Mtumikie Yehova, Si Shetani
Sisi sote tuna uchaguzi. Tunaweza kuamua kumtumikia Yehova ama kumtumikia Shetani na roho wake waovu. Hatuwezi kuwatumikia wote. Ni jambo la hekima kama nini kutumikia Yehova!
Yehova Ni Mwema
Kama tulivyoona, mashetani hufurahia kuumiza na kudanganya watu. Sivyo alivyo Yehova. Yeye anawapenda wanadamu kama vile baba anavyowapenda watoto wake. Yeye ndiye Mpaji wa “kila zawadi njema na kila tuzo kamilifu.” (Yakobo 1:17) Yeye hawanyimi wanadamu chochote kilicho chema, hata iwe atagharimika sana.—Waefeso 2:4-7.
Fikiria mambo ambayo Yesu, Mwana wa Mungu, alitenda duniani. Aliwawezesha mabubu kunena na vipofu kuona. Aliwaponya wenye ukoma na vilema. Aliwafukuza mashetani na kuponya kila aina ya magonjwa. Kwa nguvu za Mungu, Yesu, hata alifufua wafu.—Mathayo 9:32-35; 15:30, 31; Luka 7:11-15.
Badala ya kusema uwongo ili kutudanganya, sikuzote Mungu husema kweli. Yeye hamdanganyi mtu yeyote kamwe.—Hesabu 23:19.
Epuka Mazoea Machafu
Kama vile utando wa buibui hunasa nzi, mamilioni ya watu wamenaswa na ushirikina na uwongo. Wanaogopa wafu. Wanaogopa mashetani. Wanaogopa laana, ndege wabaya, na mengine mengi. Wanafungwa kwa imani na mapokeo yanayotegemea uwongo wa Shetani Ibilisi. Watumishi wa Mungu hawanaswi na lolote la mambo hayo.
Yehova ana nguvu nyingi zaidi kuliko Shetani. Ukimtumikia Yehova, atakulinda usiumizwe na mashetani. (Yakobo 4:7) Ulozi hautakudhuru. Kwa mfano, nchini Nigeria, wachawi watatu wenye nguvu nyingi walifanya ulozi ili wamwue Shahidi wa Yehova alipokataa kuondoka mjini. Uchawi wao uliposhindwa kufanya lolote, mmoja wa wachawi hao alishikwa na hofu akamwendea Shahidi huyo, na kumwomba rehema.
Mashetani wakikusumbua unaweza kumwomba Yehova kwa kutumia jina lake naye atakulinda. (Methali 18:10) Lakini ili upate ulinzi wa Mungu, lazima uvunje kabisa uhusiano na chochote kinachoshirikishwa na kuwasiliana na roho na ibada ya mashetani. Waabudu wa Mungu katika jiji la Efeso la kale walifanya hivyo. Walikusanya vitabu vyao vyote vya uchawi na kuviteketeza. (Matendo 19:19, 20) Lazima watumishi wa Mungu leo wafanye vivyo hivyo. Ondolea mbali hirizi, talasimu, kamba “za kujikinga,” mazingaombwe, vitabu vya uchawi, na kitu kingine chochote kinachohusiana na mazoea ya kuwasialiana na roho.
Mwabudu Mungu wa Kweli
Ikiwa unataka kumpendeza Mungu, haitoshi kuacha tu ibada ya uwongo na kuacha kufanya mambo mabaya. Lazima umwabudu Mungu wa kweli. Biblia inaonyesha mambo unayotakiwa kufanya:
Shirikiana na Mashahidi wa Yehova
Shetani na roho wake waovu wana watu duniani ambao hufundisha na kufanya mambo yasiyofaa. Yehova pia ana watu wake. Wao ni Mashahidi wa Yehova. (Isaya 43:10) Duniani pote, kuna Mashahidi zaidi ya milioni sita. Wote hao hujitahidi kufanya mambo mema na kuwafundisha watu ukweli. Katika nchi nyingi, unaweza kukutana nao katika Jumba la Ufalme, ambapo watakukaribisha kwa uchangamfu.
Kazi yao ni kuwasaidia watu wamtumikie Mungu. Watajifunza Biblia pamoja nawe nyumbani kwako, wakikusaidia ujifunze jinsi ya kumwabudu Yehova kwa njia inayofaa. Huhitaji kulipia chochote. Mashahidi wanafurahia kuwafundisha watu kweli kwa sababu wanawapenda watu na wanampenda Yehova Mungu.