Hamia kwenye habari

Hamia kwenye yaliyomo

Sura ya 2

Je, Kweli Unaweza ‘Kumkaribia Mungu’?

Je, Kweli Unaweza ‘Kumkaribia Mungu’?

1, 2. (a) Huenda watu wengi wakaona jambo jipi kuwa lisilowezekana, lakini Biblia inatuhakikishia nini? (b) Abrahamu alifurahia uhusiano upi wa karibu, na kwa nini?

UNGEHISIJE ikiwa Muumba wa mbingu na dunia angesema hivi kukuhusu, “Huyu ni rafiki yangu”? Huenda watu wengi wakaliona kuwa jambo lisilowezekana. Kwani, mwanadamu anawezaje kuwa rafiki ya Yehova Mungu? Lakini, Biblia inatuhakikishia kwamba tunaweza kwa kweli kumkaribia Mungu.

2 Abrahamu aliyeishi nyakati za kale alifurahia uhusiano wa karibu na Mungu. Yehova alimwita huyo mzee wa ukoo “rafiki yangu.” (Isaya 41:8) Naam, Yehova alimwona Abrahamu kuwa rafiki yake mkubwa. Abrahamu alifurahia uhusiano huo wa karibu kwa sababu “aliweka imani katika Yehova.” (Yakobo 2:23) Hali kadhalika leo, Yehova hutafuta fursa za ‘kuwapenda kwa dhati’ wale wanaomtumikia kwa sababu wanampenda. (Kumbukumbu la Torati 10:15, Biblia Habari Njema) Neno lake linatusihi hivi: “Mkaribieni Mungu, naye atawakaribia.” (Yakobo 4:8) Anatualika tumkaribie na kututolea ahadi kwa maneno hayo.

3. Yehova anatualika tufanye nini, naye anatuahidi nini?

3 Yehova anatualika tumkaribie. Yuko tayari na ana nia ya kutukubali kuwa rafiki zake. Vilevile, anaahidi kwamba tukijitahidi kumkaribia, atatukaribia pia. Kwa hiyo, tunaweza kufurahia jambo muhimu sana—kuwa ‘msiri wa BWANA.’ * (Zaburi 25:14) Neno ‘-a siri’ latoa maana ya mazungumzo ya siri na rafiki wa karibu.

4. Rafiki msiri ni rafiki wa aina gani, na Yehova huthibitikaje kuwa rafiki msiri kwa wale wanaomkaribia?

4 Je, una rafiki msiri unayezungumza naye mambo yako ya siri? Huyo ni rafiki anayekujali. Unamtumaini kwa sababu amekuwa mwaminifu. Unafurahi hata zaidi unapomwambia mambo yanayokufurahisha. Anasikiliza kwa huruma unapomweleza mambo yanayokuhuzunisha na hivyo unapata utulivu. Hata inapoonekana kwamba hakuna mtu mwingine anayeelewa hali yako, yeye hukuelewa. Vivyo hivyo, unapomkaribia Mungu, unapata Rafiki wa pekee ambaye anakuthamini sana, anakujali sana, na kukuelewa kabisa. (Zaburi 103:14; 1 Petro 5:7) Unamtumaini na kumweleza hisia zako za moyoni, kwa kuwa unajua kwamba yeye ni mwaminifu kwa wale walio waaminifu kwake. (Zaburi 18:25, Biblia Habari Njema) Hata hivyo, Mungu ndiye ametuandalia fursa ya kuwa na urafiki wa karibu sana pamoja naye.

Yehova Amefungua Njia

5. Yehova alifanya nini ili kutuwezesha tumkaribie?

5 Tukiwa wanadamu wenye dhambi hatungeweza kamwe kumkaribia Mungu pasipo msaada. (Zaburi 5:4) “Lakini Mungu apendekeza upendo wake mwenyewe kwetu kwa kuwa, tulipokuwa tungali watenda-dhambi, Kristo alikufa kwa ajili yetu,” akaandika mtume Paulo. (Waroma 5:8) Ndiyo, Yehova alipanga Yesu ‘atoe nafsi yake kuwa fidia katika kubadilishana kwa ajili ya wengi.’ (Mathayo 20:28) Imani yetu katika dhabihu hiyo ya fidia hutuwezesha kumkaribia Mungu. Kwa kuwa Mungu “alitupenda sisi kwanza,” alituwekea msingi ili tuwe na urafiki pamoja naye.—1 Yohana 4:19.

6, 7. (a) Tunajuaje kwamba Yehova si Mungu aliyejificha na asiyeeleweka? (b) Yehova amejifunua kwa njia zipi?

6 Yehova amechukua hatua nyingine: Amejifunua kwetu. Katika urafiki wowote ule, uhusiano wa karibu hutegemea kumjua mtu kabisa, kuthamini sifa na mwenendo wake. Kwa hiyo, hatungeweza kamwe kumkaribia Yehova endapo angekuwa Mungu aliyejificha na asiyeeleweka. Lakini, yeye hajifichi, anataka tumjue. (Isaya 45:19) Isitoshe, watu wote hata wale ambao huenda wanaonwa na ulimwengu kuwa watu wa hali ya chini wanaweza kujua mambo anayofunua kujihusu.—Mathayo 11:25.

Yehova amejifunua kupitia uumbaji wake na Neno lake lililoandikwa

7 Yehova amejifunuaje kwetu? Uumbaji wake unafunua sifa mbalimbali za utu wake—nguvu zake zisizo na mipaka, hekima yake isiyo na kifani, na upendo wake mkubwa. (Waroma 1:20) Lakini Yehova hujifunua kwa njia nyingine mbali na uumbaji wake. Yehova huwaelimisha watu daima kwa njia bora sana, na hivyo ametupatia Neno lake, Biblia, ambalo linafunua jinsi alivyo.

Kuutazama ‘Uzuri wa Bwana’

8. Kwa nini inaweza kusemwa kwamba Biblia yenyewe ni ushuhuda wa kwamba Yehova anatupenda?

8 Biblia yenyewe ni ushuhuda wa kwamba Yehova anatupenda. Katika Neno lake, yeye hujifunua kwa kutumia lugha tunayoweza kufahamu—na hilo huthibitisha kwamba anatupenda na anataka tumjue na kumpenda. Habari tunazosoma katika kitabu chake muhimu sana hutuwezesha tuutazame “uzuri wa BWANA” na hutufanya tutake kuwa karibu naye. (Zaburi 90:17) Na tuzungumzie baadhi ya njia zenye kuvutia ambazo Yehova hujifunua katika Neno lake.

9. Ni ipi baadhi ya mistari ya Biblia inayotaja sifa za Mungu moja kwa moja?

9 Maandiko yana mistari mingi inayotaja sifa za Mungu moja kwa moja. Angalia mifano kadhaa. “BWANA hupenda haki.” (Zaburi 37:28) Mungu ni “mkuu mwenye uweza.” (Ayubu 37:23) “‘Mimi ni mwaminifu,’ asema Yehova.” (Yeremia 3:12, NW) “Yeye ni mwenye hekima moyoni.” (Ayubu 9:4) Yeye ni “Mungu mwingi wa huruma, mwenye fadhili, si mwepesi wa hasira, mwingi wa rehema na kweli.” (Kutoka 34:6) “Wewe, Bwana, u mwema, umekuwa tayari kusamehe.” (Zaburi 86:5) Na kama ilivyotajwa katika sura iliyotangulia, kuna sifa moja kuu zaidi: “Mungu ni upendo.” (1 Yohana 4:8) Unapotafakari sifa hizi zenye kupendeza, je, huvutiwi na Mungu huyu asiye na kifani?

Biblia inatusaidia tumkaribie Yehova

10, 11. (a) Ili kutusaidia kuelewa utu wake vizuri zaidi, Yehova ametaja nini katika Neno lake? (b) Ni simulizi gani la Biblia linalotusaidia kuona Mungu akidhihirisha nguvu zake?

10 Mbali na kutueleza sifa zake, kwa upendo Yehova ametaja pia katika Neno lake mifano hususa inayoonyesha jinsi alivyodhihirisha sifa hizo kwa matendo. Masimulizi hayo yanatokeza picha akilini inayotusaidia kufahamu vizuri zaidi sifa mbalimbali za utu wake. Na hilo hutusaidia kumkaribia. Fikiria mfano mmoja.

11 Ni jambo moja kusoma kwamba Mungu “ni hodari kwa nguvu.” (Isaya 40:26) Na ni jambo tofauti kabisa kusoma kuhusu jinsi alivyokomboa Israeli walipovuka Bahari Nyekundu kisha akalitunza taifa hilo jangwani kwa miaka 40. Hebu ona yale maji yenye nguvu yakigawanyika. Ona taifa hilo—lenye jumla ya watu 3,000,000 hivi—likitembea katika bonde kavu la bahari, maji yakiwa yamegandamana na kusimama wima kama kuta kubwa upande huu na upande huu. (Kutoka 14:21; 15:8) Unaweza kuona uthibitisho wa kwamba Mungu aliwatunza na kuwalinda jangwani. Maji yalitiririka mwambani. Chakula kilichokuwa mfano wa punje nyeupe, kilisambaa ardhini. (Kutoka 16:31; Hesabu 20:11) Kisa hicho chaonyesha kwamba Yehova ana nguvu na yeye huzitumia kuwasaidia watu wake. Je, si jambo lenye kutia moyo kujua kwamba sala zetu humfikia Mungu mwenye nguvu ambaye ‘ni kimbilio letu na nguvu yetu, na msaada wetu daima wakati wa taabu’?—Zaburi 46:1, BHN.

12. Yehova hutusaidiaje kufahamu jinsi alivyo kwa kutumia usemi tunaoweza kuelewa?

12 Yehova, ambaye ni roho, amefanya mengi zaidi ili kutusaidia kumjua. Tukiwa wanadamu, uwezo wetu wa kuona una mipaka na hivyo hatuwezi kuona makao ya roho. Kama Mungu angetueleza utu wake kwa kutumia usemi wa roho ingekuwa ni kama kujaribu kumweleza mtu aliyezaliwa kipofu kila jambo kuhusu sura yako, kama vile rangi ya macho yako au madoa uliyo nayo ngozini. Badala yake, Yehova hutusaidia kwa fadhili kufahamu jinsi alivyo kwa kutumia usemi tunaoweza kuelewa. Nyakati nyingine, yeye huongea kwa kutumia semi za mlinganisho na mifano, akijifananisha na vitu tunavyojua. Hata anajieleza kuwa na viungo fulani vya kibinadamu. *

13. Andiko la Isaya 40:11 linaleta picha gani akilini, nalo linakufanya uhisije?

13 Hebu tazama jinsi Yehova anavyofafanuliwa katika Isaya 40:11: “Atalilisha kundi lake kama mchungaji, atawakusanya wana-kondoo mikononi mwake; na kuwachukua kifuani mwake.” Hapa Yehova analinganishwa na mchungaji ambaye hubeba wana-kondoo “mikononi mwake.” Hilo laonyesha uwezo wa Mungu wa kuwalinda na kuwategemeza watu wake, hata wale walio dhaifu. Tunaweza kuhisi tukiwa salama katika mikono yake yenye nguvu, kwa sababu hatatuacha kamwe tukiwa waaminifu kwake. (Waroma 8:38, 39) Mchungaji Mkuu huwachukua wana-kondoo “kifuani mwake”—usemi huo unarejezea mapindo mapana ya vazi la juu, ambamo nyakati nyingine mchungaji alibebea mwana-kondoo aliyetoka kuzaliwa. Kwa hiyo, tunahakikishiwa kwamba Yehova anatupenda sana naye anatutunza kwa upendo. Ni jambo la kawaida kutaka kuwa karibu naye.

‘Mwana Anapenda Kumfunua’

14. Kwa nini inaweza kusemwa kwamba Yehova hujifunua kindani zaidi kupitia Yesu?

14 Yehova hujifunua kindani zaidi katika Neno lake kupitia Mwanaye mpendwa, Yesu. Hakuna mtu awaye yote angeweza kudhihirisha hisia na fikira za Mungu kwa njia bora zaidi au kueleza utu Wake kwa njia wazi zaidi kuliko Yesu. Kwani, Mwana huyo mzaliwa wa kwanza aliishi na Baba yake kabla ya viumbe wengine wa roho na ulimwengu kuumbwa. (Wakolosai 1:15) Yesu alimjua Yehova kabisa. Ndiyo sababu alisema: ‘Mwana ni nani hakuna ajuaye ila Baba; na ya kwamba Baba ni nani, hakuna ajuaye ila Mwana, na yeye ambaye Mwana anapenda kumfunua.’ (Luka 10:22) Alipokuwa mwanadamu duniani, Yesu alimfunua Baba yake kwa njia mbili muhimu.

15, 16. Yesu alimfunua Baba yake katika njia zipi mbili?

15 Kwanza, mafundisho ya Yesu yanatusaidia kumjua Baba yake. Yesu alieleza jinsi Yehova alivyo kwa kutumia maneno yanayotugusa hisia. Kwa mfano, alipokuwa akieleza kuhusu Mungu mwenye rehema anayewakaribisha tena watenda-dhambi wanaotubu, Yesu alimlinganisha Yehova na baba mwenye rehema. Baba huyo anasikitika sana anapomwona mwanaye aliyepotea akirudi, anamkimbilia na kumkumbatia na kumbusu kwa upendo. (Luka 15:11-24) Yesu pia alionyesha kwamba Yehova ni Mungu ambaye ‘anavuta’ watu wenye mioyo minyofu kwa sababu anampenda kila mmoja wao. (Yohana 6:44) Yeye hata hujua shore mdogo anapoanguka kwenye ardhi. “Msiwe na hofu, nyinyi ni bora zaidi kuliko shore wengi,” akaeleza Yesu. (Mathayo 10:29, 31) Bila shaka tunavutiwa kumkaribia Mungu huyo mwenye kujali.

16 Pili, kielelezo cha Yesu kinatuonyesha utu wa Yehova. Yesu alimwiga kabisa Baba yake hata akasema hivi: “Yeye ambaye ameniona mimi amemwona Baba pia.” (Yohana 14:9) Kwa hiyo, tunaposoma habari za Yesu kwenye vitabu vya Injili—hisia alizokuwa nazo na jinsi alivyowatendea wengine—tunaweza kusema kwamba tunaona udhihirisho halisi wa Baba yake. Huo ndio ufunuo bora zaidi na ulio wazi zaidi wa sifa za Yehova. Kwa nini?

17. Toa mfano unaoonyesha jambo ambalo Yehova amefanya ili kutusaidia tumjue.

17 Kwa mfano: Hebu jiwazie ukijaribu kueleza maana ya fadhili. Huenda ukaifafanua kwa maneno. Lakini ukiashiria mtu fulani anayetenda tendo la fadhili na kusema, “Yule anafanya tendo la fadhili,” neno “fadhili” huwa wazi na hueleweka kwa urahisi zaidi. Yehova amefanya vivyo hivyo ili kutusaidia tumjue. Pamoja na kueleza utu wake kwa maneno, ametupa kielelezo halisi cha Mwanaye. Matendo ya Yesu yanadhihirisha sifa za Mungu waziwazi. Kupitia vitabu vya Injili vinavyosimulia habari za Yesu, ni kana kwamba Yehova anasema hivi: “Hivyo ndivyo nilivyo.” Maandiko yaliyopuliziwa yanasema Yesu alikuwaje alipokuwa duniani?

18. Yesu alionyeshaje sifa za nguvu, haki, na hekima?

18 Sifa nne kuu za Mungu zilidhihirishwa kwa njia ya pekee sana na Yesu. Alikuwa na nguvu za kukomesha magonjwa, njaa, hata kifo. Lakini, hakutumia kamwe nguvu zake za kufanya miujiza ili kujifaidi au kuwaumiza wengine kama wanadamu wenye ubinafsi wanavyotumia vibaya nguvu zao. (Mathayo 4:2-4) Alipenda haki. Alikasirika sana kwa njia ya uadilifu alipoona wafanyabiashara wenye hila wakiwapunja watu. (Mathayo 21:12, 13) Hakuwaonea maskini na wenye kudharauliwa, aliwasaidia kupata “burudisho” kwa ajili ya nafsi zao. (Mathayo 11:4, 5, 28-30) Mafundisho ya Yesu ambaye alikuwa “zaidi ya Solomoni,” yalikuwa na hekima isiyo na kifani. (Mathayo 12:42) Lakini Yesu hakujigamba kwa hekima hiyo. Maneno yake yaligusa hisia za watu wa hali ya chini, kwa kuwa mafundisho yake yalikuwa wazi, rahisi, na yenye kufaidi.

19, 20. (a) Yesu alionyeshaje upendo kwa njia ya pekee sana? (b) Tunaposoma na kutafakari kielelezo cha Yesu, tunapaswa kukumbuka nini?

19 Yeye alionyesha upendo kwa njia ya pekee sana. Katika huduma yake yote, alionyesha upendo kwa njia mbalimbali, alionyesha hisia-mwenzi na huruma. Alisikitika sana alipowaona watu wakiteseka. Mara nyingi, alichukua hatua kwa sababu ya kuwasikitikia wengine. (Mathayo 14:14) Ijapokuwa aliwaponya wagonjwa na kuwalisha wenye njaa, Yesu aliwahurumia watu kwa njia muhimu hata zaidi. Aliwasaidia wengine kujua, kukubali, na kupenda kweli kuhusu Ufalme wa Mungu ambao utawaletea wanadamu baraka za milele. (Marko 6:34; Luka 4:43) Zaidi ya yote, Yesu alionyesha upendo wa kujidhabihu kwa kutoa nafsi yake kwa hiari kwa niaba ya wengine.—Yohana 15:13.

20 Si ajabu kwamba watu wa kila umri na malezi walivutiwa na mwanamume huyu mchangamfu na mwenye hisia sana. (Marko 10:13-16) Hata hivyo, tunaposoma na kutafakari maisha ya Yesu, tukumbuke daima kwamba Mwana huyo anatudhihirishia waziwazi utu wa Baba yake.—Waebrania 1:3.

Kitabu cha Kutusaidia Kujifunza

21, 22. Kumtafuta Yehova kwatia ndani nini, na kitabu hiki kina mambo yapi ya kutusaidia tufikie mradi huo?

21 Hapana shaka yoyote kwamba Yehova anataka tuwe karibu naye, kwa sababu amefunua utu wake waziwazi katika Neno lake. Lakini hatulazimishi kuwa na uhusiano mzuri pamoja naye. Ni juu yetu kumtafuta Yehova “maadamu anapatikana.” (Isaya 55:6) Kumtafuta Yehova kwatia ndani kujua sifa zake na kujua njia yake ya kutenda mambo kama inavyoonyeshwa katika Biblia. Kitabu hiki kimekusudiwa kukusaidia ufikie mradi huo.

22 Utaona kwamba kitabu hiki kimegawanywa kwa sehemu zinazozungumzia sifa nne kuu za Yehova: nguvu, haki, hekima, na upendo. Kila sehemu huanza kwa kutoa muhtasari kuhusu sifa inayozungumziwa. Sura kadhaa zinazofuata zinazungumzia jinsi Yehova anavyodhihirisha sifa hiyo kwa njia mbalimbali. Kila sehemu pia ina sura inayoonyesha jinsi Yesu alivyodhihirisha sifa hiyo, na sura moja inayozungumzia jinsi tunavyoweza kudhihirisha sifa hiyo maishani mwetu.

23, 24. (a) Eleza kuhusu sehemu ya pekee ya “Maswali ya Kutafakari.” (b) Kutafakari kunatusaidiaje kumkaribia Mungu zaidi?

23 Kuanzia sura hii kuna sehemu ya pekee yenye kichwa “Maswali ya Kutafakari.” Kwa mfano, hebu angalia sanduku kwenye ukurasa wa 24. Maandiko na maswali yaliyoonyeshwa hayakusudiwi kurudia tu sura. Badala yake, yanakusudiwa kukusaidia utafakari mambo mengine muhimu kuhusiana na habari hiyo. Unaweza kutumiaje kwa manufaa sehemu hiyo? Fungua kila andiko lililotajwa, na ulisome kwa uangalifu sana. Kisha chunguza swali linaloambatana na kila andiko. Tafakari majibu yake. Unaweza kufanya utafiti. Jiulize maswali mengine ya ziada: ‘Habari hii inanifundisha nini kumhusu Yehova? Inanihusuje? Ninaweza kuitumiaje kuwasaidia wengine?’

24 Kutafakari kunaweza kutusaidia tumkaribie Yehova zaidi. Jinsi gani? Biblia inaonyesha kwamba kutafakari kunahusisha moyo. (Zaburi 19:14) Tunapothamini sana mambo tunayojifunza kumhusu Mungu, habari hizo hufika kwenye moyo wetu wa mfano, kisha zinabadili fikira zetu, zinagusa hisia zetu, na hatimaye tunachochewa kutenda. Upendo wetu kwa Mungu hutia mizizi, na upendo huo hutufanya tutake kumpendeza akiwa Rafiki yetu mpendwa. (1 Yohana 5:3) Ili kuwa na uhusiano huo, hatuna budi kujua sifa za Yehova na jinsi anavyotenda mambo. Kwanza, acheni tuzungumzie sifa moja ya utu wa Mungu ambayo hutuvutia sana tumkaribie—utakatifu wake.

^ fu. 3 Jambo la kuvutia ni kwamba, neno la Kiebrania linalotafsiriwa ‘-a siri’ limetumiwa kwenye andiko la Amosi 3:7, lisemalo kwamba Bwana Mwenye Enzi Kuu Yehova huwafunulia watumishi wake “siri yake,” na kuwajulisha kimbele mambo anayokusudia kufanya.

^ fu. 12 Kwa mfano, Biblia husema juu ya uso, macho, masikio, pua, kinywa, mikono, na miguu ya Mungu. (Zaburi 18:15; 27:8; 44:3; Isaya 60:13; Mathayo 4:4; 1 Petro 3:12) Semi hizo za mfano hazipasi kuchukuliwa kihalisi, kama tusivyoelewa kihalisi semi kama vile Yehova ni “Mwamba” au “ngao.”—Kumbukumbu la Torati 32:4; Zaburi 84:11.