Hamia kwenye habari

Hamia kwenye yaliyomo

“Haiwezi Kuwa Kweli!”

“Haiwezi Kuwa Kweli!”

MTU fulani kutoka New York (Marekani) asimulia hivi: “Mwanangu Jonathan alikuwa akiwatembelea marafiki umbali wa kilometa chache. Mke wangu, Valentina, hakupenda aende huko. Sikuzote alikuwa akiogopa mwendo wa magari. Lakini mwana wetu alipenda sana shughuli za kielektroniki, na marafiki zake walikuwa na duka la ufundi alimoweza kupata ustadi wenye kutumika. Nilikuwa nyumbani katika Manhattan magharibi, New York. Mke wangu alikuwa akitembelea familia yake katika Puerto Riko. ‘Jonathan atarudi karibuni,’ nikafikiri. Kisha kengele ya mlango ikalia. ‘Bila shaka ndiye huyo.’ Hakuwa huyo. Hao walikuwa polisi na wafanya-kazi wa tiba. ‘Je! watambua leseni (cheti) hii ya udereva?’ ofisa wa polisi akauliza. ‘Ndiyo, hiyo ni ya mwanangu, Jonathan.’ ‘Tumekuletea habari mbaya. Kumekuwa na aksidenti, na . . . mwana wako, . . . mwana wako ameuawa.’ Itikio langu la kwanza lilikuwa, ‘Haiwezi kuwa kweli!’ Tukio hilo la kushtua lilisababisha umivu mioyoni mwetu ambalo bado linapona, hata miaka kadhaa baadaye.”

‘Tumekuletea habari mbaya. Kumekuwa na aksidenti, na . . . mwana wako, . . . mwana wako ameuawa.’

Baba fulani katika Barcelona (Hispania) aandika hivi: “Huko nyuma katika Hispania miaka ya 1960, sisi tulikuwa familia yenye furaha. Kulikuwa na María, mke wangu, na watoto wetu watatu, David wa miaka 13, Paquito wa miaka 11, na Isabel wa miaka 9.

“Siku moja katika Machi 1963, Paquito alirudi nyumbani kutoka shuleni akilalamika juu ya maumivu makali ya kichwani. Tulitatanika kuhusu ni nini kingeweza kuwa chanzo chayo—lakini si kwa muda mrefu. Muda wa saa tatu baadaye yeye alikuwa amekufa. Kuvuja kwa damu ubongoni kulikuwa kumekomesha uhai wake kwa ghafula.

“Kifo cha Paquito kilitukia zaidi ya miaka 30 iliyopita. Hata hivyo, umivu lenye kina kirefu kutokana na kifo hicho labaki nasi hadi siku hii. Hakuna njia yoyote ambayo wazazi waweza kufiwa na mtoto na wasihisi kwamba wamepoteza sehemu fulani ya wao wenyewe—haidhuru ni muda gani wa wakati upitao au ni watoto wengine wangapi huenda wakapata.”

Maono haya mawili, ambayo katika hayo wazazi walifiwa na watoto, yaonyesha jinsi umivu lisababishwalo wakati mtoto anapokufa lilivyo lenye kina na lenye kudumu. Ni ya kweli kama nini yale maneno ya daktari fulani aliyeandika hivi: “Kwa kawaida kifo cha mtoto ni msiba nacho ni umivu kali la kimoyoni zaidi ya kifo cha mtu mwenye umri mkubwa zaidi kwa sababu mtoto ni mshiriki wa familia asiyetazamiwa kufa. . . . Kifo cha mtoto yeyote huwakilisha kupotezwa kwa ndoto za wakati ujao, watu wa ukoo [mwana, binti-mkwe, wajukuu], maono . . . ambayo bado hayajafurahiwa.” Na hisi hii ya kupoteza mengi sana yaweza kumhusu pia mwanamke yeyote aliyempoteza mtoto mchanga kupitia mimba iliyoharibika.

Mke fulani aliyefiwa aeleza hivi: “Mume wangu, Russell, alikuwa ametumikia akiwa msaidizi wa kitiba katika eneo la mapigano la Pasifiki wakati wa Vita ya Ulimwengu 2. Alikuwa ameona na kuokoka mapigano fulani yaliyo mabaya sana. Yeye alirudi Marekani kwenye maisha matulivu zaidi. Baadaye alitumikia akiwa mhudumu wa Neno la Mungu. Mwanzoni-mwanzoni mwa miaka yake ya 60 alianza kuwa na dalili za matatizo ya moyo. Alijaribu kuwa na maisha yenye utendaji mwingi. Halafu, siku moja katika Julai 1988, alipatwa kwa ghafula na ugonjwa mbaya sana wa moyo, akafa. Kifo chake kilihuzunisha sana. Sikupata kamwe hata nafasi ya kuagana. Yeye hakuwa mume wangu tu. Alikuwa rafiki yangu aliye bora zaidi ya wote. Tulikuwa tumeshiriki miaka 40 ya maisha pamoja. Sasa ilionekana kwamba ilinilazimu kukabili upweke usio wa kawaida.”

Haya ni machache tu kati ya yale maelfu ya misiba ambayo huathiri vibaya familia nyingi kotekote ulimwenguni kila siku. Kama vile watu wengi wanaohuzunika watakavyokuambia, kifo kimchukuapo mtoto wako, mume wako, mke wako, mzazi wako, rafiki yako, kwa kweli huwa kile ambacho mwandikaji Mkristo Paulo alikiita, “adui wa mwisho.” Mara nyingi itikio la kwanza la asili kwa habari hiyo yenye kuhofisha laweza kuwa kukana, “Haiwezi kuwa kweli! Siamini hilo.” Mara nyingi maitikio mengine hufuata, kama tutakavyoona.—1 Wakorintho 15:25, 26, New World Translation.

Hata hivyo, kabla ya sisi kuchunguza hisia za huzuni, acheni tujibu baadhi ya maswali ya maana. Je! kifo humaanisha mwisho wa mtu huyo? Je! kuna tumaini lolote kwamba twaweza kuwaona wapendwa wetu tena?

Kuna Tumaini Halisi

Mwandikaji wa Biblia Paulo alitoa tumaini la kitulizo kutoka kwa yule “adui wa mwisho,” kifo. Aliandika hivi: “Kifo kitafanywa kuwa si kitu.” “Adui wa mwisho kufutiliwa mbali ni kifo.” (1 Wakorintho 15:26, The New English Bible) Kwa nini Paulo angeweza kuwa na uhakika hivyo juu ya jambo hilo? Kwa sababu alikuwa amefundishwa na Yesu Kristo, mmoja aliyekuwa ameinuliwa kutoka kwa wafu. (Matendo 9:3-19) Hiyo ndiyo sababu pia Paulo angeweza kuandika hivi: “Kwa kuwa kifo ni kupitia mtu [Adamu], ufufuo wa wafu pia ni kupitia mtu [Yesu Kristo]. Kwa maana kama vile katika Adamu wote wanakufa, ndivyo pia katika yule Kristo wote watafanywa kuwa hai.”—1 Wakorintho 15:21,22NW.

Yesu alihuzunika sana alipokutana na mjane fulani wa Naini na kumwona mwana wake mfu. Simulizi la Biblia latuambia hivi: “[Yesu] alipokaribia lango la jiji [Naini], kumbe! tazama! kulikuwa na mtu mfu akiwa anapelekwa nje, mwana mzaliwa-pekee wa mama yake. Mbali na hilo, alikuwa ni mjane. Pia umati mkubwa kutoka kwenye jiji ulikuwa pamoja naye. Na Bwana alipomwona akamsikitikia, naye akamwambia: ‘Koma kutoa machozi.’ Ndipo akakaribia na kuligusa jeneza, na wachukuzi wakasimama tuli, naye akasema: ‘Mwanamume kijana, nakuambia, Inuka!’ Na huyo mtu mfu akaketi na kuanza kusema, naye akampa huyo kwa mama yake. Basi hofu ikawashika wote, nao wakaanza kumtukuza Mungu, wakisema: ‘Nabii mkubwa ameinuliwa miongoni mwetu,’ na, ‘Mungu ameelekeza uangalifu wake kwa watu wake.’” Ona jinsi Yesu alivyosikitika sana, hivi kwamba akamfufua mwana wa mjane huyo! Ebu wazia ni nini ambacho tukio hilo laonyesha kuhusu wakati ujao!—Luka 7:12-16, NW.

Hapo, akiwa mbele ya mashahidi wenye kujionea kwa macho yao wenyewe, Yesu alifanya ufufuo usiosahaulika. Ilikuwa dalili ya ule ufufuo aliokuwa tayari ametabiri juu yao wakati fulani kabla ya tukio hili, kurudishwa kwa uhai duniani chini ya “mbingu mpya.” Kwenye pindi hiyo Yesu alikuwa amesema hivi: “Msistaajabie hili, kwa sababu saa inakuja ambayo katika hiyo wote wale waliomo ndani ya makaburi ya ukumbusho watasikia sauti yake na kutoka.”—Ufunuo 21:1, 3, 4; Yohana 5:28, 29; 2 Petro 3:13, NW.

Mashahidi wengine wenye kujionea ufufuo kwa macho yao wenyewe ni kutia ndani Petro, pamoja na wengine wa wale 12 walioandamana na Yesu kwenye safari zake. Kwa kweli wao walimsikia Yesu aliyefufuka akisema akiwa kando ya Bahari ya Galilaya. Simulizi hilo latuambia hivi: “Yesu akawaambia: ‘Njoni, twaeni kifungua-kinywa chenu.’ Hakuna hata mmoja kati ya wanafunzi aliyekuwa na moyo wa kuulizia habari kwake: ‘Wewe ni nani?’ kwa sababu walijua alikuwa Bwana. Yesu akaja na kuchukua ule mkate na kuwapa, na samaki hivyohivyo. Sasa hiyo ilikuwa ni mara ya tatu ambayo Yesu alionekana kwa wanafunzi baada ya kuinuliwa kwake kutoka kwa wafu.”—Yohana 21:12-14, NW.

Kwa hiyo, Petro angeweza kuandika hivi akiwa na usadikisho kamili: “Mbarikiwa awe yule Mungu na Baba ya Bwana wetu Yesu Kristo, kwa maana kulingana na rehema yake kubwa alitupa sisi uzaliwa mpya kwenye tumaini lililo hai kupitia ufufuo wa Yesu Kristo kutoka kwa wafu.”—1 Petro 1:3NW.

Mtume Paulo alionyesha tumaini lake hakika aliposema hivi: “Naamini mambo yote yaliyoelezwa katika ile Sheria na kuandikwa katika Manabii; nami nina tumaini kuelekea Mungu, tumaini ambalo watu hawa wenyewe hulishikilia, kwamba kutakuwa na ufufuo wa waadilifu na wasio waadilifu pia.”—Matendo 24:14, 15NW.

Kwa hiyo mamilioni ya watu waweza kuwa na tumaini thabiti la kuona wapendwa wao wakiwa hai tena hapa duniani lakini chini ya hali zilizo tofauti sana. Hali hizo zitakuwa nini? Habari zaidi juu ya lile tumaini lenye msingi wa Biblia kwa wapendwa wetu waliokufa itazungumziwa katika sehemu ya mwisho ya broshua hii, yenye kichwa “Tumaini Hakika kwa Wafu.”

Lakini acheni kwanza tufikirie maswali ambayo huenda unayo ikiwa unahuzunika kwa sababu ya kifo cha mpendwa: Je! ni kawaida kuhuzunika hivi? Naweza kuishije nikiwa na huzuni yangu? Wengine waweza kufanya nini kunisaidia nishughulike na hali hii? Naweza kuwasaidiaje wengine walio na huzuni? Na hasa, Biblia husema nini juu ya tumaini hakika kwa wafu? Je! nitapata kuwaona wapendwa wangu tena? Na nitawaona wapi?