Hamia kwenye habari

Hamia kwenye yaliyomo

Sura ya 12

“Je, kwa Mungu Kuna Ukosefu wa Haki?”

“Je, kwa Mungu Kuna Ukosefu wa Haki?”

1. Visa vya ukosefu wa haki vinaweza kutufanya tuhisije?

MJANE mmoja mzee aibiwa kwa ujanja pesa zote alizoweka akibani. Mtoto mchanga atupwa na mama yake asiye na huruma. Mwanamume fulani afungwa gerezani isivyo haki kwa shtaka la uhalifu. Unahisije kuhusu visa hivyo? Yaelekea kwamba kila kisa kinakuhuzunisha, na sababu ni wazi. Wanadamu wote wanatambua vyema mambo yaliyo sawa na yaliyo kosa. Tunakasirika tunapoona mtu akitendewa isivyo haki. Tunataka mtu huyo alipwe na mkosaji aadhibiwe. Haki isipotekelezwa, huenda tukajiuliza hivi: ‘Je, Mungu anaona yanayotukia? Mbona hachukui hatua?’

2. Habakuki alihisije kwa sababu ya ukosefu wa haki, na kwa nini Yehova hakumshutumu?

2 Katika historia yote, watumishi waaminifu wa Yehova wameuliza maswali kama hayo. Kwa mfano, nabii Habakuki alisali hivi kwa Mungu: “Kwa nini wanifanya nishuhudie ukosefu huu mbaya wa haki? Kwa nini unaruhusu jeuri, uasi-sheria, uhalifu na ukatili uenee kotekote?” (Habakuki 1:3, Contemporary English Version) Yehova hakumshutumu Habakuki kwa sababu ya kuuliza maswali hayo yaliyo wazi, kwa kuwa Ndiye aliyewaumba wanadamu wakiwa na uwezo wa kuonyesha haki. Naam, Yehova amewapa wanadamu uwezo wa kuonyesha kwa kadiri fulani haki yake kamilifu.

Yehova Anachukia Ukosefu wa Haki

3. Kwa nini yaweza kusemwa kwamba Yehova anajua vyema ukosefu wa haki uliopo?

3 Yehova anajua kwamba kuna ukosefu wa haki. Anaona yanayotukia. Biblia yatuambia hivi kuhusu siku za Noa: “BWANA akaona ya kuwa maovu ya mwanadamu ni makubwa duniani na kwamba kila kusudi analowaza moyoni mwake ni baya tu sikuzote.” (Mwanzo 6:5) Fikiria maana ya maneno hayo. Mara nyingi, sisi hutambua kuna ukosefu wa haki baada ya kusikia visa kadhaa vya ukosefu wa haki au baada ya kutendewa isivyo haki. Kinyume chake, Yehova anaona ukosefu wote wa haki unaotukia ulimwenguni pote. Isitoshe, anaweza kutambua nia ya moyo—mawazo mapotovu yanayowafanya watu watende isivyo haki.—Yeremia 17:10.

4, 5. (a) Biblia inaonyeshaje kwamba Yehova anawajali wanaotendewa isivyo haki? (b) Yehova alitendewaje isivyo haki?

4 Lakini Yehova haangalii tu ukosefu wa haki bila kuchukua hatua. Anawajali wale wanaoteseka kwa sababu ya kutendewa isivyo haki. Watu wake walipoteswa kikatili na mataifa adui, Yehova alihuzunika ‘kwa ajili ya kuugua kwao kwa sababu watu wale waliwaonea na kuwasumbua.’ (Waamuzi 2:18) Huenda umegundua kwamba watu fulani hawana huruma kwa sababu wameona visa vingi sana vya ukosefu wa haki. Lakini Yehova ni tofauti kabisa! Ameona ukosefu wa haki wa kila namna kwa miaka ipatayo 6,000, lakini bado unamchukiza. Isitoshe, Biblia inatuhakikishia kwamba mambo kama vile “ulimi wa uongo,” “mikono imwagayo damu isiyo na hatia,” na “shahidi wa uongo asemaye uongo,” yanamchukiza.—Mithali 6:16-19.

5 Fikiria pia jinsi Yehova alivyowashutumu vikali viongozi wasiofuata haki katika Israeli. Alimpulizia nabii wake kuwaambia hivi: “Nyinyi ndio mnaopaswa kujua mambo ya haki.” Baada ya kueleza waziwazi jinsi walivyotumia vibaya mamlaka yao, Yehova alitabiri mambo yatakayowapata watu hao wafisadi: ‘Watamlilia Mwenyezi-Mungu lakini yeye hatawajibu. Atauficha uso wake wakati huo, kwa sababu wamemtenda mambo maovu.’ (Mika 3:1-4, BHN) Yehova anachukia kabisa ukosefu wa haki kwa sababu yeye pia alitendewa isivyo haki! Kwa maelfu ya miaka, Shetani amekuwa akimlaumu Mungu isivyo haki. (Mithali 27:11) Isitoshe, Yehova aliathiriwa na tendo baya zaidi la ukosefu wa haki, wakati Mwanaye aliuawa kama mhalifu ingawa “hakufanya dhambi.” (1 Petro 2:22; Isaya 53:9) Ni wazi kwamba Yehova hapuuzi wala kutojali mateso ya wale wanaotendewa isivyo haki.

6. Huenda tukahisije tunapotendewa isivyo haki, na kwa nini?

6 Licha ya hayo, tunapoona ukosefu wa haki—au tunapotendewa isivyo haki—kwa kawaida tunasononeka sana. Tumeumbwa kwa mfano wa Mungu, na ukosefu wa haki haupatani hata kidogo na utu wa Yehova. (Mwanzo 1:27) Basi, mbona Yehova anaruhusu ukosefu wa haki?

Suala la Enzi Kuu ya Mungu

7. Eleza jinsi enzi kuu ya Yehova ilivyotiliwa shaka.

7 Jibu la swali hilo linahusiana na suala la enzi kuu. Kama tulivyoona, Muumba ana haki ya kutawala dunia na wote wanaokaa humo. (Zaburi 24:1; Ufunuo 4:11) Hata hivyo, enzi kuu ya Yehova ilitiliwa shaka mapema katika historia ya wanadamu. Ilikuwaje? Yehova alimwamuru mwanadamu wa kwanza, Adamu, asile matunda ya mti fulani uliokuwa katika bustani ya Paradiso alimoishi. Ingekuwaje kama hangetii? Mungu alimwambia “utakufa hakika.” (Mwanzo 2:17) Amri ya Mungu haikumkandamiza Adamu au mkewe, Hawa. Hata hivyo, Shetani alimsadikisha Hawa kwamba Mungu alikuwa akiwawekea vizuizi vinavyopita kiasi. Hawa angepatwa na nini kama angekula kutokana na mti huo? Shetani alimwambia Hawa waziwazi: “Hakika hamtakufa, kwa maana Mungu anajua ya kwamba siku mtakayokula matunda ya mti huo, mtafumbuliwa macho, nanyi mtakuwa kama Mungu, mkijua mema na mabaya.”—Mwanzo 3:1-5.

8. (a) Mambo ambayo Shetani alimwambia Hawa yalidokeza nini? (b) Shetani alidai nini kuhusu enzi kuu ya Mungu?

8 Kwa kusema hivyo, Shetani alidokeza kwamba Yehova alimdanganya Hawa na vilevile alimnyima habari muhimu sana. Kwa tahadhari, Shetani hakupinga kwamba Mungu ndiye mtawala mwenye enzi kuu. Lakini alidai kwamba Mungu hakutawala kwa uadilifu wala hakuwa na haki ya kuwa mwenye enzi kuu. Yaani, alidai kwamba Yehova alikuwa akiwadhulumu raia wake na hakuwa akitawala kwa njia ya uadilifu.

9. (a) Adamu na Hawa walipatwa na nini kwa sababu ya kutotii, na hilo lilizusha maswali gani muhimu? (b) Kwa nini Yehova hakuwaangamiza waasi hao papo hapo?

9 Adamu na Hawa walimwasi Yehova wakala matunda ya mti uliokatazwa. Kwa sababu hawakutii, wangepokea adhabu ya kifo kama Mungu alivyokuwa amesema. Uwongo wa Shetani ulizusha maswali kadhaa muhimu. Je, kweli Yehova ana haki ya kutawala wanadamu, au wanadamu wanapaswa kujitawala? Je, Yehova anatawala kwa njia bora kabisa? Yehova angaliweza kuwaangamiza waasi hao papo hapo kwa kutumia nguvu zake kuu. Lakini masuala yaliyozushwa yalihusu utawala wa Mungu, wala si nguvu zake. Kwa hiyo, kumwangamiza Adamu, Hawa, na Shetani hakungethibitisha kwamba Mungu anatawala kwa uadilifu. Badala yake, huenda utawala wake ungetiliwa shaka hata zaidi. Njia pekee ya kujua iwapo wanadamu wangeweza kujitawala kwa mafanikio bila kumtegemea Mungu, ingekuwa ni kuwapa muda zaidi wa kuthibitisha madai hayo.

10. Historia imefunua nini kuhusu utawala wa wanadamu?

10 Historia imefunua nini? Kwa maelfu ya miaka, watu wamejaribu serikali nyingi mbalimbali, kama vile serikali za kimabavu, demokrasia, ujamaa na ukomunisti. Matokeo ya serikali hizo zote yanatajwa na maneno haya ya Biblia ambayo ni ya kweli: ‘Mtu mmoja anayo mamlaka juu ya mwenziwe kwa hasara yake.’ (Mhubiri 8:9) Kwa kufaa, nabii Yeremia alisema hivi: “Ee, BWANA, najua ya kuwa njia ya mwanadamu haimo katika nafsi yake; kuelekeza hatua zake si katika uwezo wa mwanadamu.”—Yeremia 10:23.

11. Kwa nini Yehova aliruhusu wanadamu wateseke?

11 Tangu mwanzoni, Yehova alijua kwamba wanadamu wangeteseka sana kwa sababu ya kujitegemea au kujitawala. Basi, je, alikosa haki kwa kuruhusu mateso hayo yaendelee? La hasha! Kwa mfano: Tuseme una mtoto anayehitaji kufanyiwa upasuaji ili kutibu ugonjwa hatari sana. Unahuzunika sana kwa sababu unatambua kwamba mtoto wako atateseka kwa kadiri fulani anapofanyiwa upasuaji. Lakini unajua pia kwamba upasuaji utamsaidia mtoto wako kuwa na afya bora baadaye. Vivyo hivyo, Mungu alijua—na hata alitabiri—kwamba utawala wa wanadamu ambao ameruhusu ungesababisha maumivu na mateso kwa kadiri fulani. (Mwanzo 3:16-19) Lakini alijua pia kwamba kitulizo cha kudumu na kinachofaa kingepatikana tu ikiwa angeacha wanadamu wote waone matokeo mabaya ya uasi. Hivyo suala la enzi kuu lingetatuliwa kabisa, kwa umilele wote.

Suala la Uaminifu wa Mwanadamu

12. Kama kisa cha Yobu kinavyoonyesha, Shetani ametoa shtaka gani dhidi ya wanadamu?

12 Kuna jambo jingine linalohusika. Alipodai kwamba Mungu hana haki ya kutawala na hatawali kwa uadilifu, Shetani hakusema tu uwongo kuhusu enzi kuu ya Yehova; alisema pia uwongo kuhusu uaminifu wa watumishi wa Mungu. Kwa mfano, angalia maneno ambayo Shetani alimwambia Yehova kuhusu yule mwanamume mwadilifu, Yobu: “Wewe hukumzingira kwa ukigo pande zote, pamoja na nyumba yake, na vitu vyote alivyo navyo? Kazi za mikono yake umezibarikia, nayo mali yake imeongezeka katika nchi. Lakini nyosha mkono wako sasa, uyaguse hayo yote aliyo nayo, naye atakukufuru mbele za uso wako.”—Ayubu 1:10, 11.

13. Shetani alidai nini alipomshtaki Yobu, na wanadamu wote wanahusikaje?

13 Shetani alidai kwamba Yehova alimhonga Yobu amtumikie kwa kumlinda kwa nguvu Zake. Na hilo lilimaanisha kwamba uaminifu wa Yobu ulikuwa wa kinafiki, na kwamba alimwabudu Mungu kwa ubinafsi tu. Shetani alidai kwamba Yobu angemkufuru Muumba wake kama hangebarikiwa. Shetani alijua kwamba Yobu alikuwa “mkamilifu na mwelekevu, mwenye kumcha Mungu na kuepukana na uovu.” * Basi kama Shetani angeweza kuvunja uaminifu wa Yobu, yaelekea kwamba angeweza pia kuvunja uaminifu wa wanadamu wengine wote. Kwa hiyo, Shetani alikuwa akitilia shaka uaminifu wa wanadamu wote wanaotaka kumtumikia Mungu. Kwa kweli, Shetani alihusisha wengine katika suala hilo kwa kumwambia hivi Yehova: “Yote aliyo nayo mtu [si Yobu tu] atayatoa kwa ajili ya uhai wake.”—Ayubu 1:8; 2:4.

14. Historia imeonyesha nini kuhusu dai la Shetani dhidi ya wanadamu?

14 Historia imeonyesha kwamba dai la Shetani ni la uwongo kwa sababu wengi kama Yobu, wamedumisha uaminifu kwa Yehova wakati wa majaribu. Maisha yao ya uaminifu yamemfurahisha Yehova, na hivyo ameweza kumjibu Shetani aliyedai kwa kiburi kwamba wanadamu wataacha kumtumikia Mungu wakipata magumu. (Waebrania 11:4-38) Naam, watu waadilifu wamekataa kumpa Mungu kisogo. Hata wanapokumbwa na matatizo magumu sana, wamemtegemea hata zaidi Yehova ili awape nguvu za kuvumilia.—2 Wakorintho 4:7-10.

15. Ni swali gani linaloweza kuzuka kuhusu hukumu za Mungu za wakati uliopita na za wakati ujao?

15 Lakini Yehova huonyesha haki katika mambo mengine mbali na suala la enzi kuu na suala la uaminifu wa wanadamu. Biblia hutueleza jinsi Yehova alivyohukumu watu mmoja-mmoja na hata mataifa mazima. Pia ina unabii mbalimbali wa hukumu ambazo atatekeleza wakati ujao. Kwa nini tunaweza kuwa na hakika kwamba Yehova amekuwa akihukumu kwa uadilifu na bado atahukumu kwa uadilifu wakati ujao?

Ubora wa Haki ya Mungu

Yehova ‘hataharibu kamwe mwenye haki pamoja na mwovu’

16, 17. Ni mifano gani inayoonyesha kwamba wanadamu hawafahamu kikamili haki ya kweli?

16 Ni sahihi kusema hivi kumhusu Yehova: “Njia zake zote ni haki.” (Kumbukumbu la Torati 32:4) Hakuna yeyote kati yetu anayeweza kudai hivyo, kwa kuwa mara nyingi tunashindwa kufahamu kikamili mambo yaliyo sawa. Kwa mfano, mfikirie Abrahamu. Alimsihi Yehova asiharibu Sodoma ingawa uovu ulikuwa umeenea sana. Alimwuliza Yehova hivi: “Je! Utaharibu mwenye haki pamoja na mwovu?” (Mwanzo 18:23-33) Bila shaka, jibu ni la. Yehova ‘alinyesha kiberiti na moto’ juu ya Sodoma, baada tu ya Loti mwadilifu na binti zake kufika mji wa Soari wakiwa salama. (Mwanzo 19:22-24) Kinyume chake, Yona ‘alikasirika’ sana wakati Mungu alipowaonyesha rehema watu wa Ninawi. Bila kujali toba yao ya kutoka moyoni, Yona alitaka tu waangamizwe kwa sababu tayari alikuwa ametangaza kwamba wangeangamizwa.—Yona 3:10–4:1.

17 Yehova alimhakikishia Abrahamu kwamba anatekeleza haki Yake kwa kuwaangamiza waovu na kuwaokoa pia waadilifu. Kwa upande mwingine, Yona alihitaji kujifunza kwamba Yehova ni mwenye rehema. Waovu wakiacha kabisa njia zao, yuko “tayari kusamehe.” (Zaburi 86:5) Tofauti na wanadamu fulani wanaojali mno vyeo vyao, Yehova hatoi hukumu kali ili kujionyesha ana nguvu, wala hakatai kuwahurumia watu eti kwa sababu ataonekana kuwa dhaifu. Yeye huonyesha rehema wakati wowote inapofaa kufanya hivyo.—Isaya 55:7; Ezekieli 18:23.

18. Tumia Biblia kuthibitisha kwamba Yehova haongozwi tu na hisia.

18 Hata hivyo, Yehova hapumbazwi na hisia. Watu wake walipoanza kuabudu sanamu, Yehova alisema hivi kwa uthabiti: “Nitawahukumu kadiri ya mwenendo wenu. Nitawaadhibu kwa machukizo yenu yote. Sitawaachia wala sitawaonea huruma; bali nitawaadhibu kulingana na mienendo yenu.” (Ezekieli 7:3, 4, BHN) Kwa hiyo, wanadamu wanapoendelea kufanya mabaya bila kujali, Yehova huwahukumu ifaavyo. Lakini hukumu yake inategemea ushahidi thabiti. Hivyo, Yehova aliposikia “kilio” kuhusu Sodoma na Gomora alisema hivi: “Nitashuka sasa nione kama wanayotenda ni kiasi cha kilio kilichonijia.” (Mwanzo 18:20, 21) Tunathamini kama nini kwamba Yehova si kama wanadamu wengi ambao huamua mambo haraka-haraka bila ushahidi kamili! Kwa kweli, Biblia yaeleza jinsi Yehova alivyo, “Mungu wa uaminifu . . . mwenye haki.”—Kumbukumbu la Torati 32:4.

Tumaini Haki ya Yehova

19. Tunaweza kufanya nini tukiwa na maswali yenye kutatanisha kuhusu hukumu za Yehova?

19 Biblia haijibu kila swali kuhusu matendo ya Yehova katika nyakati za kale; wala haielezi kila jambo kuhusu jinsi Yehova atakavyohukumu mtu mmoja-mmoja na vikundi vya watu wakati ujao. Tunapotatanishwa na masimulizi au unabii fulani wa Biblia ambao hauelezi kila jambo, tunaweza kuwa waaminifu kama nabii Mika, aliyeandika hivi: “Nitamngojea Mungu wa wokovu wangu.”—Mika 7:7.

20, 21. Kwa nini tunaweza kuwa na hakika kwamba sikuzote Yehova atafanya yaliyo sawa?

20 Tunaweza kuwa na hakika kwamba katika kila hali, Yehova atafanya yaliyo sawa. Hata inapoonekana kwamba wanadamu wanapuuza ukosefu wa haki, Yehova anaahidi hivi: “Kisasi ni changu; hakika mimi nitalipa.” (Waroma 12:19) Tukiwa na mtazamo wa kungoja, tutakuwa na usadikisho imara kama wa mtume Paulo aliyesema: “Je, kwa Mungu kuna ukosefu wa haki? Hilo lisipate kuwa hivyo kamwe!”—Waroma 9:14.

21 Hivi sasa tunaishi “nyakati za hatari zilizo ngumu kushughulika nazo.” (2 Timotheo 3:1) Watu wengi wametendewa kikatili kwa sababu ya ‘dhuluma’ na ukosefu wa haki. (Mhubiri 4:1) Hata hivyo, Yehova hajabadilika. Bado anachukia ukosefu wa haki, naye anawajali sana wale wanaotendewa isivyo haki. Tukiendelea kuwa waaminifu kwa enzi kuu ya Yehova, atatupatia uwezo wa kuvumilia hadi Ufalme wake utakapokomesha ukosefu wote wa haki kwa wakati barabara.—1 Petro 5:6, 7.

^ fu. 13 Yehova alisema hivi kumhusu Yobu: “Hapana mmoja aliye kama yeye duniani.” (Ayubu 1:8) Yaelekea kwamba Yobu aliishi baada ya Yosefu kufa na kabla ya Musa kuteuliwa kuwa kiongozi wa Israeli. Kwa hiyo, ni sahihi kusema kwamba wakati huo hakuwapo mtu mwingine aliyekuwa mwaminifu kama Yobu.