Hamia kwenye habari

Hamia kwenye yaliyomo

Sura ya 31

“Mkaribieni Mungu, Naye Atawakaribia”

“Mkaribieni Mungu, Naye Atawakaribia”

1-3. (a) Tunaweza kujifunza nini kuhusu wanadamu tunapofikiria uhusiano uliopo kati ya wazazi na mtoto wao? (b) Kwa kawaida sisi hutendaje tunapopendwa na mtu fulani, na ni swali gani muhimu tunaloweza kujiuliza?

WAZAZI hufurahi sana kumwona mtoto wao mchanga akitabasamu. Kwa kawaida wao humkaribia mtoto huyo, wakichekacheka na kutabasamu kwa hisia. Wana hamu ya kumwona akitabasamu pia. Na muda si muda, mtoto anaanza kutabasamu kwa shauku nyingi. Ni kana kwamba tabasamu hiyo inaonyesha upendo kwa njia fulani ya pekee. Ndivyo mtoto anavyoitikia upendo anaoonyeshwa na wazazi wake.

2 Tabasamu ya mtoto mchanga inatukumbusha jambo fulani muhimu kuhusu wanadamu. Kwa kawaida, sisi huonyesha upendo tunapoonyeshwa upendo. Tumeumbwa kwa njia hiyo. (Zaburi 22:9) Kadiri tunavyokua, ndivyo tunavyoweza kuonyesha upendo zaidi. Labda unakumbuka jinsi ambavyo wazazi wako, watu wa ukoo, au marafiki walivyokupenda ulipokuwa mtoto mchanga. Upendo huo mchangamfu ulianza kukua moyoni mwako na ulikuchochea kutenda. Ukaanza kuwapenda pia. Je, ndivyo uhusiano wako na Yehova Mungu ulivyo?

3 Biblia yasema hivi: “Kwa habari yetu, twapenda, kwa sababu yeye alitupenda sisi kwanza.” (1 Yohana 4:19) Sehemu ya 1 hadi ya 3 ya kitabu hiki ilikukumbusha kwamba Yehova Mungu ametumia nguvu zake, haki yake, na hekima yake kwa njia za upendo na kwa faida yako. Katika Sehemu ya 4 ulijifunza jinsi ambavyo ameonyesha waziwazi kwamba anakupenda na kuwapenda wanadamu wote kwa njia za pekee sana. Lakini swali lazuka na huenda likawa ndilo swali muhimu zaidi unaloweza kujiuliza: ‘Nitaonyeshaje kwamba nathamini upendo wa Yehova?’

Kumpenda Mungu Kwamaanisha Nini?

4. Watu wametatanikaje kuhusu maana ya kumpenda Mungu?

4 Yehova, aliye Chanzo cha upendo, anajua vizuri kwamba upendo una nguvu za kuwachochea wengine wafanye yote wawezayo. Kwa hiyo, licha ya kwamba wanadamu wameendelea kumwasi, ana hakika kwamba baadhi yao watampenda. Na kwa kweli, mamilioni wamefanya hivyo. Hata hivyo, inasikitisha kwamba dini za ulimwengu huu mwovu zimewatatanisha watu kiasi cha kwamba hawajui maana ya kumpenda Mungu. Watu wengi husema wanampenda Mungu, lakini wanafikiri kwamba upendo ni hisia inayoonyeshwa tu kwa maneno. Kuhisi hivyo kwaweza kuwa hatua ya kwanza ya kumpenda Mungu, kama vile mtoto mchanga anavyoanza kuwaonyesha wazazi wake upendo kwa kutabasamu. Hata hivyo, upendo wa watu wazima unatia ndani mambo mengi zaidi.

5. Biblia inafafanuaje kumpenda Mungu, na kwa nini ufafanuzi huo unatuvutia?

5 Yehova anatueleza maana ya kumpenda. Neno lake lasema: “Hivi ndivyo kumpenda Mungu humaanisha, kwamba tushike amri zake.” Basi, tunahitaji kuonyesha kwamba tunampenda Mungu kwa matendo. Ni kweli kwamba watu wengi hawapendi kutii. Lakini mstari huohuo wasema hivi kwa fadhili: “Na bado amri zake [za Mungu] si zenye kulemea.” (1 Yohana 5:3) Sheria na kanuni za Yehova zinakusudiwa kutufaidi wala si kutukandamiza. (Isaya 48:17, 18) Neno la Mungu lina kanuni nyingi sana ambazo zinatusaidia kumkaribia. Jinsi gani? Hebu tuzungumzie mambo matatu yanayohusu uhusiano wetu na Mungu. Mambo hayo ni: kuwasiliana naye, kumwabudu, na kumwiga.

Kuwasiliana na Yehova

6-8. (a) Tunaweza kumsikilizaje Yehova? (b) Twawezaje kusoma Maandiko kana kwamba tunaona matukio halisi?

6 Swali hili liliulizwa mwanzoni mwa Sura ya 1, “Je, waweza kuwazia ukizungumza na Mungu?” Tuliona kwamba hiyo si ndoto tu. Musa alizungumza na Mungu. Vipi sisi? Huu si wakati wa Yehova kutuma malaika wake ili wazungumze na wanadamu. Lakini Yehova anawasiliana nasi leo kwa njia bora sana. Tunaweza kumsikilizaje Yehova?

7 Kwa kuwa “andiko lote limepuliziwa na Mungu,” tunamsikiliza Yehova kwa kusoma Neno lake, Biblia. (2 Timotheo 3:16) Ndiyo sababu Mfalme Daudi aliwahimiza watumishi wa Yehova wasome Neno hilo “mchana na usiku.” (Zaburi 1:1, 2) Ni lazima tujitahidi sana kufanya hivyo. Lakini jitihada hizo zina faida. Kama tulivyoona katika Sura ya 18, Biblia ni kama barua muhimu kutoka kwa Baba yetu wa mbinguni. Kwa hiyo hatupaswi kuisoma tu kidesturi. Twapaswa kusoma Maandiko kana kwamba tunaona matukio halisi. Jinsi gani?

8 Piga picha akilini unaposoma masimulizi ya Biblia. Jaribu kuwazia watu wanaotajwa. Jaribu kufahamu malezi yao, hali zao, na nia zao. Kisha, tafakari yale unayosoma, jiulize maswali kama haya: ‘Simulizi hili linanifundisha nini kumhusu Yehova? Linakazia sifa gani ya Yehova? Yehova anataka nijifunze kanuni gani, na ninawezaje kuitumia maishani mwangu?’ Neno la Mungu litakufaidi ukilisoma, ukilitafakari, na kulitumia maishani.—Zaburi 77:12; Yakobo 1:23-25.

9. “Mtumwa mwaminifu na mwenye busara” ni nani, na kwa nini tunapaswa kumsikiliza kwa makini “mtumwa” huyo?

9 Pia Yehova anazungumza nasi kupitia “mtumwa mwaminifu na mwenye busara.” Kama Yesu alivyotabiri, kikundi kidogo cha wanaume Wakristo watiwa-mafuta kimewekwa rasmi ili kitoe ‘chakula [cha kiroho] kwa wakati ufaao’ katika hizi siku za mwisho zenye magumu. (Mathayo 24:45-47) Tunaposoma vichapo ambavyo vinakusudiwa kutusaidia kupata ujuzi sahihi wa Biblia, na tunapohudhuria mikutano ya Kikristo na makusanyiko, tunalishwa kiroho na mtumwa huyo. Kwa kuwa yeye ni mtumwa wa Kristo, tunatii kwa hekima maneno haya ya Yesu: “Kazieni uangalifu jinsi msikilizavyo.” (Luka 8:18) Tunasikiliza kwa makini kwa sababu tunatambua kwamba njia moja ambayo Yehova hutumia kuwasiliana nasi ni kupitia mtumwa huyo mwaminifu.

10-12. (a) Kwa nini sala ni zawadi bora kutoka kwa Yehova? (b) Tunawezaje kusali kwa njia inayomfurahisha Yehova, na kwa nini tunaweza kuwa na hakika kwamba anathamini sala zetu?

10 Lakini vipi kuhusu kuwasiliana na Mungu? Je, tunaweza kuzungumza na Yehova? Ni wazo lenye kutia kicho. Je, ni rahisi kumfikia mtawala mwenye nguvu katika nchi yenu ili umwambie matatizo yako? Nyakati nyingine, inaweza kuwa hatari sana kujaribu kufanya hivyo! Katika siku za Esta na Mordekai, mtu ambaye angeenda kumtembelea mfalme wa Uajemi bila mwaliko rasmi angeuawa. (Esta 4:10, 11) Sasa wazia kumfikia Bwana Mwenye Enzi Kuu ya ulimwengu mzima, ambaye ni mkuu hivi kwamba wanadamu wenye mamlaka zaidi “huwa kama panzi” wanapolinganishwa naye. (Isaya 40:22) Je, tuogope kumfikia? La hasha!

11 Yehova ameandaa njia rahisi ya kumfikia—sala. Hata mtoto mchanga anaweza kusali kwa Yehova kwa imani, katika jina la Yesu. (Yohana 14:6; Waebrania 11:6) Isitoshe, sala inatuwezesha kueleza mawazo na hisia zetu za ndani sana—hata zile zenye kuumiza ambazo tunashindwa kutamka. (Waroma 8:26) Hakuna haja ya kujaribu kumfurahisha Yehova kwa kutoa sala zenye ufasaha na zenye madoido au sala ndefu-ndefu zenye maneno mengi. (Mathayo 6:7, 8) Kwa upande mwingine, Yehova hatuwekei muda wa kusali au mara ambazo tunaweza kufanya hivyo. Neno lake linatusihi ‘tusali bila kukoma.’—1 Wathesalonike 5:17.

12 Kumbuka kwamba ni Yehova peke yake anayeitwa “Msikiaji wa Sala,” naye husikiliza kwa hisia-mwenzi kabisa. (Zaburi 65:2, NW) Je, yeye hustahimili tu sala za watumishi wake waaminifu? La, sala zao zinamfurahisha. Neno lake linalinganisha sala hizo na uvumba ambao ukichomwa, moshi wake wenye manukato hupaa juu. (Zaburi 141:2; Ufunuo 5:8; 8:4) Bila shaka inafariji sana kujua kwamba Bwana Mwenye Enzi Kuu husikiliza na kufurahia sala zetu za kutoka moyoni ambazo ni kama uvumba, sivyo? Kwa hiyo, ikiwa unataka kumkaribia Yehova, sali kwa unyenyekevu mara nyingi kila siku. Mwambie mambo yote yaliyo moyoni mwako; mfunulie yote. (Zaburi 62:8) Mwambie Baba yako wa mbinguni mahangaiko yako, shangwe zako, na umshukuru na kumsifu. Ukifanya hivyo uhusiano wako naye utazidi kuimarika.

Kumwabudu Yehova

13, 14. Kumwabudu Yehova kwamaanisha nini, na kwa nini tunapaswa kumwabudu?

13 Tunapowasiliana na Yehova Mungu, hatumsikilizi na kuzungumza naye kama tunavyozungumza na rafiki au mtu wetu wa ukoo. Kwa kweli, tunamwabudu Yehova na kumpa staha yenye kicho ambayo anastahili kabisa. Maisha yetu yote yanaongozwa na ibada ya kweli. Kwa njia hiyo tunaonyesha kwamba tunampenda Yehova na tunamtumikia kwa nafsi yetu yote. Ibada ya kweli inawaunganisha viumbe wote wa Yehova ambao ni waaminifu, ama mbinguni au duniani. Katika ono, mtume Yohana alimsikia malaika akitangaza amri hii: “Mwabuduni Yeye aliyezifanya mbingu na dunia na bahari na mabubujiko ya maji.”—Ufunuo 14:7.

14 Kwa nini tumwabudu Yehova? Hebu fikiria sifa ambazo tumezungumzia, kama vile utakatifu, nguvu, kujidhibiti, haki, ujasiri, rehema, hekima, unyenyekevu, upendo, huruma, uaminifu-mshikamanifu, na wema. Tumeona kwamba Yehova ndiye mfano bora kabisa, na hana kifani katika kuonyesha kila sifa inayopendeza. Tunapojaribu kuelewa sifa zote za Mungu, tunatambua kwamba yeye ni mkuu zaidi, anastahili sifa zote, ni mtukufu ajabu, na yuko juu sana kuliko sisi. (Isaya 55:9) Hapana shaka kwamba Yehova ana haki ya kuwa Mwenye Enzi Kuu, naye anastahili ibada yetu. Lakini tunapaswa kumwabuduje?

15. Tunawezaje kumwabudu Yehova “kwa roho na kweli,” na mikutano ya Kikristo hutupatia fursa ya kufanya nini?

15 Yesu alisema: “Mungu ni Roho, na wale wanaomwabudu yeye lazima waabudu kwa roho na kweli.” (Yohana 4:24) Ili tumwabudu Mungu “kwa roho” ni lazima tuwe na roho ya Mungu na ituongoze. Pia, ibada yetu inapaswa kupatana na kweli na ujuzi sahihi ulio katika Neno la Mungu. Tunapokutana na waabudu wenzetu, tunapata fursa ya kumwabudu Yehova “kwa roho na kweli.” (Waebrania 10:24, 25) Tunaonyesha kwamba tunampenda Yehova katika ibada safi tunapomsifu kwa nyimbo, tunaposali kwake kwa umoja, tunaposikiliza na kushiriki mazungumzo ya Neno lake.

Mikutano ya Kikristo ni pindi zenye kupendeza za kumwabudu Yehova

16. Ni amri gani iliyo kati ya amri kuu zaidi ambazo Wakristo wa kweli wanapaswa kutii, ni nini kinachotuchochea kutii amri hiyo?

16 Tunamwabudu Yehova pia tunapowaambia wengine juu yake, tukimsifu hadharani. (Waebrania 13:15) Kwa kweli, kuhubiri habari njema za Ufalme wa Yehova ni kati ya amri kuu zaidi ambazo Wakristo wa kweli wanapaswa kutii. (Mathayo 24:14) Tunatii kwa moyo wetu wote kwa sababu tunampenda Yehova. Tunapofikiria jinsi ambavyo “mungu wa huu mfumo wa mambo,” Shetani Ibilisi, “amepofusha akili za wasioamini,” na kusambaza uwongo kumhusu Yehova, je, hilo halituchochei tuazimie kuwa Mashahidi wa Mungu wetu, na kukomesha uchongezi huo? (2 Wakorintho 4:4; Isaya 43:10-12) Na tunapotafakari sifa nzuri sana za Yehova, je, hatuchochewi kuwaambia wengine juu yake? Kwa kweli, hakuna pendeleo linaloweza kulinganishwa na pendeleo la kuwasaidia wengine wamjue na kumpenda Baba yetu wa mbinguni kama tunavyofanya.

17. Kumwabudu Yehova kunahusisha nini, na kwa nini ni lazima tumwabudu kwa uaminifu?

17 Kumwabudu Yehova kunahusisha mambo mengi zaidi. Kunahusisha kila jambo tunalofanya maishani. (Wakolosai 3:23) Tukimkubali kikweli Yehova awe Bwana wetu Mwenye Enzi Kuu, basi tutajitahidi kufanya mapenzi yake katika kila jambo—katika maisha yetu ya familia, kazini, jinsi tunavyowatendea wengine, na hata tunapostarehe. Tutajitahidi kumtumikia Yehova “kwa moyo mkamilifu,” na kwa uaminifu. (1 Mambo ya Nyakati 28:9) Hatuwezi kumwabudu Yehova kwa moyo nusunusu au huku tunaishi maisha maradufu—yaani, tunajifanya kwa unafiki kwamba tunamtumikia Yehova na huku tunatenda dhambi nzito kisiri-siri. Watu waaminifu si wanafiki; anayempenda Mungu anachukia kabisa unafiki. Kumhofu Mungu kunasaidia pia. Biblia inaonyesha kwamba tutakuwa na uhusiano mzuri na Yehova tukiwa na hofu hiyo yenye kicho.—Zaburi 25:14.

Kumwiga Yehova

18, 19. Kwa nini si kosa kufikiri kwamba wanadamu wasiokamilika wanaweza kumwiga Yehova Mungu?

18 Sura ya mwisho katika kila sehemu ya kitabu hiki inaonyesha jinsi ya ‘kumwiga Mungu, tukiwa watoto wapendwa.’ (Waefeso 5:1) Ni muhimu kukumbuka kwamba ingawa hatujakamilika, tunaweza kuiga jinsi Yehova anavyotumia nguvu zake, haki yake, jinsi anavyotenda kwa hekima, na kuonyesha upendo. Tunajuaje kwamba kwa kweli tunaweza kumwiga Mweza Yote? Kumbuka kwamba jina Yehova linatufundisha kwamba yeye hujisababisha kuwa chochote atakacho ili atimize makusudi yake. Bila shaka uwezo huo unatutia kicho, lakini je, tunaweza kweli kumwiga Yehova? Bila shaka tunaweza.

19 Tumeumbwa kwa mfano wa Mungu. (Mwanzo 1:26) Kwa hiyo, wanadamu ni tofauti kabisa na viumbe wote duniani. Hatuongozwi tu na silika, sifa tulizorithi, au mazingira yetu. Yehova ametupatia zawadi nzuri sana—uhuru wa kuchagua. Licha ya udhaifu wetu na kutokamilika, tuna uhuru wa kuchagua tunavyotaka kuwa. Je, ungependa kuwa mtu mwenye upendo, hekima na haki, anayetumia uwezo wake ifaavyo? Roho ya Yehova inaweza kukusaidia kuwa na sifa hizo zote! Hebu fikiria mambo unayoweza kutimiza ukiwa na sifa hizo.

20. Tunatimiza mambo gani mazuri tunapomwiga Yehova?

20 Utampendeza Baba yako wa mbinguni na kuufurahisha moyo wake. (Mithali 27:11) Hata unaweza ‘kumpendeza Yehova kikamili,’ kwa sababu anajua udhaifu wako. (Wakolosai 1:9, 10) Utapata pendeleo la pekee sana unapoendelea kukuza sifa nzuri kama za Baba yako mpendwa. Utawaangazia watu nuru katika ulimwengu huu ulio gizani na uliotengwa na Mungu. (Mathayo 5:1, 2, 14) Utasaidia kutangaza duniani pote sifa za utu wa Yehova wenye utukufu. Ni heshima iliyoje!

“Mkaribieni Mungu, Naye Atawakaribia”

Na uzidi kumkaribia Yehova daima

21, 22. Wale wanaompenda Yehova watakuwa na mradi gani usio na mwisho?

21 Himizo rahisi lililo katika Yakobo 4:8 halitimizwi mara moja. Ni mradi usio na mwisho. Tutaendelea kumkaribia Yehova maadamu tunadumisha uaminifu wetu. Tutazidi kumkaribia Yehova daima kwa sababu sikuzote tutakuwa na mengi ya kujifunza kumhusu. Hatupaswi kamwe kufikiri kwamba kitabu hiki kimetufunza mambo yote kumhusu Yehova. Huu ni mwanzo tu wa kujifunza yale ambayo Biblia inasema kumhusu Mungu wetu. Na hata Biblia haituelezi mambo yote kumhusu Yehova. Mtume Yohana alikisia kwamba ikiwa mambo yote ambayo Yesu alifanya wakati wa huduma yake duniani yangeandikwa, “ulimwengu wenyewe haungeweza kuwa na nafsi ya kuziweka hati-kunjo ambazo zingeandikwa.” (Yohana 21:25) Ikiwa ilisemwa hivyo kumhusu Mwana, basi mengi zaidi yanaweza kusemwa kumhusu Baba!

22 Hata tukiishi milele, hatutaweza kujifunza mambo yote kumhusu Yehova. (Mhubiri 3:11) Basi fikiria tumaini tulilo nalo. Baada ya kuishi mamia, maelfu, mamilioni au hata mabilioni ya miaka, tutajua mengi zaidi kumhusu Yehova Mungu kuliko tujuavyo sasa. Lakini bado tutatambua kwamba kuna mambo mengi mazuri tutakayohitaji kujifunza. Tutakuwa na hamu ya kujifunza mengi zaidi, kwa kuwa sikuzote tutakuwa na sababu ya kuhisi kama mtunga-zaburi aliyeimba hivi: “Kumkaribia Mungu ni kwema kwangu.” (Zaburi 73:28) Uhai udumuo milele utakuwa na kusudi na utapendeza isivyowazika—kwa sababu tutazidi kumkaribia Yehova daima.

23. Unatiwa moyo kufanya nini?

23 Thamini upendo wa Yehova sasa kwa kumpenda kwa moyo wako wote, nafsi yako yote, akili zako zote, na nguvu zako zote. (Marko 12:29, 30) Mpende kwa uaminifu-mshikamanifu. Na maamuzi unayofanya kila siku, madogo kwa makubwa, yaonyeshe kwamba una azimio moja—kwamba sikuzote utafuata njia itakayoimarisha uhusiano wako na Baba yako wa mbinguni. Zaidi ya yote, na umkaribie Yehova zaidi, naye aendelee kukukaribia milele na milele!