Hamia kwenye habari

Hamia kwenye yaliyomo

Sura ya 18

Hekima ya “Neno la Mungu”

Hekima ya “Neno la Mungu”

1, 2. Yehova ametuandikia “barua” gani, na kwa nini?

JE, UNAKUMBUKA mara ya mwisho ulipopokea barua kutoka kwa mpendwa wako anayeishi mbali sana? Kupokea barua yenye kugusa moyo kutoka kwa mtu tunayempenda ni mojawapo ya mambo yanayotufurahisha sana. Tunafurahi sana anapotujulisha hali yake, maisha yake, na mipango yake. Tunakuwa na uhusiano wa karibu na wapendwa wetu tunapowasiliana nao, hata kama wanaishi mbali.

2 Basi, hakuna jambo jingine lolote linaloweza kutufurahisha sana kama kupokea ujumbe ulioandikwa na Mungu tunayempenda. Tunaweza kusema kwamba Yehova ametuandikia “barua,” yaani, Neno lake, Biblia. Katika Biblia, anatueleza yeye ni nani, amefanya nini, anakusudia kufanya nini, na mambo mengine mengi. Yehova ametupatia Neno lake kwa sababu anataka tumkaribie. Mungu wetu mwenye hekima kamili alichagua njia bora ya kuwasiliana nasi. Biblia imeandikwa kwa njia inayoonyesha hekima isiyo na kifani, na ujumbe wake unaonyesha hekima hiyo pia.

Kwa Nini Aliandika Neno Lake?

3. Yehova alimpa Musa Sheria kwa njia gani?

3 Huenda watu fulani wakauliza, ‘Kwa nini Yehova hakuwasiliana na wanadamu kwa njia nyingine yenye kutokeza zaidi kama vile sauti kutoka mbinguni?’ Kwa kweli, nyakati nyingine Yehova aliongea kutoka mbinguni kupitia malaika. Kwa mfano, alifanya hivyo alipowapa Waisraeli Sheria. (Wagalatia 3:19) Sauti iliyotoka mbinguni ilikuwa yenye kutia kicho sana hivi kwamba Waisraeli walioshikwa na woga walimwomba Yehova asiwasiliane nao kwa njia hiyo bali awasiliane nao kupitia Musa. (Kutoka 20:18-20) Kwa hiyo, Musa alipewa Sheria yenye amri zipatazo 600, kwa njia ya mdomo, neno kwa neno.

4. Eleza kwa nini kupitisha sheria za Mungu kwa njia ya mdomo hakungetegemeka.

4 Vipi kama Sheria haingaliandikwa? Je, Musa angaliweza kukumbuka vizuri kila neno la Sheria hiyo yenye mambo mengi, kisha aiwasilishe kwa taifa hilo bila kukosea? Vipi watu wa vizazi vijavyo? Je, wangehitaji kutegemea tu yale waliyoambiwa? Kupitisha sheria za Mungu kwa njia ya mdomo hakungetegemeka. Wazia jambo ambalo linaweza kutukia iwapo utamwambia mtu mmoja hadithi fulani kisha ipitishwe kutoka kwa mtu mmoja hadi mwingine kwenye mlolongo wa watu wengi. Yaelekea kwamba hadithi ambayo itamfikia mtu wa mwisho katika mlolongo huo itakuwa imebadilika kabisa. Sheria ya Mungu haikukabili hatari hiyo.

5, 6. Yehova alimwagiza Musa afanye nini kuhusiana na maneno Yake, na kwa nini tunafaidika kuwa na Neno la Yehova lililoandikwa?

5 Kwa hekima Yehova aliamua maneno yake yaandikwe. Alimwagiza Musa hivi: “Andika maneno haya; kwa kuwa mimi nimefanya agano nawe, na pamoja na Israeli, kwa mujibu wa maneno haya.” (Kutoka 34:27) Kwa hiyo, Biblia ikaanza kuandikwa mnamo mwaka wa 1513 K.W.K. Kwa miaka 1,610 iliyofuata, Yehova ‘alisema katika vipindi vingi na katika njia nyingi na’ wanadamu 40 hivi ambao waliandika Biblia. (Waebrania 1:1) Ili kuhifadhi Maandiko hayo, wanakili wenye bidii walifanyiza kwa uangalifu mkubwa nakala sahihi.—Ezra 7:6; Zaburi 45:1.

Yehova ametubariki kwelikweli kwa kuwasiliana nasi kupitia maandiko. Je, umewahi kupokea barua uliyothamini sana—labda kwa sababu ilikupa faraja uliyohitaji sana—hivi kwamba uliitunza na kuisoma tena na tena? Ndivyo ilivyo na “barua” ambayo Yehova ametuandikia. Kwa sababu Yehova aliandika maneno yake, tunaweza kuyasoma kwa ukawaida na kuyatafakari. (Zaburi 1:2) Tunaweza kupokea “faraja kutokana na Maandiko” wakati wowote tunapoihitaji.—Waroma 15:4.

Kwa Nini AlitumiaWanadamu Kuliandika?

7. Yehova alionyeshaje hekima kwa kuwatumia wanadamu kuandika Neno lake?

7 Yehova alionyesha hekima kwa kuwatumia wanadamu kuandika Neno lake. Hebu fikiria: Kama Yehova angalitumia malaika kuandika Biblia, je, ingalivutia kwa njia ileile? Kwa kweli, malaika wangeeleza jinsi Yehova alivyo kulingana na maoni yao yaliyotukuka, wangeeleza jinsi wanavyojitoa kwake, na kuandika kuhusu wanadamu waliomtumikia Mungu kwa uaminifu. Lakini je, tungeweza kweli kuelewa maoni ya viumbe wakamilifu wa roho, ambao wana ujuzi, ufahamu, na uwezo wa hali ya juu kuliko sisi?—Waebrania 2:6, 7.

“Andiko lote limepuliziwa na Mungu”

8. Waandishi wa Biblia waliruhusiwa kutumia akili zao jinsi gani? (Ona pia kielezi-chini.)

8 Kwa kuwatumia wanadamu kuandika Neno lake, Yehova alitupatia kile tunachohitaji—kitabu ambacho ‘kimepuliziwa na Mungu’ lakini kinachozingatia hali ya binadamu. (2 Timotheo 3:16) Alifanyaje hivyo? Mara nyingi, inaonekana kwamba aliwaruhusu waandishi watumie akili zao katika kuchagua “maneno yapendezayo, na yale yaliyoandikwa kwa unyofu, yaani, maneno ya kweli.” (Mhubiri 12:10, 11) Ndiyo sababu Biblia imeandikwa kwa njia mbalimbali; njia hizo hutegemea malezi na utu wa kila mwandishi. * Lakini, wanadamu hao “walisema kutoka kwa Mungu walipokuwa wakichukuliwa na roho takatifu.” (2 Petro 1:21) Kwa hiyo, Biblia ni “neno la Mungu.”—1 Wathesalonike 2:13.

9, 10. Kwa nini kutumia wanadamu kuiandika Biblia kunaifanya ipendeze na kuvutia zaidi?

9 Biblia inapendeza na kuvutia sana kwa sababu Mungu alitumia wanadamu kuiandika. Waandishi wa Biblia walikuwa wanadamu wenye hisia kama zetu. Wakiwa wanadamu wasiokamilika, walipata majaribu na mifadhaiko kama yetu. Nyakati nyingine, roho ya Yehova iliwaongoza kuandika kuhusu hisia zao na matatizo yaliyowapata. (2 Wakorintho 12:7-10) Kwa hiyo, waliandika kama wahusika, maneno ambayo hakuna malaika angeweza kuandika.

10 Kwa mfano, fikiria Mfalme Daudi wa Israeli. Baada ya kufanya dhambi nzito sana, Daudi alitunga zaburi ambayo inaeleza mambo yaliyokuwa moyoni mwake, na jinsi alivyomwomba Mungu msamaha. Aliandika hivi: ‘Unioshe kabisa na uovu wangu, unitakase dhambi zangu. Maana nimejua mimi makosa yangu na dhambi yangu i mbele yangu daima. Tazama, mimi naliumbwa katika hali ya uovu; mama yangu alinichukua mimba hatiani. Usinitenge na uso wako, wala roho yako takatifu usiniondolee. Dhabihu za Mungu ni roho iliyovunjika; moyo uliovunjika na kupondeka, Ee Mungu hutaudharau.’ (Zaburi 51:2, 3, 5, 11, 17) Je, huguswi moyo na uchungu wa mwandishi huyo? Ni mwanadamu asiyekamilika tu ndiye angeweza kuandika maneno hayo yenye kugusa moyo, sivyo?

Kwa Nini Aandike Kitabu Kinachohusu Watu?

11. Ni masimulizi gani halisi yameandikwa katika Biblia ili ‘kutufunza’?

11 Kuna jambo jingine linalofanya Biblia ivutie. Kwa kadiri kubwa, ni kitabu kinachohusu watu—watu halisi, wale waliomtumikia Mungu na wale ambao hawakumtumikia. Tunasoma kuhusu maisha yao, magumu yao, na shangwe yao. Tunaona matokeo ya maamuzi waliyofanya maishani. Masimulizi hayo yaliandikwa ili ‘kutufunza.’ (Waroma 15:4) Kupitia masimulizi hayo halisi, Yehova anatufundisha kwa njia ambazo zinatugusa mioyo. Fikiria mifano kadhaa.

12. Masimulizi ya Biblia kuhusu wanadamu wasio waaminifu yanatusaidiaje?

12 Biblia inatuambia kuhusu wanadamu wasio waaminifu, na hata waovu na mambo yaliyowapata. Masimulizi hayo yanaonyesha jinsi watu walivyoonyesha sifa zisizofaa, na hilo linatusaidia kuelewa sifa hizo. Kwa mfano, hakuna amri inayoweza kukazia kikiki ubaya wa kutokuwa mwaminifu kuliko mfano halisi wa Yudasi akipanga njama ya kumsaliti Yesu, sivyo? (Mathayo 26:14-16, 46-50; 27:3-10) Masimulizi kama hayo hugusa sana mioyo yetu, na kutusaidia kutambua na kuzitupilia mbali sifa zinazochukiza.

13. Biblia inatusaidiaje kuelewa sifa zinazofaa?

13 Biblia pia inasimulia kuhusu watumishi wengi wa Mungu waliokuwa waaminifu. Tunasoma kuhusu ujitoaji wao na uaminifu wao. Tunasoma kuhusu watu wenye sifa ambazo tunahitaji kukuza ili kumkaribia Mungu. Kwa mfano, fikiria sifa ya imani. Biblia inatuambia imani ni nini na kwa nini tunahitaji kuwa nayo ili kumpendeza Mungu. (Waebrania 11:1, 6) Lakini Biblia pia inaeleza mifano halisi ya watu waliokuwa na imani. Fikiria imani ambayo Abrahamu alionyesha alipojaribu kumtoa Isaka. (Mwanzo, sura ya 22; Waebrania 11:17-19) Masimulizi kama hayo yanatusaidia kuthamini na kuelewa vizuri zaidi maana ya neno “imani.” Ni hekima iliyoje kwamba Yehova, mbali na kutuhimiza tukuze sifa zinazofaa anatuonyesha mifano ya watu waliokuwa na sifa hizo!

14, 15. Biblia inatuambia nini kuhusu mwanamke fulani aliyekuja hekaluni, na simulizi hilo linatufundisha nini kumhusu Yehova?

14 Masimulizi halisi yaliyo katika Biblia mara nyingi yanatufundisha kuhusu utu wa Yehova. Fikiria simulizi la mwanamke fulani ambaye Yesu alimwona hekaluni. Alipokuwa ameketi karibu na masanduku ya hazina, Yesu aliangalia jinsi watu walivyokuwa wakitumbukiza michango yao humo. Matajiri wengi walikuja na kutumbukiza “kutokana na ziada yao.” Lakini Yesu alimtazama sana mjane mmoja maskini. Mjane huyo alitoa mchango wa “sarafu ndogo mbili, ambazo zina thamani ndogo sana.” * Alitoa fedha zote alizokuwa nazo. Yesu, ambaye alidhihirisha kikamili maoni ya Yehova, alisema hivi: ‘Mjane huyu maskini alitumbukiza ndani zaidi ya wote wale waliokuwa wakitumbukiza fedha ndani ya masanduku ya hazina.’ Kulingana na maneno hayo, alitumbukiza fedha nyingi kuliko jumla ya fedha zilizotolewa na watu wengine wote.—Marko 12:41-44; Luka 21:1-4; Yohana 8:28.

15 Je, haishangazi kwamba kati ya watu wote waliokuja hekaluni siku hiyo, ni mjane huyo peke yake ndiye aliyetajwa katika Biblia? Kupitia mfano huo, Yehova anatufundisha kwamba yeye ni Mungu anayethamini mambo tunayofanya. Anakubali kwa furaha michango tunayomtolea kwa nafsi yetu yote, pasipo kuilinganisha na michango inayotolewa na wengine. Bila shaka Yehova ametumia njia bora sana kutufundisha ukweli huo wenye kutia moyo!

Mambo Ambayo Biblia Haitaji

16, 17. Yehova anaonyeshaje hekima yake kwa kutoandika mambo fulani katika Neno lake?

16 Unapomwandikia mpendwa wako barua, huwezi kuandika kila jambo. Kwa hiyo, unachagua kwa busara mambo ya kuandika. Vivyo hivyo, Yehova alitaja watu fulani na matukio fulani katika Neno lake. Lakini Biblia haielezi kinagaubaga kila jambo kuhusiana na masimulizi hayo. (Yohana 21:25) Kwa mfano, Biblia inapozungumzia hukumu ya Mungu, haijibu kila swali tulilo nalo kuhusu hukumu hiyo. Yehova anaonyesha pia hekima yake kwa kutoandika mambo fulani katika Neno lake. Jinsi gani?

17 Biblia imeandikwa kwa njia inayokusudiwa kutambua mambo yaliyo moyoni mwetu. Andiko la Waebrania 4:12 lasema hivi: “Neno [au, ujumbe] la Mungu liko hai na hukazia nguvu na ni lenye makali zaidi kuliko upanga wowote wenye makali kuwili na hudunga hata kufikia kugawanya nafsi na roho . . . na ni lenye kuweza kufahamu fikira na makusudio ya moyo.” Ujumbe wa Biblia hupenya ndani kabisa, na kufunua mawazo yetu na nia yetu halisi. Wale wanaoisoma wakiwa na nia ya kuichambua mara nyingi wanakwazwa wanapopata masimulizi ambayo hayana habari ya kutosha kuwaridhisha. Watu wa aina hiyo huenda hata wakawa na shaka kwamba Yehova ni mwenye upendo, hekima na haki.

18, 19. (a) Kwa nini hatupaswi kutatanika wakati simulizi fulani la Biblia linazusha maswali ambayo hatuwezi kujibu mara moja? (b) Tunahitaji kufanya nini ili kufahamu Neno la Mungu, na jambo hilo linaonyeshaje hekima kuu ya Yehova?

18 Kwa upande mwingine, tunapojifunza Biblia kwa uangalifu na kwa unyofu, tunapata kumjua Yehova kama anavyofafanuliwa katika Biblia nzima. Kwa hiyo, hatutataniki wakati simulizi fulani linazusha maswali ambayo hatuwezi kupata jibu mara moja. Kwa mfano: Tunapounganisha vipande vya mchezo wa chemshabongo, huenda tusipate kipande fulani mwanzoni au huenda tusielewe jinsi kipande fulani kinavyoungana na vingine. Lakini, labda tumeunganisha vipande vya kutosha kutusaidia kuelewa jinsi picha kamili itakavyokuwa. Vivyo hivyo, tunapojifunza Biblia, pole kwa pole tunajifunza jinsi Yehova Mungu alivyo, na hatimaye tunapata kumjua vizuri kabisa. Hata ikiwa mwanzoni hatuelewi simulizi fulani au hatuoni jinsi linavyopatana na utu wa Mungu, tayari tumejifunza kupitia funzo letu la Biblia mambo mengi sana ya kutusadikisha kwamba bila shaka Yehova ni Mungu mwenye upendo, asiyependelea, na mwenye haki.

19 Basi, ili kufahamu Neno la Mungu, ni lazima tusome na kujifunza Neno hilo kwa moyo mnyofu bila kushikilia mno maoni yetu. Jambo hilo linaonyesha hekima kuu ya Yehova, sivyo? Wanadamu wenye akili nyingi wanaweza kuandika vitabu ambavyo ni watu “wenye hekima na wenye akili” tu wanaovielewa. Lakini ni Mungu tu anayeweza kuandika kitabu ambacho watu wenye mwelekeo unaofaa tu wanaweza kukielewa!—Mathayo 11:25.

Kitabu Chenye “Hekima Kamili”

20. Kwa nini ni Yehova peke yake anayeweza kutuambia njia bora ya maisha, na Biblia ina nini kinachoweza kutusaidia?

20 Katika Neno lake, Yehova hutuambia njia bora ya maisha. Anajua mahitaji yetu vizuri zaidi kuliko tunavyoyajua kwa sababu yeye ni Muumba wetu. Na sikuzote wanadamu wamekuwa na mahitaji yaleyale ya msingi, kama vile, tamaa ya kupendwa, kuwa na furaha, na kuwa na mahusiano mazuri. Biblia ina “hekima kamili” ambayo inaweza kutusaidia kuwa na kusudi maishani. (Mithali 2:7) Kila sehemu ya kitabu hiki ina sura ambayo inaonyesha jinsi tunavyoweza kutumia shauri la Biblia lenye hekima. Lakini hebu tuone mfano mmoja tu.

21-23. Ni mashauri gani yenye hekima yanayoweza kutusaidia kuepuka kufungia hasira na kinyongo moyoni?

21 Je, umegundua kwamba watu ambao wanafungia uchungu na kinyongo moyoni mara nyingi hujiumiza wenyewe? Kinyongo humlemea sana mtu. Tunapofungia kinyongo moyoni, tunajawa na mawazo, na tunakosa utulivu na shangwe. Uchunguzi wa kisayansi unadokeza kwamba kufungia hasira moyoni kunaweza kuongeza uwezekano wa kupata ugonjwa wa moyo na magonjwa mengine mengi ya kudumu. Miaka mingi kabla ya uchunguzi huo wa kisayansi, Biblia ilisema hivi kwa hekima: “Ukomeshe hasira, uache ghadhabu.” (Zaburi 37:8) Lakini tunaweza kufanyaje hivyo?

22 Neno la Mungu linatoa shauri hili la hekima: “Busara ya mtu huiahirisha hasira yake; nayo ni fahari yake kusamehe makosa.” (Mithali 19:11) Busara ni uwezo wa kuchanganua jambo kwa undani zaidi, kutambua sababu zisizoonekana wazi. Busara hutokeza ufahamu, kwa kuwa inaweza kutusaidia kutambua sababu iliyomfanya mtu mwingine aseme au kutenda kwa njia fulani. Kujitahidi kuelewa nia yake halisi, hisia zake, na hali zake kwaweza kutusaidia kuondoa mawazo au hisia zozote mbaya tulizo nazo kumwelekea.

23 Biblia ina shauri hivi tena: “Endeleeni kuchukuliana mtu na mwenzake na kusameheana kwa hiari mtu na mwenzake.” (Wakolosai 3:13) Usemi “endeleeni kuchukuliana mtu na mwenzake” unadokeza hali ya kuwastahimili wengine, kuvumilia sifa ambazo huenda zinatuudhi. Ustahimilivu wa aina hiyo unaweza kutusaidia kuepuka kufungia kinyongo moyoni kwa sababu ya mambo madogo-madogo. Neno “kusameheana” lamaanisha kuondoa kabisa kinyongo. Mungu wetu mwenye hekima anajua kwamba tunahitaji kuwasamehe wengine kunapokuwa na sababu nzuri ya kufanya hivyo. Tunapowasamehe wengine hatuwafaidi tu wale waliotukosea bali pia sisi wenyewe tunakuwa na amani ya akilini na ya moyoni. (Luka 17:3, 4) Neno la Mungu lina hekima iliyoje!

24. Inakuwaje tunapotumia hekima ya Mungu maishani?

24 Yehova alitaka kuwasiliana nasi kwa sababu ya upendo wake usio na kifani. Alichagua njia bora sana—“barua” iliyoandikwa na wanadamu walioongozwa na roho takatifu. Ndiyo sababu Biblia ina hekima ya Yehova mwenyewe. Hekima hiyo ni “amini sana.” (Zaburi 93:5) Kadiri tunavyotumia hekima hiyo maishani, na kadiri tunavyowafundisha wengine hekima hiyo, ndivyo tunavyozidi kumkaribia Mungu wetu mwenye hekima kamili. Katika sura inayofuata, tutazungumzia mfano mwingine wenye kutokeza wa hekima ya Yehova ya kuona matukio ya wakati ujao: uwezo wake wa kutabiri matukio ya wakati ujao na kutimiza kusudi lake.

^ fu. 8 Kwa mfano, Daudi, aliyekuwa mchungaji, anatumia mifano inayohusiana na ufugaji wa wanyama. (Zaburi 23) Mathayo, ambaye alikuwa mtoza-kodi hapo awali, mara nyingi anataja tarakimu na thamani ya fedha. (Mathayo 17:27; 26:15; 27:3) Luka, ambaye alikuwa daktari, anatumia maneno yanayohusiana na kazi yake ya tiba.—Luka 4:38; 14:2; 16:20.

^ fu. 14 Kila moja ya sarafu hizo iliitwa leptoni. Hiyo ndiyo iliyokuwa sarafu ya Kiyahudi yenye thamani ndogo zaidi wakati huo. Lepta mbili zilikuwa sawa na thamani ya 1/64 ya mshahara wa siku moja. Sarafu mbili hata hazikutosha kununua shore mmoja. Shore alikuwa ndege mwenye gharama ya chini sana aliyeliwa na watu maskini.