Hamia kwenye habari

Hamia kwenye yaliyomo

Sura ya 29

“Kuujua Upendo wa Kristo”

“Kuujua Upendo wa Kristo”

1-3. (a) Ni nini kilichomchochea Yesu atake kumwiga Baba yake? (b) Tutachunguza sehemu zipi za upendo wa Yesu?

JE, UMEWAHI kumwona mvulana mdogo akijaribu kumwiga baba yake? Huenda akaiga jinsi baba yake anavyotembea, anavyoongea, au anavyotenda. Muda si muda, huenda mvulana huyo akaanza kufuata maadili na kanuni za kiroho za baba yake. Naam, mvulana huyo hujitahidi kuwa kama baba yake kwa sababu anampenda na kumthamini.

2 Vipi uhusiano wa Yesu na Baba yake wa mbinguni? Yesu alisema hivi pindi moja: “Nampenda Baba.” (Yohana 14:31) Hakuna mtu yeyote anayeweza kumpenda Yehova kama Mwana huyo, ambaye alikaa na Baba yake kwa muda mrefu sana kabla kiumbe yeyote hajaumbwa. Upendo ulimchochea Mwana huyo mwaminifu kutaka kumwiga Baba yake.—Yohana 14:9.

3 Katika sura zilizotangulia za kitabu hiki, tulizungumzia jinsi ambavyo Yesu aliiga kikamili nguvu, haki, na hekima ya Yehova. Lakini Yesu alionyeshaje upendo wa Baba yake? Hebu tuchunguze sehemu tatu za upendo wa Yesu—roho yake ya kujidhabihu, huruma yake nyororo, na utayari wake wa kusamehe.

“Hakuna Aliye na Upendo Mkubwa Zaidi Kuliko Huu”

4. Yesu alionyeshaje mfano bora kabisa wa upendo wa kujidhabihu akiwa binadamu?

4 Yesu alionyesha upendo wa kujidhabihu kwa njia bora sana. Kujidhabihu ni kutanguliza mahitaji na masilahi ya wengine bila ubinafsi. Yesu alionyeshaje upendo huo? Yeye mwenyewe alieleza hivi: “Hakuna aliye na upendo mkubwa zaidi kuliko huu, kwamba mtu fulani aisalimishe nafsi yake kwa niaba ya marafiki wake.” (Yohana 15:13) Yesu alitoa uhai wake mkamilifu kwa hiari kwa ajili yetu. Huo ulikuwa wonyesho mkuu zaidi wa upendo kuwahi kuonyeshwa na mwanadamu yeyote. Lakini Yesu alionyesha upendo wa kujidhabihu kwa njia nyinginezo pia.

5. Kwa nini lile tendo la Mwana mzaliwa-pekee wa Mungu kuondoka mbinguni lilikuwa kujidhabihu kwa upendo?

5 Kabla ya kuwa mwanadamu, Mwana huyo mzaliwa-pekee wa Mungu alikuwa na cheo cha juu na cha pekee huko mbinguni. Alishirikiana kwa ukaribu sana na Yehova na viumbe wengi wa roho. Licha ya mapendeleo hayo, Mwana huyo mpendwa “alijifanya mwenyewe kuwa mtupu na kuchukua umbo la mtumwa na kuja kuwa katika ufanani wa wanadamu.” (Wafilipi 2:7) Kwa hiari, alikuja kuishi na wanadamu wenye dhambi katika ulimwengu ambao “unakaa katika nguvu ya mwovu.” (1 Yohana 5:19) Bila shaka Mwana wa Mungu alijidhabihu kwa upendo, sivyo?

6, 7. (a) Yesu alijidhabihu kwa upendo katika njia zipi wakati wa huduma yake duniani? (b) Andiko la Yohana 19:25-27 lasimulia jambo gani lenye kugusa moyo kuhusu upendo wa kujidhabihu?

6 Wakati wa huduma yake duniani, Yesu alijidhabihu kwa upendo katika njia mbalimbali. Hakuwa na ubinafsi wowote. Alijishughulisha mno na huduma yake hivi kwamba alijinyima mambo ya kawaida ambayo wanadamu wamezoea. “Mbweha wana mapango na ndege wa mbinguni wana viota, lakini Mwana wa binadamu hana mahali popote pa kulaza kichwa chake.” (Mathayo 8:20) Yesu alikuwa seremala stadi sana, kwa hiyo angeweza kujijengea nyumba nzuri sana au angeweza kupata pesa kwa kutengeneza na kuuza fanicha maridadi sana. Lakini hakutumia ustadi wake kupata vitu vya kimwili.

7 Andiko la Yohana 19:25-27 lasimulia jambo lenye kugusa moyo sana kuhusu upendo wa Yesu wa kujidhabihu. Fikiria mambo mengi ambayo yalikuwa katika akili na moyo wa Yesu alasiri ambayo angeuawa. Alipokuwa akiteseka kwenye mti wa mateso, aliwafikiria wanafunzi wake, kazi ya kuhubiri, na hasa uaminifu wake na sifa ambayo angeletea jina la Baba yake. Kwa kweli, wakati ujao wa wanadamu wote ulimtegemea! Hata hivyo, muda mfupi tu kabla ya kufa, Yesu alimhangaikia pia mama yake, Maria, ambaye yaelekea alikuwa mjane wakati huo. Yesu alimwomba mtume Yohana amtunze Maria kama mama yake. Kisha mtume Yohana alimchukua Maria na kwenda naye nyumbani. Kwa njia hiyo, Yesu alifanya mipango ili mama yake atunzwe kimwili na kiroho. Alionyesha upendo ulioje usio na ubinafsi!

‘Alisukumwa na Sikitiko’

8. Neno la Kigiriki ambalo linatumiwa na Biblia kufafanua huruma ya Yesu linamaanisha nini?

8 Yesu alikuwa na huruma kama Baba yake. Maandiko yanaonyesha jinsi ambavyo Yesu alijitahidi kuwasaidia watu waliotaabika kwa sababu aliwahurumia sana. Biblia inafafanua huruma ya Yesu kwa kutumia neno la Kigiriki linalotafsiriwa “sukumwa na sikitiko.” Msomi mmoja anasema hivi: ‘Neno hilo linafafanua hisia ya ndani sana ambayo inamchochea mtu kutoka moyoni. Hakuna neno jingine la Kigiriki linalofafanua hisia ya huruma kwa mkazo sana kama neno hilo.’ Ebu ona pindi fulani-fulani ambapo huruma ilimchochea Yesu kutenda.

9, 10. (a) Ni kwa nini Yesu na mitume wake walitafuta mahali pa faragha? (b) Yesu alihisije umati ulipovuruga faragha yake, na kwa nini?

9 Alichochewa kuwasaidia watu kiroho. Simulizi la Marko 6:30-34 laonyesha sababu iliyomfanya Yesu awasikitikie watu. Wazia hali ilivyokuwa. Mitume walifurahi sana baada ya kuhubiri kotekote. Walirudi kwa Yesu na kumsimulia kwa shauku mambo yote waliyoona na kusikia. Lakini umati mkubwa ukakusanyika, na Yesu na mitume wake wakakosa hata nafasi ya kula. Daima akiwa makini, Yesu akafahamu kwamba mitume wamechoka. Akawaambia: “Njoni, nyinyi wenyewe, kwa faragha mwingie katika mahali pa upweke mpumzike kidogo.” Walipanda mashua na kuvuka upande wa kaskazini wa Bahari ya Galilaya hadi mahali pa faragha. Lakini umati uliwaona wakienda. Wengine walipata habari hizo pia. Watu hao wote walikimbia kuzunguka ufuko wa kaskazini wa bahari hiyo na kufika ng’ambo nyingine kabla ya ile mashua!

10 Je, Yesu alikasirika kwa sababu watu walivuruga faragha yake? La hasha! Alisikitika sana alipoona umati huo wa maelfu ya watu ukimsubiri. Marko aliandika hivi: “Akaona umati mkubwa, lakini akasukumwa na sikitiko kwa ajili yao, kwa sababu walikuwa kama kondoo wasio na mchungaji. Naye akaanza kuwafundisha mambo mengi.” Yesu alitambua kwamba watu hao walikuwa na mahitaji ya kiroho. Walikuwa kama kondoo wanaozurura huku na huku bila mchungaji wa kuwaongoza au kuwalinda. Yesu alijua kwamba watu wa kawaida walipuuzwa na viongozi wa kidini ambao badala ya kuwa wachungaji wenye kujali, waliwatendea bila huruma. (Yohana 7:47-49) Aliwasikitikia sana watu, akaanza kuwafundisha “juu ya ufalme wa Mungu.” (Luka 9:11) Ona kwamba Yesu aliwasikitikia watu hata bila kujua jinsi ambavyo wangeitikia mafundisho yake. Yaani, Yesu hakuwahurumia watu kwa sababu tu walikubali mafundisho yake bali aliwafundisha kwa sababu alichochewa na huruma yake nyororo.

“Akanyoosha mkono wake akamgusa”

11, 12. (a) Wenye ukoma walitendewaje nyakati za Biblia, lakini Yesu alitendaje alipofikiwa na mtu “mwenye kujaa ukoma”? (b) Huenda mtu mwenye ukoma aliyeguswa na Yesu alihisije, na kisa halisi cha daktari mmoja kinathibitishaje jambo hilo?

11 Alichochewa kukomesha mateso. Watu wenye magonjwa mbalimbali walivutiwa na Yesu kwa sababu walijua yeye ni mwenye huruma. Jambo hilo lilionekana wazi wakati Yesu huku akifuatwa na umati alipofikiwa na mtu “mwenye kujaa ukoma.” (Luka 5:11, 12) Katika nyakati za Biblia, wenye ukoma walitengwa ili wasiwaambukize wengine. (Hesabu 5:1-4) Lakini baada ya muda, marabi wasio na huruma walikuwa na maoni mabaya kuhusu ukoma, hivyo wakatunga sheria zao wenyewe zenye kukandamiza. * Ingawa hivyo, hebu ona jinsi Yesu alivyomtendea yule mtu mwenye ukoma: “Huko pia mwenye ukoma akaja kwake, akimsihi sana hata kwa kukunja magoti, akimwambia: ‘Ikiwa tu wewe wataka, waweza kunifanya safi.’ Ndipo akasukumwa na sikitiko, naye akanyoosha mkono wake akamgusa, akamwambia: ‘Mimi nataka. Fanywa safi.’ Na mara hiyo ule ukoma ukamtoka.” (Marko 1:40-42) Yesu alijua kwamba mtu huyo mwenye ukoma hakupaswa kuwa miongoni mwa watu. Hata hivyo, badala ya kumfukuza, Yesu alimsikitikia sana hivi kwamba alifanya jambo la kushangaza. Yesu alimgusa!

12 Wafikiri mtu huyo alihisije alipoguswa na Yesu? Kwa mfano, hebu fikiria kisa hiki halisi. Dakt. Paul Brand, mtaalamu wa ukoma, asimulia kuhusu mtu mmoja mwenye ukoma ambaye alimtibu nchini India. Alipokuwa akimpima, daktari huyo alimshika begani na kumweleza kupitia mkalimani matibabu ambayo angepewa. Mtu huyo alianza kulia ghafula. Daktari akamwuliza, “Nimesema jambo baya?” Mkalimani akamwuliza kijana huyo swali hilo katika lugha yake kisha akajibu: “La, daktari. Anasema analia kwa sababu umemshika begani. Hajapata kamwe kuguswa na yeyote kwa miaka mingi isipokuwa wewe.” Yule mtu mwenye ukoma aliyemfikia Yesu alifaidika hata zaidi alipoguswa naye. Baada ya kuguswa mara moja tu, ugonjwa uliomfanya atengwe na watu ulitoweka kabisa!

13, 14. (a) Yesu alikutana na msafara gani alipokaribia jiji la Naini, na kwa nini kisa hicho kilihuzunisha sana? (b) Yesu alichochewaje na huruma kumsaidia yule mjane wa Naini?

13 Alichochewa kuondoa huzuni. Yesu alisikitishwa sana na huzuni ya wengine. Kwa mfano, fikiria simulizi la Luka 7:11-15. Jambo hilo lilitukia alipokuwa anakaribia kumaliza nusu ya huduma yake duniani. Yesu alikuwa amekaribia jiji la Naini huko Galilaya alipokutana na msafara wa mazishi karibu na lango la jiji hilo. Kilikuwa kisa chenye kuhuzunisha sana. Mwana pekee wa mjane mmoja alikuwa amekufa. Yaelekea kwamba mjane huyo aliwahi kuwa katika msafara mwingine kama huo wakati wa mazishi ya mume wake. Sasa mwanaye ambaye huenda ndiye tu aliyemruzuku alikuwa amekufa. Yaelekea kwamba miongoni mwa umati ulioandamana naye mlikuwa na waombolezaji walioimba nyimbo za maombolezo na wanamuziki waliocheza miziki ya maombolezo. (Yeremia 9:17, 18; Mathayo 9:23) Hata hivyo, Yesu alimtazama sana mama huyo aliyekuwa na majonzi tele, ambaye yaelekea alifuata kwa ukaribu jeneza lililobeba maiti ya mwanaye.

14 Yesu ‘alimsikitikia’ mama huyo. Kwa sauti yenye kutia moyo, akamwambia hivi: “Koma kutoa machozi.” Akalikaribia jeneza na kuligusa. Wale waliokuwa wamelibeba—na labda umati wote—wakasimama tuli. Kwa sauti yenye nguvu, Yesu akamwambia hivi yule maiti: “Mwanamume kijana, nakuambia, Inuka!” Halafu ikawaje? “Huyo mfu akaketi na kuanza kusema” kana kwamba ameamshwa kutoka kwa usingizi mzito! Maneno yanayofuata yanagusa moyo sana: “Naye [Yesu] akampa huyo kwa mama yake.”

15. (a) Masimulizi ya Biblia yanayoeleza jinsi Yesu alivyowasikitikia watu, yanaonyesha kuna uhusiano gani kati ya huruma na matendo? (b) Tunawezaje kumwiga Yesu?

15 Twajifunza nini kutokana na visa hivyo? Katika kila kisa, angalia uhusiano uliopo kati ya huruma na matendo. Sikuzote Yesu aliwahurumia watu waliokuwa wakitaabika, na huruma hiyo ilimchochea kutenda. Tunawezaje kuiga mfano wake? Tukiwa Wakristo, tuna wajibu wa kuhubiri habari njema na kufanya wanafunzi. Upendo wetu kwa Mungu ndio hasa unaotuchochea. Na tukumbuke kwamba kazi ya kuhubiri ni njia ya kuwaonyesha watu huruma. Tukiwahurumia watu kama alivyofanya Yesu, moyo wetu utatuchochea kujitahidi tuwezavyo kuwahubiria habari njema. (Mathayo 22:37-39) Tutawaonyeshaje huruma waamini wenzetu ambao wanateseka au wamefiwa? Hatuwezi kukomesha mateso yao kimuujiza au kufufua wafu. Lakini, tunaweza kuwahurumia kwa matendo kwa kuwaonyesha kwamba tunawajali au kwa kuwapa msaada wanaohitaji.—Waefeso 4:32.

“Baba, Wasamehe”

16. Yesu alionyeshaje kwamba alikuwa tayari kusamehe hata alipokuwa kwenye mti wa mateso?

16 Yesu aliiga kikamili upendo wa Baba yake katika njia nyingine muhimu—alikuwa “tayari kusamehe.” (Zaburi 86:5) Jambo hilo lilionekana wazi hata alipokuwa kwenye mti wa mateso. Yesu alisema nini alipokuwa amepigiliwa misumari mikononi na miguuni, kabla ya kufa kifo cha aibu? Je, alimlilia Yehova awaadhibu wale wanaomwua? La hasha! Kati ya maneno ya mwisho ambayo Yesu alisema ni: “Baba, wasamehe, kwa maana hawajui wanalofanya.”—Luka 23:34. *

17-19. Yesu alionyeshaje kwamba alimsamehe mtume Petro ambaye alikuwa amemkana mara tatu?

17 Labda kisa cha mtume Petro kinaonyesha kwa njia yenye kugusa moyo hata zaidi jinsi Yesu alivyokuwa mwenye kusamehe. Hapana shaka kwamba Petro alimpenda mno Yesu. Mnamo Nisani 14, usiku wa mwisho kabla ya Yesu kuuawa, Petro alimwambia hivi: “Bwana, mimi niko tayari kwenda pamoja nawe kuingia gerezani na pia kuingia katika kifo.” Hata hivyo, saa chache tu baadaye, Petro alikana mara tatu kwamba hata hamjui Yesu! Biblia inatueleza jambo lililotukia Petro alipokuwa akimkana mara ya tatu: “Bwana akageuka akamtazama Petro.” Petro alilemewa na majuto kwa sababu ya dhambi yake, hata ‘akaenda nje na kutoa machozi kwa uchungu.’ Yesu alipokufa baadaye siku hiyo, labda mtume huyo alijiuliza hivi: ‘Je, Bwana wangu alinisamehe?’—Luka 22:33, 61, 62.

18 Punde si punde, Petro alipata jibu. Yesu alifufuliwa asubuhi ya Nisani 16, na yaelekea kwamba alimtembelea Petro siku hiyohiyo. (Luka 24:34; 1 Wakorintho 15:4-8) Kwa nini Yesu alimzingatia mtume huyo ambaye alikuwa amemkana kabisa? Huenda Yesu alitaka kumhakikishia Petro aliyetubu kwamba angali anampenda na kumthamini. Lakini Yesu alimhakikishia jambo hilo kwa njia nyingine pia.

19 Pindi fulani baadaye, Yesu aliwatokea wanafunzi katika Bahari ya Galilaya. Wakati huo, Yesu alimwuliza mara tatu Petro (ambaye alikuwa amemkana Bwana wake mara tatu) iwapo anampenda. Baada ya swali la tatu, Petro alijibu: “Bwana, wewe wajua mambo yote; wewe wajua kwamba mimi nina shauku na wewe.” Bila shaka, Yesu, ambaye angeweza kusoma mioyo, alijua vizuri kwamba Petro alimpenda mno. Hata hivyo, Yesu akampa Petro nafasi ya kuthibitisha kwamba anampenda. Isitoshe, Yesu alimwambia Petro ‘alishe’ na ‘kuchunga kondoo Wake wadogo.’ (Yohana 21:15-17) Hapo awali, Petro alikuwa amepewa kazi ya kuhubiri. (Luka 5:10) Lakini sasa, Yesu alionyesha kwamba alimtumaini kabisa kwa kumpa daraka jingine zito—la kutunza wale ambao wangekuwa wafuasi wa Kristo. Muda mfupi baadaye, Yesu alimpa Petro pendeleo la pekee kuhusiana na utendaji wa wanafunzi. (Matendo 2:1-41) Haikosi Petro alifurahi sana alipojua kwamba Yesu alimsamehe na bado anamtumaini.

Je, ‘Wajua Upendo wa Kristo’?

20, 21. Tunawezaje ‘kuujua kikweli upendo wa Kristo’?

20 Neno la Yehova linaeleza kinaganaga juu ya upendo wa Kristo. Lakini tunapaswa kuuonaje upendo wa Yesu? Biblia inatuhimiza ‘tuujue upendo wa Kristo uzidio ujuzi.’ (Waefeso 3:19) Kama tulivyoona, masimulizi ya Injili kuhusu maisha na huduma ya Yesu yanatufundisha mengi kuhusu upendo wa Kristo. Hata hivyo, ili ‘kuujua kikweli upendo wa Kristo’ haitoshi tu kujifunza mambo ambayo Biblia inasema kumhusu.

21 Neno la Kigiriki linalotafsiriwa ‘kujua’ linamaanisha “kujua kupitia matendo, kupitia uzoefu.” Tunaweza kufahamu zaidi hisia za Yesu tunapoiga upendo wake kwa kuwatumikia wengine bila ubinafsi, kuwahurumia na kuwasaidia, na kuwasamehe kutoka moyoni. Hivyo, kupitia uzoefu tunapata “kuujua upendo wa Kristo uzidio ujuzi.” Tusisahau kamwe kwamba kadiri tunavyomwiga Kristo, ndivyo tunavyomkaribia Mungu wetu mwenye upendo, Yehova, ambaye Yesu alimwiga kikamili.

^ fu. 11 Sheria za marabi zilisema kwamba hakuna yeyote aliyeruhusiwa kusimama umbali wa futi 6 hivi kutoka kwa mwenye ukoma. Lakini kukiwa na upepo, mwenye ukoma alisimama umbali wa futi 150 hivi. Kichapo Midrash Rabbah chataja rabi mmoja ambaye alijificha alipoona wenye ukoma, na rabi mwingine ambaye aliwatupia mawe wenye ukoma ili wasimkaribie. Kwa hiyo wenye ukoma walijua uchungu wa kukataliwa, kudharauliwa na kuchukiwa.

^ fu. 16 Hati fulani za kale hazina sehemu ya kwanza ya Luka 23:34. Hata hivyo, Tafsiri ya Ulimwengu Mpya na tafsiri nyingine nyingi zina maneno hayo kwa sababu yanapatikana kwenye hati nyingi mashuhuri. Ni wazi kwamba Yesu alikuwa akizungumza kuhusu askari Waroma ambao walimtundika mtini. Hawakujua walilokuwa wanafanya, kwa sababu hawakujua Yesu ni nani. Bila shaka, viongozi wa kidini ambao walichochea mauaji hayo walikuwa na hatia kubwa zaidi, kwa sababu walifanya hivyo kimakusudi na kwa nia mbaya. Wengi wao hawangeweza kusamehewa.—Yohana 11:45-53.