Hamia kwenye habari

Hamia kwenye yaliyomo

Sura ya 16

‘Tenda Haki’ Unapotembea na Mungu

‘Tenda Haki’ Unapotembea na Mungu

1-3. (a) Kwa nini tunapaswa kumshukuru sana Yehova? (b) Mwokozi wetu mwenye upendo anataka tufanye nini?

JIWAZIE ukiwa ndani ya meli inayozama. Unapoanza kukata tamaa, mtu fulani anawasili na kukuokoa. Unafurahi kama nini mtu huyo anapokuokoa na kusema: “Sasa uko salama”! Je, hungemshukuru sana mtu huyo? Kwa kweli, ungekufa kama hangekuokoa.

2 Kwa njia fulani, mfano huo waonyesha jambo ambalo Yehova ametufanyia. Tunapaswa kumshukuru kwelikweli, kwa sababu ameandaa fidia ambayo inatuwezesha kuokolewa kutoka kwa utumwa wa dhambi na kifo. Tunajihisi tukiwa salama kwa sababu tunajua kwamba maadamu tunadhihirisha imani katika dhabihu hiyo yenye thamani, dhambi zetu zinasamehewa na tunakuwa na tumaini hakika la kuishi milele. (1 Yohana 1:7; 4:9) Kama tulivyoona katika Sura ya 14, fidia ni wonyesho mkuu zaidi wa upendo na haki ya Yehova. Tunapaswa kuionaje?

3 Inafaa tuchunguze mambo ambayo Mwokozi wetu mwenye upendo anataka tufanye. Yehova anasema hivi kupitia nabii Mika: “Amekuonyesha, Ee mutu, nini ni njema, na BWANA anataka nini kwako ila kutenda haki, na kupenda rehema na kutembea kwa unyenyekevu na Mungu wako?” (Mika 6:8, ZSB) Ona kwamba mojawapo ya mambo ambayo Yehova anataka tufanye ni “kutenda haki.” Tutafanyaje hivyo?

Kufuatia “Uadilifu wa Kweli”

4. Tunajuaje kwamba Yehova anatutarajia tuishi kupatana na kanuni zake za uadilifu?

4 Yehova anatutarajia tuishi kupatana na kanuni zake za mema na mabaya. Kwa kuwa kanuni zake ni za haki na za uadilifu, tunapozitii tunafuatia haki na uadilifu. Andiko la Isaya 1:17, ZSB, lasema: “Mujifundishe kufanya mema; mutafute hukumu za haki.” Neno la Mungu linatuhimiza ‘tutafute haki.’ (Sefania 2:3) Linatusihi pia ‘tuvae utu mpya ulioumbwa kulingana na mapenzi ya Mungu katika uadilifu wa kweli.’ (Waefeso 4:24) Uadilifu wa kweli, au haki ya kweli, huchukia jeuri, uovu, na ukosefu wa adili, kwa sababu mambo hayo huchafua mambo matakatifu.—Zaburi 11:5; Waefeso 5:3-5.

5, 6. (a) Kwa nini si vigumu kwetu kuishi kupatana na kanuni za Yehova? (b) Biblia inaonyeshaje kwamba kufuatia uadilifu ni jambo lenye kuendelea?

5 Je, ni vigumu kwetu kuishi kupatana na kanuni za Yehova za uadilifu? La. Mtu anayempenda Yehova haoni matakwa Yake kuwa yenye kulemea. Tunataka kuishi kwa njia inayomfurahisha Mungu wetu kwa sababu tunampenda na tunapenda sifa zake. (1 Yohana 5:3) Kumbuka kwamba Yehova “apenda matendo ya haki.” (Zaburi 11:7) Ikiwa tunataka kuiga kikweli haki au uadilifu wa Mungu, ni lazima tupende mambo ambayo Yehova anapenda na kuchukia yale anayochukia.—Zaburi 97:10.

6 Si rahisi kwa wanadamu wasiokamilika kufuatia uadilifu. Ni lazima tuvue utu wa zamani pamoja na mazoea yake maovu na kujivika utu mpya. Biblia inasema kwamba utu huo mpya “unafanywa kuwa mpya” kupitia ujuzi sahihi. (Wakolosai 3:9, 10) Maneno ya lugha ya awali yaliyotafsiriwa “-fanywa kuwa mpya” yanaonyesha kwamba kujivika utu mpya ni jambo lenye kuendelea, ambalo linahitaji jitihada kubwa. Hata tukijitahidi kadiri gani kufanya yaliyo mema, nyakati nyingine tunakosea katika mawazo, maneno, au matendo kwa sababu ya hali yetu ya dhambi.—Waroma 7:14-20; Yakobo 3:2.

7. Tunahitaji kuonaje vipingamizi tunavyokabili tunapojitahidi kufuatia uadilifu?

7 Tunahitaji kuonaje vipingamizi tunavyokabili tunapojitahidi kufuatia uadilifu? Bila shaka hatungetaka kupunguza uzito wa dhambi. Hata hivyo, hatupaswi kamwe kukata tamaa, na kuhisi kwamba hatufai kumtumikia Yehova kwa sababu ya kasoro zetu. Mungu wetu mwenye fadhili amefanya mipango ili kuwasamehe wale wanaotubu kikweli. Fikiria maneno haya yenye kutia moyo ya mtume Yohana: “Nawaandikia nyinyi mambo haya ili msifanye dhambi.” Kisha akataja jambo hili hakika: “Na bado, ikiwa yeyote afanya hasa dhambi [kwa sababu ya kurithi kutokamilika], tuna msaidiaji kwa Baba, Yesu Kristo.” (1 Yohana 2:1) Naam, Yehova ametoa dhabihu ya fidia ya Yesu ili tuweze kumtumikia kwa njia inayofaa licha ya hali yetu ya dhambi. Je, hilo halituchochei kujitahidi kabisa kumpendeza Yehova?

Habari Njema na Haki ya Mungu

8, 9. Kuhubiriwa kwa habari njema kunaonyeshaje haki ya Yehova?

8 Tunaweza kutenda haki—hata kuiga haki ya Mungu—kwa kushiriki kikamili katika kazi ya kuwahubiria wengine habari njema za Ufalme wa Mungu. Haki ya Yehova inahusianaje na habari njema?

9 Yehova hataharibu mfumo huu mwovu kabla onyo halijatolewa. Yesu alisema hivi alipotabiri kuhusu matukio ya siku za mwisho: “Katika mataifa yote lazima habari njema ihubiriwe kwanza.” (Marko 13:10; Mathayo 24:3) Neno “kwanza” linamaanisha kwamba kazi ya kuhubiri ulimwenguni pote itatangulia matukio mengine. Matukio hayo yatia ndani dhiki kubwa iliyotabiriwa, wakati ambapo waovu wataharibiwa ili ulimwengu mpya wenye uadilifu uwepo. (Mathayo 24:14, 21, 22) Bila shaka, hakuna mtu awaye yote anayeweza kudai kwamba Yehova anawaonea waovu. Kwa kuagiza onyo litolewe, anawapa waovu muda wa kutosha wa kubadili njia zao ili wasiangamizwe.—Yona 3:1-10.

Tunaonyesha haki ya Mungu tunapowahubiria wengine habari njema bila ubaguzi

10, 11. Tunaonyeshaje haki ya Mungu tunapohubiri habari njema?

10 Tunaonyeshaje haki ya Mungu tunapohubiri habari njema? Kwanza kabisa, inafaa tufanye yale tuwezayo ili kuwasaidia wengine wapate wokovu. Fikiria tena ule mfano wa kuokolewa kutoka kwenye meli inayozama. Bila shaka ukiwa salama kwenye mashua ya kuokolea, ungejitahidi kuwasaidia wengine ambao wangali baharini. Vivyo hivyo, tuna wajibu wa kuwasaidia wale ambao wangali wanatapatapa katika “bahari” ya ulimwengu huu mwovu. Ni kweli kwamba wengi hukataa ujumbe wetu. Lakini maadamu Yehova anaendelea kuwa mwenye subira, tuna wajibu wa kuwapa nafasi ya ‘kufikia toba’ na hivyo kuwa na tumaini la kupata wokovu.—2 Petro 3:9.

11 Tunapowahubiria watu wote tunaokutana nao habari njema, tunaonyesha haki katika njia nyingine muhimu sana: Kutoonyesha ubaguzi. Kumbuka kwamba “Mungu si mwenye ubaguzi, bali katika kila taifa mtu ambaye humhofu na kutenda uadilifu akubalika kwake.” (Matendo 10:34, 35) Tunaweza tu kuiga haki Yake kwa kutoonyesha ubaguzi. Badala yake, tunapaswa kuwahubiria wengine habari njema bila kujali kabila lao, cheo chao katika jamii, au hali yao ya kifedha. Hivyo, tunawapa watu wote nafasi ya kusikia na kukubali habari njema.—Waroma 10:11-13.

Jinsi Tunavyowatendea Wengine

12, 13. (a) Kwa nini hatupaswi kufanya haraka kuwahukumu wengine? (b) Shauri la Yesu la ‘kukoma kuhukumu’ na ‘kukoma kulaumu’ linamaanisha nini? (Ona pia kielezi-chini.)

12 Tunaweza pia kuonyesha haki kwa kuwatendea wengine jinsi Yehova anavyotutendea. Ni rahisi sana kuwahukumu wengine, kuchambua makosa yao na kutilia shaka nia yao. Lakini ni nani kati yetu angependa Yehova achambue nia yake na kasoro zake bila huruma? Yehova hatutendei hivyo. Mtunga-zaburi alisema hivi: “Kama wewe ungehesabu maovu, Ee Bwana, nani angesimama?” (Zaburi 130:3) Je, hatuthamini kwamba Mungu wetu mwenye haki na mwenye rehema hakazii fikira makosa yetu? (Zaburi 103:8-10) Hivyo basi, tunapaswa kuwatendeaje wengine?

13 Tukielewa kwamba haki ya Mungu ni yenye rehema, hatutafanya haraka kuwahukumu wengine katika mambo ambayo hayatuhusu au mambo yasiyo na maana sana. Katika Mahubiri yake ya Mlimani, Yesu alionya hivi: “Komeni kuhukumu ili msipate kuhukumiwa.” (Mathayo 7:1) Kulingana na simulizi la Luka, Yesu aliongezea hivi: “Komeni kulaumu, nanyi hamtalaumiwa kwa vyovyote.” * (Luka 6:37) Yesu alitambua kwamba wanadamu wasiokamilika wana mwelekeo wa kuhukumu-hukumu. Msikilizaji yeyote aliyekuwapo mwenye tabia ya kuhukumu-hukumu wengine vikali alipaswa kukoma kufanya hivyo.

14. Kwa nini tunapaswa ‘kukoma kuhukumu’ wengine?

14 Kwa nini ni lazima ‘tukome kuhukumu’ wengine? Kwanza, mamlaka yetu ina mipaka. Mwanafunzi Yakobo atukumbusha hivi: “Mmoja yuko ambaye ni mpaji-sheria na hakimu,” yaani, Yehova. Kisha Yakobo anauliza hivi waziwazi: “Wewe ni nani uwe ukihukumu jirani yako?” (Yakobo 4:12; Waroma 14:1-4) Isitoshe, ni rahisi sana kuwahukumu wengine isivyo haki kwa sababu sisi ni wenye dhambi. Mitazamo na mielekeo mbalimbali—kama vile ubaguzi, kuudhika, wivu, na kujiona kuwa mwadilifu—inaweza kupotosha maoni yetu juu ya wanadamu wengine. Hatutafanya haraka kutafuta makosa ya wengine ikiwa tutakumbuka kwamba hata sisi tuna udhaifu. Hatuwezi kusoma mioyo; wala hatuwezi kujua kikamili hali za wengine. Basi, sisi ni nani hata tuwatilie shaka waamini wenzetu au kuchambua jitihada zao za kumtumikia Mungu? Itakuwa vyema tukimwiga Yehova kwa kukazia fikira mambo mazuri ambayo ndugu na dada zetu wanafanya badala ya kutafuta tu kasoro zao.

15. Waabudu wa Yehova hawapaswi kamwe kutenda kwa njia gani na kutumia maneno ya aina gani, na kwa nini?

15 Vipi kuhusu watu wa familia yetu? Inasikitisha kwamba leo hukumu kali zaidi hutolewa nyumbani, mahali ambapo panapaswa kuwa na amani. Ni kawaida kusikia kuhusu waume, wake, au wazazi wakatili ambao huwatukana daima au kuwajeruhi watu wa familia yao. Lakini waabudu wa Mungu hawapaswi kamwe kutumia maneno makali, kufanya mzaha wenye kuumiza, au kuwajeruhi wengine. (Waefeso 4:29, 31; 5:33; 6:4) Shauri la Yesu la ‘kukoma kuhukumu’ na ‘kukoma kulaumu’ linapasa kufuatwa nyumbani pia. Kumbuka kwamba kuonyesha haki kunatia ndani kuwatendea wengine jinsi Yehova anavyotutendea. Na Mungu wetu hatutendei kamwe kwa ukali au kwa ukatili. Badala yake, yeye “ni mwenye wororo sana katika shauku” kwa wale wanaompenda. (Yakobo 5:11) Yeye ni mfano bora sana wa kuiga!

Wazee Wanaotumikia “kwa Haki”

16, 17. (a) Yehova anawatarajia wazee wafanye nini? (b) Ni hatua gani inayopasa kuchukuliwa mtenda-dhambi anapokataa kuonyesha toba ya kweli, na kwa nini?

16 Sote tuna wajibu wa kuonyesha haki, lakini wazee katika kutaniko la Kikristo wana wajibu wa pekee wa kufanya hivyo. Hebu ona maelezo ya kiunabii yaliyoandikwa na Isaya kuhusu “wakuu,” au wazee: “Tazama, mfalme atamiliki kwa haki, na wakuu watatawala kwa hukumu (“haki,” NW).” (Isaya 32:1) Naam, Yehova anawatarajia wazee watumikie kwa njia ya haki. Wanaweza kufanya hivyo jinsi gani?

17 Wanaume hao wenye sifa za ustahili wa kiroho wanajua kwamba ili kudumisha haki, au uadilifu, ni lazima wadumishe usafi kutanikoni. Nyakati nyingine, wazee wanalazimika kuwahukumu wale wanaotenda dhambi nzito. Wanapofanya hivyo, wanakumbuka kwamba Mungu huonyesha haki na rehema inapowezekana. Kwa hiyo, wanajaribu kumsaidia mtenda-dhambi aonyeshe toba. Lakini vipi ikiwa mtenda-dhambi anakataa kuonyesha toba ya kweli licha ya jitihada za kumsaidia? Neno la Yehova linaagiza kwamba hatua thabiti ya haki ichukuliwe: “Ondoeni yule mtu mwovu miongoni mwenu wenyewe.” Hilo lamaanisha kumtenga na ushirika wa kutaniko. (1 Wakorintho 5:11-13; 2 Yohana 9-11) Wazee wanahuzunika sana wanapolazimika kuchukua hatua hiyo, lakini wanatambua kwamba ni sharti wafanye hivyo ili kudumisha usafi wa kiadili na wa kiroho wa kutaniko. Hata hivyo, wanatumaini kwamba siku moja mtenda-dhambi huyo atarudiwa na fahamu na kurejea kutanikoni.—Luka 15:17, 18.

18. Wazee wanakumbuka nini wanapowashauri wengine kwa kutegemea Biblia?

18 Kutumikia kwa njia ya haki kunatia ndani pia kutoa shauri linalotegemea Biblia inapohitajika. Bila shaka, wazee hawajaribu kutafuta kasoro za wengine. Wala hawatumii kila nafasi wanayopata ili kutoa shauri. Lakini mwamini mwenzao anaweza ‘kuchukua hatua fulani isiyo ya kweli kabla ya yeye kuijua.’ Wazee ‘watajaribu kumrekebisha upya mtu wa namna hiyo katika roho ya upole’ huku wakikumbuka kwamba Mungu anatekeleza haki kwa kujali hisia za wengine wala si kwa ukatili. (Wagalatia 6:1) Kwa hiyo, wazee hawatamfokea mkosaji wala kumshutumu kwa maneno makali. Badala yake, mtu hutiwa moyo na shauri linalotolewa kwa njia ya upendo. Hata wanapotoa shauri la moja kwa moja linaloonyesha waziwazi matokeo ya kufuata mwenendo usiofaa, wazee wanakumbuka kwamba mwamini mwenzao aliyekosea ni kondoo wa kundi la Yehova. * (Luka 15:7) Shauri au karipio linapotolewa kwa njia ya upendo, yaelekea kwamba litamrekebisha mkosaji.

19. Wazee hufanya maamuzi gani, na maamuzi hayo yanapasa kutegemea nini?

19 Mara nyingi wazee hufanya maamuzi yanayowahusu waamini wenzao. Kwa mfano, pindi kwa pindi wazee hukutana ili kuona iwapo ndugu wengine kutanikoni wanastahili kupendekezwa kuwa wazee au watumishi wa huduma. Wazee wanajua umuhimu wa kutopendelea. Wanafuata matakwa ya Mungu wanapowapendekeza wengine, na hawategemei maoni yao binafsi. Hivyo, wanaamua “bila kuhukumu mapema, bila kufanya jambo lolote kulingana na mwelekeo wenye kuegemea upande.”—1 Timotheo 5:21.

20, 21. (a) Wazee wanajitahidi kuwa nini, na kwa nini? (b) Wazee wanawezaje kusaidia “nafsi zilizoshuka moyo”?

20 Wazee huonyesha haki ya Mungu katika njia nyinginezo pia. Baada ya kutabiri kwamba wazee wangetumikia “kwa haki,” Isaya aliongeza hivi: “Na mwanadamu atakuwa kama mahali pa kujificha na upepo, na mahali pa kujisitiri na dhoruba; kama mito ya maji mahali pakavu, kama kivuli cha mwamba mkubwa katika nchi yenye uchovu.” (Isaya 32:2) Basi, wazee hujitahidi kuwafariji na kuwaburudisha waabudu wenzao.

21 Wengi wanahitaji kutiwa moyo leo kwa sababu ya matatizo mengi ambayo yanavunja moyo. Wazee, mnawezaje kusaidia “nafsi zilizoshuka moyo”? (1 Wathesalonike 5:14) Wasikilizeni mkiwa na hisia-mwenzi. (Yakobo 1:19) Huenda wakataka kuzungumza na mtu fulani wanayemtumaini kuhusu “wasiwasi” ulio katika moyo wao. (Mithali 12:25, BHN) Wahakikishieni kwamba wanahitajiwa, wanathaminiwa, na wanapendwa na Yehova na vilevile na ndugu na dada zao. (1 Petro 1:22; 5:6, 7) Zaidi ya hayo, mnaweza kusali pamoja nao na kwa ajili yao. Wanaweza kupata faraja sana wanapomsikia mzee akisali kwa hisia sana kwa niaba yao. (Yakobo 5:14, 15) Mungu mwenye haki anathamini jitihada zenu za upendo za kuwasaidia walioshuka moyo.

Wazee huonyesha haki ya Yehova wanapowatia moyo wale walioshuka moyo

22. Tunaweza kuiga haki ya Yehova katika njia zipi, na matokeo yatakuwa nini?

22 Kwa kweli, tunamkaribia Yehova zaidi tunapoiga haki yake! Tunaonyesha haki ya Mungu tunapofuata kanuni zake za haki, tunapowahubiria wengine habari njema zinazookoa uhai, na tunapokazia fikira mambo mazuri ambayo wengine wanafanya badala ya kutafuta kasoro zao. Wazee, mnaonyesha haki ya Mungu mnapodumisha usafi wa kutaniko, mnapotoa shauri la Kimaandiko lenye kujenga, mnapofanya maamuzi bila kupendelea, na mnapowatia moyo wale walioshuka moyo. Akiwa mbinguni, Yehova anafurahi kama nini kuona watu wake wakijitahidi kabisa “kutenda haki” wanapotembea na Mungu wao!

^ fu. 13 Tafsiri nyingine husema “usihukumu” na “usilaumu.” Tafsiri hizo humaanisha “usianze kuhukumu” na “usianze kulaumu.” Hata hivyo, waandishi wa Biblia waliandika amri hizo katika njeo ya wakati uliopo ili kuonyesha kitendo kinachoendelea. Kwa hiyo, matendo hayo yalikuwa yakiendelea lakini yalihitaji kukoma kabisa.

^ fu. 18 Kwenye 2 Timotheo 4:2, Biblia inasema kwamba nyakati nyingine ni lazima wazee ‘wakaripie, wakemee, na kuhimiza kwa bidii.’ Neno la Kigiriki linalotafsiriwa “himiza kwa bidii” (pa·ra·ka·leʹo) linaweza kumaanisha “kutia moyo.” Neno jingine la Kigiriki linalohusiana nalo, pa·raʹkle·tos, linaweza kumaanisha wakili wa kisheria. Kwa hiyo, hata wakati wazee wanapokaripia kwa uthabiti, wanapaswa kuwa wasaidizi wa wale wanaohitaji msaada wa kiroho.