Hamia kwenye habari

Hamia kwenye yaliyomo

Sura ya 13

“Sheria ya Bwana Ni Kamilifu”

“Sheria ya Bwana Ni Kamilifu”

1, 2. Kwa nini watu wengi wanapuuza sheria, lakini huenda sisi tukahisije kuhusu sheria za Mungu?

“SHERIA haina mipaka, . . . huharibu mambo yote.” Maneno hayo yaliandikwa katika kitabu kilichochapishwa mnamo mwaka wa 1712. Mwandishi wa kitabu hicho alilaumu mfumo wa sheria ambao uliendeleza kesi mahakamani miaka nenda miaka rudi. Wale waliotafuta haki mahakamani walifilisika kabisa. Katika nchi nyingi, watu wengi hawaheshimu kabisa sheria kwa sababu mifumo ya sheria na ya mahakama haieleweki, haifuati haki kabisa, inapendelea watu, na haitegemeki.

2 Tofauti na maelezo hayo, fikiria maneno yaliyoandikwa miaka ipatayo 2,700 iliyopita: “Sheria yako naipenda mno ajabu.” (Zaburi 119:97) Kwa nini mtunga-zaburi aliipenda mno sheria hiyo? Kwa sababu sheria aliyosifu ilitungwa na Yehova Mungu, wala si na serikali yoyote ya wanadamu. Kadiri unavyojifunza sheria za Yehova, huenda ukazipenda zaidi kama mtunga-zaburi. Kujifunza sheria hizo kutakusaidia kumjua vyema hakimu bora zaidi ulimwenguni.

Mpaji-Sheria Mkuu Zaidi

3, 4. Yehova amethibitika kuwa Mpaji-Sheria kwa njia zipi?

3 Biblia inatuambia kwamba “mmoja yuko ambaye ni mpaji-sheria na hakimu.” (Yakobo 4:12) Kwa hakika, Yehova peke yake ndiye Mpaji-Sheria wa kweli. Hata sayari zinafuata ‘sheria zake zinazoongoza mbingu.’ (Ayubu 38:33, The New Jerusalem Bible) Kundi kubwa sana la malaika watakatifu wa Yehova wanaongozwa pia na sheria zake, kwa kuwa wamepangwa kulingana na vyeo hususa, nao hufuata amri ya Yehova wakiwa wahudumu wake.—Zaburi 104:4; Waebrania 1:7, 14.

4 Yehova amewapa pia wanadamu sheria. Kila mmoja wetu ana dhamiri, ambayo inaonyesha haki ya Yehova. Dhamiri ni sheria fulani ya asili ambayo inaweza kutusaidia kupambanua mema na mabaya. (Waroma 2:14) Wazazi wetu wa kwanza walipewa dhamiri kamilifu, kwa hiyo walihitaji sheria chache sana. (Mwanzo 2:15-17) Hata hivyo, mwanadamu asiyekamilika anahitaji sheria nyingi zaidi za kumwongoza kufanya mapenzi ya Mungu. Wazee wa ukoo kama vile Noa, Abrahamu, na Yakobo walizipa familia zao sheria ambazo walipewa na Yehova Mungu. (Mwanzo 6:22; 9:3-6; 18:19; 26:4, 5) Yehova alijisababisha kuwa Mpaji-Sheria asiye na kifani alipopatia taifa la Israeli Sheria kupitia Musa. Sheria hizo zinatusaidia kuelewa kindani zaidi haki ya Yehova.

Muhtasari wa Sheria ya Musa

5. Je, Sheria ya Musa ilikuwa na amri ngumu na zenye kulemea, na kwa nini unajibu hivyo?

5 Watu wengi wanafikiri kwamba Sheria ya Musa ilikuwa na amri ngumu zenye kulemea. Jambo hilo si kweli. Sheria hiyo ilikuwa na zaidi ya amri 600. Huenda hizo zikaonekana kuwa nyingi, lakini hebu fikiria: Kufikia mwishoni mwa karne ya 20, sheria za serikali ya Marekani zilijaza zaidi ya kurasa 150,000 za vitabu vya sheria. Sheria zipatazo 600 huongezwa baada ya kila miaka miwili! Kwa hiyo, sheria za wanadamu ni nyingi sana kuliko Sheria ya Musa. Hata hivyo, Sheria ya Mungu iliwaongoza Waisraeli katika mambo mbalimbali ya maisha ambayo hata sheria za kisasa hazitaji. Chunguza muhtasari wa sheria hiyo.

6, 7. (a) Sheria ya Musa inatofautianaje na mfumo mwingine wowote wa sheria, na amri kuu ya Sheria hiyo ni ipi? (b) Waisraeli wangeweza kuonyesha jinsi gani kwamba wanakubali enzi kuu ya Yehova?

6 Sheria ilitukuza enzi kuu ya Yehova. Kwa sababu hiyo, Sheria ya Musa haiwezi kulinganishwa na mfumo mwingine wowote wa sheria. Amri kuu zaidi ya sheria hiyo ilikuwa: “Sikiza, Ee Israeli; BWANA, Mungu wetu, BWANA ndiye mmoja. Nawe mpende BWANA, Mungu wako, kwa moyo wako wote, na kwa roho yako yote, na kwa nguvu zako zote.” Watu wa Mungu wangeonyeshaje kwamba wanampenda? Walipaswa kumtumikia, kujitiisha kwa enzi yake kuu.—Kumbukumbu la Torati 6:4, 5; 11:13.

7 Kila Mwisraeli alionyesha kwamba anakubali enzi kuu ya Yehova kwa kujitiisha kwa wale waliopewa mamlaka. Wazazi, wakuu, waamuzi, makuhani na, hatimaye, mfalme waliwakilisha mamlaka ya Mungu. Yehova aliona uasi wowote dhidi ya wenye mamlaka kuwa uasi dhidi yake. Kwa upande mwingine, wale wenye mamlaka wangeadhibiwa na Yehova iwapo wangewaonea au kuwakandamiza watu wake. (Kutoka 20:12; 22:28; Kumbukumbu la Torati 1:16, 17; 17:8-20; 19:16, 17) Basi, watu wote walikuwa na wajibu wa kuunga mkono enzi kuu ya Mungu.

8. Sheria ilidumishaje utakatifu wa Yehova?

8 Sheria ilidumisha utakatifu wa Yehova. Sheria ya Musa inataja neno “takatifu” na “utakatifu” zaidi ya mara 280. Sheria iliwasaidia watu wa Mungu kutofautisha vitu safi na visivyo safi, ilitaja vitu 70 hivi ambavyo vingemfanya Mwisraeli awe najisi. Sheria hizo zilihusu usafi wa mwili, chakula, na hata kufunika kinyesi. Sheria hizo zililinda kabisa afya yao. * Lakini zilitimiza kusudi jingine muhimu zaidi—ziliwasaidia kupata kibali cha Yehova, ziliwatenga na mazoea yenye dhambi ya mataifa yasiyo na adili yaliyokuwa jirani. Fikiria mfano mmoja.

9, 10. Agano la Sheria lilisema nini kuhusu ngono na kujifungua mtoto, na sheria hizo zilikuwa na manufaa gani?

9 Agano la Sheria lilisema kwamba mtu aliyejifungua mtoto au kufanya ngono—hata kati ya wenzi wa ndoa—angekuwa najisi kwa kipindi fulani. (Mambo ya Walawi 12:2-4; 15:16-18) Sheria hizo hazikudharau zawadi hizo safi kutoka kwa Mungu. (Mwanzo 1:28; 2:18-25) Badala yake, sheria hizo zilidumisha utakatifu wa Yehova kwa kuwazuia waabudu wake wasichafuliwe. Kumbuka kwamba mataifa jirani ya Israeli yalikuwa yakichanganya dini na ibada za ngono na uzazi. Dini ya Wakanaani ilikuwa na makahaba wa kiume na wa kike. Walitenda mambo maovu kupindukia na yakaenea kotekote. Kinyume chake, Sheria ilitenga kabisa ibada ya Yehova na mambo ya ngono. * Kulikuwa na faida nyingine pia.

10 Sheria hizo pia zilifundisha ukweli fulani muhimu sana. * Dhambi ya Adamu inapitishwaje kutoka kizazi hadi kizazi? Ni kupitia ngono na kuzaa, sivyo? (Waroma 5:12) Ndiyo, Sheria ya Mungu iliwakumbusha watu wake kwamba wao ni watenda-dhambi. Kwa kweli, sote tunazaliwa katika dhambi. (Zaburi 51:5) Tunahitaji msamaha na ukombozi ili kumkaribia Mungu wetu mtakatifu.

11, 12. (a) Sheria ilitetea kanuni gani muhimu ya haki? (b) Sheria ilizuia upotoshaji wa haki katika mambo yapi?

11 Sheria ilidumisha haki kamilifu ya Yehova. Sheria ya Musa ilitetea kanuni ya usawa, au usawaziko, katika mambo ya haki. Kwa hiyo, Sheria ilisema hivi: “Uhai utalipwa kwa uhai, jicho kwa jicho, jino kwa jino, mkono kwa mkono na mguu kwa mguu.” (Kumbukumbu la Torati 19:21, BHN) Hivyo basi, adhabu ya kesi za uhalifu ililingana na uhalifu uliofanywa. Kanuni hiyo ya haki ya Mungu ilikuwa muhimu sana katika Sheria. Na kanuni hiyo inaweza kutusaidia leo kuelewa dhabihu ya fidia ya Kristo Yesu, kama Sura ya 14 itakavyoonyesha.—1 Timotheo 2:5, 6.

12 Sheria ilizuia pia upotoshaji wa haki. Kwa mfano, angalau mashahidi wawili walihitajiwa ili kuthibitisha shtaka. Mashahidi wa uwongo walipata adhabu kali sana. (Kumbukumbu la Torati 19:15, 18, 19) Ufisadi na kupokea rushwa kulipigwa marufuku. (Kutoka 23:8; Kumbukumbu la Torati 27:25) Watu wa Mungu walihitaji kufuata kanuni za juu za Yehova za haki hata katika shughuli zao za kibiashara. (Mambo ya Walawi 19:35, 36; Kumbukumbu la Torati 23:19, 20) Mfumo huo wa sheria usiopendelea na usio na kifani ulinufaisha sana Israeli!

Sheria Zinazokazia Rehema na Kutopendelea Katika Hukumu

13, 14. Sheria ilikaziaje haki na kutopendelea kwa habari ya mwizi na yule aliyeibiwa?

13 Je, Sheria ya Musa ilikuwa kali mno, iliyotekelezwa bila rehema? La hasha! Mfalme Daudi aliongozwa kuandika hivi: “Sheria ya BWANA ni kamilifu.” (Zaburi 19:7) Daudi alijua vyema kwamba Sheria ilikazia rehema na kutopendelea. Jinsi gani?

14 Katika nchi fulani leo, yaonekana kwamba sheria huwapendelea na kuwalinda wahalifu na haiwajali waliotendewa uhalifu. Kwa mfano, huenda wezi wakafungwa gerezani. Lakini, wale walioibiwa huenda hawajarudishiwa mali yao, ingawa wanalazimika kulipa ushuru ili kuwalisha wahalifu hao wakiwa gerezani. Katika Israeli la kale, hakukuwa na magereza kama leo. Adhabu haikupaswa kupita mipaka iliyowekwa na Sheria. (Kumbukumbu la Torati 25:1-3) Mwizi alilazimika kulipa vitu alivyokuwa ameiba. Isitoshe, alitoa malipo zaidi. Alilipa kiasi gani? Ilitegemea hali. Inaonekana kwamba mahakimu waliruhusiwa kuzingatia mambo kadhaa, kama vile toba ya mtenda-dhambi. Ndiyo sababu malipo ambayo mwizi alihitajiwa kulipa yanayotajwa kwenye Mambo ya Walawi 6:1-7 ni chini zaidi kuliko malipo yanayotajwa kwenye Kutoka 22:7.

15. Sheria ilionyeshaje rehema na haki kwa mtu aliyemwua mwingine bila kukusudia?

15 Kwa rehema, Sheria ilitambua kwamba makosa yote hayakuwa ya kukusudia. Kwa mfano, mtu alipomwua mwingine bila kukusudia, hakuhitajika kulipa uhai kwa uhai ikiwa alichukua hatua ifaayo ya kukimbilia mojawapo ya miji ya makimbilio iliyokuwa kotekote katika Israeli. Baada ya kesi yake kuchunguzwa na waamuzi wa mji huo, alikaa humo hadi kifo cha kuhani mkuu. Kisha angekuwa huru kuishi popote alipotaka. Hivyo, alinufaishwa na rehema ya Mungu. Vilevile, sheria hiyo ilikazia thamani kubwa ya uhai wa mwanadamu.—Hesabu 15:30, 31; 35:12-25.

16. Sheria ililindaje haki fulani za watu?

16 Sheria ililinda haki za watu. Angalia jinsi ilivyolinda watu wenye madeni. Sheria ilikataza kuingia katika nyumba ya mdeni na kuchukua mali yake kama rehani. Badala yake, mkopeshaji alihitaji kusimama nje na kungoja mdeni amletee rehani hiyo. Hivyo, hakuna mtu aliyeruhusiwa kuvamia nyumba ya mwingine. Ikiwa mkopeshaji alichukua vazi la nje kama rehani, sharti angelirudisha jioni, kwa sababu huenda mdeni angehitaji kujifunika vazi hilo wakati wa usiku.—Kumbukumbu la Torati 24:10-14.

17, 18. Waisraeli walitofautianaje na mataifa mengine kuhusu vita, na kwa nini?

17 Hata pia kulikuwa na sheria kuhusu vita. Watu wa Mungu hawakupigana vita kwa sababu tu walitamani kupata mamlaka au ushindi, bali walimwakilisha Mungu katika “Vita vya BWANA.” (Hesabu 21:14) Mara nyingi, Waisraeli walitoa kwanza masharti ya kujisalimisha. Ikiwa jiji lilikataa masharti hayo, basi Israeli lingelizingira kupatana na amri za Mungu. Tofauti na wanajeshi wengi, wanajeshi Waisraeli hawakuruhusiwa kubaka wanawake au kuchinja watu ovyo-ovyo. Hata walihitaji kuheshimu mazingira, hawakupaswa kukata miti ya matunda ya maadui. * Wanajeshi wengine hawakuwa na sheria kama hizo.—Kumbukumbu la Torati 20:10-15, 19, 20; 21:10-13.

18 Je, wewe huudhika unaposikia kwamba katika nchi fulani watoto wadogo wanazoezwa kuwa wanajeshi? Katika Israeli la kale, mwanamume yeyote mwenye umri uliopungua miaka 20 hakuandikishwa jeshini. (Hesabu 1:2, 3) Hata mwanamume mzima mwenye hofu kubwa hakuruhusiwa kwenda vitani. Mwanamume aliyeoa karibuni hangeenda vitani kwa mwaka mzima ili aweze kumzaa mrithi kabla ya kushiriki utumishi huo hatari sana. Sheria ilieleza kwamba kwa kufanya hivyo, mume huyo kijana angepata ‘kumfurahisha’ mkewe.—Kumbukumbu la Torati 20:5, 6, 8; 24:5.

19. Sheria iliwalindaje wanawake, watoto, familia, wajane, na mayatima?

19 Sheria iliwalinda wanawake, watoto, na familia na kujali masilahi yao. Iliwaamuru wazazi wawatunze na kuwafundisha watoto mambo ya kiroho kila wakati. (Kumbukumbu la Torati 6:6, 7) Ilikataza ngono zote za maharimu, na yeyote aliyefanya hivyo aliuawa. (Mambo ya Walawi, sura ya 18) Vilevile ilikataza uzinzi, ambao mara nyingi huvunja na kuharibu amani na heshima ya familia. Sheria iliwajali sana wajane na mayatima na ilikataza katakata wasiteswe.—Kutoka 20:14; 22:22-24.

20, 21. (a) Kwa nini Sheria ya Musa iliwaruhusu Waisraeli wawe na wake wengi? (b) Kuhusu talaka, kwa nini Sheria ilitofautiana na kanuni ambazo Yesu alirudisha baadaye?

20 Hata hivyo, huenda wengine wakajiuliza hivi, ‘Mbona Sheria iliwaruhusu watu kuwa na wake wengi?’ (Kumbukumbu la Torati 21:15-17) Tunahitaji kuchunguza sheria kama hizo tukifikiria hali za wakati huo. Wale wanaojaribu kuelewa Sheria ya Musa kwa kutegemea maoni ya nyakati na tamaduni za kisasa bila shaka hawataielewa. (Mithali 18:13) Kulingana na kanuni ambazo Yehova aliweka zamani katika Edeni, ndoa ilikuwa kifungo cha kudumu kati ya mume mmoja na mke mmoja. (Mwanzo 2:18, 20-24) Hata hivyo, mazoea kama vile ndoa za wake wengi yalikuwa yameenea kwa miaka mingi sana kabla Yehova hajawapa Waisraeli Sheria. Yehova alijua vyema kwamba mara kwa mara ‘watu wake wenye shingo ngumu’ wangekosa kutii hata sheria rahisi sana, kama zile zilizokataza ibada ya sanamu. (Kutoka 32:9) Basi kwa hekima, hakuchagua wakati huo kuwa wakati wa kurekebisha mazoea yao yote ya ndoa. Lakini kumbuka kwamba Yehova hakuanzisha ndoa ya wake wengi. Hata hivyo, alitumia Sheria ya Musa kudhibiti ndoa za wake wengi miongoni mwa watu wake na kuwazuia wasitumie vibaya zoea hilo.

21 Vivyo hivyo, Sheria ya Musa ilimruhusu mwanamume kumtaliki mkewe kwa sababu mbalimbali nzito. (Kumbukumbu la Torati 24:1-4) Yesu alisema kwamba Mungu aliwapa Wayahudi idhini hiyo “kwa kufikiria ugumu [wao] wa moyo.” Hata hivyo, idhini kama hizo zilikuwa za muda tu. Yesu alirudisha tena kanuni za Yehova kuhusu ndoa ambazo zingefuatwa na wafuasi wake.—Mathayo 19:8.

Sheria Ilikazia Upendo

22. Sheria ya Musa ilikazia upendo kwa njia zipi, na kwa nani?

22 Je, waweza kuwazia mfumo wowote wa kisasa wa sheria unaokazia upendo? Sheria ya Musa ilikazia sana upendo. Kwani, katika kitabu cha Kumbukumbu la Torati pekee, neno “upendo” limetumiwa zaidi ya mara 20 katika njia mbalimbali. Amri ya pili iliyo kuu zaidi katika Sheria ilikuwa, “umpende jirani yako kama nafsi yako.” (Mambo ya Walawi 19:18; Mathayo 22:37-40) Waisraeli walipaswa kuwapenda wenzao na pia wageni walioishi kati yao, huku wakikumbuka kwamba pindi moja wao pia walikuwa wageni. Walipaswa kuwapenda maskini na wanyonge, na kuwasaidia kimwili bila kuwadhulumu. Hata waliagizwa kuwa wenye fadhili na kuwajali wanyama wanaobeba mizigo.—Kutoka 23:6; Mambo ya Walawi 19:14, 33, 34; Kumbukumbu la Torati 22:4, 10; 24:17, 18.

23. Mtungaji wa Zaburi 119 alichochewa kufanya nini, nasi tunaweza kuazimia kufanya nini?

23 Hakuna taifa jingine lililobarikiwa na sheria kama hizo. Si ajabu kwamba mtunga-zaburi aliandika hivi: “Naipenda sana sheria yako!” Lakini hakuwa tu na hisia ya upendo. Upendo huo ulimchochea kutenda, kwa kuwa alijitahidi kutii sheria hiyo na kuishi kupatana nayo. Aliendelea kusema hivi: “Naitafakari [sheria yako] mchana kutwa.” (Zaburi 119:11, 97, BHN) Naam, alijifunza sheria za Yehova kwa ukawaida. Hapana shaka yoyote kwamba upendo wake uliongezeka kadiri alivyojifunza sheria hizo. Wakati huohuo, alizidi kumpenda Yehova Mungu, yule Mpaji-Sheria. Na umkaribie zaidi Yehova, Mpaji-Sheria Mkuu na Mungu wa haki unapoendelea kujifunza sheria zake.

^ fu. 8 Kwa mfano, sheria zilizoamuru kinyesi cha mwanadamu kifunikwe, wagonjwa watengwe, na mtu yeyote anayegusa maiti aoge, zilikuwapo muda mrefu kabla ya manufaa yake kutambuliwa.—Mambo ya Walawi 13:4-8; Hesabu 19:11-13, 17-19; Kumbukumbu la Torati 23:13, 14.

^ fu. 9 Mahekalu ya Wakanaani yalikuwa na vyumba vya kufanyia ngono, lakini Sheria ya Musa ilisema kwamba watu wote walio najisi hawangeweza hata kuingia hekaluni. Kwa hiyo, hakuna mtu yeyote angechanganya ngono na ibada katika nyumba ya Yehova, kwa sababu ngono ilimfanya mtu awe najisi kwa kipindi fulani.

^ fu. 10 Kusudi kuu la Sheria lilikuwa kufundisha. Hata kichapo Encyclopaedia Judaica kinasema kwamba neno la Kiebrania linalotafsiriwa “sheria,” toh·rah’, linamaanisha “mafundisho.”

^ fu. 17 Sheria iliuliza hivi waziwazi: “Mti wa kondeni, je! ni mtu, hata ukauzuie?” (Kumbukumbu la Torati 20:19) Philo, msomi Myahudi wa karne ya kwanza, alitaja sheria hiyo, na kusema kwamba Mungu anaona “haifai hasira inayoelekezwa kwa watu itumiwe kuharibu vitu ambavyo havina hatia yoyote.”