Hamia kwenye habari

Hamia kwenye yaliyomo

Sura ya 19

“Hekima ya Mungu Katika Siri Takatifu”

“Hekima ya Mungu Katika Siri Takatifu”

1, 2. Tunapaswa kupendezwa na ‘siri gani takatifu,’ na kwa nini?

SIRI! Mara nyingi wanadamu hushindwa kuficha siri, kwa sababu zinavutia na kustaajabisha. Hata hivyo, Biblia inasema hivi: “Ni utukufu wa Mungu kuficha jambo.” (Mithali 25:2) Naam, akiwa Muumba na Mtawala Mwenye Enzi Kuu, Yehova ana haki ya kuweka mambo fulani yakiwa siri kwa wanadamu hadi wakati wake wa kuyafunua unapowadia.

2 Lakini, kuna siri moja yenye kuvutia na kustaajabisha ambayo Yehova amefunua katika Neno lake. Inaitwa “siri takatifu ya mapenzi [ya Mungu].” (Waefeso 1:9) Kujifunza kuhusu siri hiyo si jambo la kufurahisha tu. Kujua siri hiyo kunaweza kukusaidia upate wokovu na kufahamu kidogo hekima ya Yehova isiyo na kifani.

Siri Takatifu Yafunuliwa Hatua kwa Hatua

3, 4. Unabii wa Mwanzo 3:15 ulitoaje tumaini, na ulikuwa na fumbo gani, au ‘siri gani takatifu’?

3 Adamu na Hawa walipofanya dhambi, huenda ilionekana kana kwamba kusudi la Yehova la wanadamu wakamilifu kuishi katika paradiso duniani lilikuwa limezuiwa. Lakini Mungu alishughulikia tatizo hilo mara moja. Alisema hivi: “Nitaweka uadui kati yako na huyo mwanamke, na kati ya uzao wako na uzao wake; huo utakuponda kichwa, na wewe utamponda kisigino.”—Mwanzo 3:15.

4 Maneno hayo yalikuwa ya kifumbo na yasiyoeleweka. Ni mwanamke yupi huyo? Nyoka alikuwa nani? Ni nani angekuwa “uzao” ambao ungemponda nyoka kichwa? Adamu na Hawa waliweza kukisia-kisia tu. Hata hivyo, maneno hayo ya Mungu yalimpa tumaini mzao yeyote mwaminifu wa wenzi hao walioasi. Uadilifu ungeshinda. Kusudi la Yehova lingetimizwa. Lakini jinsi gani? Ahaa, hilo lilikuwa fumbo! Biblia inasema kwamba fumbo hilo ni “hekima ya Mungu katika siri takatifu, hekima iliyofichwa.”—1 Wakorintho 2:7.

5. Toa mfano ambao unaonyesha kwa nini Yehova alifunua siri yake hatua kwa hatua.

5 Hatimaye, Yehova, “afunuaye siri,” angefunua kila jambo kuhusu utimizo wa siri hiyo. (Danieli 2:28) Lakini angeifunua siri hiyo polepole, hatua kwa hatua. Kwa mfano, fikiria jinsi ambavyo baba mwenye upendo anavyomjibu mvulana wake mdogo anayemwuliza, “Baba, nilitoka wapi?” Baba mwenye hekima anamwambia mvulana huyo mdogo habari chache tu ambazo anaweza kuelewa. Kadiri mvulana huyo anavyokua, ndivyo baba anavyomweleza habari zaidi. Vivyo hivyo, Yehova huamua wakati ambapo watu wake wanaweza kuelewa unabii kuhusu mapenzi yake na kusudi lake.—Mithali 4:18; Danieli 12:4.

6. (a) Agano au mapatano hutimiza kusudi gani? (b) Kwa nini inavutia kwamba Yehova hufanya maagano na wanadamu?

6 Yehova alifunuaje siri hizo? Alifunua mambo mengi kwa kufanya maagano au mapatano kadhaa. Huenda wakati fulani umewahi kufanya mapatano—labda ya kununua nyumba au ya kuomba mkopo au ya kumkopesha mtu pesa. Mapatano hayo yalithibitisha kisheria kwamba masharti mliyokubaliana yatatimizwa. Lakini kwa nini Yehova alihitaji kufanya maagano rasmi au mapatano na wanadamu? Bila shaka, neno lake ni uthibitisho wa kutosha wa kwamba ahadi zake zitatimia. Hiyo ni kweli, lakini kwa fadhili Mungu amethibitisha neno lake katika visa kadhaa kwa kufanya maagano ya kisheria. Maagano hayo yenye masharti ya kisheria hutupatia sisi wanadamu wasiokamilika msingi thabiti zaidi wa kutumaini ahadi za Yehova.—Waebrania 6:16-18.

Agano Pamoja na Abrahamu

7, 8. (a) Yehova alifanya agano gani na Abrahamu, nalo lilifunua nini kuhusu ile siri takatifu? (b) Yehova alifunuaje hatua kwa hatua ukoo wa Mzao aliyeahidiwa?

7 Zaidi ya miaka elfu mbili baada ya mwanadamu kufukuzwa kutoka Paradiso, Yehova alimwambia hivi mtumishi wake mwaminifu Abrahamu: “Katika kuzidisha, nitauzidisha uzao wako kama nyota za mbinguni . . . na katika uzao wako mataifa yote ya dunia watajibarikia; kwa sababu umetii sauti yangu.” (Mwanzo 22:17, 18) Hiyo haikuwa ahadi tu; Yehova aliitoa kama agano la kisheria na kuithibitisha kwa kiapo chake kisichoweza kuvunjwa. (Mwanzo 17:1, 2; Waebrania 6:13-15) Ni jambo la pekee kama nini kwamba Bwana Mwenye Enzi Kuu kwa kweli alifanya agano la kuwabariki wanadamu!

“Nitauzidisha uzao wako kama nyota za mbinguni”

8 Agano la Kiabrahamu lilifunua kwamba Mzao aliyeahidiwa angekuwa mwanadamu, kwa sababu angekuwa mzao wa Abrahamu. Lakini angekuwa nani? Baada ya muda, Yehova alifunua kwamba Isaka, mmoja wa wana wa Abrahamu angekuwa babu ya Mzao huyo. Yakobo ndiye aliyechaguliwa kati ya wana wawili wa Isaka. (Mwanzo 21:12; 28:13, 14) Baadaye, Yakobo alimwambia mmoja wa wanaye 12 maneno haya ya kiunabii: “Fimbo ya enzi haitaondoka katika Yuda, wala mfanya sheria kati ya miguu yake, hata atakapokuja Yeye, mwenye milki, ambaye mataifa watamtii.” (Mwanzo 49:10) Basi ikawa wazi kwamba Mzao huyo angekuwa mfalme kutoka kwa kabila la Yuda!

Agano Pamoja na Israeli

9, 10. (a) Yehova alifanya agano gani na taifa la Israeli, na agano hilo lililinda nini? (b) Sheria ilionyeshaje kwamba wanadamu wanahitaji fidia?

9 Mwaka wa 1513 K.W.K., Yehova alifanya mpango ambao ungefunua mambo mengi zaidi kuhusu ile siri takatifu. Alifanya agano na wazao wa Abrahamu, taifa la Israeli. Ingawa agano hilo la Sheria ya Musa halitumiki leo, lilikuwa sehemu muhimu sana ya kusudi la Yehova la kutoa Mzao aliyeahidiwa. Jinsi gani? Fikiria njia hizi tatu. Kwanza, Sheria hiyo ilikuwa kama ukuta wenye kulinda. (Waefeso 2:14) Sheria zake adilifu ziliwatenganisha Wayahudi na wasio Wayahudi. Kwa hiyo, Sheria ilisaidia kulinda ukoo wa Mzao aliyeahidiwa. Kwa sababu ya ulinzi huo, taifa hilo bado lilikuwapo wakati wa Mungu ulipowadia wa Mesiya kuzaliwa katika kabila la Yuda.

10 Pili, Sheria ilionyesha waziwazi kwamba wanadamu wanahitaji fidia. Sheria hiyo kamilifu ilionyesha kwamba wanadamu wenye dhambi hawawezi kuitii kikamili. Kwa hiyo, ilikusudiwa “kufanya mikiuko-sheria iwe dhahiri, mpaka mbegu iwasili ambayo kwayo ahadi ilikuwa imetolewa.” (Wagalatia 3:19) Sheria hiyo ilikuwa na mipango ya kusamehe dhambi kwa muda kupitia dhabihu za wanyama. Lakini, dhabihu hizo ziliashiria dhabihu ya fidia ya Kristo, kwa kuwa kama Paulo alivyoandika, “haiwezekani damu ya mafahali na ya mbuzi kuziondolea mbali dhambi.” (Waebrania 10:1-4) Kwa hiyo, kwa Wayahudi waaminifu, agano hilo lilikuwa ‘mfunzi aliyeongoza kwa Kristo.’—Wagalatia 3:24.

11. Agano la Sheria liliandalia Israeli tumaini gani tukufu, lakini kwa nini karibu taifa hilo lote lilipoteza tumaini hilo?

11 Tatu, agano hilo liliandalia taifa la Israeli tumaini tukufu. Yehova aliwaambia kwamba ikiwa wangetii agano hilo, wangekuwa “ufalme wa makuhani, na taifa takatifu.” (Kutoka 19:5, 6) Hatimaye, Waisraeli wa asili wakaja kuwa washiriki wa kwanza wa ufalme wa makuhani wa kimbingu. Hata hivyo, karibu taifa lote la Israeli liliasi agano la Sheria, likamkataa yule Mzao wa Kimesiya, na likapoteza tumaini hilo. Basi, ni nani wangekamilisha ufalme wa makuhani? Na taifa hilo lililobarikiwa lingekuwa na uhusiano gani na Mzao aliyeahidiwa? Mambo hayo ya siri takatifu yangefunuliwa katika wakati barabara wa Mungu.

Agano la Ufalme la Daudi

12. Yehova alifanya agano jipi na Daudi, na lilifunua mambo gani kuhusu siri takatifu ya Mungu?

12 Katika karne ya 11 K.W.K., Yehova alifunua mambo zaidi kuhusu ile siri takatifu alipofanya agano jingine. Alimwahidi hivi Mfalme Daudi aliyekuwa mwaminifu: “Nitainua mzao wako nyuma yako, . . . nami nitaufanya imara ufalme wake. . . . Nacho kiti cha enzi cha ufalme wake nitakifanya imara milele.” (2 Samweli 7:12, 13; Zaburi 89:3) Wakati huo ilijulikana kwamba ukoo wa Mzao aliyeahidiwa ungetokea katika nyumba ya Daudi. Lakini je, mwanadamu wa kawaida angeweza kutawala “milele”? (Zaburi 89:20, 29, 34-36) Na je, mfalme huyo wa kibinadamu angeweza kuwaokoa wanadamu kutoka kwa dhambi na kifo?

13, 14. (a) Kulingana na Zaburi 110, Yehova anamwahidi nini Mfalme wake aliyetiwa mafuta? (b) Manabii wa Yehova walifunua mambo gani mengine kuhusu Mzao ambaye angekuja?

13 Daudi aliongozwa kuandika hivi: “Neno la BWANA kwa Bwana wangu, Uketi mkono wangu wa kuume, hata niwafanyapo adui zako kuwa chini ya miguu yako. BWANA ameapa, wala hataghairi, Ndiwe kuhani hata milele, kwa mfano wa Melkizedeki.” (Zaburi 110:1, 4) Maneno hayo ya Daudi yalimhusu moja kwa moja, Mzao aliyeahidiwa, au Mesiya. (Matendo 2:35, 36) Mfalme huyo hangetawala kutoka Yerusalemu, bali kutoka mbinguni kwenye ‘mkono wa kuume’ wa Yehova. Basi angekuwa na mamlaka, si juu ya nchi ya Israeli tu, bali juu ya dunia yote. (Zaburi 2:6-8) Jambo jingine lilifunuliwa. Angalia kwamba Yehova aliapa kwa dhati kwamba huyo Mesiya angekuwa “kuhani . . . kwa mfano wa Melkizedeki.” Kama Melkizedeki, ambaye alitumika akiwa mfalme na kuhani katika siku za Abrahamu, Mzao ambaye angekuja angechaguliwa na Mungu moja kwa moja awe Mfalme na Kuhani!—Mwanzo 14:17-20.

14 Kwa miaka mingi, Yehova alitumia manabii wake kufunua mambo zaidi kuhusu siri yake takatifu. Kwa mfano, Isaya alitabiri kwamba Mzao huyo angekufa kifo cha kidhabihu. (Isaya 53:3-12) Mika alitabiri mahali ambapo Mesiya angezaliwa. (Mika 5:2) Danieli hata alitabiri wakati hususa ambapo Mzao huyo angetokea na wakati ambapo angekufa.—Danieli 9:24-27.

Siri Takatifu Yafunuliwa!

15, 16. (a) Mwana wa Yehova ‘alitokana na mwanamke’ kwa njia gani? (b) Yesu alirithi nini kutoka kwa wazazi wake wa kibinadamu, naye akawa Mzao aliyeahidiwa lini?

15 Utimizo wa unabii huo mbalimbali haukujulikana hadi Mzao huyo alipotokea. Andiko la Wagalatia 4:4 lasema: “Kikomo kamili cha wakati kilipowasili, Mungu alimtuma Mwana wake, aliyekuja kuwa kutokana na mwanamke.” Mnamo mwaka wa 2 K.W.K., malaika alimwambia hivi bikira Myahudi aliyeitwa Maria: “Tazama! utachukua mimba katika tumbo lako la uzazi na kuzaa mwana, nawe itakupasa kumwita jina lake Yesu. Huyu atakuwa mkubwa na ataitwa Mwana wa Aliye Juu Zaidi Sana; na Yehova Mungu atampa kiti cha ufalme cha Daudi baba yake . . . Roho takatifu itakuja juu yako, na nguvu ya Aliye Juu Zaidi Sana itakufunika kivuli. Kwa sababu hiyo pia kitakachozaliwa kitaitwa kitakatifu, Mwana wa Mungu.”—Luka 1:31, 32, 35.

16 Baadaye, Yehova alihamisha uhai wa Mwanaye kutoka mbinguni hadi kwenye tumbo la uzazi la Maria, hivyo, akatokana na mwanamke. Maria hakuwa mwanamke mkamilifu. Lakini, Yesu hakurithi kutokamilika kutoka kwa Maria, kwa sababu alikuwa “Mwana wa Mungu.” Lakini, wazazi wa kibinadamu wa Yesu, ambao walikuwa wazao wa Daudi, walimwezesha kuwa mrithi wa Daudi kiasili na kisheria. (Matendo 13:22, 23) Yesu alipobatizwa mwaka wa 29 W.K., Yehova alimtia mafuta kwa roho takatifu na kusema: “Huyu ni Mwana wangu, mpendwa.” (Mathayo 3:16, 17) Hatimaye, Mzao aliyeahidiwa alikuwa amewasili! (Wagalatia 3:16) Wakati wa kufunua mambo mengi zaidi kuhusu ile siri takatifu ulikuwa umewadia.—2 Timotheo 1:10.

17. Andiko la Mwanzo 3:15 lilifafanuliwaje?

17 Wakati wa huduma yake, Yesu alimtambulisha yule nyoka aliyetajwa katika Mwanzo 3:15 kuwa Shetani, na uzao wa nyoka kuwa wafuasi wa Shetani. (Mathayo 23:33; Yohana 8:44) Baadaye, ilifunuliwa jinsi ambavyo hao wote watapondwa milele. (Ufunuo 20:1-3, 10, 15) Na mwanamke alitambuliwa kuwa “Yerusalemu la juu,” tengenezo la Yehova la mbinguni la viumbe wa roho, ambalo ni kama mke. *Wagalatia 4:26; Ufunuo 12:1-6.

Agano Jipya

18. Ni nini kusudi la “agano jipya”?

18 Huenda jambo la kutokeza hata zaidi lilifunuliwa siku iliyotangulia kifo cha Yesu, alipowaambia wanafunzi wake waaminifu kuhusu “agano jipya.” (Luka 22:20) Agano hilo jipya, sawa na agano la Sheria ya Musa, lilikusudiwa kufanyiza “ufalme wa makuhani.” (Kutoka 19:6; 1 Petro 2:9) Hata hivyo, agano hilo halingefanyiza taifa la kiasili bali taifa la kiroho, yaani, “Israeli wa Mungu.” Taifa hilo lingekuwa tu na wafuasi waaminifu wa Kristo waliotiwa mafuta. (Wagalatia 6:16) Washiriki hao wa agano jipya wangeshirikiana na Yesu kubariki wanadamu!

19. (a) Kwa nini agano jipya linafanikiwa kufanyiza “ufalme wa makuhani”? (b) Kwa nini Wakristo watiwa-mafuta wanaitwa “kiumbe kipya,” na ni wangapi watakaotawala na Kristo wakiwa mbinguni?

19 Lakini kwa nini agano jipya linafanikiwa kufanyiza “ufalme wa makuhani” ambao utawabariki wanadamu? Kwa sababu badala ya kuwahukumu wanafunzi wa Kristo kuwa watenda-dhambi, linafungua njia ya dhambi zao kusamehewa kupitia dhabihu yake. (Yeremia 31:31-34) Mara tu baada ya kuhesabiwa kuwa waadilifu machoni pa Yehova, anawakubali kuwa wana wa familia yake ya mbinguni na kuwatia mafuta kwa roho takatifu. (Waroma 8:15-17; 2 Wakorintho 1:21) Kwa hiyo, wanapata ‘uzaliwa mpya kwenye tumaini lililo hai ambao umewekwa akiba katika mbingu.’ (1 Petro 1:3, 4) Wakristo watiwa-mafuta waliozaliwa kwa roho wanaitwa “kiumbe kipya,” kwa sababu cheo chao cha juu ni kipya kabisa kwa wanadamu. (2 Wakorintho 5:17) Biblia inafunua kwamba hatimaye watu 144,000 wakiwa mbinguni watashiriki kutawala wanadamu waliokombolewa.—Ufunuo 5:9, 10; 14:1-4.

20. (a) Ni jambo gani lililofunuliwa mwaka wa 36 W.K. kuhusu ile siri takatifu? (b) Ni nani watakaofurahia baraka ambazo Abrahamu aliahidiwa?

20 Yesu pamoja na hao watiwa-mafuta wanakuwa “mbegu ya Abrahamu.” * (Wagalatia 3:29) Wayahudi wa asili ndiyo waliochaguliwa kwanza. Lakini mwaka wa 36 W.K., jambo jingine la siri takatifu lilifunuliwa: Watu wa Mataifa, au wasio Wayahudi, wangekuwa pia na tumaini la kwenda mbinguni. (Waroma 9:6-8; 11:25, 26; Waefeso 3:5, 6) Je, ni Wakristo watiwa-mafuta peke yao ambao wangefurahia baraka ambazo Abrahamu aliahidiwa? La, kwa sababu dhabihu ya Yesu inafaidi ulimwengu wote. (1 Yohana 2:2) Baada ya muda, Yehova alifunua kwamba “umati mkubwa” usiohesabika ungeokoka mwisho wa mfumo wa mambo wa Shetani. (Ufunuo 7:9, 14) Halaiki kubwa zaidi ya watu wangefufuliwa wakiwa na tumaini la kuishi milele katika Paradiso!—Luka 23:43; Yohana 5:28, 29; Ufunuo 20:11-15; 21:3, 4.

Hekima ya Mungu na Siri Takatifu

21, 22. Siri takatifu ya Yehova inaonyeshaje hekima yake?

21 Siri takatifu ni wonyesho wenye kustaajabisha wa “hekima ya Mungu ya namna nyingi.” (Waefeso 3:8-10) Yehova alionyesha hekima iliyoje alipotunga siri hiyo na kuifunua hatua kwa hatua! Kwa hekima alifikiria udhaifu wa wanadamu, akawaruhusu waonyeshe hali yao halisi ya moyoni.—Zaburi 103:14.

22 Yehova pia alionyesha hekima isiyo na kifani alipomchagua Yesu kuwa Mfalme. Mwana wa Yehova ni mwenye kutumainika kuliko kiumbe mwingine yeyote ulimwenguni. Yesu alipata magumu ya kila namna alipokuwa mwanadamu. Anaelewa kabisa matatizo yanayotupata. (Waebrania 5:7-9) Vipi watawala-wenzi wa Yesu? Kwa miaka mingi, wanaume na wanawake waliochaguliwa kutoka kwa makabila, lugha, na malezi mbalimbali wametiwa mafuta. Kila mmoja wao amepata matatizo ya kila namna na kuyashinda. (Waefeso 4:22-24) Itakuwa furaha iliyoje kutawaliwa na wafalme na makuhani hao wenye huruma!

23. Wakristo wana pendeleo gani kuhusiana na siri takatifu ya Yehova?

23 Mtume Paulo aliandika hivi: “Siri takatifu iliyokuwa imefichwa tangu mifumo ya mambo iliyopita na tangu vizazi vilivyopita . . . imefanywa dhahiri kwa watakatifu wake.” (Wakolosai 1:26) Naam, watakatifu wa Yehova waliotiwa mafuta wamepata kuelewa mengi kuhusu siri hiyo takatifu, nao wamewafundisha mamilioni ya watu ujuzi huo. Basi sote tuna pendeleo lililoje! Yehova ‘ametujulisha siri takatifu ya mapenzi yake.’ (Waefeso 1:9) Na tuwaambie wengine siri hiyo ya ajabu, na kuwasaidia pia wachunguze hekima isiyo na kifani ya Yehova Mungu!

^ fu. 17 “Siri takatifu ya ujitoaji-kimungu” ilifunuliwa pia katika maisha ya Yesu. (1 Timotheo 3:16) Kwa muda mrefu, haikujulikana kama mwanadamu yeyote angeweza kubaki mwaminifu kabisa kwa Yehova. Yesu alijibu suala hilo. Alibaki mwaminifu licha ya majaribu yote ambayo Shetani alimletea.—Mathayo 4:1-11; 27:26-50.

^ fu. 20 Yesu pia alifanya “agano . . . kwa ajili ya ufalme” na kikundi hichohicho. (Luka 22:29, 30) Kwa kweli, Yesu alifanya mapatano na “kundi [hilo] dogo” ili watawale pamoja naye mbinguni wakiwa sehemu ya pili ya mbegu ya Abrahamu.—Luka 12:32.