Hamia kwenye habari

Hamia kwenye yaliyomo

Sura ya 8

Uwezo wa Kurudisha Hali Nzuri—Yehova ‘Anafanya Vitu Vyote Kuwa Vipya’

Uwezo wa Kurudisha Hali Nzuri—Yehova ‘Anafanya Vitu Vyote Kuwa Vipya’

1, 2. Wanadamu hukumbwa na matatizo gani leo, nayo yanatuathirije?

MTOTO hulia kwa uchungu sana kitu cha kuchezea anachopenda kinapoharibika. Kilio chake huhuzunisha sana! Lakini je, umewahi kuona jinsi mtoto anavyosisimuka mzazi anapokirekebisha kitu hicho na kukirudisha katika hali nzuri? Huenda mzazi akarekebisha kitu hicho kwa urahisi sana. Lakini mtoto anafurahi sana na kupigwa na bumbuazi. Kitu cha kuchezea alichofikiri kimeharibika kabisa kimerudishwa katika hali nzuri!

2 Yehova ambaye ni Baba bora zaidi, ana uwezo wa kurudisha katika hali nzuri vitu na hali mbalimbali ambazo watoto wake wa kidunia huenda wakadhani haziwezi kuboreshwa. Bila shaka, hatumaanishi vitu vya kuchezea. Hatuna budi kupatwa na matatizo makubwa zaidi katika ‘nyakati hizi za hatari zilizo ngumu kushughulika nazo.’ (2 Timotheo 3:1-5) Vitu ambavyo watu wanathamini sana, kama vile makao, mali, kazi, hata afya viko hatarini daima. Huenda pia tukafadhaika kuona mazingira yakiharibiwa na kuona hasara kubwa inayosababishwa na uharibifu huo, au kuona jamii nyingi za viumbe zikitoweka kabisa. Hata hivyo, hakuna jambo linalotuhuzunisha zaidi kuliko kifo cha mpendwa wetu. Uchungu wa kumpoteza mpendwa na kuhisi tukiwa hoi unaweza kutulemea sana.—2 Samweli 18:33.

3. Ni taraja gani lenye kufariji linalotajwa kwenye Matendo 3:21, na Yehova atalitimizaje?

3 Basi inafariji kama nini kujua kwamba Yehova ana uwezo wa kurudisha mambo yote katika hali nzuri! Kama tutakavyoona, Mungu ana uwezo wa kurudisha katika hali nzuri mambo mengi sana yaliyoharibika duniani. Kwa kweli, Biblia inaonyesha kwamba Yehova anakusudia ‘kurudisha mambo yote.’ (Matendo 3:21) Yehova atatumia Ufalme wa Kimesiya, unaotawaliwa na Mwanaye, Yesu Kristo ili kutimiza hayo. Kuna uthibitisho kwamba Ufalme huo ulianza kutawala mbinguni mwaka wa 1914. * (Mathayo 24:3-14) Ni mambo gani yatakayorudishwa katika hali nzuri? Tuchunguze baadhi ya mambo matukufu ambayo Yehova amenuia kurudisha katika hali nzuri. Tunaweza kuona na kufurahia mojawapo ya mambo hayo hivi sasa. Mambo mengineyo yatarudishwa kikamili wakati ujao.

Kurudishwa kwa Ibada Safi

4, 5. Ni nini kilichowapata watu wa Mungu mwaka wa 607 K.W.K., na Yehova aliwaahidi nini?

4 Jambo moja ambalo Yehova tayari amerudisha sasa ni ibada safi. Ili kufahamu jambo hilo, tuchunguze kifupi historia ya ufalme wa Yuda. Uchunguzi huo wenye kusisimua utatusaidia kuelewa jinsi ambavyo Yehova amekuwa akitumia uwezo wake wa kurudisha mambo katika hali nzuri.—Waroma 15:4.

5 Hebu wazia jinsi Wayahudi waaminifu walivyohisi mwaka wa 607 K.W.K. wakati jiji la Yerusalemu lilipoharibiwa. Jiji lao walilopenda liliharibiwa, na kuta zake zikabomolewa. Jambo la kusikitisha hata zaidi ni kwamba hekalu tukufu lililojengwa na Solomoni, kitovu pekee cha ibada safi ya Yehova duniani kote, liliharibiwa kabisa. (Zaburi 79:1) Wale walionusurika walipelekwa uhamishoni Babiloni. Waliacha nchi yao ikiwa makao ya wanyama wa mwitu tu. (Yeremia 9:11) Kwa wanadamu, ilionekana ni kana kwamba hakukuwa na tumaini tena. (Zaburi 137:1) Lakini Yehova, aliyekuwa ametabiri hapo kale kuhusu uharibifu huo, aliwaahidi kwamba angewarudisha nchini mwao na kurudisha ibada safi.

6-8. (a) Manabii Waebrania waliandika tena na tena kuhusu nini, na unabii huo mbalimbali ulitimizwaje kwa mara ya kwanza? (b) Katika nyakati za kisasa, unabii mbalimbali wa kurudishwa umetimizwaje kuhusiana na watu wa Mungu?

6 Kwa kweli, manabii Waebrania waliandika tena na tena kuhusu kurudishwa huko. * Kupitia manabii hao, Yehova aliahidi kwamba angewarudisha katika nchi yenye rutuba, na kuwalinda dhidi ya maadui na wanyama wakali. Alieleza kuwa nchi yao iliyofanywa upya ingekuwa kama paradiso! (Isaya 65:25; Ezekieli 34:25; 36:35) Zaidi ya yote, ibada safi ingeanzishwa tena, na hekalu lingejengwa upya. (Mika 4:1-5) Unabii huo mbalimbali uliwapa Wayahudi hao waliohamishwa tumaini, na uliwasaidia kuvumilia kwa miaka 70 walipokuwa uhamishoni huko Babiloni.

7 Hatimaye, wakati wa kurudishwa ulifika. Wayahudi walipoachiliwa huru kutoka Babiloni, walirudi Yerusalemu na kujenga upya hekalu la Yehova. (Ezra 1:1, 2) Maadamu walishikamana na ibada safi, Yehova aliwabariki na kufanya nchi yao kuwa na rutuba na ufanisi. Aliwalinda dhidi ya maadui na wanyama wakali ambao walikuwa wamevamia nchi yao kwa miaka mingi. Walishangilia kama nini kuona Yehova akitumia uwezo wake wa kurudisha mambo katika hali nzuri! Lakini mambo hayo yalikuwa utimizo mdogo wa kwanza wa unabii mbalimbali wa kurudishwa. Utimizo mkubwa ungetukia “katika siku za mwisho,” katika siku zetu, wakati ambapo Mrithi aliyeahidiwa tangu kale wa Mfalme Daudi angetawazwa.—Isaya 2:2-4; 9:6, 7.

8 Punde tu baada ya Yesu kutawazwa katika Ufalme wa mbinguni mwaka wa 1914, alianza kushughulikia mahitaji ya kiroho ya watu waaminifu wa Mungu duniani. Kama vile mshindi Mwajemi aitwaye Koreshi alivyowaachilia huru mabaki ya Wayahudi kutoka Babiloni mwaka wa 537 K.W.K., Yesu aliweka huru mabaki ya Wayahudi wa kiroho, yaani, wafuasi wake, kutoka kwa uvutano wa Babiloni la kisasa, milki ya ulimwenguni pote ya dini za uwongo. (Waroma 2:29; Ufunuo 18:1-5) Tangu mwaka wa 1919 na kuendelea, ibada safi imerudishwa mahali pafaapo katika maisha ya Wakristo wa kweli. (Malaki 3:1-5) Tangu hapo, watu wa Yehova wamekuwa wakimwabudu katika hekalu la kiroho lililosafishwa, yaani, mpango wa Mungu wa ibada safi. Kwa nini jambo hilo ni muhimu kwetu leo?

Kurudishwa kwa Ibada Safi Ni Muhimu Sana

9. Baada ya mitume kufa, makanisa ya Jumuiya ya Wakristo yaliathirije ibada ya Mungu, lakini Yehova amechukua hatua gani wakati wetu?

9 Fikiria matukio ya kihistoria. Wakristo walioishi katika karne ya kwanza walibarikiwa sana kiroho. Lakini Yesu na mitume walitabiri kwamba ibada ya kweli ingechafuliwa na kutokomea. (Mathayo 13:24-30; Matendo 20:29, 30) Jumuiya ya Wakristo ilitokea baada ya mitume kufa. Makasisi wake walifuata mafundisho na mazoea ya kipagani. Waliwazuia watu wasiwe na uhusiano na Mungu kwa sababu walifundisha fundisho la Utatu lisiloeleweka, na waliwafundisha watu kuungama mbele ya makasisi na kusali kwa Maria na “watakatifu” mbalimbali badala ya kusali kwa Yehova. Sasa, Yehova amechukua hatua gani baada ya watu kuacha ibada safi kwa miaka mingi? Katika ulimwengu wa leo uliojaa mafundisho ya uwongo ya dini na mazoea yake maovu, Yehova amechukua hatua ya kurudisha ibada safi! Si kutilia chumvi kusema kwamba kurudishwa kwa ibada safi ni mojawapo ya matukio muhimu katika nyakati za kisasa.

10, 11. (a) Paradiso ya kiroho inahusisha mambo gani mawili muhimu, na yanakuhusuje? (b) Yehova amekusanya watu wa aina gani katika paradiso ya kiroho, nao watakuwa na pendeleo la kuona nini?

10 Basi Wakristo wa kweli leo wanafurahia paradiso ya kiroho. Paradiso hiyo inahusisha nini? Inahusisha hasa mambo mawili muhimu. Jambo la kwanza ni ibada safi ya Mungu wa kweli, Yehova. Ametubariki kwa kutupatia ibada isiyo na upotovu wala uwongo. Ametuandalia chakula cha kiroho. Hilo hutusaidia tujifunze kuhusu Baba yetu wa mbinguni, tumpendeze, na tumkaribie. (Yohana 4:24) Jambo la pili katika paradiso ya kiroho linahusu watu. Kama Isaya alivyotabiri, “katika siku za mwisho,” Yehova amewafundisha waabudu wake njia za amani. Amekomesha vita miongoni mwetu. Licha ya hali yetu ya kutokamilika, yeye hutusaidia kuvaa “utu mpya.” Anabariki jitihada zetu kwa kutupatia roho yake takatifu, ambayo inatokeza matunda bora sana maishani mwetu. (Waefeso 4:22-24; Wagalatia 5:22, 23) Unapotenda kupatana na roho ya Mungu, unakuwa kwelikweli sehemu ya paradiso ya kiroho.

11 Yehova amekusanya watu anaowapenda katika paradiso hiyo ya kiroho, yaani, watu wanaompenda, wanaopenda amani, na ‘wanaona uhitaji wao wa kiroho.’ (Mathayo 5:3) Watu hao watakuwa na pendeleo la pekee la kuona wanadamu na dunia nzima ikirudishwa katika hali nzuri ajabu.

“Tazama! Mimi Ninafanya Vitu Vyote Kuwa Vipya”

12, 13. (a) Kwa nini kutakuwa na utimizo mwingine wa unabii wa kurudisha hali nzuri? (b) Katika Edeni, Yehova alisema kusudi lake ni nini kwa dunia, na kwa nini hilo linatupatia tumaini la wakati ujao?

12 Yaonekana kwamba unabii mbalimbali wa kurudisha haurejezei tu kurudishwa kwa ibada safi. Kwa mfano, Isaya alitabiri kuhusu wakati ambapo wagonjwa, walemavu, vipofu, na viziwi wataponywa na hata kifo kitamezwa milele. (Isaya 25:8; 35:1-7) Ahadi hizo hazikutimizwa kihalisi katika Israeli la kale. Na ijapokuwa tumeona ahadi hizo zikitimizwa kwa njia ya kiroho nyakati zetu, kuna msingi thabiti wa kuamini kwamba ahadi hizo zitatimizwa kihalisi na kikamili wakati ujao.

13 Katika Edeni, Yehova alitaja waziwazi kusudi lake kwa dunia: Ilipasa kukaliwa na familia ya wanadamu wenye furaha, afya na umoja. Mwanamume na mwanamke walipaswa kutunza dunia na viumbe wake wote, na kufanya dunia yote iwe paradiso. (Mwanzo 1:28) Leo, hali ni tofauti kabisa. Hata hivyo, tunaweza kuwa na hakika kwamba makusudi ya Yehova hayawezi kuzuiwa kamwe. (Isaya 55:10, 11) Yesu, ambaye ni Mfalme wa Kimesiya aliyeteuliwa na Yehova, atafanya dunia yote kuwa Paradiso.—Luka 23:43.

14, 15. (a) Yehova ‘atafanyaje vitu vyote viwe vipya’? (b) Maisha yatakuwaje katika Paradiso, na ni jambo gani linalokuvutia zaidi?

14 Hebu wazia dunia yote ikiwa Paradiso! Yehova anasema hivi kuhusu wakati huo: “Tazama! Mimi ninafanya vitu vyote kuwa vipya.” (Ufunuo 21:5) Fikiria hali itakavyokuwa. Baada ya Yehova kuharibu mfumo huu mwovu wa kale kwa kutumia nguvu zake za kuangamiza, “mbingu mpya na dunia mpya” zitabaki. Hilo lamaanisha kwamba serikali mpya ikiwa mbinguni, itatawala jamii mpya ya kidunia ya wanadamu wanaompenda Yehova na kufanya mapenzi yake. (2 Petro 3:13) Shetani pamoja na mashetani wake, watafungwa ili wasiweze kutenda. (Ufunuo 20:3) Baada ya maelfu ya miaka kupita, kwa mara ya kwanza kabisa wanadamu hawataathiriwa tena na uvutano wake wenye kupotosha, wa chuki, na wenye kuumiza. Hapana shaka kwamba wanadamu watapata faraja isiyo na kifani.

15 Hatimaye, tutaweza kutunza dunia hii maridadi kama ilivyokusudiwa mwanzoni. Dunia ina uwezo wa kujisafisha yenyewe. Maziwa na mito michafu inaweza kujisafisha yenyewe isipoendelea kuchafuliwa; sehemu zilizoharibiwa na vita zinaweza kuwa nzuri endapo vita vitakoma. Itafurahisha kama nini kufanya kazi kwa kupatana na maumbile ya dunia, na kuifanya iwe bustani maridadi, yaani, Edeni ya duniani pote yenye viumbe na mimea ya kila namna! Badala ya kuangamiza wanyama na mimea mbalimbali, mwanadamu ataishi kwa amani na uumbaji wote. Hata watoto hawataogopa wanyama wa mwitu.—Isaya 9:6, 7; 11:1-9.

16. Katika Paradiso, watu wote waaminifu watarudishwa katika hali gani?

16 Tutafurahi pia kurudishiwa afya njema. Baada ya Har–Magedoni, waokokaji wataona maponyo ya kimuujiza ulimwenguni pote. Yesu atatumia nguvu alizopewa na Mungu kuwaponya vipofu, viziwi, walemavu na walio wagonjwa kama alivyofanya alipokuwa duniani. (Mathayo 15:30) Watu wazee watafurahi kuwa tena na nguvu, afya, na juhudi za ujanani. (Ayubu 33:25) Makunyanzi yatatoweka, viungo vitanyooka, na misuli itakuwa na nguvu tena. Wanadamu wote waaminifu wataona madhara ya dhambi na kutokamilika yakididimia hatua kwa hatua, na hatimaye kutokomea. Tutamshukuru Yehova Mungu kama nini kwa sababu ya nguvu zake za kustaajabisha za kufanya mambo yote kuwa mapya! Sasa tukazie fikira jambo moja lenye kuchangamsha litakalotukia wakati huo wenye kusisimua wa kufanya mambo kuwa mapya.

Kuwafufua Wafu

17, 18. (a) Kwa nini Yesu aliwashutumu Masadukayo? (b) Ni tukio gani lililomfanya Eliya amwombe Yehova amfufue mfu?

17 Katika karne ya kwanza W.K., viongozi fulani wa kidini, wanaoitwa Masadukayo, hawakuamini ufufuo. Yesu aliwashutumu hivi: “Mwakosea, kwa sababu hamjui wala Maandiko wala nguvu ya Mungu.” (Mathayo 22:29) Naam, Maandiko yanafunua kwamba Yehova ana nguvu za kufufua. Jinsi gani?

18 Hebu wazia jambo lililotukia siku za Eliya. Mjane mmoja alikuwa amebeba mwili wa mwanaye pekee. Mvulana huyo alikuwa mfu. Haikosi jambo hilo lilimshtua nabii Eliya, aliyekuwa ameishi katika nyumba ya mjane huyo kwa muda fulani. Mapema, alimwokoa mtoto huyo asife njaa. Yaelekea Eliya alimpenda sana mvulana huyo. Mamaye alihuzunika sana. Mvulana huyo pekee ndiye aliyemfanya amkumbuke mume wake aliyekuwa amekufa. Huenda alitumaini kwamba mwanaye angemtunza akizeeka. Mjane huyo aliyefadhaika alidhani kwamba labda alikuwa akiadhibiwa kwa sababu ya dhambi fulani aliyotenda zamani. Eliya hakuweza kuvumilia msiba huo wenye kusikitisha sana. Alitwaa huyo mfu kwa upole kutoka katika kifua cha mamaye, akampeleka katika chumba chake orofani, kisha akamwomba Yehova Mungu arudishe nafsi au uhai, wa mtoto huyo.—1 Wafalme 17:8-21.

19, 20. (a) Abrahamu alionyeshaje imani kwamba Yehova anaweza kufufua, na imani hiyo ilitegemea nini? (b) Yehova alimthawabishaje Eliya kwa sababu ya imani yake?

19 Eliya hakuwa mtu wa kwanza kuamini ufufuo. Miaka mingi mapema, Abrahamu aliamini kwamba Yehova ana uwezo wa kufufua. Na alikuwa na sababu nzuri ya kuamini hivyo. Abrahamu alipokuwa na umri wa miaka 100 na Sara miaka 90, Yehova alirudisha uwezo wao wa kuzaa, na Sara akamzaa mwana kimuujiza. (Mwanzo 17:17; 21:2, 3) Baadaye, kijana huyo alipokuwa mtu mzima, Yehova alimwamuru Abrahamu amtoe kuwa dhabihu. Abrahamu alikuwa na imani, alitambua kwamba Yehova angeweza kumfufua Isaka mwanaye mpendwa. (Waebrania 11:17-19) Yaonekana imani hiyo thabiti ndiyo iliyomfanya Abrahamu, kabla ya kukwea mlimani kumtoa mwanaye, awahakikishie watumishi wake kwamba yeye na Isaka wangerudi pamoja.—Mwanzo 22:5.

“Tazama, mwanao yu hai”!

20 Yehova aliingilia na Isaka hakuuawa, hivyo ufufuo haukuhitajiwa wakati huo. Hata hivyo, katika kisa cha Eliya, mwana wa mjane tayari alikuwa amekufa—lakini si kwa muda mrefu. Yehova alimthawabisha nabii huyo mwenye imani kwa kumfufua mwana huyo! Kisha Eliya akamrudisha mvulana huyo kwa mamaye, akanena maneno haya yasiyoweza kusahaulika: “Tazama, mwanao yu hai”!—1 Wafalme 17:22-24.

21, 22. (a) Ufufuo mbalimbali unaosimuliwa katika Maandiko ulikuwa na kusudi gani? (b) Ni watu wangapi watakaofufuliwa katika Paradiso, na ni nani atakayewafufua?

21 Hivyo basi, kwa mara ya kwanza kabisa katika Biblia, twaona Yehova akitumia uwezo wake wa kuwafufua wanadamu. Baadaye, Yehova pia aliwapa Elisha, Yesu, Paulo, na Petro uwezo wa kufufua wafu. Bila shaka, wale waliofufuliwa walikufa hatimaye. Hata hivyo, matukio hayo ya Biblia yanatuonyesha mambo mazuri yatakayotukia wakati ujao.

22 Katika Paradiso, Yesu atakuwa “ufufuo na uhai.” (Yohana 11:25) Atafufua mamilioni ya wafu, na kuwapa fursa ya kuishi milele katika Paradiso duniani. (Yohana 5:28, 29) Hebu wazia jinsi marafiki wapendwa na watu wa jamaa waliotenganishwa na kifo watakavyokumbatiana kwa shangwe kubwa ajabu! Wanadamu wote watamsifu Yehova kwa ajili ya uwezo wake wa kufufua.

23. Ni tukio gani lililokuwa uthibitisho mkuu zaidi wa uwezo wa Yehova, na hilo linatuhakikishia jinsi gani tumaini letu la wakati ujao?

23 Yehova ametuhakikishia kabisa kwamba tumaini hilo ni hakika. Yehova alithibitisha uwezo wake kwa njia kuu kupita zote alipomfufua Mwanaye, Yesu, akiwa kiumbe wa roho mwenye uwezo, na kumpa cheo cha pili katika ulimwengu mzima. Mamia ya watu walimwona Yesu aliyefufuliwa. (1 Wakorintho 15:5, 6) Ushahidi huo unatosha kuwasadikisha wale wanaotilia shaka jambo hilo. Yehova ana uwezo wa kufufua.

24. Kwa nini tunaweza kuwa na uhakika kwamba Yehova atafufua wafu, na sote tunaweza kuthamini tumaini gani?

24 Si kwamba tu Yehova ana uwezo wa kufufua wafu bali pia ana tamaa ya kufanya hivyo. Mwanamume mwaminifu Yobu alipuliziwa kusema kwamba kwa kweli Yehova ana tamaa ya kuwafufua wafu. (Ayubu 14:15) Je, wewe huvutiwa na Mungu wetu, ambaye anatamani kutumia kwa upendo uwezo wake wa kufufua? Kumbuka kwamba ufufuo ni sehemu moja tu ya kazi kubwa ambayo Yehova atafanya wakati ujao ya kufanya mambo kuwa mapya. Kadiri unavyomkaribia zaidi, endelea kuthamini tumaini la pekee sana la kwamba huenda ukawapo Yehova ‘atakapofanya vitu vyote kuwa vipya.’—Ufunuo 21:5.

^ fu. 3 “Nyakati za kurudishwa kwa mambo yote” zilianza wakati Ufalme wa Kimesiya uliposimamishwa, mrithi wa Mfalme Daudi aliyekuwa mwaminifu alipowekwa kuwa mtawala wa Ufalme huo. Yehova alikuwa amemwahidi Daudi kwamba mrithi wake angetawala milele. (Zaburi 89:35-37) Lakini baada ya Babiloni kuharibu Yerusalemu mnamo mwaka wa 607 K.W.K., kiti cha enzi cha Mungu hakikukaliwa na mwanadamu mwingine yeyote aliye mzao wa Daudi. Yesu, aliyezaliwa duniani akiwa mrithi wa Daudi, akawa Mfalme aliyeahidiwa tangu kale alipotawazwa mbinguni.

^ fu. 6 Kwa mfano, Musa, Isaya, Yeremia, Ezekieli, Hosea, Yoeli, Amosi, Obadia, Mika, na Sefania walikazia jambo hilo.