Hamia kwenye habari

Hamia kwenye yaliyomo

SURA YA 3

Yule Aliyeviumba Vitu Vyote

Yule Aliyeviumba Vitu Vyote

Ni nani aliyeviumba vitu vyote?

NINAJUA jambo zuri ajabu. Nikuambie?— Angalia mkono wako. Kunja vidole vyako. Sasa inua kitu. Mkono wako unaweza kufanya mambo mengi kwa njia nzuri sana. Je, unajua ni nani aliyeumba mikono yetu?—

Ni Yule aliyeumba mdomo wetu, pua yetu, na macho yetu. Ni Mungu, Baba ya Mwalimu Mkuu. Tunafurahi kwamba Mungu alitupatia macho, sivyo?— Yanatusaidia kuona vitu vingi. Tunaweza kuona maua. Tunaweza kuona nyasi na anga la buluu. Tunaweza hata kuwaona ndege wakila, kama hawa katika picha. Ni ajabu kwamba tunaweza kuona vitu kama hivi, sivyo?—

Lakini ni nani aliyeviumba vitu hivi? Je, ni mwanadamu fulani? La. Wanadamu wanaweza kujenga nyumba. Lakini hakuna mwanadamu anayeweza kuumba nyasi inayokua. Wanadamu hawawezi kuumba mtoto wa ndege, maua, ama kitu chochote kilicho na uhai. Je, ulijua hivyo? —

Mungu ndiye aliyeviumba vitu vyote hivi. Mungu aliumba mbingu na dunia. Aliwaumba watu pia. Aliwaumba mwanamume na mwanamke wa kwanza. Yule Mwalimu Mkuu, Yesu, alifundisha hivyo. —Mathayo 19:4-6.

Yesu alijuaje kwamba Mungu aliwaumba mwanamume na mwanamke? Je, Yesu alimwona Mungu akiwaumba?— Ndiyo. Mungu alipowaumba mwanamume na mwanamke, Yesu alikuwa pamoja naye. Mungu alimwumba Yesu kwanza kabisa. Yesu alikuwa malaika na aliishi na Baba yake mbinguni.

Biblia inatuambia kwamba Mungu alisema hivi: “Na tufanye mtu.” (Mwanzo 1:26) Unajua Mungu alikuwa akiongea na nani?— Alikuwa akiongea na Mwana wake. Alikuwa akiongea na yule ambaye baadaye alikuja duniani akawa Yesu.

Inafurahisha sana, sivyo? Hebu fikiria! Tunapomsikiliza Yesu, tunafundishwa na yule aliyekuwa na Mungu wakati Mungu aliumba dunia na vitu vingine vyote. Yesu alipokuwa mbinguni alijifunza mambo mengi kutoka kwa Baba yake. Hiyo ndiyo sababu yeye ni Mwalimu Mkuu.

Unafikiri Mungu alihuzunika kuwa peke yake kabla ya kuumba Mwana wake?— La. Lakini kama hakuwa na huzuni, kwa nini aliumba viumbe wengine?— Aliwaumba viumbe wengine kwa sababu yeye ni Mungu mwenye upendo. Alitaka wengine pia waishi na kufurahia maisha. Tunapaswa kumshukuru Mungu kwa kutupatia uhai.

Kila kitu ambacho Mungu ameumba kinaonyesha upendo wake. Mungu aliumba jua. Jua hutupatia mwangaza na joto. Kama hakungekuwa na jua, kila kitu kingekuwa baridi na uhai haungekuwapo duniani. Bila shaka unafurahi kwamba Mungu aliumba jua, sivyo?—

Mungu hufanya mvua inyeshe pia. Labda wakati mwingine hupendi mvua kwa sababu huwezi kucheza nje ikinyesha. Lakini mvua husaidia maua kukua. Kwa hiyo tunapoona maua maridadi, tunapaswa kumshukuru Mungu, sivyo?— Tunapaswa kumshukuru Mungu tunapokula matunda matamu na mboga tamu kwa sababu jua na mvua zinazofanya vitu vikue vinatoka kwake.

Utasema nini mtu akikuuliza, ‘Je, Mungu ndiye aliyeumba wanadamu na wanyama pia?’ Ni sawa kusema: “Ndiyo, Mungu aliwaumba wanadamu na wanyama.”Lakini namna gani ikiwa mtu fulani haamini kwamba Mungu aliumba wanadamu? Namna gani ikiwa yeye anasema kwamba wanadamu walitokana na wanyama? Biblia haifundishi hivyo. Inasema kwamba Mungu aliumba vitu vyote vilivyo hai.—Mwanzo 1:26-31.

Ikiwa mtu fulani alijenga nyumba hii, ni nani aliyeumba maua, miti, na wanyama?

Mtu akisema haamini kuna Mungu, utamwambia nini?— Mwonyeshe nyumba, kisha mwulize: “Ni nani aliyejenga nyumba ile?” Kila mtu anajua kwamba mtu fulani aliijenga. Bila shaka nyumba hiyo haikujijenga yenyewe!—Waebrania 3:4.

Kisha mpeleke mtu huyo nje na umwonyeshe maua. Mwulize: “Ni nani aliyeyaumba?” Hakuna mwanadamu aliyeumba maua. Kama vile nyumba haikujijenga yenyewe, maua haya pia hayakujiumba yenyewe. Mungu ndiye aliyeyaumba.

Mwambie mtu huyo asikilize ndege anapoimba. Kisha mwulize hivi: “Ni nani aliyewaumba ndege na kuwafundisha kuimba?” Ni Mungu. Yeye ndiye aliyeumba mbingu na dunia na viumbe vyote! Mungu ndiye mwanzilishi wa uhai.

Hata hivyo, mtu anaweza kusema anaamini tu kile anachoona. Labda atasema: ‘Mimi siwezi kuamini kitu nisichoona.’ Hiyo ndiyo sababu watu wengine husema kwamba hawamwamini Mungu kwa sababu hawawezi kumwona.

Ni kweli kwamba hatuwezi kumwona Mungu. Biblia inasema: ‘Hakuna mtu awezaye kumwona Mungu.’ Hakuna mwanamume, mwanamke, au mtoto duniani anayeweza kumwona Mungu. Kwa hiyo, hakuna mtu anayepaswa kutengeneza picha au sanamu ya Mungu. Mungu anatuambia tusitengeneze kitu chochote cha kumfananisha. Basi Mungu hawezi kufurahi tukiwa na vitu kama hivyo nyumbani. —Kutoka 20:4, 5; 33:20; Yohana 1:18.

Lakini ikiwa huwezi kumwona Mungu, unajuaje kwamba kweli yeye yuko? Hebu fikiria. Je, unaweza kuona upepo? La. Hakuna mtu anayeweza kuona upepo. Lakini unaweza kuona mambo ambayo upepo unafanya. Upepo unapovuma, unaweza kuona miti ikitikisika. Na hiyo inafanya uamini kuna upepo.

Unajuaje kwamba kuna upepo?

Vilevile unaweza kuona mambo ambayo Mungu amefanya. Unapoona maua au ndege, unaona kile ambacho Mungu ameumba. Na hiyo inafanya uamini kwamba kuna Mungu.

Mtu anaweza kukuuliza hivi, ‘Ni nani aliyeumba jua na dunia?’ Biblia inasema: “Mungu aliumba mbingu na dunia.” (Mwanzo 1:1) Ndiyo, Mungu aliumba vitu hivi vyote vizuri! Unavionaje? —

Je, hatufurahi kuwa hai? Tunaweza kusikia nyimbo tamu za ndege. Tunaweza kuona maua na vitu vingine ambavyo Mungu ameumba. Na tunaweza kula vyakula ambavyo Mungu ametupatia.

Tunapaswa kumshukuru Mungu kwa vitu hivi vyote. Na zaidi, tunapaswa kumshukuru kwa kutupatia uhai. Ikiwa sisi ni wenye shukrani kwa Mungu, tutafanya jambo fulani. Jambo gani?— Tutamsikiliza Mungu na kufanya yale ambayo anatuambia katika Biblia. Kwa kufanya hivyo tutaonyesha kwamba tunampenda Mungu aliyeviumba vitu vyote.

Tunapaswa kumshukuru Mungu kwa yote ambayo amefanya. Tumshukuru kwa njia gani? Soma Zaburi 139:14; Yohana 4:23, 24; 1 Yohana 5:21; na Ufunuo 4:11.