Hamia kwenye habari

Hamia kwenye yaliyomo

Sura ya 25

“Huruma Nyororo ya Mungu Wetu”

“Huruma Nyororo ya Mungu Wetu”

1, 2. (a) Mama hutendaje mtoto wake mchanga anapolia? (b) Ni hisia gani ambayo ni yenye nguvu zaidi kuliko huruma ya mama?

MTOTO mchanga aanza kulia usiku wa manane. Mama yake anaamka mara moja. Mama halali kwa utulivu tangu alipojifungua mtoto huyo. Amejua kutofautisha vilio mbalimbali vya mtoto wake mchanga. Kwa hiyo, kwa kawaida anaweza kujua iwapo mtoto wake anahitaji kunyonya, kubebwa, au kushughulikiwa kwa njia nyingine. Mama humshughulikia mtoto wake haidhuru sababu inayomfanya alie. Hawezi kupuuza mahitaji ya mtoto wake kwa sababu anampenda sana.

2 Huruma ya mama kwa mtoto wake ni mojawapo ya hisia zenye nguvu sana ambazo wanadamu huonyesha. Hata hivyo, kuna hisia ambayo ni yenye nguvu kupita hisia zote—huruma nyororo ya Mungu wetu Yehova. Tunaweza kumkaribia Yehova zaidi tukichunguza sifa hii yenye kuvutia. Basi na tuzungumzie maana ya huruma na jinsi ambavyo Mungu wetu huonyesha sifa hiyo.

Huruma Ni Nini?

3. Kitenzi cha Kiebrania kinachotafsiriwa “onyesha rehema” au “hurumia” kinamaanisha nini?

3 Katika Biblia, huruma na rehema zinahusiana sana. Maneno kadhaa ya Kiebrania na Kigiriki yanadokeza sifa ya huruma yenye upendo. Kwa mfano, fikiria kitenzi cha Kiebrania ra·chamʹ, ambacho mara nyingi hutafsiriwa “onyesha rehema” au “hurumia.” Kichapo kimoja cha marejeo kinaeleza kwamba kitenzi ra·chamʹ “kinaonyesha huruma nyingi na yenye upendo, kama ile tunayohisi tunapowaona wapendwa wetu au wale wanaohitaji msaada wetu wakiteseka au kuumia.” Neno hilo la Kiebrania, ambalo Yehova anatumia kujihusu, linahusiana na neno linalomaanisha “tumbo la uzazi” nalo linaweza kufasiriwa kuwa “huruma ya mama.” *Kutoka 33:19; Yeremia 33:26.

“Je, mwanamke aweza kumsahau . . . mwana wa tumbo lake? ”

4, 5. Biblia inatumiaje hisia ambazo mama huwa nazo kwa mtoto wake mchanga kutufundisha kuhusu huruma ya Yehova?

Biblia inatumia hisia ambazo mama huwa nazo kwa mtoto wake mchanga kutufundisha maana ya huruma ya Yehova. Twasoma hivi kwenye Isaya 49:15: “Je! mwanamke aweza kumsahau mtoto wake anyonyaye, hata asimhurumie [ra·chamʹ] mwana wa tumbo lake? naam, hawa waweza kusahau, lakini mimi sitakusahau wewe.” Maelezo hayo yenye kugusa moyo yanakazia jinsi Yehova alivyo na huruma nyingi kwa watu wake. Jinsi gani?

5 Ni vigumu kuwazia kwamba mama anaweza kusahau kumnyonyesha na kumtunza mtoto wake mchanga. Kwani, mtoto mchanga ni hoi; anahitaji kupendwa na kutunzwa na mama yake usiku na mchana. Ingawa hivyo, inasikitisha kupata habari kuhusu akina mama wanaowatupa watoto wao, hasa katika ‘nyakati hizi za hatari’ kwa sababu watu hawana “shauku ya kiasili.” (2 Timotheo 3:1, 3) “Lakini mimi sitakusahau wewe,” atangaza Yehova. Yehova hakosi kamwe kuwaonyesha watumishi wake huruma nyororo. Huruma hiyo ni yenye nguvu zaidi ya hisia yenye nguvu tunayoweza kuwazia, yaani, huruma ambayo kwa kawaida mama humwonyesha mtoto wake mchanga. Haishangazi kwamba mtoa-maoni mmoja alisema hivi kuhusu Isaya 49:15: “Hili ni mojawapo, au ndilo neno linalofafanua upendo wa Mungu waziwazi zaidi katika Agano la Kale.”

6. Wanadamu wengi wasiokamilika wamekuwa na maoni gani kuhusu huruma nyororo, lakini Yehova anatuhakikishia nini?

6 Je, kuwa na huruma nyororo ni udhaifu? Wanadamu wengi wasiokamilika wamekuwa na maoni hayo. Kwa mfano, mwanafalsafa Mroma Seneca, msomi maarufu wa Roma ambaye aliishi wakati wa Yesu, alifundisha kwamba “huruma ni udhaifu wa akili.” Seneca aliunga mkono Ustoiki, falsafa inayokazia kuwa na utulivu bila hisia zozote. Mtu mwenye hekima anaweza kuwasaidia wale wanaotaabika, akasema Seneca, lakini hapaswi kuwahurumia kwa sababu atakosa utulivu akifanya hivyo. Maoni hayo ya ubinafsi kuhusu maisha yaliwazuia watu wasionyeshe huruma kutoka moyoni. Lakini sivyo alivyo Yehova! Yehova anatuhakikishia katika Neno lake kwamba yeye “ni mwenye wororo sana katika shauku na mwenye rehema [kihalisi, “mwenye huruma”].” (Yakobo 5:11) Kama tutakavyoona, kuonyesha huruma si udhaifu bali ni sifa muhimu sana yenye nguvu. Hebu tuone jinsi Yehova anavyoonyesha sifa hiyo kama mzazi mwenye upendo.

Yehova Alipolihurumia Taifa

7, 8. Waisraeli walitesekaje katika Misri ya kale, na Yehova alichukua hatua gani kwa sababu ya mateso yao?

7 Huruma ya Yehova yaonekana wazi kutokana na jinsi alivyoshughulika na taifa la Israeli. Kufikia mwishoni mwa karne ya 16 K.W.K., mamilioni ya Waisraeli waliteswa sana walipokuwa watumwa katika Misri ya kale. Wamisri ‘walifanya maisha yao kuwa uchungu kwa kazi ngumu; kazi ya chokaa na ya matofali.’ (Kutoka 1:11, 14) Waisraeli walimlilia Yehova awasaidie walipokuwa wakiteseka. Mungu mwenye huruma nyororo alichukua hatua gani?

8 Yehova aliwahurumia. Akasema: “Hakika nimeyaona mateso ya watu wangu walioko Misri, nami nimekisikia kilio chao kwa sababu ya wasimamizi wao; maana nayajua maumivu yao.” (Kutoka 3:7) Yehova hakuweza kamwe kutazama watu wake wakiteseka au kusikia vilio vyao na asiwahurumie. Kama tulivyoona katika Sura ya 24 ya kitabu hiki, Yehova ni Mungu mwenye hisia-mwenzi. Na hisia-mwenzi, yaani, sifa ya kuguswa moyo na uchungu wa wengine inahusiana sana na huruma. Lakini Yehova hakuwahurumia tu watu wake; alichochewa kuwasaidia. Andiko la Isaya 63:9 lasema: “Kwa mapenzi yake, na huruma zake, aliwakomboa mwenyewe.” Yehova aliwaokoa Waisraeli kutoka Misri kwa “mkono hodari.” (Kumbukumbu la Torati 4:34) Baadaye, aliwalisha kimuujiza na kuwapa nchi yenye rutuba.

9, 10. (a) Kwa nini Yehova aliwakomboa Waisraeli tena na tena baada ya kuingia katika Nchi Iliyoahidiwa? (b) Katika siku za Yeftha, Yehova aliwakomboa Waisraeli kutoka katika mateso gani, ni nini kilichomchochea kufanya hivyo?

9 Huruma ya Yehova haikuishia hapo. Waisraeli walimwasi tena na tena baada ya kuingia katika Nchi Iliyoahidiwa na hivyo wakateseka. Lakini walirudiwa na fahamu na kumlilia Yehova. Aliwakomboa tena na tena. Kwa nini? “Kwa sababu aliwahurumia watu wake.”—2 Mambo ya Nyakati 36:15; Waamuzi 2:11-16.

10 Fikiria mambo yaliyotukia siku za Yeftha. Waisraeli walipoanza kuitumikia miungu ya uwongo, Yehova aliwaacha wateswe na Waamoni kwa miaka 18. Mwishowe, walitubu. Biblia inatuambia hivi: “Nao wakaiondoa hiyo miungu ya kigeni iliyokuwa kati yao, nao wakamtumikia BWANA; na roho yake ilihuzunika kwa sababu ya msiba wa Israeli.” * (Waamuzi 10:6-16) Mara tu baada ya watu wake kutubu kikweli, Yehova hakuweza kuvumilia kuwaona wakiteseka. Kwa hiyo, Mungu mwenye huruma nyororo alimpa Yeftha nguvu ili awakomboe Waisraeli kutoka mikononi mwa adui zao.—Waamuzi 11:30-33.

11. Twajifunza nini kuhusu huruma tunapozingatia jinsi Yehova alivyoshughulika na Waisraeli?

11 Twajifunza nini kuhusu huruma nyororo ya Yehova tunapozingatia jinsi alivyoshughulika na taifa la Israeli? Jambo moja ambalo tunajifunza ni kwamba hawaonei huruma watu wanaoteseka na kuwaacha tu. Kumbuka yule mama ambaye anachochewa na huruma kumsaidia mtoto wake mchanga anayelia. Vivyo hivyo, Yehova hapuuzi vilio vya watu wake. Huruma yake nyororo humchochea kukomesha mateso yao. Zaidi ya hayo, twajifunza pia kwamba huruma si udhaifu kamwe, kwa sababu sifa hii ya kutoka moyoni ilimchochea achukue hatua madhubuti ya kuwatetea watu wake. Lakini je, Yehova anawahurumia watumishi wake wakiwa kikundi tu?

Yehova Amhurumia Mtu Mmoja-Mmoja

12. Sheria ilionyeshaje huruma ya Yehova kwa mtu mmoja-mmoja?

12 Sheria ambayo Mungu alilipa taifa la Israeli ilionyesha kwamba alimhurumia mtu mmoja-mmoja. Kwa mfano, fikiria jinsi alivyowajali maskini. Yehova alijua kwamba Mwisraeli angeweza kuwa maskini kwa sababu ya hali zisizotazamiwa. Maskini walipaswa kutendewaje? Yehova aliwapa Waisraeli amri hii kali: “Usifanye moyo wako kuwa mgumu, wala usimfumbie mkono wako nduguyo maskini. Mpe kwa kweli, wala moyo wako usisikitike utakapompa; kwa kuwa atakubarikia BWANA, Mungu wako, kwa neno hili katika kazi yako yote.” (Kumbukumbu la Torati 15:7, 10) Yehova pia aliwaagiza Waisraeli wasivune kabisa pembeni mwa mashamba yao au kukusanya masazo. Masazo hayo yaliachwa kwa ajili ya maskini. (Mambo ya Walawi 23:22; Ruthu 2:2-7) Taifa la Israeli lilipotii sheria hiyo, maskini hawakuhitaji kuombaomba chakula. Hilo laonyesha huruma nyororo ya Yehova, sivyo?

13, 14. (a) Maneno ya Daudi yanatuhakikishiaje kwamba Yehova anamjali sana kila mmoja wetu? (b) Toa mfano kuonyesha kwamba Yehova yu karibu na wale “waliovunjika moyo” au “waliopondeka roho.”

13 Leo pia, Mungu wetu mwenye upendo anamjali sana kila mmoja wetu. Tunaweza kuwa na hakika kwamba anajua kabisa mateso yoyote ambayo huenda yakatupata. Mtunga-zaburi Daudi aliandika hivi: “Macho ya BWANA huwaelekea wenye haki, na masikio yake hukielekea kilio chao. BWANA yu karibu nao waliovunjika moyo, na waliopondeka roho huwaokoa.” (Zaburi 34:15, 18) Mtoa-maoni mmoja wa Biblia aeleza hivi kuhusu wale wanaotajwa na andiko hilo: “Ni watu waliovunjika moyo na wenye majuto, yaani, watu walionyenyekezwa na dhambi, wasiojiheshimu; wanaojiona kuwa duni, na wasiojiamini.” Huenda wakahisi kwamba Yehova yu mbali na wao, na kwamba wao ni duni hivi kwamba hawezi kuwajali. Lakini sivyo ilivyo. Maneno ya Daudi yanatuhakikishia kwamba Yehova hawaachi wale “wanaojiona kuwa duni.” Mungu wetu mwenye huruma anajua kwamba tunahitaji msaada wake sana tunapohisi hivyo, naye yu tayari kutusaidia.

14 Fikiria kisa hiki halisi. Mama mmoja nchini Marekani alimpeleka mwanaye mwenye umri wa miaka miwili hospitalini kwa sababu alikuwa na ugonjwa mbaya wa kifaduro. Baada ya kumchunguza, madaktari walimwambia mama kwamba mwanaye angelazwa hospitalini usiku huo. Mama alikesha wapi usiku huo? Alikesha kwenye kiti humohumo hospitalini, karibu na kitanda cha mwanaye! Mwanaye alikuwa mgonjwa kwa hiyo mama alitaka sana kuwa karibu naye. Bila shaka, tunaweza kumtarajia Baba yetu wa mbinguni mwenye upendo atufanyie mengi zaidi! Kwani, tumeumbwa kwa mfano wake. (Mwanzo 1:26) Maneno yenye kugusa moyo ya Zaburi 34:18 yanatueleza kwamba ‘tunapovunjika moyo’ au ‘kupondeka roho,’ Yehova, kama baba mwenye upendo, “yu karibu”—sikuzote akiwa mwenye huruma na tayari kutusaidia.

15. Yehova anamsaidiaje kila mmoja wetu?

15 Basi, Yehova anamsaidiaje kila mmoja wetu? Haondoi kisababishi cha mateso yetu sikuzote. Lakini Yehova amewapa maandalizi tele wale wanaomwomba msaada. Neno lake, Biblia, lina mashauri yanayofaa ambayo yanaweza kuboresha hali. Katika kutaniko, Yehova ameweka waangalizi wanaostahili kiroho, ambao wanajitahidi kuwa na huruma kama yeye wanapowasaidia waabudu wenzao. (Yakobo 5:14, 15) Akiwa “Msikiaji wa sala,” yeye huwapa “roho takatifu wale wanaomwomba.” (Zaburi 65:2, NW; Luka 11:13) Roho hiyo inaweza kututia “nguvu ipitayo iliyo ya kawaida” ili tuweze kuvumilia hadi Ufalme wa Mungu utakapokomesha matatizo yote yanayofadhaisha. (2 Wakorintho 4:7) Tunamshukuru kwelikweli kwa sababu ya maandalizi hayo yote, sivyo? Tusisahau kwamba maandalizi hayo ni uthibitisho wa huruma nyororo ya Yehova.

16. Yehova alionyesha huruma yake kwa njia gani bora, na inamfaidije kila mmoja wetu?

16 Hapana shaka kwamba Yehova alionyesha huruma yake kwa njia bora zaidi alipomtoa Yule anayempenda sana awe fidia kwa ajili yetu. Yehova alionyesha upendo kwa kutoa dhabihu hiyo ambayo ilitufungulia njia ya kupata wokovu. Kumbuka kwamba fidia hiyo inamfaidi kila mmoja wetu. Ndiyo sababu Zekaria, baba ya Yohana Mbatizaji, alitabiri kwamba zawadi hiyo ilithibitisha “huruma nyororo ya Mungu wetu.”—Luka 1:78.

Huruma ya Yehova Inapofikia Kikomo

17-19. (a) Biblia inaonyeshaje kwamba huruma ya Yehova ina kikomo? (b) Kwa nini huruma ya Yehova kwa watu wake ilifikia kikomo?

17 Je, tufikiri kwamba huruma nyororo ya Yehova haina kikomo? La hasha, Biblia inaonyesha waziwazi kwamba Yehova hawahurumii watu ambao wanakataa njia zake adilifu. (Waebrania 10:28) Ili kuelewa sababu inayomfanya atende hivyo, kumbuka taifa la Israeli.

18 Ijapokuwa Yehova aliwakomboa tena na tena kutoka kwa maadui wao, mwishowe huruma yake ilifikia kikomo. Watu hao wakaidi waliabudu sanamu, hata walileta sanamu zao zenye kuchukiza ndani ya hekalu la Yehova! (Ezekieli 5:11; 8:17, 18) Zaidi ya hayo, twaambiwa hivi: “Waliwadhihaki wajumbe wa Mungu, na kuyadharau maneno yake, na kuwacheka manabii wake, hata ilipozidi ghadhabu ya BWANA juu ya watu wake, hata kusiwe na kuponya.” (2 Mambo ya Nyakati 36:16) Hatimaye Waisraeli walizidi hivi kwamba hakukuwa na msingi wowote ufaao wa kuwahurumia, nao walichochea hasira adilifu ya Yehova. Matokeo yakawa nini?

19 Yehova hakuweza tena kuwahurumia watu wake. Alitangaza hivi: “Sitawahurumia, sitawaachia wala sitawarehemu, bali nitawaangamiza.” (Yeremia 13:14, BHN) Basi, Yerusalemu na hekalu lake liliharibiwa, na Waisraeli wakachukuliwa mateka hadi Babiloni. Matokeo yanakuwa mabaya kama nini wanadamu wenye dhambi wanapoasi sana hivi kwamba huruma ya Mungu inafikia kikomo!—Maombolezo 2:21.

20, 21. (a) Ni nini kitakachotukia huruma ya Mungu itakapofikia kikomo katika siku zetu? (b) Tutazungumzia zawadi gani ya huruma ya Yehova katika sura inayofuata?

20 Vipi leo? Yehova hajabadilika. Kwa sababu ya huruma yake, amewaamuru Mashahidi wake wahubiri ‘habari njema ya ufalme’ katika dunia yote inayokaliwa. (Mathayo 24:14) Watu wenye mioyo minyoofu wanapoitikia, Yehova huwasaidia kuelewa ujumbe wa Ufalme. (Matendo 16:14) Lakini kazi hii haitaendelea milele. Bila shaka ni kinyume cha huruma ya Yehova kuruhusu ulimwengu huu mwovu pamoja na mateso na taabu zake ziendelee milele. Yehova atahukumu mfumo huu wa mambo huruma yake itakapofikia kikomo. Hata wakati huo, atakuwa akionyesha huruma—huruma kwa ajili ya ‘jina lake takatifu’ na kwa ajili ya watumishi wake waaminifu. (Ezekieli 36:20-23) Yehova atakomesha kabisa uovu na kuleta ulimwengu mpya wenye uadilifu. Yehova atangaza hivi kuhusu waovu: “Jicho langu halitaachilia, wala sitaona huruma; lakini nitaleta njia yao juu ya vichwa vyao.”—Ezekieli 9:10.

21 Kabla ya wakati huo, Yehova anawahurumia watu, hata wale ambao wanakabili uharibifu. Wanadamu wenye dhambi ambao wanatubu kikweli wanaweza kufaidika na mojawapo ya zawadi bora zaidi za huruma ya Yehova, yaani, msamaha. Katika sura inayofuata, tutazungumzia baadhi ya masimulizi ya Biblia yanayoonyesha jinsi Yehova anavyosamehe kabisa.

^ fu. 3 Hata hivyo, kwenye Zaburi 103:13, kitenzi cha Kiebrania ra·chamʹ kinamaanisha rehema, au huruma, ambayo baba huwaonyesha watoto wake.

^ fu. 10 Usemi unaotafsiriwa “roho yake ilihuzunika” wamaanisha kihalisi ‘subira yake ilifikia kikomo.’ Biblia Habari Njema yasema: “Hakuweza kuvumilia zaidi kuona taabu za Waisraeli.” Kichapo Tanakh—A New Translation of the Holy Scriptures chasema hivi: “Hakuweza kustahimili kuona Israeli ikitaabika.”