Hamia kwenye habari

Hamia kwenye yaliyomo

SURA YA 18

Je, Wewe Hukumbuka Kusema Asante?

Je, Wewe Hukumbuka Kusema Asante?

JE, ULIKULA leo?— Ni nani aliyepika?— Labda ni mama au mtu mwingine, lakini kwa nini tumshukuru Mungu kwa chakula hicho?— Kwa sababu Mungu ndiye anayefanya mimea ikue. Hata hivyo, tunapaswa pia kumshukuru yule aliyetayarisha chakula hicho au aliyetupakulia.

Wakati mwingine tunasahau kusema asante wengine wanapotufanyia mambo mazuri, sivyo? Mwalimu Mkuu alipokuwa duniani, watu fulani wenye ukoma walisahau kusema asante.

Je, unajua jinsi ukoma unavyomdhuru mtu?— Ugonjwa huo hata unaweza kuharibu mwili. Yesu alipokuwa duniani, wenye ukoma walipaswa kukaa mbali na watu wengine. Na ikiwa mwenye ukoma angemwona mtu mwingine akija, alipaswa kumwonya kwa sauti na kumwambia akae mbali naye. Walifanya hivyo ili watu wengine wasiwakaribie sana wenye ukoma na kuupata ugonjwa huo.

Yesu alikuwa mwenye fadhili sana kwa watu wenye ukoma. Siku moja Yesu alikuwa akienda Yerusalemu, akapitia mji fulani mdogo. Alipokaribia mji huo, watu kumi wenye ukoma wakatoka ili wamlaki. Walikuwa wamesikia kwamba Yesu ana nguvu kutoka kwa Mungu za kuponya magonjwa ya kila aina.

Watu hao hawakumkaribia Yesu. Walisimama mbali. Lakini waliamini kwamba Yesu angewaponya. Basi watu hao wenye ukoma walipomwona Mwalimu Mkuu, wakamwambia kwa sauti: ‘Yesu, Mwalimu, tusaidie!’

Je, wewe huwahurumia wagonjwa?— Yesu aliwahurumia. Alijua jinsi ilivyohuzunisha kuwa na ukoma. Basi Yesu akawaambia: “Nendeni mkajionyeshe kwa makuhani.”—Luka 17:11-14.

Yesu anawaambia hawa watu wenye ukoma wafanye nini?

Kwa nini Yesu aliwaambia waende kwa makuhani? Ni kwa sababu ya sheria ambayo Yehova aliwapa watu wake kuhusu wagonjwa wa ukoma. Sheria hiyo ilisema kwamba kuhani wa Mungu anapaswa kuchunguza ngozi ya mwenye ukoma. Kuhani angeweza kumwambia mwenye ukoma kwamba ugonjwa wake umekwisha. Mgonjwa alipopona, angeweza kukaa tena na watu wasio na ugonjwa huo.—Mambo ya Walawi 13:16, 17.

Lakini watu hao bado walikuwa na ukoma. Je, walimwendea kuhani kama vile Yesu alivyowaambia?— Ndiyo, walifanya hivyo mara moja. Ni lazima watu hao waliamini kwamba Yesu anaweza kuwaondolea ugonjwa. Basi ikawaje?

Wakiwa njiani kwenda kwa kuhani, walipona. Nyama ya mwili wao ikapona. Wakapona kabisa! Walibarikiwa kwa sababu ya kuweka imani katika nguvu za Yesu. Walifurahi sana. Lakini walipaswa kufanya nini ili kuonyesha shukrani? Wewe ungefanya nini?—

Mtu huyu mwenye ukoma alikumbuka kufanya nini?

Mmoja wa wale watu walioponywa alimrudia Yesu. Akaanza kumtukuza Yehova, akisema mambo mazuri kumhusu Mungu. Alifanya vizuri kwa sababu nguvu za kuponya zilitoka kwa Mungu. Mtu huyo alipiga magoti miguuni pa Mwalimu Mkuu na kumshukuru pia. Alishukuru sana kwa sababu ya vile Yesu alivyofanya.

Vipi wale wengine tisa? Yesu akauliza: ‘Watu kumi waliponywa, sivyo? Wako wapi wale tisa? Ni mmoja tu aliyerudi ili kumpa Mungu utukufu?’

Ni kweli. Ni mmoja tu kati ya wale kumi aliyemtukuza, au kumsifu Mungu, na kurudi kumwambia Yesu asante. Na mtu huyo alikuwa Msamaria, mtu wa nchi nyingine. Wale wengine tisa hawakumshukuru Mungu wala hawakumshukuru Yesu.—Luka 17:15-19.

Wewe ni kama nani kati ya watu hao? Tunataka kuwa kama yule Msamaria, sivyo?— Basi mtu anapotufanyia jambo la fadhili, tunapaswa kukumbuka kufanya nini?— Inafaa tuonyeshe shukrani. Mara nyingi watu wanasahau kusema asante. Lakini ni vizuri kusema asante. Tunaposema asante, Yehova Mungu na Mwanaye, Yesu, wanafurahi.

Unawezaje kumwiga mtu mwenye ukoma aliyerudi kwa Yesu?

Ukifikiria sana, utakumbuka kwamba watu wamekufanyia mambo mengi mazuri. Kwa mfano, umewahi kuwa mgonjwa?— Labda hujawahi kuwa mgonjwa kama wale watu kumi wenye ukoma, lakini inawezekana ulikuwa na mafua makali au maumivu ya tumbo. Je, kuna mtu aliyekutunza?— Labda walikupa dawa na kukufanyia mambo mengine. Je, ulifurahi kwamba walikusaidia ukapata nafuu?—

Yule Msamaria alimshukuru Yesu kwa kumponya, na Yesu akafurahi. Unafikiri mama na baba watafurahi ukisema asante wanapokufanyia mambo fulani?— Ndiyo, watafurahi.

Kwa nini ni jambo la maana kukumbuka kusema asante?

Watu wengine hukufanyia mambo kila siku au kila juma. Labda ni daraka lao kufanya mambo hayo. Hata labda watu hao wanafurahi kufanya mambo hayo. Lakini unaweza kusahau kuwaambia asante. Mwalimu shuleni anaweza kujitahidi kukusaidia ujifunze mambo mengi. Hiyo ni kazi yake. Lakini atafurahi ukimwambia asante kwa msaada wake.

Watu wengine wanaweza kukufanyia mambo madogo-madogo. Wakati mwingine mtu anaweza kukufungulia mlango? Au kukupitishia chakula mnapokuwa mezani? Ni vizuri kusema asante hata kwa hayo mambo madogo-madogo.

Ikiwa tunakumbuka kuwaambia watu walio duniani asante, tutakumbuka kumwambia asante Baba yetu aliye mbinguni. Na kuna vitu vingi ambavyo vinapasa kutufanya tumshukuru Yehova! Alitupatia uhai na vitu vyote vizuri ambavyo vinafanya maisha yapendeze. Basi tuna sababu nyingi za kumpa Mungu utukufu kwa kusema mambo mazuri kumhusu kila siku..