Hamia kwenye habari

Hamia kwenye yaliyomo

Sura ya 11

“Njia Zake Zote Ni Haki”

“Njia Zake Zote Ni Haki”

1, 2. (a) Yosefu alikumbwa na ukosefu upi mkubwa wa haki? (b) Yehova alikomeshaje ukosefu huo wa haki?

MWANAMUME fulani kijana mwenye sura nzuri alitendewa isivyo haki kabisa, hakuwa amefanya uhalifu wowote, lakini alitiwa gerezani kwa mashtaka ya uwongo ya kujaribu kumbaka mwanamke. Alitendewa isivyo haki pindi nyingine pia. Miaka mingi mapema, kijana huyo aitwaye Yosefu, akiwa na umri wa miaka 17, alisalitiwa na ndugu zake ambao nusura wamwue. Aliuzwa utumwani katika nchi ya kigeni. Akiwa huko alikataa kutongozwa na mke wa bwana wake. Mwanamke huyo alimsingizia Yosefu kwa mashtaka ya uwongo, ndipo Yosefu akatiwa gerezani. Kwa kusikitisha, ilionekana kwamba hakukuwa na mtu yeyote wa kumtetea Yosefu.

Yosefu aliteseka isivyo haki “gerezani”

2 Hata hivyo, Mungu ambaye ‘anapenda uadilifu na haki’ alikuwa akitazama. (Zaburi 33:5, BHN) Yehova alichukua hatua ya kukomesha ukosefu huo wa haki, aliingilia mambo na mwishowe Yosefu akaachiliwa. Isitoshe, Yosefu—aliyekuwa ametiwa “gerezani”—hatimaye alipewa cheo cha juu sana na heshima ya pekee. (Mwanzo 40:15; 41:41-43; Zaburi 105:17, 18) Mwishowe, mashtaka hayo ya uwongo yalifutiliwa mbali na Yosefu akatumia cheo chake cha juu kuendeleza kusudi la Mungu.—Mwanzo 45:5-8.

3. Kwa nini haishangazi kwamba sote hutamani kutendewa kwa haki?

3 Simulizi hilo linatugusa moyo, sivyo? Sote tumepata kutendewa isivyo haki au kuona mwingine akitendewa isivyo haki. Bila shaka, sote hutamani kutendewa kwa haki, bila uonevu. Hilo halishangazi, kwa kuwa Yehova alituumba tukiwa na sifa kama zake, na haki ni mojawapo ya sifa zake kuu. (Mwanzo 1:27) Ili kumjua Yehova vyema, tunahitaji kuelewa sifa yake ya haki. Ndipo tutakapothamini hata zaidi matendo yake ya ajabu na kuchochewa kumkaribia zaidi.

Haki Ni Nini?

4. Kwa kawaida wanadamu huelewaje haki?

4 Kwa kawaida, wanadamu huelewa haki kuwa utekelezaji wa sheria bila upendeleo. Kitabu Right and Reason—Ethics in Theory and Practice chasema kwamba ‘haki inahusiana na sheria, wajibu, haki za watu, na madaraka, nayo hutekelezwa bila kupendelea na kwa yule anayestahili.’ Hata hivyo, Yehova hatekelezi haki kwa kushikilia tu sheria bila kujali ili kutimiza tu wajibu.

5, 6. (a) Maneno ya lugha ya awali yanayotafsiriwa “haki” yanamaanisha nini? (b) Mungu ni mwenye haki katika maana gani?

5 Tunaweza kuelewa kwa undani haki ya Yehova kwa kuchunguza maneno ya lugha za awali yaliyotumiwa katika Biblia. Katika Maandiko ya Kiebrania, maneno matatu muhimu yanatumiwa. Neno ambalo mara nyingi hutafsiriwa “haki” laweza pia kumaanisha “yaliyo sawa.” (Mwanzo 18:25, BHN) Maneno mawili yanayosalia hutafsiriwa kwa kawaida kuwa “uadilifu.” Katika Maandiko ya Kigiriki ya Kikristo, neno linalotafsiriwa “uadilifu” linafafanuliwa kuwa “sifa ya kuwa sawa au mwenye haki.” Hivyo basi, hakuna tofauti kati ya uadilifu na haki.—Amosi 5:24, BHN.

6 Basi, Biblia inaposema kwamba Mungu ni mwenye haki, inamaanisha kwamba sikuzote yeye hutenda yaliyo sawa bila kupendelea, na bila ubaguzi. (Waroma 2:11) Kwa kweli, Mungu hawezi kamwe kutenda isivyo haki. Elihu aliyekuwa mwaminifu alisema hivi: “Mungu asidhaniwe kutenda udhalimu; wala Mwenyezi kufanya uovu.” (Ayubu 34:10) Ni kweli kwamba Yehova hawezi kamwe “kutenda udhalimu.” Kwa nini? Kwa sababu mbili muhimu.

7, 8. (a) Kwa nini Yehova hawezi kutenda isivyo haki? (b) Ni nini kinachomchochea Yehova atende kwa uadilifu, au kwa haki?

7 Kwanza, yeye ni mtakatifu. Kama tulivyoona kwenye Sura ya 3, Yehova ni mtakatifu na mwadilifu kabisa. Kwa hiyo, hawezi kutenda uovu au kutenda isivyo haki. Fikiria maana yake. Tunasadiki kabisa kwamba Baba yetu wa mbinguni hawezi kamwe kuwatesa watoto wake kwa sababu yeye ni mtakatifu. Yesu alisadiki vivyo hivyo. Usiku wa mwisho wa maisha yake duniani, alisali hivi: “Baba Mtakatifu, walinde [wanafunzi] kwa sababu ya jina lako mwenyewe.” (Yohana 17:11) Katika Maandiko, usemi “Baba Mtakatifu” humhusu Yehova peke yake. Usemi huo unafaa kwa sababu hakuna baba yeyote wa kibinadamu aliye mtakatifu kama Yehova. Yesu aliamini kabisa kwamba wanafunzi wake wangelindwa na Baba yake, ambaye ni mtakatifu na asiye na dhambi yoyote.—Mathayo 23:9.

8 Pili, upendo usio wa ubinafsi ni sifa kuu ya utu wa Mungu. Upendo huo humchochea kuwatendea wengine kwa uadilifu au haki. Lakini ukosefu mwingi wa haki—kutia ndani ukabila, ubaguzi wa rangi, na kupendelea—mara nyingi husababishwa na pupa na ubinafsi, mambo ambayo ni kinyume cha upendo. Biblia inatuhakikishia hivi kumhusu Mungu huyo mwenye upendo: “BWANA ndiye mwenye haki, apenda matendo ya haki.” (Zaburi 11:7) Yehova asema hivi kujihusu: “Mimi, BWANA, naipenda hukumu ya haki.” (Isaya 61:8) Bila shaka inatia moyo kujua kwamba Mungu wetu anapenda kutenda yaliyo sawa, au yaliyo haki.—Yeremia 9:24.

Rehema na Haki Kamilifu ya Yehova

9-11. (a) Kuna uhusiano gani kati ya haki ya Yehova na rehema yake? (b)Yehova anaonyeshaje haki na rehema anaposhughulika na wanadamu wenye dhambi?

9 Haki ya Yehova, kama sifa nyinginezo za utu wake usio na kifani, ni kamilifu, haijapungukiwa kwa vyovyote. Musa alimtukuza Yehova kwa kuandika hivi: “Yeye Mwamba, kazi yake ni kamilifu; maana, njia zake zote ni haki. Mungu wa uaminifu, asiye na uovu, yeye ndiye mwenye haki na adili.” (Kumbukumbu la Torati 32:3, 4) Yehova hutenda kwa haki kamilifu—yeye si mpole mno wala si mkali mno.

10 Haki ya Yehova inahusiana sana na rehema yake. Zaburi 116:5 yasema: “BWANA ni mwenye neema na haki, naam, Mungu wetu ni mwenye rehema.” Ndiyo, Yehova ni mwenye haki na mwenye rehema. Sifa hizo mbili hazipingani. Haki ya Yehova haiwezi kupita kiasi, kwa hivyo haonyeshi rehema ili kusawazisha haki yake. Badala yake, mara nyingi yeye huonyesha sifa hizo pamoja. Ona mfano ufuatao.

11 Wanadamu wote wamerithi dhambi na hivyo wanastahili kupata mshahara wa dhambi, yaani, kifo. (Waroma 5:12) Lakini Yehova hafurahii watenda-dhambi wakifa. Yeye ni ‘Mungu, aliye tayari kusamehe, mwenye neema, mwenye huruma nyingi.’ (Nehemia 9:17) Hata hivyo, kwa kuwa yeye ni mtakatifu, hawezi kupuuza tu uovu. Basi, angewezaje kuwaonyesha rehema wanadamu ambao wamerithi dhambi? Jibu linapatikana katika mojawapo ya kweli muhimu zinazopatikana katika Neno la Mungu: mpango wa Yehova wa kuwaokoa wanadamu kupitia fidia. Katika Sura ya 14 tutajifunza mengi zaidi kuhusu mpango huo wa upendo. Mpango huo unaonyesha haki na rehema ya pekee sana. Kupitia mpango huo, Yehova anaweza kuwaonyesha watenda-dhambi wanaotubu rehema yenye fadhili huku akidumisha kanuni zake za haki kamilifu.—Waroma 3:21-26.

Haki ya Yehova Inachangamsha Moyo

12, 13. (a) Kwa nini haki ya Yehova inatuvuta kwake? (b) Daudi alifikia mkataa gani kuhusu haki ya Yehova, na hilo linawezaje kututia moyo?

12 Haki ya Yehova si sifa inayochukiza, bali ni sifa ya kupendeza inayotuvuta kwake. Biblia inaeleza waziwazi kwamba haki au uadilifu wa Yehova unaambatana na huruma. Hebu tuchunguze baadhi ya njia za Yehova za haki zinazochangamsha moyo.

13 Haki kamilifu ya Yehova humchochea kuonyesha uaminifu na ushikamanifu kwa watumishi wake. Mtunga-zaburi Daudi alipata kuelewa na kuthamini wonyesho huo wa haki ya Yehova maishani mwake. Daudi alifikia mkataa gani kutokana na mambo yaliyompata na yale aliyojifunza kuhusu njia za Yehova za kufanya mambo? Alitangaza hivi: “BWANA hupenda haki, wala hawaachi watauwa wake. Wao hulindwa milele.” (Zaburi 37:28) Ahadi hiyo inatia moyo kama nini! Mungu wetu hatawaacha kamwe wale walio waaminifu kwake. Kwa hiyo, tunaweza kuwa na hakika kwamba atatutunza kwa upendo na hatatuacha kamwe. Jambo hilo ni hakika kwa sababu yeye ni mwenye haki!—Mithali 2:7, 8.

14. Sheria ambayo Yehova aliwapa Waisraeli inaonyeshaje kwamba anawajali wanaotaabika?

14 Mungu huzingatia mahitaji ya wale wanaotaabika kwa sababu yeye ni mwenye haki. Sheria ambayo Yehova aliwapa Waisraeli inaonyesha kwamba anawajali wanaotaabika. Kwa mfano, Sheria ilitaja mipango ya pekee ya kuhakikisha kwamba mayatima na wajane walitunzwa. (Kumbukumbu la Torati 24:17-21) Huku akitambua magumu ambayo yangekumba familia hizo, Yehova aliwajali akiwa Hakimu na Mlinzi wao, ambaye ‘anamfanyia yatima na mjane hukumu ya haki.’ (Kumbukumbu la Torati 10:18; Zaburi 68:5) Yehova aliwaonya Waisraeli kwamba endapo wangewatesa wanawake na watoto hao wasio na msaidizi, angesikia kilio chao pasina shaka yoyote. Alisema: “Hasira yangu itawaka moto.” (Kutoka 22:22-24) Ijapokuwa hasira si mojawapo ya sifa kuu za Yehova, hasira yake adilifu huwaka anapoona watu wa hali ya chini na wanyonge wakionewa kimakusudi.—Zaburi 103:6.

15, 16. Kuna uthibitisho gani wa pekee unaoonyesha kwamba Yehova hana upendeleo?

15 Yehova pia anatuhakikishia kwamba ‘hapendelei nyuso za watu, wala hakubali rushwa.’ (Kumbukumbu la Torati 10:17) Yehova si kama wanadamu wengi mashuhuri na wenye mamlaka ambao huangalia utajiri au sura ya mtu. Hana ubaguzi wala upendeleo wowote. Fikiria uthibitisho huu wa pekee ambao unaonyesha kwamba Yehova hana upendeleo. Hakuwapa watu wachache tu wenye elimu nafasi ya kuwa waabudu wake wa kweli wenye tumaini la kuishi milele. Badala yake, “katika kila taifa mtu ambaye humhofu na kutenda uadilifu akubalika kwake.” (Matendo 10:34, 35) Watu wote wanaweza kuwa na tumaini hilo zuri ajabu bila kujali wadhifa wao katika jamii, rangi yao, au nchi wanamoishi. Je, huo si uthibitisho bora kabisa wa haki ya kweli?

16 Tunastahili kufikiria na kuheshimu njia nyingine muhimu ambayo Yehova anaonyesha haki yake kamilifu: jinsi anavyoshughulika na wale wanaovunja kanuni zake za uadilifu.

Huwaadhibu Wenye Hatia

17. Eleza kwa nini maovu yaliyo ulimwenguni hayaonyeshi kwamba Yehova hatendi haki.

17 Huenda wengine wakauliza: ‘Kama Yehova hapuuzi uovu, kwa nini ufisadi na ukosefu wa haki unaosababisha kuteseka umeenea ulimwenguni leo?’ Maovu hayo hayaonyeshi kwa vyovyote kwamba Yehova hatendi haki. Ukosefu wa haki uliojaa katika ulimwengu huu mwovu umesababishwa na dhambi ambayo wanadamu wamerithi kutoka kwa Adamu. Ukosefu wa haki umeenea ulimwenguni kwa sababu wanadamu wasiokamilika wameamua kufuata njia zao wenyewe zenye dhambi. Lakini utakomeshwa hivi karibuni.—Kumbukumbu la Torati 32:5.

18, 19. Ni nini kinachoonyesha kwamba Yehova hatavumilia milele wale wanaovunja kimakusudi sheria zake adilifu?

18 Ijapokuwa Yehova huwarehemu kabisa wale wanaomkaribia kwa unyofu, hatavumilia milele hali inayoletea jina lake takatifu lawama. (Zaburi 74:10, 22, 23) Mungu mwenye haki hawezi kudhihakiwa; hawezi kuwalinda wale wanaotenda dhambi kimakusudi wasipate adhabu kali wanayostahili kwa sababu ya mwenendo wao. Yehova ni “Mungu mwingi wa huruma, mwenye fadhili, si mwepesi wa hasira, mwingi wa rehema na kweli; . . . wala si mwenye kumhesabia mtu mwovu kuwa hana hatia kamwe.” (Kutoka 34:6, 7) Kwa kupatana na maneno hayo, nyakati nyingine imembidi Yehova kuwaadhibu wale wanaovunja kimakusudi sheria zake adilifu.

19 Kwa mfano, fikiria jinsi Mungu alivyoshughulika na Israeli la kale. Hata baada ya kumiliki Nchi ya Ahadi, Waisraeli waliasi tena na tena. Yehova hakuwatupilia mbali mara moja licha ya kwamba matendo yao maovu ‘yalimhuzunisha.’ (Zaburi 78:38-41) Badala yake, kwa rehema aliwapa nafasi ya kubadili mwenendo wao. Aliwasihi hivi: “Sikufurahii kufa kwake mtu mwovu; bali aghairi mtu mwovu, na kuiacha njia yake mbaya, akaishi. Ghairini, ghairini, mkaache njia zenu mbaya; mbona mnataka kufa, Enyi nyumba ya Israeli?” (Ezekieli 33:11) Kwa sababu Yehova anathamini sana uhai, alituma manabii wake tena na tena ili Waisraeli waache njia zao mbaya. Lakini wengi wa watu hao wenye mioyo migumu walikataa kusikiliza na kutubu. Mwishowe, Yehova aliwatia mikononi mwa adui zao ili kutetea jina lake takatifu na kile kinachowakilishwa na jina hilo.—Nehemia 9:26-30.

20. (a) Twajifunza nini kumhusu Yehova kutokana na jinsi alivyoshughulika na Waisraeli? (b) Kwa nini simba ni mfano ufaao wa haki ya Yehova?

20 Tunajifunza mambo mengi kumhusu Yehova tunapochunguza jinsi alivyoshughulika na Waisraeli. Tunajifunza kwamba macho yake huona maovu yote nayo humhuzunisha sana. (Mithali 15:3) Pia, inatia moyo sana kujua kwamba yeye hujitahidi kuonyesha rehema inapofaa. Isitoshe, tunajifunza kwamba hatekelezi haki yake haraka-haraka. Kwa sababu ya subira na uvumilivu wa Yehova, watu wengi hufikiri kimakosa kwamba hatawaadhibu kamwe waovu. Lakini maoni hayo si kweli. Tunapofikiria jinsi Mungu alivyoshughulika na Waisraeli, tunajifunza kwamba subira yake ina mipaka. Yehova hutekeleza uadilifu kwa uthabiti. Tofauti na wanadamu, ambao mara nyingi huogopa kutenda haki, yeye hutetea kwa ujasiri yaliyo sawa. Kwa hiyo, simba ambaye anawakilisha haki ya kijasiri, anaonekana karibu na Mungu na kiti chake cha enzi. * (Ezekieli 1:10; Ufunuo 4:7) Kwa hiyo tunaweza kuwa na hakika kwamba atatimiza ahadi yake ya kukomesha ukosefu wa haki duniani. Naam, twaweza kusema hivi kwa ufupi kuhusu hukumu yake: Yehova hutekeleza hukumu yake kwa uthabiti inapohitajika na kwa rehema inapowezekana.—2 Petro 3:9.

Kumkaribia Mungu Mwenye Haki

21. Tunapotafakari jinsi Yehova anavyotekeleza haki yake, tunapaswa kumwonaje, na kwa nini?

21 Tunapotafakari jinsi Yehova anavyotekeleza haki, hatupaswi kumwona kama hakimu mkali asiye na hisia ambaye anapenda tu kuwahukumu watenda-maovu. Badala yake, tunapaswa kumwona kuwa Baba mwenye upendo, aliye thabiti, ambaye huwatunza watoto wake kwa njia bora kabisa. Akiwa Baba mwadilifu au mwenye haki, Yehova ni thabiti kwa mambo yaliyo sawa na vilevile huwaonyesha rehema nyororo watoto wake wa kidunia ambao wanahitaji msaada na msamaha wake.—Zaburi 103:10, 13.

22. Akiongozwa na haki yake, Yehova ametuwezesha kuwa na tumaini gani, na kwa nini anashughulika nasi kwa njia hiyo?

22 Tunashukuru kama nini kwamba haki ya Mungu haimaanishi kuwahukumu tu watenda-maovu! Akiongozwa na haki yake, Yehova ametuwezesha kuwa na tumaini lenye kusisimua sana—kuishi milele na kwa ukamilifu katika ulimwengu ambamo “uadilifu utakaa.” (2 Petro 3:13) Mungu wetu anashughulika nasi kwa njia hiyo kwa sababu haki yake humchochea ajitahidi kuokoa badala ya kuhukumu. Kwa kweli, tunavutiwa kumkaribia Yehova tunapoelewa vyema haki yake! Katika sura zifuatazo, tutachunguza kwa undani zaidi jinsi Yehova anavyoonyesha sifa hiyo yenye kuvutia.

^ fu. 20 Kwa kufaa, Yehova alijilinganisha na simba alipowahukumu Waisraeli wenye kuasi.—Yeremia 25:38; Hosea 5:14.