Hamia kwenye habari

Hamia kwenye yaliyomo

Sura ya 23

“Alitupenda Sisi Kwanza”

“Alitupenda Sisi Kwanza”

1-3. Ni mambo yapi yaliyofanya kifo cha Yesu kiwe cha pekee sana katika historia yote?

SIKU moja miaka 2,000 hivi iliyopita, mtu fulani asiye na hatia alishtakiwa, akahukumiwa kwa sababu ya uhalifu ambao hakufanya, kisha akateswa hadi akafa. Jambo la kuhuzunisha ni kwamba yeye ni baadhi tu ya watu ambao wameuawa kikatili katika historia. Lakini kifo chake kilikuwa cha pekee sana.

2 Mtu huyo alipokuwa akiteseka kwa maumivu makali saa chache kabla ya kufa, kulikuwa na ishara mbinguni kuonyesha kwamba hilo lilikuwa tukio muhimu sana. Giza liliifunika dunia yote ghafula yapata saa sita mchana. Mwanahistoria mmoja alisema kwamba “nuru ya jua ilikosekana.” (Luka 23:44, 45) Kisha, kabla tu ya kufa, akasema maneno haya yasiyosahaulika: “Imetimizwa!” Kwa kweli, alitimiza jambo zuri sana alipodhabihu uhai wake. Kwa kudhabihu uhai wake, alionyesha upendo ambao hakuna mwanadamu yeyote amewahi kuonyesha.—Yohana 15:13; 19:30.

3 Mtu huyo alikuwa Yesu Kristo. Mateso na kifo chake katika siku hiyo ya kuhuzunisha, Nisani 14, mwaka wa 33 W.K., ni mambo yanayojulikana sana. Hata hivyo, jambo fulani muhimu limepuuzwa mara nyingi. Ingawa Yesu aliteseka sana, kuna mwingine aliyeteseka hata zaidi. Kwa kweli, kuna mwingine aliyejidhabihu kwa njia kubwa hata zaidi siku hiyo—alitenda tendo kuu zaidi la upendo ambalo halijawahi kufanywa na yeyote katika ulimwengu mzima. Ni tendo gani hilo? Jibu la swali hilo ni utangulizi ufaao wa habari muhimu zaidi ya habari zote: Upendo wa Yehova.

Tendo Kuu Zaidi la Upendo

4. Askari Mroma alipataje kujua kwamba Yesu hakuwa mtu wa kawaida, naye alikata kauli gani?

4 Askari Mroma aliyesimamia mauaji ya Yesu alipigwa na bumbuazi alipoona giza lililotokea kabla ya Yesu kufa na tetemeko kubwa la dunia lililotokea baadaye. Alisema hivi: “Hakika huyu alikuwa Mwana wa Mungu.” (Mathayo 27:54) Ni wazi kwamba Yesu hakuwa mtu wa kawaida. Askari huyo aliunga mkono mauaji ya Mwana mzaliwa-pekee wa Mungu Mwenyezi! Mwana huyo alipendwa na Baba yake kwa kadiri gani?

5. Ni mfano gani umetolewa ili kutusaidia kuelewa kwamba Yehova na Mwanaye wamekuwa pamoja mbinguni kwa muda mrefu sana?

5 Biblia inamwita Yesu “mzaliwa wa kwanza wa uumbaji wote.” (Wakolosai 1:15) Hebu fikiria—Mwana wa Yehova alikuwapo kabla ya ulimwengu kuumbwa. Basi, Mwana huyo alikaa na Baba yake kwa muda gani? Wanasayansi fulani wanakisia kwamba ulimwengu umekuwapo kwa muda wa miaka bilioni 13. Huo ni muda usiowazika, sivyo? Ili kuwasaidia watu waelewe muda ambao wanasayansi wanakisia kwamba ulimwengu umekuwapo, jengo moja lenye mitambo ya kuigiza miendo ya sayari lina chati ya tarehe yenye urefu wa meta 110. Wageni wanapotembea kando ya chati hiyo, kila hatua wanayopiga inawakilisha miaka ipatayo milioni 75 ya muda ambao ulimwengu umekuwapo. Alama ndogo inayolingana na unene wa unywele wa mwanadamu imewekwa mwishoni mwa chati hiyo ili kuwakilisha muda ambao wanadamu wameishi duniani! Lakini, hata ikiwa makisio hayo ni sahihi, urefu wa chati hiyo hauwezi kamwe kuwakilisha umri wa Mwana wa Yehova! Alikuwa akifanya kazi gani wakati huo wote?

6. (a) Mwana wa Yehova alikuwa akifanya nini kabla ya kuwa mwanadamu? (b) Yehova na Mwanaye wanaunganishwa na kifungo cha aina gani?

6 Mwana huyo alifurahi kutumiwa na Baba yake akiwa “stadi wa kazi.” (Mithali 8:30) Biblia inasema hivi: “Na bila yeye [Mwana] hata kitu kimoja hakikuja kuwako.” (Yohana 1:3) Kwa hiyo Yehova na Mwanaye walishirikiana kuumba vitu vingine vyote. Walikuwa na kazi zenye kuvutia na kufurahisha kwelikweli. Watu wengi hukubali kwamba mzazi na mtoto hupendana sana. Na upendo “ni kifungo kikamilifu cha muungano.” (Wakolosai 3:14) Basi, ni nani kati yetu anayeweza kuelewa kwa ukamili nguvu za kifungo ambacho kimekuwapo kwa muda mrefu hivyo? Ni wazi kwamba Yehova Mungu na Mwanaye wameunganishwa na kifungo cha upendo chenye nguvu kuliko kifungo chochote kile.

7. Yesu alipobatizwa, Yehova alionyeshaje hisia zake kumwelekea?

7 Hata hivyo, Baba alimtuma Mwanaye duniani ili azaliwe akiwa mwanadamu. Kwa hivyo, Yehova hakuweza kushirikiana kwa ukaribu na Mwanaye mpendwa huko mbinguni kwa miaka kadhaa. Akiwa mbinguni, Yehova alipendezwa sana kumtazama Yesu akikua hadi akawa mwanamume mkamilifu. Yesu alibatizwa alipokuwa na umri wa miaka 30 hivi. Tunajua jinsi Yehova Baba yake alivyohisi kumhusu, hata alisema moja kwa moja kutoka mbinguni: “Huyu ni Mwana wangu, mpendwa, ambaye nimemkubali.” (Mathayo 3:17) Bila shaka Baba ya Yesu alifurahi sana kumwona akifanya kwa uaminifu yote yaliyotabiriwa, mambo yote ambayo alipaswa kufanya!—Yohana 5:36; 17:4.

8, 9. (a) Yesu alitendewaje Nisani 14, mwaka wa 33 W.K., na Baba yake wa mbinguni alihisije? (b) Kwa nini Yehova alimruhusu Mwanaye ateseke na kufa?

8 Hata hivyo, Yehova alihisije Nisani 14, mwaka wa 33 W.K.? Alihisije Yesu aliposalitiwa na kukamatwa na umati usiku? Alihisije Yesu alipoachwa na rafiki zake na kushtakiwa isivyo haki? Alihisije Yesu alipodhihakiwa, kutemewa mate, na kupigwa ngumi? Alihisije alipopigwa mijeledi iliyochanachana mgongo wake? Alihisije mikono na miguu yake ilipopigiliwa misumari kwenye mti, kisha akaachwa akiwa amening’inia huku watu wakimtukana? Baba alihisije Mwanaye mpendwa alipokuwa akimlilia kwa maumivu makali? Yehova alihisije Yesu alipokata pumzi, na kwa mara ya kwanza kabisa tangu mwanzo wa uumbaji wote, Mwanaye mpendwa akakoma kuwapo?—Mathayo 26:14-16, 46, 47, 56, 59, 67; 27:38-44, 46; Yohana 19:1.

’Mungu alitoa Mwana wake mzaliwa pekee’

9 Hatuna la kusema. Kwa kuwa Yehova ana hisia, hatuwezi kamwe kueleza uchungu ambao alihisi kwa sababu ya kifo cha Mwanaye. Lakini tunaweza kueleza kusudi la Yehova la kuruhusu jambo hilo litukie. Kwa nini Baba ya Yesu alijiruhusu kupatwa na uchungu huo? Yehova anatueleza jambo la kupendeza katika Yohana 3:16—mstari huu wa Biblia ni muhimu sana hivi kwamba umeitwa Injili ndogo. Andiko hilo lasema: “Mungu aliupenda ulimwengu sana hivi kwamba akatoa Mwana mzaliwa-pekee wake, ili kila mtu anayedhihirisha imani katika yeye asipate kuangamizwa bali awe na uhai udumuo milele.” Kwa hiyo, Yehova alifanya hivyo kwa sababu ya upendo. Zawadi ambayo Yehova alitoa—kumtuma Mwanaye ateseke na kufa kwa ajili yetu—ndiyo tendo kuu zaidi la upendo ambalo limewahi kufanywa.

Maana ya Upendo wa Mungu

10. Wanadamu wana uhitaji gani, na kwa nini ni vigumu kuelewa maana ya neno “upendo”?

10 Neno “upendo” lamaanisha nini? Imesemwa kwamba upendo ndio uhitaji mkubwa zaidi wa wanadamu. Tangu wanapozaliwa hadi wanapokufa, watu hutamani sana kupendwa, wanaishi kwa furaha wanapopendwa, na hata wanadhoofika na kufa wasipopendwa. Hata hivyo, jambo la kushangaza ni kwamba si rahisi kueleza maana ya upendo. Bila shaka, watu huongea sana kuhusu upendo. Watu wanaendelea kuandika vitabu, kutunga nyimbo, na mashairi mengi sana kuhusu upendo. Hata hivyo, nyakati nyingine hawafafanui ifaavyo maana ya upendo. Neno hilo limetumiwa sana hivi kwamba inaonekana limepoteza maana.

11, 12. (a) Ni wapi tu tunaweza kujifunza mambo mengi kuhusu upendo, na kwa nini? (b) Kigiriki cha awali kinataja kihususa upendo gani mbalimbali, na ni “upendo” gani unaotajwa mara nyingi katika Maandiko ya Kigiriki ya Kikristo? (Ona pia kielezi-chini.) (c) A·gaʹpe ni nini?

11 Hata hivyo, Biblia inafundisha waziwazi kuhusu upendo. Kamusi ya Vine’s Expository Dictionary of New Testament Words yasema hivi: “Upendo unaweza kuonyeshwa tu kupitia matendo.” Masimulizi ya Biblia kuhusu matendo ya Yehova yanatufundisha mengi kuhusu upendo wake ambao unamchochea kuwatendea viumbe wake kwa fadhili. Kwa mfano, ni jambo gani linaloweza kuonyesha sifa hiyo kwa njia bora kuliko tendo kuu zaidi la upendo wa Yehova tulilozungumzia awali? Tutaona matendo mengi ya Yehova ya upendo katika sura zinazofuata. Zaidi ya hayo, tunaweza kupata ufahamu wa ndani kutokana na maneno ya awali yanayotafsiriwa “upendo” katika Biblia. Kigiriki cha awali kilikuwa na maneno manne yaliyotafsiriwa “upendo.” * Kati ya maneno hayo, a·gaʹpe hutumiwa mara nyingi katika Maandiko ya Kigiriki ya Kikristo. Kamusi moja ya Biblia inasema kwamba hilo “ndilo neno linaloeleza upendo kwa njia nzuri zaidi.” Kwa nini?

12 A·gaʹpe ni upendo unaoongozwa na kanuni. Si hisia tunayokuwa nayo bila kufikiri. Upendo huo unatia ndani mambo mengi, unahusisha fikira na una kusudi fulani. Zaidi ya yote, upendo wa a·gaʹpe hauna ubinafsi. Kwa mfano, soma tena Yohana 3:16. Ni “ulimwengu” upi ambao Mungu aliupenda sana hivi kwamba akamtoa Mwanaye mzaliwa-pekee? Ulimwengu huo ni wanadamu wanaoweza kukombolewa. Unatia ndani watu wengi ambao wanaendelea kutenda dhambi maishani. Je, Yehova anampenda kila mtu kama alivyompenda Abrahamu mwaminifu, aliyekuwa rafiki yake? (Yakobo 2:23) La, lakini kwa upendo, Yehova anawatendea watu wote mema hata kwa hasara yake. Anataka watu wote watubu na kubadili njia zao. (2 Petro 3:9) Wengi hufanya hivyo. Naye hufurahi kuwa rafiki yao.

13, 14. Ni nini kinachoonyesha kwamba mara nyingi a·gaʹpe huhusisha shauku ya kirafiki?

13 Hata hivyo, watu fulani wana maoni yasiyofaa kuhusu a·gaʹpe. Wanafikiri kwamba huo ni upendo usio na hisia, unaoongozwa na akili tu. Ukweli ni kwamba mara nyingi a·gaʹpe huhusisha uhusiano wa karibu wenye upendo. Kwa mfano, Yohana alipoandika, “Baba humpenda Mwana,” alitumia aina fulani ya neno a·gaʹpe. Je, upendo huo hauna shauku ya kirafiki? Ona kwamba Yesu alisema “Baba ana shauku na Mwana,” na hapo anatumia aina fulani ya neno phi·leʹo. (Yohana 3:35; 5:20) Mara nyingi upendo wa Yehova hutia ndani shauku ya moyoni. Lakini, upendo wake hautegemei kamwe hisia. Sikuzote unaongozwa na kanuni zake za hekima na haki.

14 Kama tulivyoona, sifa zote za Yehova ni bora sana, ni kamilifu, na zinavutia. Lakini upendo unavutia kuliko sifa nyingine zote. Hakuna kitu kinachotufanya tumkaribie Yehova kama upendo. Inafurahisha kwamba upendo ndio sifa kuu zaidi ya Yehova. Twajuaje?

“Mungu Ni Upendo”

15. Biblia inasema nini kuhusu sifa ya Yehova ya upendo, na kwa nini usemi huo ni wa pekee sana? (Ona pia kielezi-chini.)

15 Biblia inasema jambo fulani la pekee kuhusu upendo ambalo haisemi kuhusu zile sifa nyingine kuu za Yehova. Maandiko hayasemi kwamba Mungu ni nguvu wala hayasemi kwamba Mungu ni haki au hata Mungu ni hekima. Ana sifa hizo, yeye ndiye chanzo chake, na hana kifani katika sifa hizo tatu. Hata hivyo, kuhusu sifa ya nne, Biblia inasema jambo fulani la pekee sana: “Mungu ni upendo.” * (1 Yohana 4:8) Hilo lamaanisha nini?

16-18. (a) Kwa nini Biblia inasema kwamba “Mungu ni upendo”? (b) Kati ya viumbe wote duniani, kwa nini mwanadamu ni mfano unaofaa wa sifa ya Yehova ya upendo?

16 Usemi “Mungu ni upendo” haulingani na usemi, “Mungu ni sawa na upendo.” Hatuwezi kamwe kugeuza usemi huo na kusema “upendo ni Mungu.” Yehova si sifa fulani tu. Ana utu, na mbali na upendo ana hisia na sifa nyingi mbalimbali. Hata hivyo, Yehova ana upendo mwingi sana. Kichapo kimoja cha marejeo kinasema hivi kuhusu mstari huo: “Upendo ni utu au sifa ya asili ya Mungu.” Kwa ujumla, tunaweza kulifikiria jambo hilo kwa njia hii: Nguvu za Yehova humwezesha kutenda. Haki na hekima yake humwongoza kutenda. Lakini upendo wa Yehova humchochea kutenda. Naye sikuzote hutumia sifa nyingine zote kupatana na upendo wake.

17 Mara nyingi imesemwa kwamba Yehova ni wonyesho halisi wa upendo. Kwa hiyo, tukitaka kujifunza kuhusu upendo unaotegemea kanuni, ni lazima tujifunze kumhusu Yehova. Bila shaka, wanadamu pia wana sifa hiyo yenye kupendeza. Lakini kwa nini wanadamu wana sifa hiyo? Wakati wa uumbaji, Yehova alimwambia hivi Mwanaye: “Na tumfanye mtu kwa mfano wetu, kwa sura yetu.” (Mwanzo 1:26) Kati ya viumbe wote duniani, ni wanaume na wanawake tu wanaoweza kupenda na hivyo kumwiga Baba yao wa mbinguni. Kumbuka kwamba Yehova alitumia viumbe mbalimbali kuwa mifano ya sifa zake kuu. Hata hivyo, Yehova alimtumia mwanadamu—kiumbe bora zaidi duniani—kuwa mfano wa sifa Yake kuu zaidi ya upendo.—Ezekieli 1:10.

18 Tunapowapenda wengine bila ubinafsi kupatana na kanuni, tunaonyesha sifa kuu zaidi ya Yehova. Ni kama mtume Yohana alivyoandika: “Kwa habari yetu, twapenda, kwa sababu yeye alitupenda sisi kwanza.” (1 Yohana 4:19) Lakini Yehova alitupenda kwanza kwa njia zipi?

Yehova Alitupenda Kwanza

19. Kwa nini yaweza kusemwa kwamba upendo ndio uliomfanya Yehova aumbe?

19 Upendo si sifa mpya. Ni nini kilichomfanya Yehova aanze kuumba? Si kwa sababu alikuwa mpweke na alihitaji mwandani. Yehova ni kamili, hapungukiwi kwa vyovyote wala hahitaji msaada wa yeyote. Lakini alichochewa na sifa yake ya upendo ambayo inaonyeshwa kwa matendo, awape uhai viumbe wake wenye akili ambao wangeweza kuthamini zawadi hiyo. Mwanaye mzaliwa-pekee alikuwa “mwanzo wa uumbaji wa Mungu.” (Ufunuo 3:14) Yehova alimtumia Stadi huyo wa Kazi kuumba vitu vinginevyo vyote, kuanzia malaika. (Ayubu 38:4, 7; Wakolosai 1:16) Wakiwa wamepewa uhuru, akili, na hisia, viumbe hao wa roho wenye nguvu waliweza kuwa na uhusiano wenye upendo—kati yao wenyewe na, zaidi ya yote, pamoja na Yehova Mungu. (2 Wakorintho 3:17) Kwa hiyo, walipendana kwa sababu walipendwa kwanza.

20, 21. Ni mambo gani yaliyoonyesha kwamba Yehova aliwapenda Adamu na Hawa, lakini walitendaje?

20 Ndivyo na wanadamu. Tangu mwanzo, Adamu na Hawa walionyeshwa upendo mwingi sana. Kulikuwa na mambo mengi katika makao yao ya Paradiso ya Edeni yaliyowathibitishia kwamba Baba yao aliwapenda. Angalia jinsi Biblia inavyosema: “BWANA Mungu akapanda bustani upande wa mashariki wa Edeni, akamweka ndani yake huyo mtu aliyemfanya.” (Mwanzo 2:8) Je, umewahi kutembelea bustani maridadi kwelikweli? Ni nini kilichokupendeza zaidi? Je, ni nuru iliyopenya majani ya miti kwenye sehemu ya bustani iliyo kimya na yenye kivuli? Je, ni rangi zenye kuvutia sana za maua? Je, ni sauti ya bubujiko la kijito, ndege wanaoimba, na wadudu wanaovuma? Vipi harufu nzuri ya miti, matunda na maua yaliyochanua? Kwa vyovyote vile, hakuna bustani leo inayoweza kulinganishwa na bustani ya Edeni. Kwa nini?

21 Bustani hiyo ilipandwa na Yehova mwenyewe! Bila shaka ilikuwa maridadi isivyoelezeka. Ilikuwa na kila aina ya mti wenye kuvutia na wenye matunda matamu. Bustani hiyo ilikuwa na maji ya kutosha, ilikuwa kubwa sana, na ilikuwa na wanyama mbalimbali wenye kuvutia. Adamu na Hawa walikuwa na kila kitu walichohitaji ili kuishi maisha yenye furaha na yenye kuridhisha, na walikuwa na kazi yenye kuridhisha na urafiki mkamilifu. Yehova aliwapenda kwanza, na walikuwa na kila sababu ya kumpenda vilevile. Lakini walishindwa kufanya hivyo. Badala ya kumtii Baba yao wa mbinguni kwa upendo, walimwasi kwa sababu ya ubinafsi.—Mwanzo, sura ya 2.

22. Hatua ambayo Yehova alichukua baada ya uasi katika Edeni ilithibitishaje kwamba upendo wake ni mwaminifu?

22 Jambo hilo lilimhuzunisha Yehova sana. Lakini je, uasi huo ulitia uchungu moyo wake wenye upendo? La! “Fadhili zake [au, “upendo-mwaminifu,” NW, kielezi-chini] ni za milele.” (Zaburi 136:1) Kwa hiyo, kwa upendo, alikusudia mara moja kufanya mipango ya kumkomboa mzao yeyote wa Adamu na Hawa ambaye ana mwelekeo unaofaa. Kama tulivyoona, mipango hiyo ilitia ndani dhabihu ya fidia ya Mwanaye mpendwa, ambayo ilimgharimu sana Baba yake.—1 Yohana 4:10.

23. Taja sababu moja inayomfanya Yehova awe “Mungu mwenye furaha,” na sura inayofuata itajibu swali gani muhimu?

23 Naam, tangu mwanzo Yehova amechukua hatua ya kwanza kuwapenda wanadamu. ‘Alitupenda kwanza’ katika njia nyingi sana. Upendo hudumisha amani na shangwe, ndiyo sababu Yehova anaitwa “Mungu mwenye furaha.” (1 Timotheo 1:11) Hata hivyo, swali muhimu linazuka. Je, kweli Yehova anampenda kila mmoja wetu? Sura inayofuata itajibu swali hilo.

^ fu. 11 Kitenzi phi·leʹo, kinachomaanisha ‘kuwa na shauku, kuthamini, au kupenda (kama mtu anavyompenda rafiki wa karibu au ndugu),” hutumiwa mara nyingi katika Maandiko ya Kigiriki ya Kikristo. Aina fulani ya neno stor·geʹ, au upendo uliopo kati ya watu wa familia, inatumiwa kwenye 2 Timotheo 3:3 kuonyesha kwamba upendo huo ungekuwa haba katika siku za mwisho. Neno Eʹros, au upendo wa kimahaba kati ya watu wa jinsia tofauti, halitajwi katika Maandiko ya Kigiriki ya Kikristo, ijapokuwa upendo huo unazungumziwa katika Biblia.—Mithali 5:15-20.

^ fu. 15 Maandiko mengine yanatumia semi kama hizo. Kwa mfano, “Mungu ni nuru” na “Mungu . . . ni moto unaokula kabisa.” (1 Yohana 1:5; Waebrania 12:29) Lakini semi hizo zinapasa kuonwa kuwa milinganisho (sitiari), kwa kuwa zinamlinganisha Yehova na vitu vya asili. Yehova ni kama nuru, kwa kuwa yeye ni mtakatifu na mwadilifu. Hana “giza” wala uchafu wowote. Naye anaweza kulinganishwa na moto kwa sababu ya nguvu zake za kuangamiza.