Hamia kwenye habari

Hamia kwenye yaliyomo

SURA YA 19

Je, Ni Vizuri Kupigana?

Je, Ni Vizuri Kupigana?

JE, KUNA wavulana au wasichana wowote unaowajua ambao wanajifanya mashujaa au wenye nguvu?— Je, unapenda kuwa nao? Au ungependa kuwa na mtu mwenye fadhili na anayependa amani?— Mwalimu Mkuu alisema: “Wenye furaha ni wale wanaofanya amani, kwa kuwa wataitwa ‘wana wa Mungu.’”—Mathayo 5:9.

Lakini wakati mwingine watu hufanya mambo ambayo yanatuudhi, sivyo?— Huenda tukataka kulipiza kisasi. Jambo hilo liliwapata wanafunzi wa Yesu siku moja walipokuwa wakisafiri na Yesu kuelekea Yerusalemu. Hebu nikuambie ilivyokuwa.

Walipokuwa wamesafiri kidogo, Yesu aliwatuma baadhi ya wanafunzi wake watangulie kwenda kutafuta mahali pa kupumzikia katika kijiji kimoja cha Wasamaria. Lakini watu wa huko hawakuwakaribisha, kwa sababu Wasamaria walikuwa wa dini tofauti. Na hawakumpenda mtu yeyote ambaye alisafiri kwenda kuabudu jijini Yerusalemu.

Yakobo na Yohana walitaka kufanya nini ili kulipiza kisasi dhidi ya Wasamaria?

Kama ni wewe ungefanyaje? Je, ungekasirika? Je, ungelipiza kisasi?— Hivyo ndivyo wanafunzi Yakobo na Yohana walivyotaka. Walimwambia Yesu: “Je, unataka tuuambie moto ushuke kutoka mbinguni na kuwaangamiza?” Si ajabu Yesu aliwaita Wana wa Ngurumo! Lakini Yesu aliwaambia kwamba si vizuri kuwatendea watu wengine hivyo.—Luka 9:51-56; Marko 3:17.

Ni kweli kwamba wakati mwingine watu wanaweza kututendea vibaya. Watoto wengine wanaweza kukataa kucheza nasi. Hata wanaweza kukuambia: “Hatukutaki hapa.” Jambo kama hilo likitokea, tunaweza kukosa furaha, sivyo? Na tunaweza kutaka kulipiza kisasi. Lakini, je, inafaa?

Hebu chukua Biblia yako na tufungue Mithali sura ya 24, mstari wa 29. Andiko hilo linasema hivi: “Usiseme: ‘Nitamtendea kama vile tu alivyonitendea. Nitamlipa kila mtu kulingana na tendo lake.’”

Unafikiri mstari huo unamaanisha nini?— Unasema tusilipize kisasi. Tusimtendee mtu vibaya eti kwa sababu ametutendea vibaya. Lakini vipi ikiwa mtu anakuchokoza? Anaweza kujaribu kukutukana ili ukasirike. Labda atakucheka na kukuambia kwamba unaogopa. Vipi akikuita mwoga? Ufanye nini? Je, upigane naye?—

Tuone tena maoni ya Biblia. Fungua Mathayo sura ya 5, mstari wa 39. Yesu alisema: “Msimpinge yeye aliye mwovu; bali yeyote anayekupiga kofi kwenye shavu lako la kuume, mgeuzie lile lingine pia.” Unafikiri Yesu alimaanisha nini aliposema hivyo? Je, alimaanisha kwamba mtu akikupiga ngumi upande mmoja wa uso, unapaswa kuacha akupige upande ule mwingine?—

La, Yesu hakumaanisha hivyo. Kofi si kama kupigwa ngumi. Ni kama kusukumwa tu. Mtu anaweza kutupiga kofi ili tupigane. Anataka tukasirike. Na ikiwa tutakasirika na kumsukuma, ni nini kitakachotokea?— Labda tutaanza kupigana.

Lakini Yesu hakutaka wafuasi wake wapigane. Kwa hiyo alisema kwamba mtu akitupiga kofi, tusilipize kisasi. Tusikasirike na kuanza kupigana. Ikiwa tutapigana, basi inaonyesha hakuna tofauti kati yetu na yule aliyetuchokoza.

Ikiwa tatizo linaanza, unafikiri ni vizuri kufanya nini?— Kuondoka mahali hapo. Huyo mchokozi anaweza kutusukuma tena. Lakini baadaye anaweza kuacha. Kuondoka hakumaanishi kwamba huna nguvu. Inamaanisha una nguvu za kutenda yaliyo mema.

Tunapaswa kufanya nini ikiwa mwingine anajaribu kutuchokoza?

Lakini vipi ikiwa utakubali kupigana na ushinde? Ni nini kinachoweza kutokea?— Yule uliyempiga anaweza kuja na rafiki zake. Wanaweza kukupiga kwa fimbo au kukuchoma kisu na kukujeruhi. Je, unaelewa sasa ni kwa nini Yesu hataki tupigane?—

Tufanye nini basi tukiona wengine wanapigana? Je, tumsaidie mmoja wao?— Biblia inatuambia jambo linalofaa kufanya. Fungua Mithali sura ya 26, mstari wa 17. Mstari huo unasema: “Mpita-njia yeyote anayekasirishwa na ugomvi usio wake ni kama mtu anayemshika mbwa masikio.”

Kuingilia vita ya wengine kunafananaje na kumshika mbwa masikio? Ukifanya hivyo unaweza kuumia, basi usithubutu kuingilia vita ya wengine!

Ni nini kinachoweza kutokea ukimshika mbwa kwa masikio? Mbwa atasikia uchungu, naye atakuuma, sivyo? Kadiri mbwa anavyojaribu kung’ang’ana ili umwachilie, ndivyo itakavyokubidi uendelee kumshika masikio na ndivyo atakavyozidi kukasirika. Ukimwachilia, labda atakuuma sana. Lakini kweli utaweza tu kusimama hapo na kumshika masikio daima?—

Hilo ndilo tatizo linaloweza kutupata tukiingilia vita ya wengine. Huenda tusijue aliyeanzisha pigano au kinachofanya wapigane. Labda yule anayepigwa alimwibia mwingine. Tukimsaidia tunasaidia mwizi. Si vizuri, sivyo?

Basi, ufanye nini ukiona wengine wakipigana?— Ikiwa ni shuleni, unaweza kukimbia na kumwambia mwalimu. Na ikiwa ni mbali na shule, unaweza kuita mzazi wako au polisi. Ndiyo, hata wakati wengine wanataka kupigana, sisi tunapaswa kuwa wenye amani.

Ufanye nini unapoona wengine wakipigana?

Wanafunzi wa kweli wa Yesu wanajaribu kuepuka kabisa mapigano. Kwa kufanya hivyo tunaonyesha kwamba tuna nguvu za kufanya yaliyo mema. Biblia inasema kwamba mwanafunzi wa Yesu “hahitaji kupigana, bali anahitaji kuwa mpole kwa wote.”—2 Timotheo 2:24.

Sasa tusome mashauri zaidi yanayoweza kutusaidia kuepuka mapigano: Waroma 12:17-21 na 1 Petro 3:10, 11.