Hamia kwenye habari

Hamia kwenye yaliyomo

Sura ya 1

“Tazama! Huyu Ni Mungu Wetu”

“Tazama! Huyu Ni Mungu Wetu”

1, 2. (a) Ungependa kumwuliza Mungu maswali gani? (b) Musa alimwuliza Mungu swali gani?

JE, UNAWEZA kuwazia ukizungumza na Mungu? Hilo ni wazo lenye kutia kicho kama nini—kuzungumza na Mwenye Enzi Kuu ya ulimwengu! Unasitasita mwanzoni, hatimaye unafaulu kumjibu. Anakusikiliza, anaitikia, na hata anakuruhusu kuuliza swali lolote ulilo nalo. Basi sasa, utamwuliza swali gani?

2 Hapo kale, mtu mmoja alijikuta katika hali hiyohiyo. Aliitwa Musa. Lakini, swali aliloamua kumwuliza Mungu huenda likakushangaza. Hakuuliza kuhusu hali yake binafsi, wakati wake ujao, wala hata matatizo ya wanadamu. Badala yake, aliuliza jina la Mungu. Huenda hilo likakushangaza, kwa kuwa tayari Musa alijua jina la Mungu. Basi, lazima swali lake liwe lilikuwa na maana kubwa zaidi. Kwa kweli, Musa aliuliza swali muhimu zaidi ya yote. Jibu la swali hilo linatuhusu sote. Linaweza kukusaidia kuchukua hatua muhimu sana ya kumkaribia Mungu. Jinsi gani? Hebu tuchunguze mazungumzo hayo ya pekee.

3, 4. Ni matukio gani yaliyotangulia mazungumzo ya Musa na Mungu, na jambo kuu la mazungumzo hayo lilikuwa nini?

3 Musa alikuwa na umri wa miaka 80. Kwa muda wa miaka 40 alikuwa uhamishoni mbali na watu wake Waisraeli, waliokuwa watumwa nchini Misri. Siku moja, alipokuwa akichunga mifugo ya baba-mkwe wake, aliona jambo la ajabu. Kichaka kiliwaka moto, lakini hakikuteketea. Kiliendelea kuwaka moto, na kung’aa kama ishara mlimani. Musa alikikaribia ili akitazame. Haikosi alishtuka sana aliposikia sauti ikizungumza naye kutoka katikati ya moto huo! Mungu alizungumza na Musa kwa muda mrefu kwa kutumia malaika. Na huenda unajua kwamba Mungu alimwagiza Musa aliyesitasita aache maisha yake matulivu na kurudi Misri ili kuwakomboa Waisraeli kutoka utumwani.—Kutoka 3:1-12.

4 Wakati huo, Musa angaliweza kumwuliza Mungu swali lolote. Hata hivyo, hebu ona swali aliloamua kuuliza: “Tazama, nitakapofika kwa wana wa Israeli, na kuwaambia, Mungu wa baba zenu amenituma kwenu; nao wakaniuliza, Jina lake n’nani? niwaambie nini?”—Kutoka 3:13.

5, 6. (a) Swali la Musa latufundisha ukweli gani sahili ulio muhimu sana? (b) Ni jambo gani lenye kuchukiza ambalo limefanywa kuhusiana na jina la Mungu? (c) Kwa nini ni muhimu kwamba Mungu amewafunulia wanadamu jina lake?

5 Kwanza kabisa, swali hilo latufundisha kwamba Mungu ana jina. Hatupaswi kamwe kupuuza ukweli huo sahili. Lakini, watu wengi hupuuza jambo hilo. Jina la Mungu limeondolewa kwenye tafsiri nyingi sana za Biblia na kubadilishwa na majina ya cheo, kama vile “Bwana” na “Mungu.” Hilo ni mojawapo ya mambo yenye kusikitisha sana na yenye kuchukiza ambayo yamefanywa kwa sababu za kidini. Kwani, wewe hufanya nini kwanza unapokutana na mtu fulani? Unamwuliza jina lake, sivyo? Ndivyo ilivyo na kumjua Mungu. Yeye si Mungu tu asiye na jina, asiye na hisia, asiyeweza kujulikana wala kufahamika. Ijapokuwa haonekani, ana utu, na ana jina—Yehova.

6 Zaidi ya hayo, Mungu anapofunua jina lake, yeye hukusudia kutenda mambo makuu na yenye kuvutia. Anatukaribisha tumjue. Anataka tufanye uamuzi bora zaidi maishani, yaani, kumkaribia yeye. Lakini Yehova amefanya mengi zaidi ya kutuambia jina lake. Ametufundisha pia kuhusu yule anayewakilishwa na jina hilo.

Maana ya Jina la Mungu

7. (a) Jina la Mungu linaweza kumaanisha nini? (b) Musa alitaka kujua nini alipomwuliza Mungu jina Lake?

7 Yehova alijichagulia jina lenye maana sana. Jina “Yehova“ linaweza kumaanisha “Yeye Husababisha Kuwe.“ Kwa kweli, Yeye ni wa pekee katika ulimwengu wote kwa kuwa aliumba vitu vyote, naye husababisha makusudi yake yote yatimie. Wazo hilo linatufanya tumheshimu sana. Lakini je, kuna maana nyingine ya jina la Mungu? Ni wazi kwamba Musa alitaka kujifunza mengi zaidi. Ukweli ni kwamba alijua kuwa Yehova ndiye Muumba, na alilijua jina la Mungu. Jina hilo la Mungu halikuwa geni. Watu walikuwa wamelitumia kwa karne nyingi. Hapana shaka kwamba Musa alipouliza kuhusu jina la Mungu, alitaka kumjua yule anayewakilishwa na jina hilo. Ni kama alikuwa akisema hivi: ‘Niwaambie nini watu wako Israeli kukuhusu ili waweze kukuamini na kusadiki kwamba kwa kweli utawakomboa?’

8, 9. (a) Yehova alijibuje swali la Musa, na kwa nini tafsiri nyingi zimekosea katika kutafsiri jibu Lake? (b) Usemi “Nitathibitika kuwa kile nitakachothibitika kuwa” unamaanisha nini”?

8 Yehova alimjibu kwa kufunua jambo lenye kusisimua kuhusu utu wake. Jambo hilo linahusiana na maana ya jina lake. Alimwambia Musa hivi: “Nitathibitika kuwa kile nitakachothibitika kuwa.” (Kutoka 3:14, NW) Andiko hilo husomeka hivi kwenye tafsiri nyingi za Biblia: “MIMI NIKO AMBAYE NIKO.” Lakini tafsiri sahihi zaidi ya maneno hayo inaonyesha kwamba Mungu hakuwa tu akithibitisha kwamba yeye yupo. Badala yeke, Yehova alikuwa akimfundisha Musa—na sisi sote—kwamba ’angethibitika kuwa,’ au angeamua kuwa chochote alichohitaji kuwa ili kutimiza ahadi Zake.” Tafsiri ya J.B. Rotherham yatafsiri waziwazi mstari huo: “Nitakuwa chochote nipendacho.” Mtaalamu mmoja wa Kiebrania cha Biblia aeleza hivi kuhusu maneno hayo: “Haidhuru ni hali au uhitaji gani uliopo . . . , Mungu ‘atakuwa’ suluhisho la uhitaji huo.”

9 Hilo lilimaanisha nini kwa Waisraeli? Licha ya kizuizi kilichowakabili au magumu ambayo wangepata, Yehova angewakomboa kutoka utumwani na kuwapeleka katika Nchi Iliyoahidiwa. Bila shaka jina hilo liliwatia moyo wamtumaini Mungu. Laweza kuwa na matokeo yayo hayo kwetu. (Zaburi 9:10) Kwa nini?

10, 11. Jina la Yehova linatusaidia jinsi gani kuwa na uhakika kwamba yeye ni Baba bora anayeweza kutimiza wajibu wowote ule? Toa mfano.

10 Kwa mfano: Wazazi wanajua jinsi wanavyotimiza wajibu mbalimbali wanapowatunza watoto wao. Kwa siku moja tu, mzazi anaweza kutenda kama muuguzi, mpishi, mwalimu, mtoa-nidhamu, hakimu, na kadhalika. Wengi hulemewa na wajibu mbalimbali walio nao. Wazazi wengi wanajua kwamba watoto wao huwatumaini kabisa, hawana shaka kwamba Baba au Mama anaweza kupunguza maumivu ya jeraha, kusuluhisha mabishano, kurekebisha kitu chochote cha kuchezea kilichoharibika, na kujibu maswali yoyote wanayouliza kwa sababu ya udadisi-dadisi wa kitoto. Wazazi fulani wanahisi kwamba hawastahili kutumainiwa na watoto wao na mara kwa mara wanavunjika moyo kwa sababu wanashindwa kutimiza kikamili wajibu mwingi walio nao. Jambo hilo linawasikitisha sana.

11 Yehova pia ni Baba mwenye upendo. Yeye huwa chochote atakacho ili kuwatunza watoto wake wa kidunia kwa njia nzuri zaidi, bila kukiuka sheria zake kamilifu. Kwa hiyo, maana ya jina lake, Yehova, inatuhakikishia kwamba yeye ni Baba bora kabisa. (Yakobo 1:17) Punde si punde, Musa na Waisraeli wengine waaminifu waliona kwamba kwa kweli Yehova hutenda kupatana na maana ya jina lake. Walistaajabu kwa kicho Mungu alipoamua kuwa Amiri Jeshi asiyeshindwa, Mdhibiti wa hali zote za asili, Mtunga-sheria asiye na kifani, Hakimu, Msanifu-ujenzi, Mpaji wa chakula na maji, Mtunzaji wa mavazi na viatu—na kadhalika.

12. Maoni ya Farao juu ya Yehova yalitofautiana na ya Musa jinsi gani?

12 Hivyo basi, Mungu amejulisha jina lake, amefunua mambo yenye kusisimua kuhusu yule anayewakilishwa na jina hilo, na hata ameonyesha kwamba yale anayosema kujihusu ni ya kweli. Hapana shaka kwamba Mungu anataka tumjue. Tunaitikiaje? Musa alitaka kumjua Mungu. Hamu hiyo kubwa iliongoza mwenendo wa Musa maishani na ikamsaidia kumkaribia sana Baba yake wa mbinguni. (Hesabu 12:6-8; Waebrania 11:27) Inasikitisha kwamba watu wengi walioishi pindi hiyo hawakuwa na hamu ya kumjua Mungu kama Musa. Musa alipomtajia Farao jina la Yehova, mfalme huyo wa Misri mwenye kiburi aliuliza hivi kwa ukali: “Yehova ni nani?” (Kutoka 5:2, NW) Farao hakutaka kujifunza mengi kumhusu Yehova. Badala yake, alimpuuza Mungu wa Israeli na kumdhihaki kuwa Mungu duni au asiyefaa. Watu wengi leo wana maoni hayohayo. Maoni hayo huwafanya watu wakose kutambua mojawapo ya kweli muhimu zaidi—kwamba Yehova ni Bwana Mwenye Enzi Kuu.

Bwana Mwenye Enzi Kuu Yehova

13, 14. (a) Kwa nini Yehova amepewa majina mengi ya cheo kwenye Biblia? Taja baadhi yake. (Ona sanduku kwenye ukurasa wa 14.) (b) Kwa nini Yehova peke yake ndiye anayestahili kuitwa “Bwana Mwenye Enzi Kuu”?

13 Yehova anaweza kutimiza wajibu mbalimbali, hivi kwamba kwa kufaa Maandiko yanamtaja kwa majina mengi ya cheo. Majina hayo hayachukui mahali pa jina lake; badala yake, yanatufundisha mengi kuhusu maana ya jina lake. Kwa mfano, anaitwa “Bwana Mwenye Enzi Kuu Yehova.” (2 Samweli 7:22, NW) Cheo hicho kitukufu, ambacho kinatajwa tena na tena katika Biblia, hutufahamisha wadhifa wa Yehova. Yeye peke yake ndiye aliye na haki ya kuwa Mtawala wa ulimwengu mzima. Hebu chunguza sababu.

14 Yehova ni wa pekee kwa sababu ni Muumba. Andiko la Ufunuo 4:11 lasema hivi: “Wewe wastahili, Yehova, naam, Mungu wetu, kupokea utukufu na heshima na nguvu, kwa sababu uliumba vitu vyote, na kwa sababu ya mapenzi yako vilikuwako na vikaumbwa.” Maneno hayo ya fahari hayawezi kurejezea mtu mwingine yeyote. Kila kitu ulimwenguni kiliumbwa na Yehova! Hapana shaka kwamba Yehova anastahili heshima, na nguvu, na utukufu kwa sababu yeye ni Bwana Mwenye Enzi Kuu na Muumba wa vitu vyote.

15. Kwa nini Yehova anaitwa “Mfalme wa umilele”?

15 Jina jingine la cheo linalotumiwa kumhusu Yehova peke yake ni “Mfalme wa umilele.” (1 Timotheo 1:17; Ufunuo 15:3) Hilo lamaanisha nini? Akili zetu duni haziwezi kufahamu maana yake, lakini Yehova ni Mungu wa umilele kwa sababu hana mwanzo wala mwisho. Andiko la Zaburi 90:2 lasema: “Na tangu milele hata milele ndiwe Mungu.” Kwa hiyo Yehova hakuwa na mwanzo; amekuwapo daima dawamu. Anaitwa kwa kufaa “Mzee wa Siku,” kwa sababu amekuwapo kwa umilele kabla ya mtu yeyote na kabla ya kitu chochote kuwapo! (Danieli 7:9, 13, 22) Ni nani anayeweza kupinga kihalali haki yake ya kuwa Bwana Mwenye Enzi Kuu?

16, 17. (a) Kwa nini hatuwezi kumwona Yehova, na kwa nini hilo halipasi kutushangaza? (b) Yehova yukoje halisi kuliko kitu chochote tunachoweza kuona au kugusa?

16 Lakini watu fulani hupinga haki yake kama alivyofanya Farao. Tatizo hilo linazuka kwa sababu wanadamu wasiokamilika huamini hasa vitu wanavyoweza kuona. Hatuwezi kumwona Bwana Mwenye Enzi Kuu. Yeye ni roho, na wanadamu hawawezi kumwona. (Yohana 4:24) Isitoshe, mwanadamu mwenye mwili wa damu na nyama hawezi kumwona Yehova Mungu uso kwa uso na aishi. Yehova mwenyewe alimwambia Musa hivi: “Huwezi kuniona uso wangu, maana mwanadamu hataniona akaishi.”—Kutoka 33:20; Yohana 1:18.

17 Jambo hilo halipasi kutushangaza. Ni wazi kwamba Musa aliona kwa kiasi kidogo utukufu wa Yehova kupitia kwa malaika aliyemwakilisha. Matokeo yalikuwa nini? Uso wa Musa ‘uling’aa’ kwa muda fulani baadaye. Waisraeli hata waliogopa kumtazama Musa usoni. (Kutoka 33:21-23; 34:5-7, 29, 30) Hivyo basi, ni wazi kwamba hakuna mwanadamu awaye yote anayeweza kumtazama Bwana Mwenye Enzi Kuu katika utukufu wake wote! Je, hilo lamaanisha kwamba yeye si halisi kama vitu tunavyoweza kuona na kugusa? La hasha, kuna vitu vingi tunavyokubali ni halisi ijapokuwa hatuwezi kuviona—kwa mfano, upepo, mawimbi ya redio, na mawazo. Zaidi ya hayo, Yehova hudumu milele, haathiriwi na kupita kwa wakati, hata mabilioni mengi ya miaka! Katika maana hiyo, yeye ni halisi kuliko kitu chochote tunachoweza kugusa au kuona, kwa kuwa vitu vya kimwili huzeeka na kuoza. (Mathayo 6:19) Basi je, tumwone tu kuwa nguvu fulani isiyoonekana na isiyo na utu, au Kisababishi kisichoeleweka? Hebu tuone.

Mungu Mwenye Utu

18. Ezekieli alipewa ono gani, na zile nyuso nne za “viumbe hai” walio karibu na Yehova zinawakilisha nini?

18 Ijapokuwa hatuwezi kumwona Mungu, kuna maandiko ya Biblia yenye kusisimua yanayotusaidia kuelewa hali ya mbinguni. Mojawapo ni sura ya kwanza ya Ezekieli. Ezekieli alipewa ono la tengenezo la kimbingu la Yehova, lililofananishwa na gari kubwa mno la kimbingu. Jambo linalovutia zaidi ni maelezo kuhusu viumbe wa roho wenye nguvu wanaomzingira Yehova. (Ezekieli 1:4-10) Hao “viumbe hai” wanashirikiana kwa ukaribu na Yehova, na umbo lao latusaidia kuelewa jambo muhimu sana kuhusu Mungu wanayemtumikia. Kila kiumbe ana nyuso nne—uso wa fahali, simba, tai, na mwanadamu. Ni wazi kwamba nyuso hizo zinawakilisha sifa nne kuu za utu wa Yehova.—Ufunuo 4:6-8, 10.

19. Ni sifa ipi inayowakilishwa na (a) uso wa fahali? (b) uso wa simba? (c) uso wa tai? (d) uso wa mwanadamu?

19 Mara nyingi fahali hutumiwa katika Biblia kuwakilisha nguvu, na hilo linafaa kwa sababu ni mnyama mwenye nguvu sana. Kwa upande mwingine, simba mara nyingi huwakilisha haki, kwa sababu haki ya kweli inahitaji ujasiri, sifa kuu ya simba. Tai ni maarufu kwa sababu ya uwezo wao makini wa kuona, wanaweza kuona hata vitu vidogo sana vilivyo umbali wa kilometa nyingi. Kwa hiyo, uso wa tai unawakilisha ifaavyo hekima ya Mungu ya kutambua mambo kimbele. Vipi uso wa mwanadamu? Kwa kweli, mwanadamu, aliyeumbwa kwa mfano wa Mungu, hana kifani katika kuonyesha sifa kuu zaidi ya Mungu—upendo. (Mwanzo 1:26) Sifa hizo mbalimbali za utu wa Yehova—nguvu, haki, hekima, na upendo—hukaziwa tena na tena katika Maandiko hivi kwamba zinaweza kuitwa sifa kuu za Mungu.

20. Je, tuwe na wasiwasi kwamba huenda utu wa Yehova umebadilika, na kwa nini unajibu hivyo?

20 Je, tuwe na wasiwasi kwamba huenda Mungu amebadilika tangu Biblia ilipotaja sifa zake maelfu ya miaka iliyopita? La, utu wa Mungu haubadiliki. Anatuambia hivi: “Mimi, BWANA, sina kigeugeu.” (Malaki 3:6) Yehova habadili maoni yake ovyoovyo, badala yake yeye hujithibitisha kuwa Baba anayefaa kabisa kwa kukabiliana na kila hali inayozuka. Yeye hudhihirisha sifa muhimu za utu wake kwa wakati unaofaa. Kati ya zile sifa nne, sifa kuu zaidi ni upendo. Upendo hudhihirika katika kila jambo ambalo Mungu anafanya. Yeye hutumia nguvu, haki, na hekima yake kwa njia ya upendo. Kwa kweli, Biblia husema jambo fulani la pekee kuhusu Mungu na sifa hii. Inasema: “Mungu ni upendo.” (1 Yohana 4:8) Hebu ona kwamba haisemi Mungu ana upendo wala haisemi Mungu hupenda. Badala yake, inasema kwamba Mungu ni upendo. Upendo, ambao ni utu wake wa asili, huongoza matendo yake yote.

“Tazama, Huyu Ndiye Mungu Wetu”

21. Tutahisije tunapoendelea kujua sifa za Yehova vizuri zaidi?

21 Je, umewahi kumwona mtoto mdogo akiwaonyesha rafiki zake babaye na kusema hivi kwa furaha na fahari, “Huyu ni baba yangu”? Waabudu wa Mungu wana sababu nzuri sana za kuhisi vivyo hivyo kumhusu Yehova. Biblia inatabiri kuhusu wakati ambapo watu waaminifu watasema hivi kwa shauku: “Tazama, huyu ndiye Mungu wetu.” (Isaya 25:8, 9) Kadiri unavyojua sifa za Yehova vizuri zaidi, ndivyo utakavyohisi kwamba una Baba bora zaidi.

22, 23. Biblia inasema Baba yetu wa mbinguni yukoje, nasi twajuaje kwamba anataka tumkaribie?

22 Huyu si Baba asiye na hisia au asiyejali kama vile wanadini na wanafalsafa fulani washupavu wanavyofundisha. Hatuwezi kumkaribia Mungu asiye na hisia, wala Biblia haisemi kwamba Baba yetu wa mbinguni yuko hivyo. Badala yake, inamwita “Mungu mwenye furaha.” (1 Timotheo 1:11) Ana hisia changamfu na zenye upendo. Yeye ‘huhuzunika moyo’ viumbe wake wenye akili wanapokosa kutii maagizo anayowapa ili kuwalinda. (Mwanzo 6:6; Zaburi 78:41) Lakini tunapotenda kwa hekima kupatana na Neno lake, ‘tunaufurahisha moyo’ wake.—Mithali 27:11.

23 Baba yetu anataka tumkaribie. Neno lake hutuhimiza ‘tupapase-papase tukimtafuta na kwa kweli tumpate, ijapokuwa, kwa kweli yeye hayuko mbali sana na kila mmoja wetu.’ (Matendo 17:27) Lakini, wanadamu wanaweza kumkaribia jinsi gani Bwana Mwenye Enzi Kuu ya ulimwengu?