Hamia kwenye habari

Hamia kwenye yaliyomo

SURA YA 2

Barua Kutoka kwa Mungu Mwenye Upendo

Barua Kutoka kwa Mungu Mwenye Upendo

NIAMBIE, ni kitabu gani unachopenda zaidi?— Watoto wengine wanapenda kitabu cha wanyama. Wengine wanapenda kitabu chenye picha nyingi. Inaweza kufurahisha kusoma vitabu hivyo.

Lakini vitabu bora zaidi ulimwenguni ni vile vinavyotuambia kweli kumhusu Mungu. Kimojawapo cha vitabu hivyo ni chenye faida sana kuliko vyote. Unakijua kitabu hicho?— Ni Biblia.

Kwa nini Biblia ni ya maana sana?— Kwa sababu ilitoka kwa Mungu. Biblia hutuambia kumhusu Mungu na mambo mazuri ambayo atatufanyia. Na inatuonyesha mambo ambayo tunapaswa kufanya ili kumpendeza. Ni kama barua kutoka kwa Mungu.

Mungu angeweza kuandika Biblia nzima huko mbinguni na kuwapa wanadamu. Lakini hakufanya hivyo. Ijapokuwa mawazo yalitoka kwa Mungu, yeye alitumia watumishi wake waliokuwa duniani kuandika sehemu kubwa ya Biblia.

Mungu alifanya hivyo namna gani?— Ili kuelewa, fikiria jambo hili. Tunaposikia sauti ya mtu kwenye redio, labda mtu huyo yuko mbali sana. Tunapotazama televisheni, tunaweza kuona picha za watu katika nchi nyingine ulimwenguni na kusikia wanayosema.

Wanadamu wanaweza hata kusafiri mpaka kwenye mwezi wakitumia vyombo vya angani, na wanaweza kutuma habari kutoka angani mpaka duniani. Je, unajua hivyo?— Ikiwa wanadamu wanaweza kutuma habari kutoka angani, je, Mungu hawezi kutuma habari kutoka mbinguni?— Bila shaka anaweza! Naye alifanya hivyo zamani kabla ya wanadamu kuwa na redio au televisheni.

Tunajuaje kwamba Mungu anaweza kuzungumza nasi kutoka mbali sana?

Musa alisikia Mungu akizungumza. Musa hangeweza kumwona Mungu, lakini alisikia sauti yake. Mamilioni ya watu walikuwapo mambo hayo yalipotokea. Siku hiyo, Mungu alifanya mlima wote utikisike, na kukawa na ngurumo na radi. Watu walijua kwamba Mungu amezungumza, lakini waliogopa sana. Kwa hiyo, wakamwambia Musa: “Mungu asiseme nasi tusije tukafa.” Baadaye Musa aliandika mambo ambayo Mungu alisema. Na mambo ambayo Musa aliandika yako katika Biblia. —Kutoka 20:18-21.

Musa aliandika vitabu vitano vya kwanza vya Biblia. Lakini si yeye peke yake aliyeandika Biblia. Mungu alitumia wanaume 40 hivi kuandika sehemu mbalimbali za Biblia. Watu hao waliishi zamani sana, na ilichukua miaka mingi kumaliza kuandika Biblia. Karibu miaka 1,600 hivi! Jambo la kushangaza ni kwamba watu hao waliandika mambo yanayopatana kabisa ijapokuwa wengine wao hata hawakujuana.

Waandikaji hawa wa Biblia wanaitwaje?

Wengine waliotumiwa na Mungu kuandika Biblia walijulikana sana. Ijapokuwa Musa alikuwa mchungaji, baadaye alikuwa kiongozi wa taifa la Israeli. Sulemani alikuwa mfalme tajiri na mwenye hekima kuliko watu wote duniani. Lakini waandikaji wengine hawakujulikana sana. Amosi alifanya kazi ya kutunza shamba la matunda aina ya tini.

Mmoja wa waandikaji wa Biblia alikuwa daktari. Unajua jina lake?— Yeye ni Luka. Mwingine alikuwa mkusanya-kodi. Naye aliitwa Mathayo. Na pia mwingine alikuwa mwanasheria, na alijua sana sheria ya dini ya Wayahudi. Aliandika vitabu vingi vya Biblia kuliko waandikaji wengine wote. Unajua jina lake?— Ni Paulo. Na wanafunzi wa Yesu, Petro na Yohana, ambao pia waliandika Biblia, walikuwa wavuvi.

Waandikaji wengi wa Biblia waliandika mambo ambayo Mungu atafanya wakati ujao. Walijuaje mambo hayo hata kabla hayajatokea?— Mungu aliwaambia mambo ambayo yangetokea.

Sehemu kubwa ya Biblia ilikuwa tayari imeandikwa kufikia wakati Yesu, yule Mwalimu Mkuu, alipokuwa hapa duniani. Kumbuka kwamba Mwalimu Mkuu alikuwa mbinguni kabla ya kuja duniani. Alijua mambo ambayo Mungu alikuwa amefanya. Je, aliamini kwamba Biblia ilitoka kwa Mungu?— Ndiyo, aliamini hivyo.

Yesu aliwasomea watu Biblia alipowaambia kuhusu kazi za Mungu. Wakati mwingine aliwaambia kutoka akilini yale ambayo Biblia inasema. Pia, Yesu alituletea habari nyingi kutoka kwa Mungu. Alisema hivi: “Mambo yale niliyoyasikia kutoka kwake ninayasema ulimwenguni.” (Yohana 8:26) Kwa sababu alikuwa ameishi na Mungu, Yesu alisikia mambo mengi kutoka kwake. Tunaweza kuyapata wapi mambo hayo ambayo Yesu alisema?— Katika Biblia. Mambo hayo yaliandikwa ili tuyasome.

Bila shaka, watu waliotumiwa na Mungu kuandika Biblia waliandika katika lugha rahisi ambayo watu walielewa. Kwa hiyo sehemu kubwa ya Biblia iliandikwa katika Kiebrania, nyingine katika Kiaramu, na sehemu nyingine kubwa katika Kigiriki. Kwa kuwa watu wengi leo hawajui kusoma lugha hizo, Biblia imetafsiriwa katika lugha nyingi. Leo, sehemu za Biblia zinaweza kupatikana katika lugha zaidi ya 2,260. Hebu fikiria jambo hilo! Biblia ni barua ya Mungu kwa watu wote kila mahali. Lakini hata kama imeandikwa kwa kurudiwa-rudiwa mara ngapi, bado habari yake inatoka kwa Mungu.

Yale ambayo Biblia inasema ni ya maana kwetu. Iliandikwa zamani sana. Lakini inatuambia mambo yanayotendeka leo. Inatuambia pia yale ambayo Mungu atafanya hivi karibuni. Ina mambo ya kupendeza sana! Inatupatia tumaini zuri ajabu.

Unaweza kujifunza mambo gani kwa kusoma Biblia?

Biblia inatuambia pia jinsi Mungu anavyotaka tuishi. Inatuambia yaliyo mema na yaliyo mabaya. Sisi sote tunahitaji kujua mambo hayo. Inatuambia kuhusu watu waliofanya mabaya na hasara ambayo walipata ili sisi tusirudie makosa hayo. Inatuambia pia kuhusu watu waliofanya mema na faida ambayo walipata. Yote hayo yaliandikwa kwa faida yetu.

Lakini ili tupate faida zaidi kutoka kwa Biblia, tunahitaji kupata jibu la swali fulani. Swali hilo ni: Ni nani aliyetupatia Biblia? Unaonaje?— Biblia nzima ilitoka kwa Mungu. Hivyo basi, tutaonyeshaje kwamba sisi tuna hekima?— Ni kwa kumsikiliza Mungu na kufanya yale anayosema.

Kwa hiyo, tunahitaji kutafuta nafasi ili tusome Biblia pamoja. Tunapopata barua kutoka kwa mtu ambaye tunampenda sana, sisi tunaisoma tena na tena. Barua hiyo ni ya maana kwetu. Biblia pia inapaswa kuwa ya maana kwetu kwa sababu ni barua kutoka kwa Yule anayetupenda zaidi. Ni barua kutoka kwa Mungu mwenye upendo.

Chukua muda mfupi sasa usome maandiko haya yanayoonyesha kwamba kwa kweli Biblia ni Neno la Mungu, na imeandikwa kwa faida yetu: Waroma 15:4; 2 Timotheo 3:16, 17; na 2 Petro 1:20, 21.