Kutokana na masimulizi hayo ya kweli, tunajifunza kwamba Shetani ni mwasi na mwongo. Alimwambia Hawa kwamba akikosa kumtii Mungu, hatakufa. Huo ulikuwa uwongo. Alikufa. Adamu pia alikufa. Shetani hakufa wakati huo, ijapokuwa atakufa hatimaye kwa sababu alitenda dhambi. Hata hivyo, kwa sasa, yuko hai naye anaendelea kupotosha wanadamu. Angali mwongo, naye hujaribu kuwafanya watu wavunje sheria za Mungu.—Yohana 8:44.

Malaika Wengine Waasi

Baadaye, malaika wengine walibadilika wakawa wabaya. Malaika hao waliwaona wanawake wazuri duniani nao wakataka kuwa na mahusiano ya kingono pamoja nao. Kwa hiyo walikuja duniani na kujivika miili ya kiume ya kibinadamu. Kisha wakajitwalia wanawake. Hilo lilikuwa kinyume na kusudi la Mungu.—Mwanzo 6:1, 2; Yuda 6.

Malaika waovu walikuja duniani kufanya mambo mapotovu pamoja na wanawake

Pia, jambo hilo lilitokeza taabu nyingi kwa wanadamu. Wake za malaika hao walizaa watoto. Watoto hao hawakuwa watoto wa kawaida. Walikua wakawa majitu wenye jeuri na wakatili. Hatimaye dunia ikajaa ukatili sana hivi kwamba Yehova akaamua kuwaangamiza watu hao waovu kwa furiko kubwa. Wanadamu pekee waliookoka Furiko hilo ni Noa mwadilifu na familia yake.—Mwanzo 6:4, 11; 7:23.

Hata hivyo, malaika waovu walirudi katika makao ya roho; hawakufa. Hata hivyo waliadhibiwa. Hawakuruhusiwa kujiunga tena na familia ya Mungu ya malaika waadilifu. Isitoshe, Yehova hakuwaruhusu tena wajivike miili ya kibinadamu. Na hatimaye watakufa wakati wa hukumu ya ile siku kuu.—2 Petro 2:4; Yuda 6.

Shetani Atupwa Kutoka Mbinguni

Shetani na malaika zake wabaya walitupwa kutoka mbinguni

Mapema katika karne ya 20, kulikuwa na vita mbinguni. Kitabu cha Biblia cha Ufunuo kinaeleza yaliyotokea: “Na vita vikatokea ghafla mbinguni: Mikaeli [Yesu Kristo aliyefufuliwa] na malaika zake [wema] wakapigana na yule joka [Shetani], naye joka na malaika zake [wabaya] wakapigana nao lakini hawakushinda, wala mahali hapakupatikana tena mbinguni kwa ajili yao. Basi yule joka mkubwa akatupwa chini, yule nyoka wa zamani, anayeitwa Ibilisi na Shetani, anayeipotosha dunia nzima inayokaliwa; akatupwa chini duniani, na malaika zake [wabaya] wakatupwa chini pamoja naye.”

Matokeo yakawa nini? Masimulizi yaendelea: “Kwa sababu hiyo furahini, enyi mbingu nanyi mnaokaa ndani yake!” Malaika wema wangeweza kufurahi kwa sababu Shetani na malaika, au roho wake wabaya, hawangeendelea kuwapo tena mbinguni. Lakini vipi watu walio duniani? Biblia inasema: “Ole wa dunia na wa bahari, kwa sababu Ibilisi ameshuka kwenu, akiwa na hasira kali, akijua kwamba ana kipindi kifupi cha wakati.”—Ufunuo 12:7-9, 12.

Ndiyo, Shetani na malaika zake waovu huwapotosha watu na kusababisha ole duniani. Malaika hao waovu wanaitwa mashetani. Wao ni adui za Mungu. Wote ni waovu.