Hamia kwenye habari

Hamia kwenye yaliyomo

Sura ya 7

Nguvu za Kulinda—“Mungu Ni Kimbilio Letu”

Nguvu za Kulinda—“Mungu Ni Kimbilio Letu”

1, 2. Waisraeli walikabili hatari gani walipofika eneo la Sinai mwaka wa 1513 K.W.K., na Yehova aliwatiaje moyo?

WAISRAELI walikuwa hatarini walipofika eneo la Sinai mapema mwaka wa 1513 K.W.K. Wangefunga safari ndefu yenye kuogofya sana, wangesafiri katika “lile jangwa kubwa na la kutisha, lenye nyoka wenye sumu na ng’e.” (Kumbukumbu la Torati 8:15, BHN) Walikabili pia tisho la kushambuliwa na mataifa yenye uadui. Yehova aliwaleta watu wake katika hali hiyo. Je, angeweza kuwalinda akiwa Mungu wao?

2 Maneno ya Yehova yalikuwa yenye kutia moyo sana: “Mmeona jinsi nilivyowatendea Wamisri, na jinsi nilivyowachukua ninyi juu ya mbawa za tai, nikawaleta ninyi kwangu mimi.” (Kutoka 19:4) Yehova aliwakumbusha watu wake kwamba aliwakomboa kutoka kwa Wamisri, ni kama aliwachukua juu ya mbawa za tai na kuwapeleka mahali salama. Lakini kuna sababu nyingine zinazofanya “mbawa za tai” ziwe mfano ufaao wa ulinzi wa Mungu.

3. Kwa nini “mbawa za tai” ni mfano ufaao wa ulinzi wa Mungu?

3 Tai hutumia mbawa zake pana na zenye nguvu sana kwa sababu nyingine mbali na kupaa hewani. Kunapokuwa na joto kali wakati wa mchana, tai mama hukunja mbawa zake—ambazo zinaweza kuwa na upana wa zaidi ya meta mbili—ili kufunika na kulinda makinda yake dhaifu kutokana na joto kali sana la jua. Nyakati nyingine, yeye huyafunika makinda yake kwa mbawa zake na kuyalinda na upepo wenye baridi. Yehova alilinda na kukinga taifa changa la Israeli kama tai anavyolinda makinda yake. Sasa wakiwa jangwani, watu wake wangeendelea kukimbilia uvuli wa mbawa zake za mfano zenye nguvu maadamu walibaki waaminifu. (Kumbukumbu la Torati 32:9-11; Zaburi 36:7) Lakini je, leo tunaweza kutarajia kwa kufaa kupata ulinzi wa Mungu?

Ahadi ya Kupata Ulinzi wa Mungu

4, 5. Kwa nini tunaweza kutumaini kabisa ahadi ya Mungu ya kutulinda?

4 Bila shaka Yehova anaweza kuwalinda watumishi wake. Yeye ni “Mungu Mwenyezi”—cheo hicho kinamaanisha kwamba ana nguvu zisizoweza kushindwa. (Mwanzo 17:1) Kama wimbi lenye nguvu sana, nguvu za Yehova haziwezi kuzuiwa. Kwa kuwa anaweza kufanya jambo lolote kulingana na mapenzi yake, huenda tukauliza hivi, ‘Je, ni mapenzi ya Yehova kutumia nguvu zake ili kuwalinda watu wake?

5 Kwa neno moja, jibu ni ndiyo! Yehova anatuhakikishia kwamba atawalinda watu wake. “Mungu ni kimbilio letu na nguvu yetu, yeye ni msaada wetu daima wakati wa taabu,” yasema Zaburi 46:1, BHN. Kwa kuwa Mungu ‘hawezi kusema uwongo,’ tunaweza kutumaini kabisa ahadi yake ya kutulinda. (Tito 1:2) Hebu tuchunguze baadhi ya mifano dhahiri ambayo Yehova anatumia ili kuonyesha ulinzi wake.

6, 7. (a) Mchungaji katika nyakati za Biblia aliwalinda kondoo wake kutokana na nini? (b) Biblia inatoa mfano gani unaoonyesha jinsi Yehova anavyotaka kwa dhati kulinda na kutunza kondoo wake?

6 Yehova ni Mchungaji, nasi tu “watu wake, na kondoo wa malisho yake.” (Zaburi 23:1; 100:3) Wanyama wengi si hoi kama kondoo anayefugwa. Mchungaji katika nyakati za Biblia alihitaji kuwa jasiri ili kuwalinda kondoo wake kutoka kwa simba, mbwa-mwitu, na dubu, na vilevile wezi. (1 Samweli 17:34, 35; Yohana 10:12, 13) Lakini nyakati nyingine kuwalinda kondoo kulihitaji wororo. Kondoo alipozalia mbali na zizi, mchungaji mwenye kujali angemlinda mama huyo pindi hiyo alipohitaji sana ulinzi, kisha angembeba mwana-kondoo wake dhaifu na kumpeleka zizini.

’Atawachukua kifuani mwake’

7 Kwa kujilinganisha na mchungaji, Yehova anatuhakikishia kwamba anataka kwa dhati kutulinda. (Ezekieli 34:11-16) Hebu kumbuka jinsi Yehova anavyoelezwa kwenye Isaya 40:11, kama Sura ya 2 ya kitabu hiki ilivyoonyesha: “Atalilisha kundi lake kama mchungaji, atawakusanya wana-kondoo mikononi mwake; na kuwachukua kifuani mwake.” Mwana-kondoo mchanga anafikaje “kifuani” mwa mchungaji—katika mapindo ya vazi lake la juu? Huenda mwana-kondoo huyo akamkaribia mchungaji, na hata kugusa mguu wake kwa upole. Hata hivyo, ni lazima mchungaji ainame, amchukue mwana-kondoo huyo, na kumweka taratibu kifuani penye usalama. Huo ni mfano wenye kugusa moyo kama nini unaoonyesha jinsi Mchungaji wetu Mkuu alivyo tayari kutukinga na kutulinda!

8. (a) Ni nani wanaoahidiwa kupata ulinzi wa Mungu, na hilo linaonyeshwaje na Mithali 18:10? (b) Kukimbilia jina la Mungu kunahusisha nini?

8 Ahadi ya Mungu ya kuandaa ulinzi ina masharti—wale tu wanaomkaribia ndiyo wanaopata ulinzi huo. Andiko la Mithali 18:10 lasema: “Jina la BWANA ni ngome imara. Mwenye haki huikimbilia, akawa salama.” Katika nyakati za Biblia, mara kwa mara ngome zilijengwa jangwani kama mahali salama pa kukimbilia. Lakini yule aliyekuwa hatarini ndiye aliyekuwa na daraka la kukimbilia kwenye ngome hizo ili kupata usalama. Ndivyo ilivyo na kukimbilia jina la Mungu. Hilo halimaanishi kurudia-rudia tu jina la Mungu; jina la Mungu si hirizi ya kimizungu. Badala yake, tunahitaji kumjua na kumtumaini Yule anayeitwa kwa jina hilo na kuishi kwa kupatana na viwango vyake vya uadilifu. Yehova ni mwenye fadhili kama nini kwa kutuhakikishia kwamba endapo tutamfikia kwa imani, atakuwa ngome ya kutulinda!

“Mungu Wetu . . . Aweza Kutuokoa”

9. Yehova amefanyaje mengi mbali na kuahidi ulinzi?

9 Yehova amefanya mengi mbali na kuahidi tu ulinzi. Katika nyakati za Biblia, alionyesha kupitia miujiza kwamba anaweza kuwalinda watu wake. Katika historia yote ya Waisraeli, mara nyingi “mkono” wa Yehova wenye uwezo uliwakomesha maadui wenye nguvu. (Kutoka 7:4) Lakini Yehova alitumia pia nguvu zake za kulinda kwa niaba ya watu fulani.

10, 11. Ni mifano gani ya Kibiblia inayoonyesha jinsi Yehova alivyotumia nguvu zake za kulinda kwa niaba ya watu fulani?

10 Vijana watatu Waebrania—Shadraka, Meshaki, na Abednego—walipokataa kuisujudia sanamu ya dhahabu ya Mfalme Nebukadneza, mfalme huyo mwenye hasira alitisha kuwatupa katika tanuru yenye moto mkali sana. “Ni nani Mungu yule atakayewaokoa ninyi na mikono yangu?” akadhihaki Nebukadneza, mtawala mwenye nguvu zaidi duniani. (Danieli 3:15) Vijana hao watatu walijua kwa hakika kwamba Mungu wao alikuwa na nguvu za kuwalinda, lakini hawakutarajia kwamba angewalinda. Kwa hiyo, walijibu hivi: “Kama ni hivyo, Mungu wetu tunayemtumikia aweza kutuokoa.” (Danieli 3:17) Kwa kweli, tanuru hiyo ijapotiwa moto mara saba kuliko ilivyo kawaida, haikuwa kitu kwa Mungu wao mwenye nguvu zote. Aliwalinda, na mfalme huyo alilazimika kukiri hivi: “Hakuna Mungu mwingine awezaye kuokoa namna hii.”—Danieli 3:29.

11 Yehova alionyesha pia nguvu zake kuu za kulinda alipohamisha uhai wa Mwanaye mzaliwa-pekee hadi kwenye tumbo la uzazi la bikira Myahudi Maria. Malaika alimwambia Maria kwamba ‘angechukua mimba katika tumbo [lake] la uzazi na kuzaa mwana.’ Malaika huyo alieleza hivi: “Roho takatifu itakuja juu yako, na nguvu ya Aliye Juu Zaidi Sana itakufunika kivuli.” (Luka 1:31, 35) Yaonekana kwamba Mwana wa Mungu angeweza kushambuliwa kwa urahisi sana pindi hiyo. Je, dhambi na kutokamilika kwa mama yake wa kibinadamu kungechafua kiini-tete hicho? Je, Shetani angeweza kumjeruhi au kumwua Mwana huyo kabla hajazaliwa? Haiwezekani! Kwa kweli Yehova alimlinda Maria tangu mimba ilipotungwa na kuendelea ili kitu chochote—iwe ni kutokamilika, hatari yoyote, mwanadamu yeyote mwenye nia ya kuua, wala roho yeyote mwovu asiweze kuharibu kiini-tete hicho. Yehova aliendelea kumlinda Yesu alipokuwa kijana. (Mathayo 2:1-15) Mwana mpendwa wa Mungu hangeweza kushambuliwa hadi wakati uliowekwa na Mungu.

12. Kwa nini Yehova aliwalinda kimuujiza watu fulani katika nyakati za Biblia?

12 Kwa nini Yehova aliwalinda watu fulani kimuujiza? Katika visa vingi, Yehova aliwalinda watu fulani akiwa na kusudi la kulinda jambo muhimu zaidi: kutimia kwa kusudi lake. Kwa kielelezo, kuokoka kwa mtoto mchanga Yesu kulikuwa muhimu katika utimizo wa kusudi la Mungu, ambalo litafaidi wanadamu wote hatimaye. Masimulizi ya maonyesho hayo ya nguvu za kulinda ni sehemu ya Maandiko yaliyopuliziwa, ambayo “yaliandikwa kwa kufunzwa kwetu, ili kupitia uvumilivu wetu na kupitia faraja kutokana na Maandiko tupate kuwa na tumaini.” (Waroma 15:4) Naam, mifano hiyo inaimarisha imani yetu katika Mungu wetu mwenye nguvu zote. Lakini tunaweza kutarajia kupata ulinzi gani kutoka kwa Mungu leo?

Ahadi ya Kupata Ulinzi wa Mungu Haimaanishi Nini?

13. Je, Yehova ana wajibu wa kutuokoa kimuujiza? Eleza.

13 Ahadi ya kupata ulinzi wa Mungu haimaanishi kwamba Yehova ana wajibu wa kutuokoa kimuujiza. La, Mungu wetu hajaahidi kwamba tutaishi bila matatizo katika mfumo huu wa kale. Watumishi wengi waaminifu wa Yehova wanakumbwa na taabu nyingi sana, kutia ndani umaskini, vita, magonjwa, na kifo. Yesu aliwaambia wanafunzi wake waziwazi kwamba huenda baadhi yao wakauawa kwa sababu ya imani yao. Ndiyo sababu Yesu alikazia uhitaji wa kuvumilia hadi mwisho. (Mathayo 24:9, 13) Ikiwa Yehova angetumia nguvu zake kuokoa watu kimuujiza kila wakati, yamkini Shetani angekuwa na sababu ya kumdhihaki Yehova na kutilia shaka unyofu wetu wa kumtumikia Mungu.—Ayubu 1:9, 10.

14. Ni mifano gani inayoonyesha kwamba sikuzote Yehova hawalindi watumishi wake wote kwa njia ileile?

14 Hata katika nyakati za Biblia, Yehova hakutumia nguvu zake za kulinda ili kuwakinga watumishi wake wote na kifo cha mapema. Kwa mfano, Herode alimwua mtume Yakobo kwa upanga yapata mwaka wa 44 W.K.; lakini, muda mfupi baadaye, Petro alikombolewa “kutoka kwenye mkono wa Herode.” (Matendo 12:1-11) Na Yohana, ndugu ya Yakobo, aliishi kwa muda mrefu kuliko Petro na Yakobo. Ni wazi kwamba hatuwezi kumtarajia Mungu wetu awalinde watumishi wake wote kwa njia ileile. Isitoshe, “wakati na tukio lisilotazamiwa” hutupata sote. (Mhubiri 9:11, NW) Basi, Yehova anatulindaje leo?

Yehova Anatulinda Kimwili

15, 16. (a) Kuna uthibitisho gani kwamba Yehova amewalinda kimwili waabudu wake wakiwa kikundi? (b) Kwa nini tunaweza kuwa na hakika kwamba Yehova atawalinda watumishi wake sasa na wakati wa ile “dhiki kubwa”?

15 Kwanza, fikiria kuhusu ulinzi wa kimwili. Tukiwa waabudu wa Yehova, tunaweza kutarajia kulindwa kimwili tukiwa kikundi. La sivyo, tungeshambuliwa kwa urahisi na Shetani. Hebu fikiria jambo hili: Shetani, “mtawala wa ulimwengu huu,” angependa sana kukomesha ibada ya kweli. (Yohana 12:31; Ufunuo 12:17) Baadhi ya serikali zenye nguvu sana duniani zimepiga marufuku kazi yetu ya kuhubiri na kujaribu kutuangamiza kabisa. Hata hivyo, watu wa Yehova wamedumu wakiwa imara na wameendelea kuhubiri bila kuacha! Kwa nini mataifa yenye nguvu yameshindwa kukomesha utendaji wa kikundi hiki kidogo cha Wakristo kinachoonekana kuwa bila ulinzi? Kwa sababu Yehova ametufunika kwa mbawa zake za mfano zenye nguvu!—Zaburi 17:7, 8.

16 Je, atatulinda kimwili wakati wa ile “dhiki kubwa” inayokuja? Hatuhitaji kuogopa hukumu ya Mungu. Kwa sababu “Yehova ajua jinsi ya kukomboa watu wenye ujitoaji-kimungu kutoka katika jaribu, bali kuweka akiba watu wasio waadilifu kwa ajili ya siku ya hukumu ili kukatiliwa mbali.” (Ufunuo 7:14; 2 Petro 2:9) Kwa sasa, tunaweza kuwa na hakika kabisa kuhusu mambo mawili. Kwanza, Yehova hataruhusu kamwe watumishi wake waaminifu waangamizwe kabisa duniani. Pili, atawapa wale wanaobaki waaminifu zawadi ya kuishi milele katika ulimwengu wake mpya wa uadilifu—hata kama itambidi awafufue. Kwa wale wanaokufa, hakuna mahali pengine salama pa kuwa isipokuwa katika kumbukumbu ya Mungu.—Yohana 5:28, 29.

17. Yehova anatulindaje kupitia Neno lake?

17 Hata sasa, Yehova anatulinda kupitia “neno” lake lililo hai, ambalo lina nguvu ya kuponya watu mioyo na kubadili maisha yao. (Waebrania 4:12) Tunapoishi kwa kupatana na kanuni zake, tunaweza kulindwa kutokana na madhara fulani ya kimwili. “Mimi ni BWANA, . . . nikufundishaye ili upate faida,” yasema Isaya 48:17. Bila shaka, kuishi kwa kupatana na Neno la Mungu kunaweza kuboresha afya yetu na kurefusha maisha yetu. Kwa mfano, tunapotii shauri la Biblia la kujiepusha na uasherati na kujisafisha na kila unajisi, tunaepuka mazoea machafu na yenye kuumiza ambayo yanaharibu kabisa maisha ya watu wengi wasiomtii Mungu. (Matendo 15:29; 2 Wakorintho 7:1) Tunashukuru kama nini kwamba tunalindwa na Neno la Mungu!

Yehova Anatulinda Kiroho

18. Yehova anatulindaje kiroho?

18 Jambo muhimu zaidi ni kwamba Yehova anatulinda kiroho. Mungu wetu mwenye upendo anatulinda kutokana na madhara ya kiroho kwa kutupatia chochote tunachohitaji ili kuvumilia majaribu na kulinda uhusiano wetu naye. Kwa hiyo, Yehova huhifadhi uhai wetu, si kwa miaka michache tu bali kwa umilele. Fikiria baadhi ya maandalizi ya Mungu yanayoweza kutulinda kiroho.

19. Roho ya Yehova inaweza kutusaidiaje kukabiliana na jaribu lolote ambalo huenda likatukumba?

19 Yehova ni “msikiaji wa sala.” (Zaburi 65:2, NW) Tunaweza kupata kitulizo wakati mikazo ya maisha inapotulemea, kwa kumwambia mambo yaliyo mioyoni mwetu. (Wafilipi 4:6, 7) Huenda asiondoe majaribu yetu kimuujiza, lakini anaweza kujibu sala zetu za kutoka moyoni kwa kutupa hekima ya kukabiliana nayo. (Yakobo 1:5, 6) Na zaidi ya hayo, Yehova huwapa roho takatifu wale wanaomwomba. (Luka 11:13) Roho hiyo yenye nguvu inaweza kutusaidia kukabiliana na jaribu au tatizo lolote ambalo huenda likatukumba. Inaweza kututia “nguvu ipitayo iliyo ya kawaida” ili tuvumilie hadi Yehova atakapoondoa matatizo yote yenye kuumiza katika ulimwengu mpya ulio karibu sana.—2 Wakorintho 4:7.

20. Nguvu za Yehova za kulinda zinaweza kuonekanaje kupitia waamini wenzetu?

20 Nyakati nyingine, nguvu za Yehova za kulinda zinaweza kuonekana kupitia waabudu wenzetu. Yehova amewakusanya watu wake katika ‘ushirika [wa ulimwenguni pote] wa ndugu.’ (1 Petro 2:17; Yohana 6:44) Kupitia ushirika huo wenye upendo, tunaona kihalisi jinsi roho takatifu ya Mungu ilivyo na nguvu za kuboresha maisha ya watu. Roho hiyo hukuza matunda ndani yetu, yaani, sifa muhimu zenye kuvutia sana kama vile upendo, fadhili, na wema. (Wagalatia 5:22, 23) Kwa hiyo, tunapokuwa taabani na mwamini mwenzetu anachochewa kutupa shauri lenye kusaidia au kututia moyo inapohitajika, tunaweza kumshukuru Yehova kwa sababu ya ulinzi na utunzaji anaotoa kwa njia hiyo.

21. (a) Yehova anaandaa chakula kipi cha kiroho kwa wakati ufaao kupitia “mtumwa mwaminifu na mwenye busara”? (b) Je, wewe binafsi umefaidika na maandalizi ya Yehova ya kutulinda kiroho?

21 Yehova hutayarisha mambo mengine ya kutulinda: chakula cha kiroho kwa wakati ufaao. Ili kutusaidia kuimarishwa na Neno lake, Yehova amemwagiza “mtumwa mwaminifu na mwenye busara” aandae chakula cha kiroho. Mtumwa huyo mwaminifu hutumia vichapo, kama magazeti ya Mnara wa Mlinzi na Amkeni!, vilevile mikutano, na makusanyiko ili kutupatia ‘chakula kwa wakati ufaao’—chochote tunachohitaji, wakati tunapokihitaji. (Mathayo 24:45) Je, umewahi kusikia jambo fulani kwenye mikutano ya Kikristo—katika maelezo, hotuba, au hata katika sala—ambalo lilikupa nguvu na kitia-moyo ulichohitaji sana? Je, maisha yako yamewahi kuathiriwa na makala fulani hususa iliyochapishwa katika mojawapo ya magazeti yetu? Kumbuka kwamba Yehova hutayarisha maandalizi hayo yote ili kutulinda kiroho.

22. Sikuzote Yehova hutumia nguvu zake kwa njia gani, na kwa nini jambo hilo linatufaidi?

22 Hapana shaka kwamba Yehova ni ngao ‘ya wote wanaomkimbilia.’ (Zaburi 18:30) Tunafahamu kwamba yeye hatumii nguvu zake kutulinda tusipatwe na misiba sasa. Hata hivyo, sikuzote yeye hutumia nguvu zake za kulinda kuhakikisha kwamba kusudi lake linatimizwa. Yeye hufanya hivyo ili kuwafaidi watu wake hatimaye. Tukimkaribia na kudumu katika upendo wake, Yehova atatupatia uhai mkamilifu utakaodumu milele. Tukikumbuka tumaini hilo, kwa kweli tunaweza kuona mateso yoyote yanayotupata katika mfumo huu kuwa ‘ya dakika na mepesi.’—2 Wakorintho 4:17.