Hamia kwenye habari

Hamia kwenye yaliyomo

Sura ya 17

‘Lo! Kina cha Hekima ya Mungu!’

‘Lo! Kina cha Hekima ya Mungu!’

1, 2. Kusudi la Yehova kwa siku ya saba lilikuwa nini, na hekima Yake ilijaribiwaje mwanzoni mwa siku hiyo?

WAMEHARIBIKA! Wanadamu, upeo wa fahari ya siku ya sita ya uumbaji, walitumbukia ghafula katika hali mbaya yenye kusikitisha. Yehova alikuwa ametangaza kwamba “kila kitu alichokifanya,” kutia ndani mwanadamu, “ni chema sana.” (Mwanzo 1:31) Lakini mwanzoni mwa siku ya saba, Adamu na Hawa waliamua kumfuata Shetani katika uasi. Wakatumbukia katika dhambi, kutokamilika, na kifo.

2 Huenda ilionekana kwamba kusudi la Yehova kwa siku ya saba lilikuwa limeenda mrama kabisa. Siku hiyo, kama siku sita zilizotangulia, ingekuwa na urefu wa maelfu ya miaka. Yehova alikuwa ameitangaza kuwa takatifu. Hatimaye katika siku hiyo, dunia yote ingekuwa paradiso iliyojaa wanadamu wakamilifu. (Mwanzo 1:28; 2:3) Lakini kusudi hilo lingetimizwaje baada ya ule uasi ulioleta msiba? Mungu angechukua hatua gani? Wakati huo, hekima ya Yehova ilijaribiwa kwa njia isiyo na kifani—labda hilo ndilo lililokuwa jaribu kuu zaidi.

3, 4. (a) Kwa nini hatua ambayo Yehova alichukua baada ya uasi katika Edeni inaonyesha hekima yake yenye kutia kicho? (b) Kwa unyenyekevu, tunapaswa kukumbuka jambo gani hakika tunapojifunza juu ya hekima ya Yehova?

3 Yehova alichukua hatua mara moja. Aliwahukumu hao waasi katika Edeni, na wakati huohuo, akatangaza tumaini zuri la wakati ujao: alikusudia kukomesha taabu ambazo walikuwa wameanzisha tu. (Mwanzo 3:15) Kusudi la Yehova la muda mrefu lilianzia Edeni na kuendelea kwa maelfu ya miaka ambayo mwanadamu amekuwapo, na litaendelea hadi wakati ujao. Ni kusudi rahisi sana lakini lenye mambo mengi muhimu hivi kwamba msomaji wa Biblia anaweza kufurahia kujifunza kusudi hilo na kulitafakari maisha yake yote. Isitoshe, hapana shaka yoyote kwamba kusudi la Yehova litafanikiwa. Litakomesha kabisa uovu, dhambi, na kifo. Mungu anakusudia kuwafanya wanadamu waaminifu wawe wakamilifu. Mambo hayo yote yatatukia kabla ya siku ya saba kwisha. Yehova atakuwa ametimiza kusudi lake kuhusu dunia na wanadamu kwa wakati barabara licha ya vipingamizi vyote!

4 Hekima ya aina hiyo inatutia kicho, sivyo? Mtume Paulo alichochewa kuandika hivi: ‘Lo! kina cha hekima ya Mungu!’ (Waroma 11:33) Tunapojifunza wonyesho mbalimbali wa sifa hii ya Mungu, na tukumbuke kwa unyenyekevu jambo moja hakika—kwamba hatuwezi kamwe kufahamu kikamili hekima ya Yehova yenye kina sana. (Ayubu 26:14) Kwanza, hebu tufafanue sifa hii yenye kutia kicho.

Hekima ya Mungu Ni Nini?

5, 6. Kuna uhusiano gani kati ya ujuzi na hekima, na ujuzi wa Yehova ni mwingi kadiri gani?

5 Hekima si sawa na ujuzi. Kompyuta zinaweza kuhifadhi ujuzi mwingi sana, lakini hakuna mtu anayeweza kusema kwamba mashine hizo ni zenye hekima. Hata hivyo, ujuzi na hekima zinahusiana. (Mithali 10:14) Kwa mfano, kama ungehitaji shauri la hekima ili kutibu ugonjwa hatari, je, ungemwomba msaada mtu asiye na ujuzi wowote au mwenye ujuzi wa kijuu-juu tu wa tiba? La hasha! Kwa hiyo, ujuzi sahihi ni muhimu ili kuwa na hekima ya kweli.

6 Yehova ana ujuzi usio na kikomo. Akiwa “Mfalme wa umilele,” yeye peke yake ndiye ambaye ameishi milele. (Ufunuo 15:3) Na amejua mambo yote yaliyotukia kwa miaka hiyo yote. Biblia inasema hivi: “Hakuna kiumbe kisichokuwa dhahiri machoni pake, bali vitu vyote viko uchi na vikiwa vimefunuliwa wazi machoni pake ambaye kwake sisi tuna kutoa hesabu.” (Waebrania 4:13; Mithali 15:3) Akiwa Muumba, Yehova anajua kabisa vitu alivyoumba, naye ameona utendaji wote wa wanadamu tangu mwanzo. Yeye huchunguza moyo wa kila mwanadamu, na anaona kila jambo. (1 Mambo ya Nyakati 28:9) Anafurahi anapoona tukifanya maamuzi ya hekima maishani kwa sababu alituumba tukiwa na hiari. Akiwa “Msikiaji wa sala,” yeye husikiliza sala nyingi sana kwa wakati mmoja! (Zaburi 65:2, NW) Na bila shaka Yehova ana kumbukumbu kamilifu.

7, 8. Yehova anaonyeshaje ufahamu, utambuzi, na hekima?

7 Mbali na ujuzi, Yehova ana uwezo mwingine. Anaona jinsi mambo mbalimbali yanavyohusiana, na anatambua matokeo kamili ya mambo yote. Anachanganua mambo na kufanya maamuzi, anatofautisha mema na mabaya, mambo muhimu na yasiyo muhimu. Zaidi ya hayo, hachunguzi mambo kijuujuu tu bali anachunguza ndani ya moyo. (1 Samweli 16:7) Kwa hiyo, Yehova ana ufahamu na utambuzi, sifa ambazo ni bora zaidi ya ujuzi. Lakini hekima ni bora zaidi ya sifa hizo zote.

8 Hekima ni kutumia ujuzi, utambuzi, na ufahamu ili kutekeleza jambo fulani. Kwa kweli, baadhi ya maneno ya awali ya Biblia yaliyotafsiriwa “hekima” yanamaanisha kihalisi “kufanya kazi kwa matokeo” au “hekima inayofanya kazi kwa matokeo.” Kwa hiyo, hekima ya Yehova si ya kuwazia tu, bali inafanya kazi na ina matokeo. Sikuzote Yehova hufanya maamuzi bora kabisa kwa kutumia hekima na ufahamu wake usio na mipaka, na anatekeleza maamuzi hayo kwa njia bora kabisa. Hiyo ni hekima ya kweli! Yehova anaonyesha ukweli wa maneno haya ya Yesu: “Hekima huthibitishwa kuwa yenye uadilifu kwa kazi yayo.” (Mathayo 11:19) Kazi za Yehova ulimwenguni pote huthibitisha pasina shaka yoyote kwamba ana hekima.

Uthibitisho wa Hekima ya Mungu

9, 10. (a) Yehova ana hekima ya aina gani, naye ameionyeshaje? (b) Chembe huthibitishaje hekima ya Yehova?

9 Je, umewahi kustaajabia ustadi wa fundi anayetengeneza vifaa maridadi vinavyofanya kazi vizuri? Hekima hiyo inavutia sana. (Kutoka 31:1-3) Yehova mwenyewe ndiye chanzo hasa cha hekima hiyo. Mfalme Daudi alisema hivi kumhusu Yehova: “Nitakushukuru kwa kuwa nimeumbwa kwa jinsi ya ajabu ya kutisha. Matendo yako ni ya ajabu, na nafsi yangu yajua sana.” (Zaburi 139:14) Kwa kweli, kadiri tunavyojifunza kuhusu mwili wa mwanadamu, ndivyo tunavyozidi kutiwa kicho na hekima ya Yehova.

10 Kwa mfano: Uhai wako ulianza kwa chembe moja—mbegu ya mama yako iliungana na mbegu ya baba yako. Baada ya muda, chembe hiyo ilianza kugawanyika. Mwishowe mwili wako ukawa na chembe ndogo sana zipatazo trilioni 100. Chembe 10,000 hivi zenye ukubwa wa wastani zinaweza kutoshea kwenye kichwa kidogo sana cha pini. Lakini, kila chembe ina umbo tata sana. Chembe moja ni tata sana kushinda kiwanda au mashine yoyote iliyotengenezwa na mwanadamu. Wanasayansi wanasema kwamba chembe moja ni kama jiji lililozingirwa na ukuta—lenye malango yanayolindwa, lenye mfumo wa usafiri, mfumo wa mawasiliano, mitambo ya nguvu, viwanda, mifumo ya kuondoa na kusafisha maji machafu, walinzi, na hata kuna aina fulani ya makao makuu ya serikali katika kiini chake. Isitoshe, chembe inaweza kutengeneza chembe nyingine pacha kwa saa chache tu!

11, 12. (a) Ni nini kinachofanya chembe za kiini-tete kinachokua zigawanyike, na hilo linapatanaje na Zaburi 139:16? (b) Ubongo wa mwanadamu unaonyeshaje kwamba ‘tumeumbwa kwa jinsi ya ajabu’?

11 Bila shaka chembe zote hazifanani. Chembe za kiini-tete zinapoendelea kugawanyika, chembe mpya zinafanya kazi mbalimbali. Baadhi yake zitakuwa chembe za neva; nyingine zitakuwa chembe za mifupa, misuli, damu, au za macho. Utaratibu huo wa kugawanyika kwa chembe umehifadhiwa kiasili katika “maktaba” yenye ramani za chembe za urithi, DNA. Inastaajabisha kwamba Daudi aliongozwa kumwambia Yehova hivi: “Wewe uliniona hata kabla sijazaliwa, uliandika kila kitu kitabuni mwako.”—Zaburi 139:16, BHN.

12 Viungo fulani vya mwili ni tata kupindukia. Kwa mfano, fikiria ubongo wa mwanadamu. Baadhi ya watu wamesema kwamba ubongo ndicho kitu tata zaidi katika ulimwengu wote. Una chembe za neva zipatazo bilioni 100—idadi hiyo inakaribia idadi ya nyota katika kundi letu la nyota. Kila moja ya chembe hizo inaungana na maelfu ya chembe nyingine. Wanasayansi wanasema kwamba ubongo wa mwanadamu unaweza kuhifadhi habari zilizo katika maktaba zote ulimwenguni na kwamba uwezo wake haupimiki. Licha ya kuchunguza kwa miaka mingi sana ubongo ‘ulioumbwa kwa jinsi ya ajabu,’ wanasayansi wanakubali kwamba huenda wasifaulu kamwe kufahamu kikamili jinsi unavyofanya kazi.

13, 14. (a) Chungu na viumbe wengine wanaonyeshaje kwamba wana “akili nyingi sana,” na hilo linatufundisha nini kumhusu Muumba? (b) Kwa nini tunaweza kusema kwamba vitu vilivyoumbwa kama vile utando wa buibui vimefanywa “kwa hekima”?

13 Lakini wanadamu ni mojawapo tu ya mambo yanayoonyesha hekima ya Yehova ya uumbaji. Zaburi 104:24 yasema hivi: “Ee, BWANA, jinsi yalivyo mengi matendo yako! Kwa hekima umevifanya vyote pia. Dunia imejaa mali zako.” Kila kiumbe kinadhihirisha hekima ya Yehova. Kwa mfano, chungu ana “akili nyingi sana.” (Mithali 30:24) Kwa kweli, makundi ya chungu yana utaratibu wa hali ya juu sana. Makundi fulani ya chungu hutunza, hufuga, na kupata chakula kutoka kwa wadudu fulani kana kwamba ni mifugo. Chungu wengine ni kama wakulima, wanapanda “mimea” ya kuvu. Viumbe wengine wengi wanafanya mambo yenye kustaajabisha kwa kutumia hekima ya kisilika. Nzi wa kawaida huruka kwa njia za kustaajabisha sana ambazo ndege bora ya kisasa iliyobuniwa na mwanadamu haiwezi. Ndege wanaohama huongozwa na nyota, nguvu za sumaku za dunia, au aina fulani ya ramani iliyo akilini mwao. Wanabiolojia hujifunza kwa miaka mingi tabia tata za kisilika za viumbe hao. Mungu aliyeumba viumbe hao ana hekima iliyoje!

14 Wanasayansi wamejifunza mengi kutokana na hekima ya Yehova ya uumbaji. Hata kuna elimu fulani ya uhandisi inayojaribu kuiga ubuni wa maumbile inayoitwa biomimetics. Kwa mfano, labda umewahi kustaajabia umaridadi wa utando wa buibui. Lakini mhandisi anaona kwamba utando huo umebuniwa kwa njia ya pekee sana. Tando fulani nyembamba ni ngumu kuliko chuma, ni ngumu kushinda nyuzi za mavazi yasiyopenywa na risasi. Ni ngumu kadiri gani? Hebu wazia utando wa buibui uliorefushwa kufikia ukubwa wa wavu unaovutwa na mashua ya uvuvi. Utando wa aina hiyo ungeweza kusimamisha ndege ya abiria inayosafiri kwa kasi angani! Naam, Yehova amefanya vitu hivyo vyote “kwa hekima.”

Ni nani aliyeumba viumbe hawa ambao wana “akili nyingi sana”?

Hekima ya Vitu Visivyo Duniani

15, 16. (a) Nyota zinatoa uthibitisho gani kuhusu hekima ya Yehova? (b) Wadhifa wa Yehova akiwa Amiri Mkuu wa malaika wengi sana unaonyesha nini kuhusu hekima yake akiwa Msimamizi?

15 Hekima ya Yehova inaonekana wazi katika kazi zake ulimwenguni pote. Nyota ambazo tulizungumzia kwa undani katika Sura ya 5, hazijatapakaa kiholela-holela angani. Yehova amepanga nyota kwa njia maridadi sana katika magalaksi, kwa kutumia hekima yake ya “sheria za angani.” Magalaksi hayo yamepangwa katika makundi makubwa, ambayo huungana na kufanyiza makundi mengine makubwa hata zaidi. (Ayubu 38:33, The New Jerusalem Bible) Si ajabu Yehova anasema kwamba nyota zilizo mbinguni ni kama “jeshi”! (Isaya 40:26) Hata hivyo, kuna jeshi jingine ambalo linaonyesha wazi zaidi hekima ya Yehova.

16 Kama tulivyoona katika Sura ya 4, Mungu anaitwa “BWANA wa majeshi” kwa sababu ya wadhifa wake akiwa Amiri Mkuu wa jeshi la mamia ya mamilioni ya viumbe wa roho. Hilo lathibitisha nguvu za Yehova. Hata hivyo, hekima yake inahusikaje? Fikiria hili: Yehova na Yesu wanafanya kazi daima. (Yohana 5:17) Basi, ni jambo la kiakili kwamba hata malaika wanaomtumikia Mwenye Enzi Kuu wanafanya kazi daima. Na kumbuka kwamba malaika wana wadhifa wa juu kuliko mwanadamu, wana akili na nguvu nyingi sana. (Waebrania 1:7; 2:7) Lakini Yehova amewapa malaika hao wote kazi ya kutosha. Kwa furaha na uradhi, wamekuwa ‘wakitenda neno lake’ na ‘kufanya mapenzi yake,’ kwa mabilioni ya miaka. (Zaburi 103:20, 21) Msimamizi huyo ana hekima yenye kustaajabisha sana!

Yehova Ndiye “Mwenye Hekima Peke Yake”

17, 18. Kwa nini Biblia inasema kwamba Yehova ndiye “mwenye hekima peke yake,” na kwa nini hekima yake inapaswa kututia kicho?

17 Tukizingatia ushuhuda huo wote, haishangazi kwamba Biblia hutukuza hekima ya Yehova. Kwa mfano, inasema kwamba Yehova ndiye “mwenye hekima peke yake.” (Waroma 16:27) Ni Yehova peke yake aliye na hekima kamili. Ndiye chanzo cha hekima yote ya kweli. (Mithali 2:6) Ndiyo sababu Yesu, ajapokuwa na hekima nyingi kushinda viumbe wote wa Yehova, hakutegemea hekima yake mwenyewe bali alisema yale aliyoagizwa na Baba yake.—Yohana 12:48-50.

18 Angalia jinsi mtume Paulo alivyofafanua hekima ya pekee ya Yehova: “Lo! kina cha utajiri wa Mungu na hekima na ujuzi! Jinsi hukumu zake zisivyotafutikana na njia zake zapita uwezo wa kufuatilia!” (Waroma 11:33) Neno la mshangao, “Lo!” ambalo Paulo alitaja mwanzoni mwa mstari huo, lilionyesha hisia yenye nguvu—kicho cha hali ya juu sana. Neno la Kigiriki ambalo alitumia kurejezea “kina” linahusiana sana na neno “shimo lenye kina kirefu.” Kwa hiyo, maneno yake yanatokeza picha dhahiri sana akilini. Tunapotafakari hekima ya Yehova, ni kana kwamba tunatazama katika shimo kubwa sana lisilo na mwisho, shimo lenye kina kirefu sana hivi kwamba hatuwezi kamwe kufahamu ukubwa wake, sembuse kuweka mipaka au kuchora ramani yake kwa usahihi. (Zaburi 92:5) Wazo hilo linatunyenyekeza, sivyo?

19, 20. (a) Kwa nini tai ni mfano ufaao wa hekima ya Mungu? (b) Yehova ameonyeshaje kwamba ana uwezo wa kuona matukio ya wakati ujao!

19 Yehova ni “mwenye hekima peke yake” kwa njia nyingine: Ni yeye tu anayeweza kuona matukio ya wakati ujao. Kumbuka kwamba Yehova hutumia tai mwenye uwezo wa kuona mbali kuwa mfano wa hekima yake. Tai mkubwa anaweza kuwa na uzito wa kilogramu tano tu, lakini macho yake ni makubwa kuliko macho ya mtu mzima. Tai ana uwezo bora sana wa kuona. Ndege huyo anaweza kuona mnyama mdogo sana kutoka umbali wa mamia ya meta angani, au hata mamia ya kilometa! Pindi moja, Yehova alisema hivi kumhusu tai: ‘Macho yake huangalia toka mbali.’ (Ayubu 39:29) Vivyo hivyo, Yehova anaweza kuona ‘mbali’ sana. Anaweza kuona matukio ya wakati ujao!

20 Biblia ina mambo chungu nzima yanayothibitisha jambo hilo. Ina mamia ya unabii, au mambo yaliyoandikwa kabla hayajatukia. Biblia ilitabiri matokeo ya vita, kutokea na kuanguka kwa serikali kuu za ulimwengu, na hata mbinu za kivita ambazo zingetumiwa na maamiri wa jeshi. Nyakati nyingine ilitabiri matukio hayo mamia ya miaka kabla hayajatukia.—Isaya 44:25–45:4; Danieli 8:2-8, 20-22.

21, 22. (a) Kwa nini haifai kusema kwamba Yehova anajua maamuzi ambayo utafanya maishani? Toa mfano. (b) Tunajuaje kwamba Yehova hatumii hekima yake bila kujali hisia za watu?

21 Lakini je, hilo lamaanisha kwamba tayari Mungu anajua maamuzi ambayo utafanya maishani? Baadhi ya watu ambao wanafundisha kwamba maisha yetu yameamuliwa kimbele husisitiza hivyo. Hata hivyo, imani hiyo kwa kweli inadharau hekima ya Yehova, kwa kuwa inamaanisha kwamba hawezi kudhibiti uwezo wake wa kujua matukio ya wakati ujao. Kwa mfano: Kama ungekuwa mwimbaji mwenye sauti tamu sana, je, ungeimba tu kila wakati? Hilo ni wazo la kipumbavu! Vivyo hivyo, Yehova ana uwezo wa kujua matukio ya wakati ujao, lakini hatumii uwezo huo kila wakati. Akifanya hivyo huenda akaingilia uhuru wetu wa kuchagua. Uhuru huo ni zawadi yenye thamani ambayo Yehova hawezi kutunyima kamwe.—Kumbukumbu la Torati 30:19, 20.

22 Imani ya kwamba maisha yameamuliwa kimbele inasikitisha hata zaidi kwa sababu inadokeza kuwa hekima ya Yehova haijali hisia za watu, haiambatani na upendo, hisia-mwenzi, au huruma. Lakini hilo si kweli hata kidogo! Biblia inafundisha kwamba Yehova ni “mwenye hekima moyoni.” (Ayubu 9:4) Si kwamba ana moyo halisi, lakini mara nyingi Biblia hutumia neno hilo kumaanisha utu wa ndani kabisa, kutia ndani nia ya mtu na hisia kama vile upendo. Kwa hiyo, hekima ya Yehova, kama sifa zake nyingine, inaongozwa na upendo.—1 Yohana 4:8.

23. Hekima ya Yehova iliyo bora sana inapaswa kutuchochea kufanya nini?

23 Bila shaka, hekima ya Yehova inaweza kutumainika kabisa. Ni bora kuliko hekima yetu ndiposa Neno la Mungu linatuhimiza hivi kwa upendo: “Mtumaini BWANA kwa moyo wako wote, wala usizitegemee akili zako mwenyewe; katika njia zako zote mkiri yeye, naye atayanyosha mapito yako.” (Mithali 3:5, 6) Na tuchunguze kwa undani hekima ya Yehova ili tuweze kumkaribia zaidi Mungu wetu mwenye hekima kamili.