Hamia kwenye habari

Hamia kwenye yaliyomo

SURA YA 4

Mungu Ana Jina

Mungu Ana Jina

UNAPOKUTANA na mtu kwa mara ya kwanza, unamwuliza jina lake, sivyo?— Sisi sote tuna majina. Mungu alimpa mwanamume wa kwanza duniani jina. Alimwita Adamu. Mke wa Adamu aliitwa Hawa.

Hata hivyo, si watu tu walio na majina. Fikiria vitu vingine pia ambavyo vina majina. Mtu akikupa kitu cha kuchezea, unakipatia jina, sivyo?— Kuwa na jina ni jambo la maana sana.

Hebu zitazame nyota nyingi sana wakati wa usiku. Unafikiri zina majina?— Ndiyo, Mungu aliipatia kila nyota jina lake. Biblia inatuambia hivi: “Anahesabu idadi ya nyota; zote anaziita kwa majina yake.” —Zaburi 147:4.

Je, unajua kwamba nyota zote zina majina?

Unafikiri ni nani aliye wa maana sana katika ulimwengu wote?— Ni Mungu. Je, unafikiri yeye ana jina?— Yesu alisema kwamba Mungu ana jina. Wakati mmoja Yesu alisema hivi aliposali kwa Mungu: ‘Nimejulisha wanafunzi wangu jina lako.’ (Yohana 17:26) Je, unajua jina la Mungu?— Mungu mwenyewe anatuambia jina lake anaposema hivi: “Mimi ni Yehova. Hilo ni jina langu.” Kwa hiyo, jina la Mungu ni YEHOVA. —Isaya 42:8.

Wewe unajisikiaje watu wanapokumbuka jina lako?— Unafurahi, sivyo?— Yehova pia anataka watu wajue jina lake. Kwa hiyo, tunapozungumza kuhusu Mungu, tutumie jina Yehova. Mwalimu Mkuu alitumia jina la Mungu, Yehova, alipozungumza na watu. Wakati mmoja Yesu alisema: “Lazima umpende Yehova Mungu wako kwa moyo wako wote.” —Marko 12:30.

Yesu alijua kwamba “Yehova” ni jina la maana sana. Kwa hiyo, aliwafundisha wanafunzi wake kulitumia jina la Mungu. Hata aliwafundisha kutumia jina la Mungu wanaposali. Yesu alijua kwamba Mungu anataka watu wote walijue jina Lake, Yehova.

Hapo zamani Mungu alimwonyesha Musa aliyekuwa mmoja wa wana wa Israeli, umaana wa jina lake. Wana wa Israeli ambao waliitwa Waisraeli waliishi katika nchi inayoitwa Misri. Watu wa nchi hiyo wanaitwa Wamisri. Watu hao walikuwa wabaya sana, hata waliwafanya Waisraeli kuwa watumwa. Musa alipokuwa mtu mzima, alijaribu kumsaidia Mwisraeli mmoja. Jambo hilo likamkasirisha Farao, mfalme wa Misri. Akataka kumuua Musa! Basi Musa akatoroka Misri.

Musa akaenda nchi nyingine. Nchi hiyo iliitwa Midiani. Akiwa huko, Musa alioa, akawa na watoto. Pia alifanya kazi ya kuchunga kondoo. Siku moja, Musa alipokuwa akichunga kondoo karibu na mlima, aliona jambo la kushangaza. Aliona kichaka kikiwaka moto, lakini hakikuteketea! Musa akaenda karibu ili aone vizuri.

Je, unajua kilichotokea?— Musa alisikia sauti ikiita kutoka katikati ya kichaka hicho chenye kuwaka moto. Akasikia akiitwa, “Musa! Musa!” Ni nani aliyekuwa akimwita?— Ni Mungu! Mungu alitaka kumpa Musa kazi nyingi. Mungu alisema: ‘Njoo nikutume kwa Farao, mfalme wa Misri, ili uwatoe watu wangu, hao wana wa Israeli, katika Misri.’ Mungu akaahidi kumsaidia Musa kufanya kazi hiyo.

Musa alijifunza jambo gani la maana katika kile kichaka kilichokuwa kikiwaka moto?

Lakini Musa akamwambia Mungu: ‘Nikifika kwa wana wa Israeli huko Misri na kuwaambia kwamba Mungu amenituma. Namna gani wakiniuliza, “Jina lake ni nani?” Nitasema nini?’ Mungu akamwambia Musa awaambie wana wa Israeli hivi: ‘Yehova amenituma kwenu. Yehova ndilo jina langu milele.’ (Kutoka 3:1-15) Hii inamaanisha kwamba Mungu angeendelea kuitwa Yehova, na hangebadilisha jina lake kamwe. Yeye alitaka ajulikane milele kwa jina lake, Yehova.

Mungu alilitangazaje jina lake katika Bahari Nyekundu?

Musa aliporudi Misri, Wamisri walifikiri kwamba Yehova ni mungu mdogo sana wa Waisraeli. Hawakufikiri kwamba yeye ni Mungu wa dunia yote. Basi Yehova akamwambia mfalme wa Misri: ‘Nitalitangaza jina langu katika dunia yote.’ (Kutoka 9:16) Kwa kweli, Yehova alilitangaza jina lake. Je, unajua jinsi alivyolitangaza? —

Alimtumia Musa kuwaongoza Waisraeli kutoka Misri. Walipofika Bahari Nyekundu, Yehova alitengeneza njia kavu katikati ya maji. Waisraeli walivuka salama na kufikia nchi kavu. Lakini baada ya Farao na majeshi yake yote kuingia ndani kwenye bahari kavu, maji yaliyokuwa yamezuiwa pande zote yakawafunika Wamisri, na wote wakafa.

Habari ikaenea haraka duniani pote juu ya mambo ambayo Yehova alifanya katika Bahari Nyekundu. Tunajuaje kwamba watu walisikia habari hiyo?— Tunajua hivyo kwa sababu miaka 40 baadaye, Waisraeli walienda Kanaani, nchi ambayo Yehova alikuwa ameahidi kuwapa. Wakiwa huko, mwanamke mmoja aliyeitwa Rahabu aliwaambia wanaume wawili wa Israeli hivi: “Tumesikia jinsi ambavyo Yehova aliyakausha maji ya Bahari Nyekundu mbele yenu wakati mlipotoka Misri.” —Yoshua 2:10.

Leo, watu wengi ni kama Wamisri hao. Hawaamini kwamba Yehova ndiye Mungu wa dunia yote. Kwa hiyo, Yehova anataka watu wake wawaambie wengine juu yake. Na Yesu alifanya hivyo. Alipokuwa karibu kufa, alimwambia Yehova hivi katika sala: “Nimewajulisha jina lako.” —Yohana 17:26.

Yesu alijulisha watu jina la Mungu. Je, unaweza kutaja mahali jina la Mungu linapatikana katika Biblia?

Je, ungependa kuwa kama Yesu? Basi waambie wengine kwamba Mungu anaitwa Yehova. Huenda ukapata kwamba watu wengi hawalijui jina hilo. Labda unaweza kuwaonyesha Zaburi 83:18 katika Biblia. Hebu tuchukue Biblia zetu na tusome andiko hilo pamoja. Linasema: “Ili watu wajue kwamba wewe, ambaye jina lako ni Yehova, Wewe peke yako ndiye Uliye Juu Zaidi, juu ya dunia yote.”

Tunajifunza nini tunaposoma andiko hili?— Tunajifunza kwamba Yehova ni jina la maana sana. Ni jina la Mwenyezi Mungu, Baba ya Yesu na Muumba wa vitu vyote. Kumbuka pia kwamba Yesu alisema tumpende Yehova Mungu kwa moyo wetu wote. Je, wewe unampenda Yehova? —

Tunaweza kuonyesha namna gani kwamba tunampenda Yehova?— Njia moja ni kwa kumfanya awe Rafiki. Njia nyingine ni kwa kuwaambia wengine jina lake. Tunaweza kuwaonyesha katika Biblia kwamba jina lake ni Yehova. Tunaweza pia kusema juu ya vitu vizuri ambavyo Yehova ameumba na mambo mazuri ambayo amefanya. Tukifanya hivyo Yehova anafurahi kwa sababu yeye anataka watu wamjue. Tunaweza kuwaambia wengine kumhusu, sivyo? —

Si kila mtu atasikiliza tunapomwambia kumhusu Yehova. Watu wengi hata hawakusikiliza wakati Yesu, yule Mwalimu Mkuu, alipowaambia kumhusu Yehova. Lakini hiyo haikumzuia Yesu kusema kuhusu Yehova.

Na tuwe kama Yesu. Tuendelee kusema juu ya Yehova. Tukifanya hivyo, Yehova Mungu atapendezwa nasi kwa sababu tunapenda jina lake.

Sasa someni pamoja maandiko mengine machache ya Biblia yanayoonyesha kwamba jina la Mungu ni la maana: Isaya 12:4, 5; Mathayo 6:9; Yohana 17:6; na Waroma 10:13.