Hamia kwenye habari

Hamia kwenye yaliyomo

Sura ya 21

Yesu Afunua “Hekima Kutoka kwa Mungu”

Yesu Afunua “Hekima Kutoka kwa Mungu”

1-3. Majirani wa awali wa Yesu waliitikiaje mafundisho yake, na hawakutambua nini kumhusu?

WASIKILIZAJI walistaajabu. Kijana Yesu alikuwa amesimama mbele yao katika sinagogi akiwafundisha. Walimfahamu sana kwa sababu alikulia na kufanya kazi ya useremala katika mji wao kwa miaka mingi. Huenda baadhi yao waliishi katika nyumba ambazo Yesu alisaidia kujenga, au huenda walilima mashamba yao kwa plau na nira ambazo Yesu alitengeneza. * Lakini je, wangekubali mafundisho ya mtu huyo aliyekuwa seremala hapo awali?

2 Watu wengi waliokuwa wakimsikiliza walistaajabu na kuuliza: “Mtu huyu alipata wapi hekima hii?” Walisema hivi pia: “Huyu si seremala mwana wa Maria?” (Mathayo 13:54-58; Marko 6:1-3) Kwa kusikitisha, watu hao waliokuwa majirani wa Yesu pindi fulani, walisababu hivi, ‘Huyu seremala ni mtu wa kawaida tu kama sisi.’ Walimkataa ingawa alinena maneno yenye hekima. Hawakujua kwamba alipewa hekima hiyo.

3 Yesu alipata wapi hekima hiyo? Alisema hivi: “Kile nifundishacho si changu, bali ni chake yeye aliyenituma.” (Yohana 7:16) Mtume Paulo alieleza kwamba Yesu “amekuwa kwetu hekima kutoka kwa Mungu.” (1 Wakorintho 1:30) Yehova anafunua hekima yake kupitia Mwanaye, Yesu. Ndiyo sababu Yesu alisema hivi: “Mimi na Baba ni mmoja.” (Yohana 10:30) Hebu tuchunguze sehemu tatu ambazo Yesu alionyesha “hekima kutoka kwa Mungu.”

Mafundisho Yake

4. (a) Ujumbe wa Yesu ulihusu nini hasa, na kwa nini ujumbe huo ulikuwa muhimu sana? (b) Kwa nini mashauri ya Yesu yalifaa na kuwafaidi wasikilizaji wake sikuzote?

4 Kwanza, fikiria mafundisho ya Yesu. Ujumbe wake ulihusu hasa “habari njema ya ufalme.” (Luka 4:43) Huo ulikuwa ujumbe muhimu sana kwa sababu Ufalme huo utatetea enzi kuu ya Yehova na kuwaletea wanadamu baraka za kudumu. Alipokuwa akifundisha, Yesu alitoa pia mashauri ya hekima kuhusu maisha ya kila siku. Alijithibitisha kuwa yule “Mshauri wa Ajabu” aliyetabiriwa. (Isaya 9:6) Kwa kweli, mashauri yake yalikuwa bora sana. Alijua Neno la Mungu na mapenzi yake kwa undani, alifahamu vyema utu wa wanadamu, naye aliwapenda sana. Kwa hiyo, sikuzote alitoa mashauri yaliyofaa ambayo yaliwafaidi wasikilizaji wake. Yesu alinena “semi za uhai udumuo milele.” Naam, mtu anayefuata mashauri yake atapata wokovu.—Yohana 6:68.

5. Yesu alizungumzia mambo gani katika Mahubiri ya Mlimani?

5 Mahubiri ya Mlimani yanaonyesha hekima isiyo na kifani ya mafundisho ya Yesu. Mahubiri hayo yaliyo katika Mathayo 5:3–7:27, yanaweza kutolewa kwa muda wa dakika 20 tu. Hata hivyo, yana mashauri yenye faida ya kudumu, yanayofaa sana leo sawa na yalivyofaa wakati yalipotolewa. Yesu alizungumzia mambo mengi mbalimbali, kutia ndani jinsi ya kuboresha mahusiano na wengine (5:23-26, 38-42; 7:1-5, 12), jinsi ya kuwa safi kiadili (5:27-32), na jinsi ya kuishi maisha yenye kusudi (6:19-24; 7:24-27). Lakini Yesu hakuwaambia tu wasikilizaji wake jinsi ya kuishi kwa hekima; aliwaonyesha kwa kuwaeleza, kwa kusababu nao, na kwa kuwapa uthibitisho.

6-8. (a) Yesu anataja sababu zipi nzuri za kuepuka mahangaiko? (b) Ni nini kinachoonyesha kwamba Shauri la Yesu lina hekima ya kutoka juu?

6 Kwa mfano, fikiria shauri la Yesu lenye hekima katika Mathayo sura ya 6 linaloonyesha jinsi ya kupambana na mahangaiko ya vitu vya kimwili. Yesu anatushauri hivi: “Komeni kuhangaikia nafsi zenu kuhusu ni nini mtakula au ni nini mtakunywa, au juu ya miili yenu kuhusu ni nini mtavaa.” (Mstari wa 25) Chakula na mavazi ni mahitaji ya lazima, na ni jambo la kawaida tu kuhangaikia vitu hivyo. Lakini Yesu anatuambia ‘tukome kuhangaikia’ vitu hivyo. * Kwa nini?

7 Msikilize Yesu anaposababu kwa njia yenye kusadikisha. Kwa kuwa Yehova ametupatia uhai na mwili, je, anaweza kushindwa kutuandalia chakula cha kuendeleza uhai huo na mavazi ya kujivika? (Mstari wa 25) Ikiwa Mungu anawalisha ndege na kuyapamba maua, basi, hatawatunza zaidi wanadamu wanaomwabudu! (Mstari wa 26, 28-30) Kwa kweli, haifai kuwa na mahangaiko yasiyofaa. Hatuwezi kuongeza muda wetu wa uhai hata kwa dhiraa moja kwa kuhangaika. * (Mstari wa 27) Tunawezaje kuepuka mahangaiko? Yesu anatushauri hivi: Endeleeni kuitanguliza ibada ya Mungu maishani mwenu. Wale wanaofanya hivyo wanaweza kuwa na uhakika kwamba Baba yao wa mbinguni ‘atawaongezea’ mahitaji yao ya kila siku. (Mstari wa 33) Mwishowe, Yesu atoa dokezo nzuri sana—usihangaikie mambo ya kesho. Mbona uzidishe mahangaiko ya leo kwa kuhangaikia mambo ya kesho? (Mstari wa 34) Licha ya hayo, mbona uhangaikie mambo ambayo huenda yasitukie kamwe? Tunaweza kuepuka maumivu makali ya moyoni tukifuata shauri hilo la hekima katika ulimwengu huu uliojaa mikazo.

8 Ni wazi kwamba shauri la Yesu linafaa sana leo kama lilivyofaa miaka 2,000 hivi iliyopita. Je, hilo halithibitishi kwamba hekima hiyo ni ya kutoka juu? Hata mashauri bora ya wanadamu huhitaji kurekebishwa au kubadilishwa baada ya muda kupita. Lakini, miaka nenda miaka rudi, mafundisho ya Yesu yangali yanatumika na ni yenye faida. Hilo halipaswi kutushangaza kwa sababu Mshauri huyo wa Ajabu alisema “semi za Mungu.”—Yohana 3:34.

Njia Yake ya Kufundisha

9. Askari fulani walisema nini kuhusu ufundishaji wa Yesu, na kwa nini hawakuwa wakitia chumvi?

Njia ya Yesu ya kufundisha ni sehemu ya pili inayoonyesha hekima ya Mungu. Pindi moja, askari fulani waliotumwa kumkamata Yesu walirudi mikono mitupu na kusema: “Hajasema kamwe mtu mwingine kama hivi.” (Yohana 7:45, 46) Hawakuwa wakitia chumvi. Yesu, ambaye ‘alitoka kwenye makao ya juu,’ alikuwa na ujuzi na uzoefu mwingi sana kuliko wanadamu wote waliopata kuishi. (Yohana 8:23) Hakuna mwanadamu yeyote aliyeweza kufundisha kama Yesu. Hebu fikiria njia mbili alizotumia Mwalimu huyo mwenye hekima.

“Umati ulistaajabishwa na njia yake ya kufundisha”

10, 11. (a) Kwa nini tunastaajabia jinsi Yesu alivyotumia vielezi? (b) Vielezi ni nini, na ni mfano upi unaoonyesha kwamba vielezi vya Yesu vina matokeo katika kufundisha?

10 Alitumia vielezi vinavyofaa. Twaambiwa kwamba ‘Yesu alisema na umati kwa vielezi. ‘Kwa kweli, bila kielezi hakuwa akisema nao.’ (Mathayo 13:34) Tunastaajabia uwezo wake usio na kifani wa kufundisha kweli muhimu kwa kutumia mambo ya kawaida. Alitumia mambo ambayo wasikilizaji wake walizoea, kama vile wakulima wanaopanda mbegu, wanawake wanaojitayarisha kuoka mikate, watoto wanaocheza sokoni, wavuvi wanaokokota nyavu, na wachungaji wanaotafuta kondoo waliopotea. Kweli muhimu zinapohusianishwa na mambo ya kawaida, zinatia mizizi mara moja katika akili na moyo.—Mathayo 11:16-19; 13:3-8, 33, 47-50; 18:12-14.

11 Mara nyingi Yesu alitumia vielezi au hadithi fupi ili kufundisha kweli za kiroho na za kiadili. Watu waliweza kukumbuka mafundisho ya Yesu kwa sababu hadithi fupi hueleweka na kukumbukwa kwa urahisi kuliko hoja za kuwaziwa tu. Katika vielezi vingi, Yesu alitumia mifano rahisi isiyosahaulika ili kuonyesha jinsi Baba yake alivyo. Kwa mfano, ni nani asiyeweza kuelewa maana ya kielezi cha mwana mpotevu—kwamba Yehova atamhurumia na kumkaribisha kwa upendo mtu aliyeasi anayetubu kikweli?—Luka 15:11-32.

12. (a) Yesu alitumiaje maswali alipofundisha? (b) Yesu aliwanyamazishaje wale waliotilia shaka mamlaka yake?

12 Alitumia maswali kwa ustadi. Yesu alitumia maswali ili kuwasaidia wasikilizaji wake wafikie mikataa yao wenyewe, wachunguze madhumuni yao, au wafanye maamuzi. (Mathayo 12:24-30; 17:24-27; 22:41-46) Viongozi wa kidini walipotilia shaka mamlaka aliyopewa na Mungu, Yesu aliwauliza: “Je, ubatizo wa Yohana ulikuwa wa kutoka mbinguni au wa kutoka kwa wanadamu?” Swali hilo liliwaduwaza, wakaanza kusababu hivi miongoni mwao: “Tukisema, ‘Kutoka mbinguni,’ atatuambia, ‘Basi, kwa nini hamkumwamini?’ Ingawa hivyo, tukisema, ‘Kutoka kwa wanadamu,’ tunao umati kuuhofu, kwa maana wao wote wamchukua Yohana kuwa nabii.” Hatimaye, wakajibu: “Hatujui.” (Marko 11:27-33; Mathayo 21:23-27) Yesu aliwauliza swali rahisi ambalo liliwanyamazisha na kufunua unafiki wao.

13-15. Hadithi ya Msamaria mwema inaonyeshaje hekima ya Yesu?

13 Nyakati nyingine Yesu alitumia mbinu mbalimbali kwa pamoja, alitoa vielezi na kuuliza maswali yenye kuchochea fikira. Mwanasheria mmoja Myahudi alipomwuliza Yesu jambo ambalo alipaswa kufanya ili apate uhai wa milele, Yesu alimkumbusha Sheria ya Musa ambayo inawaamuru watu wampende Mungu na jirani. Mtu huyo aliuliza hivi ili kujithibitisha kuwa mwadilifu: “Ni nani kwa kweli aliye jirani yangu?” Yesu alimjibu kwa kusimulia hadithi. Myahudi fulani alikuwa akisafiri peke yake aliposhambuliwa na wanyang’anyi na kuachwa akiwa mahututi. Wayahudi wawili walimpita, kwanza kuhani kisha Mlawi. Wote wakampuuza. Lakini baadaye Msamaria fulani alipitia hapo na kumwona. Kwa huruma nyingi, alifunga kwa uangalifu majeraha ya mtu huyo na akaonyesha upendo kwa kumpeleka kwenye nyumba ndogo ya wageni ili apate nafuu. Alipomaliza hadithi hiyo, Yesu alimwuliza yule mwanasheria hivi: “Ni nani kati ya watatu hawa aonekana kwako kuwa alijifanya mwenyewe jirani kwa mtu aliyeanguka miongoni mwa wapokonyaji?” Mwanasheria huyo hakuwa na budi kujibu: “Yeye aliyetenda kwa rehema kumwelekea.”—Luka 10:25-37.

14 Hadithi hiyo inaonyeshaje hekima ya Yesu? Katika siku za Yesu, Wayahudi walitumia neno “jirani” kuwarejelea tu wale waliofuata mapokeo yao, na bila shaka hawakuwaona Wasamaria kuwa “jirani.” (Yohana 4:9) Kama Yesu angesema kwamba Msamaria ndiye aliyeshambuliwa na akasaidiwa na Myahudi, je, hilo lingekomesha ubaguzi wao? Kwa hekima, Yesu alitunga hadithi hiyo kwa njia ya kwamba Msamaria ndiye anayemtunza kwa upendo Myahudi. Fikiria pia swali ambalo Yesu aliuliza baada ya kusimulia hadithi hiyo. Alionyesha maana nyingine ya neno “jirani.” Ni kana kwamba yule mwanasheria aliuliza: ‘Ni nani jirani ninayepaswa kumpenda?’ Lakini Yesu akamwuliza: “Ni nani kati ya watatu hawa aonekana kwako kuwa alijifanya mwenyewe jirani?” Yesu alikazia fikira yule Msamaria aliyeonyesha fadhili, wala si yule Myahudi aliyeonyeshwa fadhili. Jirani wa kweli huchukua hatua ya kuwapenda wengine bila kujali kabila lao. Yesu alifundisha somo hilo kwa njia bora kabisa.

15 Haishangazi kwamba watu walivutiwa na Yesu na kustaajabia “njia yake ya kufundisha.” (Mathayo 7:28, 29) Pindi moja, “umati mkubwa” ulikaa naye kwa siku tatu bila kula!—Marko 8:1, 2.

Maisha Yake

16. Yesu ‘alithibitishaje’ kwamba aliongozwa na hekima ya Mungu?

16 Maisha ya Yesu ni sehemu ya tatu inayoonyesha hekima ya Yehova. Hekima huonyeshwa kwa matendo; inazaa matunda. Mwanafunzi Yakobo aliuliza: “Ni nani mwenye hekima miongoni mwenu?” Kisha akajibu swali hilo kwa kusema: “Basi, mwenendo wake bora uthibitishe jambo hilo.” (Yakobo 3:13, The New English Bible) Mwenendo wa Yesu ‘ulithibitisha’ kwamba aliongozwa na hekima ya Mungu. Hebu tuone jinsi alivyotumia busara maishani mwake na aliposhughulika na wengine.

17. Ni nini kinachoonyesha kwamba Yesu alikuwa na usawaziko kamili maishani?

17 Je, umeona kwamba mara nyingi watu wasio na busara hupita kiasi? Naam, mtu anahitaji hekima ili kuwa na usawaziko. Yesu alionyesha hekima ya Mungu kwa kuwa na usawaziko kamili. Zaidi ya yote, alitanguliza mambo ya kiroho maishani mwake. Alijishughulisha sana na kazi ya kutangaza habari njema. “Ni kwa kusudi hilo nimetokea,” akasema. (Marko 1:38) Bila shaka, vitu vya kimwili havikuwa muhimu sana kwake; inaonekana kwamba alikuwa na vitu vichache sana. (Mathayo 8:20) Hata hivyo, hakujinyima starehe. Yesu alikuwa mwenye shangwe kama Baba yake, ambaye ni “Mungu mwenye furaha,” naye alizidisha shangwe ya wengine. (1 Timotheo 1:11; 6:15) Yesu hakuhudhuria karamu ya arusi—ambayo kwa kawaida huwa na muziki, uimbaji, na furaha—ili awaharibie wengine starehe. Divai ilipokwisha, aligeuza maji yakawa divai bora, kinywaji ambacho ‘kinaufurahisha moyo wa mtu.’ (Zaburi 104:15; Yohana 2:1-11) Yesu alikubali mialiko mingi ya chakula, na mara nyingi alitumia pindi hizo kufundisha.—Luka 10:38-42; 14:1-6.

18. Yesu alishughulikaje na wanafunzi wake kwa njia ya busara?

18 Yesu alishughulika na wengine kwa njia ya busara. Aliwajua wanafunzi wake vizuri kwa sababu alifahamu kabisa utu wa wanadamu. Alijua kwamba hawakuwa wakamilifu. Lakini, alitambua sifa zao nzuri. Alitambua kwamba wanafunzi hao waliovutwa na Yehova wangeweza kufanya mengi. (Yohana 6:44) Yesu alikuwa tayari kuwatumaini licha ya kasoro zao. Kwa mfano, alionyesha kwamba aliwatumaini wanafunzi wake kwa kuwakabidhi daraka zito. Aliwaagiza wahubiri habari njema, na alikuwa na hakika kwamba wangeweza kutimiza kazi hiyo. (Mathayo 28:19, 20) Kitabu cha Matendo kinathibitisha kwamba walitimiza kwa uaminifu kazi ambayo aliwaamuru wafanye. (Matendo 2:41, 42; 4:33; 5:27-32) Basi ni wazi kwamba Yesu alionyesha hekima kwa kuwatumaini.

19. Yesu alionyeshaje kwamba alikuwa “mwenye tabia-pole na wa hali ya chini moyoni”?

19 Kama tulivyoona kwenye Sura ya 20, Biblia inaonyesha kwamba unyenyekevu na upole zinahusiana na sifa ya hekima. Bila shaka, Yehova ndiye mfano bora kabisa wa sifa hizo. Lakini vipi Yesu? Inapendeza kuona jinsi Yesu alivyoshughulika na wanafunzi wake kwa unyenyekevu. Alikuwa bora kuliko wanafunzi wake kwa sababu alikuwa mkamilifu. Lakini, hakuwadharau wanafunzi wake. Hakujaribu kamwe kuwafanya wajione hawafai au wao ni bure tu. Kinyume chake, alijua udhaifu wao na alikuwa mwenye subira walipokosea. (Marko 14:34-38; Yohana 16:12) Je, haipendezi kwamba hata watoto walifurahi sana kuwa na Yesu? Bila shaka, walivutiwa naye kwa sababu waliona kwamba alikuwa “mwenye tabia-pole na wa hali ya chini moyoni.”—Mathayo 11:29; Marko 10:13-16.

20. Yesu alionyeshaje kwamba anasikiliza maoni ya wengine aliposhughulika na yule mwanamke asiye Myahudi ambaye alikuwa na binti aliyesumbuliwa na roho waovu?

20 Yesu aliiga unyenyekevu wa Mungu kwa njia nyingine muhimu. Alizingatia maoni ya wengine, wakati ilipofaa kuonyesha rehema. Kwa mfano, kumbuka wakati mwanamke fulani asiye Myahudi alipomsihi Yesu amponye binti yake aliyesumbuliwa sana na roho waovu. Mwanzoni, Yesu alionyesha kwa njia tatu kwamba hangemsaidia—kwanza, hakumjibu; pili, alimwambia moja kwa moja kwamba alikuwa ametumwa kwa Wayahudi wala si kwa wasio Wayahudi; na tatu, alitoa mfano ambao ulikazia kwa fadhili jambo hilo. Hata hivyo, mwanamke huyo hakuchoka, alionyesha kwamba alikuwa na imani ya pekee sana. Yesu alifanya nini kuhusiana na kisa hicho cha pekee? Alifanya jambo ambalo alikuwa amesema hangefanya. Alimponya binti ya mwanamke huyo. (Mathayo 15:21-28) Huo ni unyenyekevu wa pekee sana, sivyo? Kumbuka kwamba unyenyekevu ndio msingi wa hekima ya kweli.

21. Kwa nini tunapaswa kujitahidi kuiga utu, usemi, na njia ya Yesu ya kutenda mambo?

21 Tunashukuru kama nini kwamba Vitabu vya Injili vinatujulisha maneno na matendo ya mtu mwenye hekima zaidi aliyepata kuishi! Na tukumbuke kwamba Yesu alimwiga Baba yake kikamili. Tukiiga utu, usemi, na njia ya Yesu ya kutenda mambo, tutakuwa tukikuza hekima ya kutoka juu. Katika sura ifuatayo, tutaona jinsi tunavyoweza kutumia hekima ya Mungu maishani mwetu.

^ fu. 1 Katika nyakati za Biblia, maseremala walijenga nyumba, walitengeneza fanicha, na vifaa vya kilimo. Justin Martyr, aliyeishi katika karne ya pili W.K., aliandika hivi kumhusu Yesu: “Alikuwa seremala maarufu aliyetengeneza plau na nira alipokuwa duniani.”

^ fu. 6 Kitenzi cha Kigiriki kinachotafsiriwa “hangaikia” kinamaanisha “kukengeushwa fikira.” Katika Mathayo 6:25, neno hilo linamaanisha woga na wasiwasi ambao unakengeusha au kupotosha fikira, na kumfanya mtu akose shangwe maishani.

^ fu. 7 Uchunguzi wa sayansi umeonyesha kwamba kuhangaika na kufadhaika kupita kiasi kwaweza kusababisha ugonjwa wa moyo na magonjwa mengine yanayoweza kusababisha kifo.