Hamia kwenye habari

Hamia kwenye yaliyomo

SURA YA 1

Kwa Nini Yesu Alikuwa Mwalimu MKuu

Kwa Nini Yesu Alikuwa Mwalimu MKuu

ZAIDI ya miaka 2,000 iliyopita, mtoto mmoja wa kipekee alizaliwa. Mtoto huyo akawa mtu mkuu zaidi aliyewahi kuishi duniani. Watu walioishi hapo zamani hawakuwa na ndege wala magari. Hawakuwa na televisheni wala redio.

Mtoto huyu aliitwa Yesu. Akawa mtu mwenye hekima nyingi sana aliyewahi kuishi duniani. Yesu akawa pia mwalimu bora. Alifafanua mambo magumu kwa njia rahisi sana.

Yesu alifundisha watu popote alipowapata. Aliwafundisha wakiwa kando-kando ya bahari na kwenye mashua. Aliwafundisha wakiwa nyumbani na wakisafiri. Yesu hakuwa na gari, wala hakusafiri kwa basi au gari-moshi. Yesu alitembea huko na huko akiwafundisha watu.

Sisi tunajifunza mambo mengi kutoka kwa watu wengine. Lakini tunaweza kujifunza mambo muhimu zaidi kutoka kwa Mwalimu Mkuu, Yesu. Basi, tunaposoma Biblia tunapata maneno ya Yesu. Tunaposoma maneno hayo katika Biblia, ni kama tunazungumza na Yesu mwenyewe.

Kwa nini Yesu alikuwa Mwalimu Mkuu? Kwanza ni kwa sababu Yesu mwenyewe alifundishwa. Na alijua kwamba ni muhimu kusikiliza. Lakini Yesu alimsikiliza nani? Alifundishwa na nani?— Alifundishwa na Baba yake. Na Baba ya Yesu ni Mungu.

Kabla ya Yesu kuja duniani akiwa binadamu, aliishi mbinguni na Mungu. Kwa hiyo, Yesu alikuwa tofauti na watu wengine kwa sababu hakuna mtu mwingine aliyewahi kuishi mbinguni kabla ya kuzaliwa hapa duniani. Akiwa mbinguni, Yesu alikuwa Mwana mzuri ambaye alimsikiliza Baba yake. Kwa hiyo, Yesu aliweza kufundisha watu mambo aliyojifunza kutoka kwa Mungu. Unaweza kumwiga Yesu kwa kuwasikiliza baba yako na mama yako.

Yesu alikuwa Mwalimu Mkuu pia kwa sababu aliwapenda watu. Alitaka kuwasaidia watu wajifunze kumhusu Mungu. Yesu aliwapenda watu wazima na watoto pia. Nao watoto walipenda kuwa na Yesu kwa sababu alizungumza nao na kuwasikiliza.

Kwa nini watoto walipenda kuwa na Yesu?

Siku moja, wazazi fulani walimpelekea Yesu watoto wao. Lakini rafiki za Yesu wakafikiri kwamba Mwalimu Mkuu ana shughuli nyingi na hawezi kuzungumza na watoto. Basi wakawaambia wazazi hao na watoto wao waondoke. Lakini Yesu akawakataza rafiki zake, akasema: “Waacheni watoto wachanga waje kwangu; msijaribu kuwazuia.” Ndiyo, Yesu alitaka watoto waje kwake. Basi, hata kama Yesu alikuwa mtu mkuu na mwenye hekima nyingi sana, alitafuta nafasi ili kuwafundisha watoto wadogo. —Marko 10:13, 14.

Unajua ni kwa nini Yesu aliwafundisha watoto na kuwasikiliza? Sababu moja ni kwamba alitaka kuwafurahisha kwa kuwaambia mambo kumhusu Mungu, Baba yake wa mbinguni. Unaweza kuwafurahisha watu namna gani?— Kwa kuwaambia yale ambayo umejifunza kumhusu Mungu.

Wakati mmoja, Yesu alitumia mtoto mdogo kuwafundisha rafiki Zake somo muhimu. Alimchukua mtoto huyo na kumsimamisha katikati ya wanafunzi Wake. Kisha Yesu akawaambia watu hao kwamba wanapaswa kubadili tabia zao na kuwa kama mtoto huyo.

Ni somo gani ambalo watoto wakubwa na watu wazima wanaweza kujifunza kutoka kwa mtoto mdogo?

Yesu alimaanisha nini aliposema hivyo? Unajua vile mtu mzima, au hata mtoto mkubwa, anavyoweza kuwa kama mtoto mdogo?— Mtoto mdogo hajui mambo mengi kama mtu mzima naye yuko tayari kujifunza. Kwa hiyo, Yesu alimaanisha kwamba wanafunzi wake walipaswa kuwa wanyenyekevu kama watoto wadogo. Tunaweza kujifunza mambo mengi kutoka kwa watu wengine. Na tunapaswa kutambua kwamba mafundisho ya Yesu ni muhimu sana kuliko maoni yetu. —Mathayo 18:1-5.

Sababu nyingine inayomfanya Yesu awe Mwalimu Mkuu ni kwamba alijua namna ya kufanya mambo yawapendeze watu. Alieleza mambo kwa njia yenye kueleweka. Alizungumza kuhusu ndege na maua na vitu vingine vya kawaida ili kuwasaidia watu waelewe mambo fulani kumhusu Mungu.

Siku moja Yesu alikuwa mlimani. Watu wengi wakaja kwake. Yesu akaketi na kuwatolea hotuba kama unavyoona kwenye picha. Hotuba hii inaitwa Mahubiri ya Mlimani. Yeye alisema hivi: ‘Waangalie ndege wa mbinguni. Hawapandi mbegu. Hawakusanyi chakula katika ghala. Lakini Mungu akiwa mbinguni huwalisha wao. Je, nyinyi si bora kuliko wao?’

Yesu alifunza somo gani alipotaja ndege na maua?

Yesu alisema hivi pia: ‘Jifunzeni kutokana na maua ya shambani. Hayo yanakua bila kufanya kazi. Lakini hayo ni maridadi wee! Hata Mfalme Sulemani aliyekuwa tajiri sana hakuvalia maridadi kama maua ya shambani. Ikiwa basi Mungu huvisha maua yanayomea, je, hatakujali wewe?’ —Mathayo 6:25-33.

Je, unaelewa somo ambalo Yesu alikuwa akifundisha?— Yeye hakutaka tuhangaike eti tutakula nini au tutavaa nini. Mungu anajua kwamba tunahitaji vitu hivi vyote. Yesu hakusema kwamba tusifanye kazi ili tupate chakula na mavazi. Lakini alisema, tumweke Mungu kwanza. Tukifanya hivyo, Mungu atahakikisha tunapata chakula na mavazi. Je, unaamini mambo haya?—

Watu walifikiria nini Yesu alipomaliza kuongea?— Biblia inasema walishangazwa na njia yake ya kufundisha. Watu walifurahia kumsikiliza. Maneno yake yaliwasaidia watu wafanye mema.—Mathayo 7:28.

Kwa hiyo ni jambo la maana sana tujifunze kutoka kwa Yesu. Lakini tunaweza kujifunza namna gani?— Kupitia maneno yake ambayo yameandikwa katika kitabu. Je unakijua kitabu hicho?— Ni Biblia Takatifu. Hii inamaanisha kwamba tunaweza kumsikiliza Yesu kwa kufuata kwa makini yale tunayosoma katika Biblia. Kwa kweli, Biblia ina hadithi yenye kupendeza kuhusu jinsi Mungu mwenyewe alivyotuambia tumsikilize Yesu. Hebu tuone ni nini kilichotokea.

Siku moja Yesu aliwapeleka rafiki zake watatu juu mlimani. Waliitwa Yakobo, Yohana, na Petro. Tutajifunza mambo mengi kuhusu watu hawa baadaye, kwa sababu wote walikuwa rafiki wa karibu sana wa Yesu. Lakini wakati huo wa pekee, uso wa Yesu ulianza kung’aa. Na nguo zake pia zilianza kung’aa kama nuru vile unavyoona kwenye picha hii.

“Huyu ni Mwanangu, . . . msikilizeni”

Baadaye, Yesu na rafiki zake walisikia sauti kutoka mbinguni. Sauti hiyo ilisema: “Huyu ni Mwanangu, mpendwa, ambaye nimemkubali; msikilizeni.” (Mathayo 17:1-5) Unajua hiyo ilikuwa sauti ya nani?— Ilikuwa sauti ya Mungu! Ndiyo, ni Mungu mwenyewe aliyesema wamsikilize Mwana wake.

Namna gani sisi leo? Je, tutamtii Mungu kwa kumsikiliza Mwana wake, ambaye ni Mwalimu Mkuu?— Tunapaswa kufanya hivyo. Je, unakumbuka jinsi tunavyoweza kumsikiliza?—

Ndiyo, tunaweza kumsikiliza Mwana wa Mungu kwa kusoma masimulizi ya Biblia kuhusu maisha yake. Kuna mambo mengi mazuri ambayo Mwalimu Mkuu anatuambia. Utafurahi kujifunza mambo hayo yaliyoandikwa katika Biblia. Pia utakuwa na furaha zaidi iwapo utawaambia rafiki zako mambo mazuri unayojifunza.

Ili kujua mengi zaidi kuhusu faida ya kumsikiliza Yesu, fungua Biblia yako na usome Yohana 3:16; 8:28-30; na Matendo 4:12.