Hamia kwenye habari

Hamia kwenye yaliyomo

Sura ya 14

Yehova Atoa “Fidia Katika Kubadilishana kwa Ajili ya Wengi”

Yehova Atoa “Fidia Katika Kubadilishana kwa Ajili ya Wengi”

1, 2. Biblia inasema nini kuhusu hali ya wanadamu, na suluhisho pekee ni nini?

“VIUMBE vyote vinafuliza kupiga kite pamoja na kuwa katika maumivu pamoja.” (Waroma 8:22) Maneno hayo ya mtume Paulo yanaeleza hali yetu yenye kusikitisha. Huenda mwanadamu akaona kwamba mateso, dhambi, na kifo haziwezi kukomeshwa. Lakini Yehova ana uwezo unaozidi wa wanadamu. (Hesabu 23:19) Mungu huyo wa haki ametuandalia suluhisho la matatizo yetu. Suluhisho hilo ni fidia.

2 Fidia ndiyo zawadi bora ambayo Yehova amewapa wanadamu. Kupitia fidia tutaweza kukombolewa kutoka kwa dhambi na kifo. (Waefeso 1:7) Ndiyo msingi wa tumaini la kuishi milele, ama mbinguni au katika paradiso duniani. (Luka 23:43; Yohana 3:16; 1 Petro 1:4) Lakini fidia ni nini hasa? Inatusaidiaje kuelewa haki ya Yehova isiyo na kifani?

Kwa Nini Fidia Ilihitajiwa?

3. (a) Kwa nini fidia ilihitajiwa? (b) Kwa nini Mungu hangeweza kupunguza adhabu ya kifo kwa wazao wa Adamu?

3 Fidia ilihitajiwa kwa sababu ya dhambi ya Adamu. Kwa sababu ya kutomtii Mungu, Adamu aliwaletea wazao wake magonjwa, kilio, maumivu, na kifo. (Mwanzo 2:17; Waroma 8:20) Mungu hangeweza kupunguza adhabu ya kifo kwa sababu tu ya kuwahurumia wazao wa Adamu. Kufanya hivyo kungekuwa kupuuza sheria yake mwenyewe inayosema kwamba “Mshahara ambao dhambi hulipa ni kifo.” (Waroma 6:23) Na endapo Yehova angevunja kanuni zake mwenyewe za haki, basi kungekuwa na mvurugo na uasi ulimwenguni pote!

4, 5. (a) Shetani alitoa mashtaka gani ya uwongo kumhusu Mungu, na kwa nini Yehova alikuwa na wajibu wa kujibu mashtaka hayo? (b) Shetani alitoa shtaka gani kuhusu watumishi waaminifu wa Yehova?

4 Kama tulivyoona katika Sura ya 12, uasi uliotukia Edeni ulizusha masuala muhimu sana. Shetani alichafua jina zuri la Mungu. Ni kana kwamba alimshtaki Yehova kuwa mwongo na mtawala mkatili wa kimabavu, anayewanyima viumbe wake uhuru. (Mwanzo 3:1-5) Kwa kujaribu kukatisha kusudi la Mungu la kuwa na wanadamu waadilifu duniani, Shetani pia alitoa shtaka la kwamba Mungu hawezi kutimiza makusudi yake. (Mwanzo 1:28; Isaya 55:10, 11) Kama Yehova hangejibu mashtaka hayo, huenda viumbe wake wengi wenye akili wangetilia shaka utawala wake.

5 Shetani alieneza pia uwongo kuhusu watumishi waaminifu wa Yehova. Alidai kwamba wanamtumikia Yehova kwa sababu ya ubinafsi na kwamba hakuna yeyote ambaye angeendelea kuwa mwaminifu kwa Mungu akipata magumu. (Ayubu 1:9-11) Masuala hayo yalikuwa muhimu sana kuliko magumu ambayo yangewakabili wanadamu. Kwa kufaa, Yehova alihisi kwamba ana wajibu wa kujibu mashtaka ya uwongo ya Shetani. Lakini Mungu angesuluhishaje masuala hayo na kuwaokoa wanadamu?

Fidia—Bei Inayolingana

6. Ni maneno gani yanayotumiwa katika Biblia kueleza njia ya Mungu ya kuwaokoa wanadamu?

6 Yehova alisuluhisha jambo hilo kwa rehema nyingi sana na haki. Hakuna mwanadamu angeweza kusuluhisha jambo hilo kwa njia hiyo. Alisuluhisha jambo hilo kwa njia rahisi sana. Mara nyingine njia aliyotumia huitwa ununuzi, ukombozi, ufuniko, na upatanisho. (Zaburi 49:8ZSB; Danieli 9:24, BHN; Wagalatia 3:13; Wakolosai 1:20; Waebrania 2:17) Lakini Yesu alitumia neno ambalo huenda linafaa kabisa. Alisema: ‘Mwana wa binadamu alikuja, si kuhudumiwa, bali kuhudumu na kutoa nafsi yake kuwa fidia [Kigiriki, lyʹtron] katika kubadilishana kwa ajili ya wengi.”—Mathayo 20:28.

7, 8. (a) Neno “fidia” linamaanisha nini katika Maandiko? (b) Fidia inaonyeshaje ulinganifu?

7 Fidia ni nini? Neno la Kigiriki linalotumiwa hapa linatokana na kitenzi kinachomaanisha “kuweka huru, kuachilia.” Neno hilo lilihusiana na pesa zinazolipwa ili wafungwa wa vita waweze kuachiliwa huru. Basi, kwa ufupi fidia inaweza kufafanuliwa kuwa kitu kinacholipwa ili kununua tena kitu fulani. Katika Maandiko ya Kiebrania, neno linalotafsiriwa “fidia” (koʹpher) linatokana na kitenzi kinachomaanisha “kufunika.” Kwa mfano, Mungu alimwambia Noa ‘aifunike’ (muundo fulani wa neno hilo) safina kwa lami. (Mwanzo 6:14) Habari hiyo inatusaidia kuelewa kwamba kutoa fidia humaanisha pia kufunika dhambi.—Zaburi 65:3.

8 Kichapo Theological Dictionary of the New Testament kinasema kwamba neno hilo (koʹpher) “sikuzote hudokeza usawa,” au ulinganifu. Kwa hiyo, kifuniko cha sanduku la agano kilikuwa na umbo sawa na sanduku hilo. Vivyo hivyo, ili kutoa fidia, au kufunika dhambi, ni lazima bei inayolipwa ilingane kabisa, au ifunike kikamili hasara iliyosababishwa na dhambi. Ndiyo sababu Sheria ambayo Mungu aliwapa Waisraeli ilisema hivi: “Uhai utalipwa kwa uhai, jicho kwa jicho, jino kwa jino, mkono kwa mkono na mguu kwa mguu.”—Kumbukumbu la Torati 19:21, BHN.

9. Kwa nini watu waaminifu walitoa dhabihu za wanyama, na Yehova alionaje dhabihu hizo?

9 Watu waaminifu kuanzia Abeli na kuendelea walimtolea Mungu dhabihu za wanyama. Kwa kufanya hivyo, walionyesha kwamba walitambua kuwapo kwa dhambi na umuhimu wa ukombozi. Walikuwa na imani katika ahadi ya Mungu ya kuwakomboa wanadamu kupitia “uzao” wake. (Mwanzo 3:15; 4:1-4; Mambo ya Walawi 17:11; Waebrania 11:4) Yehova alikubali dhabihu hizo na wakawa na uhusiano mzuri naye. Hata hivyo, matoleo ya wanyama yalikuwa ishara tu ya jambo jingine. Wanyama hawangeweza kufunika kabisa dhambi za wanadamu, kwa kuwa wanyama ni viumbe wa hali ya chini wanapolinganishwa na wanadamu. (Zaburi 8:4-8) Hivyo basi, Biblia yasema hivi: “Haiwezekani damu ya mafahali na ya mbuzi kuziondolea mbali dhambi.” (Waebrania 10:1-4) Dhabihu hizo zilikuwa mifano tu ya dhabihu ya kweli ya fidia ambayo ingetolewa.

“Fidia Inayolingana”

10. (a) Mfidi alihitaji kulingana na nani, na kwa nini? (b) Kwa nini ni mwanadamu mmoja tu aliyehitaji kutolewa dhabihu?

10 Mtume Paulo alisema kwamba “katika Adamu wote wanakufa.” (1 Wakorintho 15:22) Kwa hiyo mtu aliyelingana kabisa na Adamu—mwanadamu mkamilifu—alihitaji kufa ili kutoa fidia. (Waroma 5:14) Hakuna kiumbe mwingine yeyote ambaye angeweza kusawazisha mizani ya haki. Ni mwanadamu mkamilifu peke yake, mtu ambaye hakurithi dhambi ya Adamu, ndiye tu aliyeweza kutoa “fidia inayolingana” kikamili kabisa na Adamu. (1 Timotheo 2:6) Hakungekuwa na uhitaji wa mamilioni ya wanadamu kutolewa dhabihu ili kumkomboa kila mzao wa Adamu. Mtume Paulo alieleza hivi: “Kupitia mtu mmoja [Adamu] dhambi iliingia katika ulimwengu na kifo kupitia dhambi.” (Waroma 5:12) Na “kwa kuwa kifo ni kupitia mwanadamu,” Mungu alifanya mpango wa kuwakomboa wanadamu “kupitia mwanadamu.” (1 Wakorintho 15:21) Jinsi gani?

“Fidia inayolingana kwa ajili ya wote”

11. (a) Mfidi ‘angeonja kifo kwa ajili ya kila mtu’ jinsi gani? (b) Kwa nini Adamu na Hawa hawangefaidika kutokana na fidia? (Ona kielezi-chini.)

11 Yehova alipanga mwanadamu mmoja mkamilifu adhabihu uhai wake kwa hiari. Andiko la Waroma 6:23 lasema, “mshahara ambao dhambi hulipa ni kifo.” Mfidi huyo ‘angeonja kifo kwa ajili ya kila mtu’ kwa kudhabihu uhai wake. Yaani, angelipa mshahara wa dhambi ya Adamu. (Waebrania 2:9; 2 Wakorintho 5:21; 1 Petro 2:24) Kufanya hivyo kungekuwa na matokeo makubwa kisheria. Fidia ingekomesha kabisa dhambi yenye kuangamiza kwa kuwaondolea wazao watiifu wa Adamu hukumu ya kifo. *Waroma 5:16.

12. Toa mfano ambao unaonyesha jinsi watu wengi wanavyoweza kufaidika baada ya deni moja kulipwa.

12 Kwa mfano: Wazia kwamba wakazi wengi wa mji wenu wameajiriwa katika kiwanda kikubwa. Wewe na jirani zako mnalipwa mshahara mnono na mnaishi raha mustarehe. Siku moja kiwanda hicho kinafungwa kabisa na mambo yanabadilika. Kwa nini? Kiwanda hicho kimefilisika kwa sababu ya ufisadi wa meneja wake. Kwa ghafula, wewe na jirani zako mnafutwa kazi na hamwezi kulipa madeni yenu. Wenzi wa ndoa, watoto, na wakopeshaji wanateseka kwa sababu ya ufisadi wa mtu mmoja tu. Je, kuna suluhisho? Ndiyo! Mfadhili tajiri anaamua kuwasaidia. Anajua umuhimu wa kiwanda hicho. Anawahurumia pia watu wote walioajiriwa humo na familia zao. Kwa hiyo anapanga kulipa deni la kampuni hiyo ili kiwanda kifunguliwe. Kulipwa kwa deni hilo kunawafaidi watu wote walioajiriwa humo, familia zao na wakopeshaji. Vivyo hivyo, kulipwa kwa deni la Adamu kunawafaidi mamilioni ya watu.

Ni Nani Anayetoa Fidia?

13, 14. (a) Yehova aliwaandalia wanadamu fidia jinsi gani? (b) Ni nani anayelipwa fidia, na kwa nini malipo hayo ni muhimu?

13 Ni Yehova peke yake angeweza kumtoa “Mwana-Kondoo . . . ambaye huondolea mbali dhambi ya ulimwengu.” (Yohana 1:29) Lakini Yehova hakumtuma malaika yeyote tu aje kuwaokoa wanadamu. Badala yake, alimtuma Yule ambaye angeweza kujibu kikamili na kwa uhakika shtaka la Shetani dhidi ya watumishi wa Yehova. Naam, Yehova alijitoa kabisa kwa kumtuma Mwanaye mzaliwa-pekee, ‘aliyekuwa furaha yake.’ (Mithali 8:30) Kwa hiari, Mwana wa Mungu “alijifanya mwenyewe kuwa mtupu” kwa kuacha mwili wake wa kimbingu. (Wafilipi 2:7) Yehova alihamisha kimuujiza uhai na utu wa Mwanaye mzaliwa wa kwanza wa mbinguni hadi kwenye tumbo la uzazi la bikira Myahudi aliyeitwa Maria. (Luka 1:27, 35) Akiwa mwanadamu, angeitwa Yesu. Lakini kisheria, angeweza kuitwa Adamu wa pili, kwa kuwa alilingana kikamili na Adamu. (1 Wakorintho 15:45, 47) Kwa hiyo, Yesu aliweza kujitoa mwenyewe kuwa dhabihu ya fidia kwa ajili ya wanadamu wenye dhambi.

14 Ni nani ambaye angelipwa fidia? Zaburi 49:7 yasema wazi kwamba “Mungu” ndiye anayelipwa fidia. Lakini ni Yehova anayefanya mpango wa fidia, sivyo? Ndivyo, lakini hilo halimaanishi kwamba fidia ni badilishano lisilo na kusudi wala maana—kama kutoa pesa katika mfuko mmoja na kuzitia katika mfuko mwingine. Ni lazima tuelewe kwamba fidia si badilishano halisi, bali ni badilishano la kisheria. Yehova alithibitisha kwamba anafuata kabisa haki yake kamilifu kwa kulipa fidia, ijapokuwa ilimgharimu sana.—Mwanzo 22:7, 8, 11-13; Waebrania 11:17; Yakobo 1:17.

15. Kwa nini ilikuwa lazima Yesu ateseke na kufa?

15 Katika masika ya mwaka wa 33 W.K., Yesu Kristo alijitolea kuteseka ili alipe fidia. Alijiruhusu kukamatwa kwa mashtaka ya uwongo, kuhukumiwa kuwa na hatia, na kupigiliwa misumari kwenye mti wa mateso. Je, ilikuwa lazima Yesu apatwe na mateso hayo makali? Ndiyo, kwa sababu suala la uaminifu wa watumishi wa Mungu lilihitaji kuamuliwa. Mungu hakumruhusu Herode amwue Yesu akiwa mtoto mchanga. (Mathayo 2:13-18) Lakini akiwa mtu mzima, Yesu aliweza kuvumilia mashambulizi makali ya Shetani akiwa na ujuzi kamili wa masuala yaliyohusika. * Yesu alithibitisha waziwazi kwamba Yehova ana watumishi wanaobaki waaminifu chini ya majaribu kwa sababu ajapoteswa vibaya sana, aliendelea kuwa “mwaminifu-mshikamanifu, asiye na hila, asiyetiwa unajisi, aliyetengwa na watenda-dhambi.” (Waebrania 7:26) Ndiyo sababu kabla tu ya kufa, Yesu alipaaza kilio kwa ushindi: “Imetimizwa!”—Yohana 19:30.

Kumaliza Kazi Yake ya Ukombozi

16, 17. (a) Yesu aliendeleaje na kazi yake ya ukombozi? (b) Kwa nini ilikuwa lazima Yesu aonekane “mbele ya uso wa Mungu kwa ajili yetu”?

16 Yesu hakuwa amemaliza kazi yake ya ukombozi. Yehova alimfufua Yesu siku ya tatu baada ya kufa. (Matendo 3:15; 10:40) Kupitia tendo hilo muhimu sana, Yehova alimthawabisha Mwanaye kwa sababu alimtumikia kwa uaminifu. Pia alimpa nafasi ya kumaliza kazi yake ya ukombozi akiwa Kuhani wa Cheo cha Juu wa Mungu. (Waroma 1:4; 1 Wakorintho 15:3-8) Mtume Paulo aeleza hivi: “Kristo alipokuja akiwa kuhani wa cheo cha juu . . . , aliingia, si kwa damu ya mbuzi na ya mafahali wachanga, sivyo, bali kwa damu yake mwenyewe, mara moja kwa wakati wote ndani ya mahali patakatifu na kupata ukombozi udumuo milele kwa ajili yetu. Kwa maana Kristo aliingia, si mahali patakatifu palipofanywa kwa mikono, ambapo ni nakala ya uhalisi, bali mbinguni kwenyewe, ili sasa aonekane mbele ya uso wa Mungu kwa ajili yetu.”—Waebrania 9:11, 12, 24.

17 Kristo hakuweza kupeleka damu yake halisi mbinguni. (1 Wakorintho 15:50) Badala yake, alipeleka kile kilichofananishwa na damu hiyo: thamani halali ya uhai wake mkamilifu wa kibinadamu uliotolewa dhabihu. Halafu, akiwa mbele ya uso wa Mungu, alitoa rasmi thamani ya uhai wake iwe fidia ya kuwakomboa wanadamu wenye dhambi. Je, Yehova alikubali dhabihu hiyo? Ndiyo, na hilo lilithibitishwa wakati roho takatifu ilipomiminwa juu ya wanafunzi 120 hivi huko Yerusalemu wakati wa Pentekoste ya 33 W.K. (Matendo 2:1-4) Ingawa tukio hilo lilikuwa lenye kusisimua sana, fidia ilikuwa tu imeanza kuwafaidi wanadamu kwa njia kubwa ajabu.

Faida za Fidia

18, 19. (a) Ni vikundi gani viwili vya watu vinavyonufaika na upatanisho ambao umewezeshwa na damu ya Kristo? (b) Fidia inawafaidije wale wa “umati mkubwa,” sasa na wakati ujao?

18 Katika barua yake kwa Wakolosai, Paulo aeleza kwamba Mungu aliona vema kupitia Kristo kupatanisha kwake Mwenyewe vitu vingine vyote kwa kufanya amani kupitia damu ya Yesu iliyomwagwa juu ya mti wa mateso. Paulo aeleza pia kwamba upatanisho huo unahusu vikundi viwili vya watu, yaani, “vitu vilivyomo katika mbingu” na “vitu vilivyo duniani.” (Wakolosai 1:19, 20; Waefeso 1:10) Kikundi cha kwanza ni cha Wakristo 144,000 ambao wanapewa tumaini la kutumikia wakiwa makuhani mbinguni na kutawala juu ya dunia pamoja na Kristo Yesu. (Ufunuo 5:9, 10; 7:4; 14:1-3) Kupitia wao, wanadamu watiifu watapata manufaa ya dhabihu hatua kwa hatua katika kipindi cha miaka 1,000.—1 Wakorintho 15:24-26; Ufunuo 20:6; 21:3, 4.

19 “Vitu vilivyo duniani” ni watu wanaotarajia kufurahia maisha makamilifu katika Paradiso duniani. Andiko la Ufunuo 7:9-17 linawaita “umati mkubwa” ambao utaokoka “dhiki kubwa” inayokuja. Lakini si lazima wangoje hadi wakati huo ili wanufaike na fidia. Tayari “wamefua kanzu zao na kuzifanya nyeupe katika damu ya Mwana-Kondoo.” Hata sasa wanapata faida za kiroho za mpango huo wa upendo kwa sababu wanadhihirisha imani katika fidia. Wamehesabiwa kuwa waadilifu wakiwa rafiki za Mungu! (Yakobo 2:23) Kwa sababu ya dhabihu ya Yesu, wanaweza ‘kukaribia kwa uhuru wa usemi kwenye kiti cha ufalme cha fadhili isiyostahiliwa.’ (Waebrania 4:14-16) Wanapokosea, wanasamehewa kikweli. (Waefeso 1:7) Wana dhamiri safi ijapokuwa hawajakamilika. (Waebrania 9:9; 10:22; 1 Petro 3:21) Kwa hiyo, kupatanishwa na Mungu si tukio tu la wakati ujao, bali ni jambo linalotukia leo! (2 Wakorintho 5:19, 20) Katika kile kipindi cha miaka 1,000, ‘watawekwa huru kutoka katika utumwa wa uharibifu’ hatua kwa hatua na mwishowe ‘watakuwa na uhuru wenye utukufu wa watoto wa Mungu.’—Waroma 8:21.

20. Wewe unahisije unapotafakari juu ya fidia?

20 “Shukrani kwa Mungu kupitia Yesu Kristo” kwa ajili ya fidia! (Waroma 7:25) Mpango wa fidia ni rahisi sana, lakini ni wa hali ya juu sana hivi kwamba unatustaajabisha. (Waroma 11:33) Tunapotafakari na kuthamini sana fidia, mioyo yetu inatuchochea kumkaribia zaidi Mungu wa haki. Kama mtunga-zaburi, tuna sababu nyingi sana za kumsifu Yehova ambaye ‘anapenda haki na hukumu.’—Zaburi 33:5.

^ fu. 11 Adamu na Hawa hawangefaidika kutokana na fidia. Sheria ya Musa ilisema hivi kumhusu mwuaji wa kukusudia: “Msipokee fidia kwa ajili ya uhai wa mwuaji, ambaye amekuwa na hatia ya mauti.” (Hesabu 35:31) Ni wazi kwamba Adamu na Hawa walistahili kufa kwa sababu walikataa kimakusudi kumtii Mungu. Hivyo wakapoteza tumaini lao la kuishi milele.

^ fu. 15 Ili kufutilia mbali dhambi ya Adamu, Yesu alilazimika kufa akiwa mtu mzima mkamilifu wala si mtoto mkamilifu. Kumbuka kwamba Adamu alitenda dhambi kimakusudi, alijua vizuri kabisa ubaya na matokeo ya tendo lake. Kwa hiyo, ili kuwa “Adamu wa mwisho” na kufunika dhambi hiyo, Yesu alihitaji kuamua kudumisha uaminifu wake kwa Yehova kupatana na ujuzi aliokuwa nao. (1 Wakorintho 15:45, 47) Kwa hiyo, maisha ya Yesu ya uaminifu akiwa duniani kutia ndani kifo chake cha dhabihu yalikuwa “tendo moja la kutetewa kuwa haki.”—Waroma 5:18, 19.