Hamia kwenye habari

Hamia kwenye yaliyomo

SURA YA 25

Je, Watu Wanaofanya Mabaya Wanaweza Kubadilika?

Je, Watu Wanaofanya Mabaya Wanaweza Kubadilika?

LINGEKUWA jambo zuri kama kila mtu angefanya mema, sivyo?— Lakini hakuna mtu anayefanya mambo mema kila wakati. Je, unajua ni kwa nini sisi sote tunafanya mabaya wakati mwingine hata tunapotaka kufanya mema?— Kwa sababu sote tumerithi dhambi. Lakini watu wengine hufanya mambo mengi mabaya sana. Wao huwachukia watu wengine na kuwaumiza kimakusudi. Unafikiri wanaweza kubadilika na kufanya mema?—

Mtazame mtu huyu anayelinda nguo za wale wanaompiga Stefano kwa mawe. Jina lake la Kiebrania ni Sauli, lakini jina lake la Kiroma ni Paulo. Anafurahi kwamba Stefano ambaye ni mwanafunzi wa Mwalimu Mkuu anauawa. Tuone ni kwa nini Sauli anafanya mambo mabaya kama hayo.

Sauli anashirikiana na wafuasi wa dini ya Wayahudi wanaoitwa Mafarisayo. Mafarisayo wanajua Neno la Mungu, lakini wanashikilia sana mafundisho ya viongozi wao wa kidini. Hiyo inamfanya Sauli atende mambo mabaya.

Sauli yuko Stefano anapokamatwa huko Yerusalemu. Stefano anapelekwa mahakamani, ambapo baadhi ya mahakimu ni Mafarisayo. Ijapokuwa anashtakiwa mambo mabaya, Stefano haogopi. Anaongea kwa ujasiri na kuwahubiria mahakimu kumhusu Yehova Mungu na kumhusu Yesu.

Lakini mahakimu hao hawafurahii ujumbe huo. Tayari wanajua mambo mengi kumhusu Yesu. Muda mfupi tu kabla ya wakati huu, Mafarisayo walipanga Yesu auawe. Lakini baadaye, Yehova alimrudisha Yesu mbinguni. Na sasa, badala ya mahakimu kubadili njia zao, wanawapinga wanafunzi wa Yesu.

Mahakimu wanamkamata Stefano na kumpeleka nje ya mji. Wanamwangusha chini na kumpiga kwa mawe. Na kama unavyoona kwenye picha, Sauli yupo papo hapo anatazama. Kwa maoni yake, Stefano anapaswa kuuawa.

Kwa nini Sauli anafikiri kwamba Stefano anapaswa kuuawa?

Unajua ni kwa nini Sauli alifikiri hivyo? Yeye amekuwa Farisayo maisha yake yote na aliamini kwamba mafundisho ya Mafarisayo ndiyo ya kweli na basi akaiga mfano wao.—Matendo 7:54-60.

Baada ya Stefano kuuawa, Sauli anafanya nini?— Anajaribu kuwaua wanafunzi wengine wote wa Yesu! Anaenda hadi kwao na kuwavuruta nje wanaume kwa wanawake. Kisha anawafunga gerezani. Wanafunzi wengi wanatoroka Yerusalemu, lakini hawaachi kuhubiri kumhusu Yesu.—Matendo 8:1-4.

Jambo hilo linamfanya Sauli awachukie wanafunzi wa Yesu hata zaidi. Basi anaenda kwa Kuhani Mkuu Kayafa na kuomba aruhusiwe kuwakamata Wakristo katika mji wa Damasko. Sauli anataka kuwaleta Yerusalemu wakiwa wafungwa ili waadhibiwe. Lakini akiwa njiani kwenda Damasko, jambo la ajabu linatokea.

Ni nani anayeongea na Sauli, na anamtuma Sauli afanye nini?

Nuru inaangaza kutoka mbinguni, na sauti inasema: “Sauli, Sauli, kwa nini unanitesa?” Ni Yesu anayezungumza kutoka mbinguni! Nuru hiyo ni kali sana mpaka inampofusha Sauli macho hivi kwamba watu waliokuwa naye wanamwongoza hadi Damasko.

Siku tatu baadaye Yesu anamtokea mwanafunzi aitwaye Anania katika ndoto huko Damasko. Yesu anamwambia Anania amtembelee Sauli ili amponye upofu wake na azungumze naye. Anania anapozungumza na yeye, Sauli anakubali kweli kumhusu Yesu. Macho yake yanafumbuliwa. Maisha yake yote yanabadilika, naye anakuwa mtumishi mwaminifu wa Mungu.—Matendo 9:1-22.

Unaelewa sasa ni kwa nini Sauli alifanya mambo mabaya?— Ni kwa sababu alifundishwa uwongo. Aliwafuata watu ambao hawakuwa waaminifu kwa Mungu. Naye alishirikiana na watu ambao walitanguliza mawazo ya wanadamu kuliko Neno la Mungu. Lakini kwa nini Sauli anabadili maisha yake na kuanza kutenda mema ijapokuwa Mafarisayo wengine wanaendelea kumpinga Mungu?— Ni kwa sababu moyoni Sauli hachukii kweli. Kwa hiyo anapojifunza yaliyo kweli, yuko tayari kuyafanya.

Je, unajua Sauli alikuja kuwa nani baadaye?— Baadaye aliitwa mtume Paulo, mtume wa Yesu. Kumbuka pia kwamba Paulo aliandika vitabu vingi katika Biblia kuliko mtu mwingine yeyote.

Kuna watu wengi walio kama Sauli ambao wanaweza kubadilika. Lakini si rahisi wabadilike kwa sababu kuna mtu anayefanya bidii sana kufanya watu watende mambo mabaya. Unamjua mtu huyo?— Yesu alimtaja mtu huyo alipomtokea Sauli akiwa barabarani kuelekea Damasko. Yesu akiwa mbinguni alizungumza na Sauli na kumwambia: ‘Ninakutuma kufungua macho ya watu, kuwageuza kutoka katika giza kuingia katika nuru na kutoka katika mamlaka ya Shetani na kumgeukia Mungu.’—Matendo 26:17, 18.

Bila shaka, Shetani Ibilisi ndiye anayejaribu kuwafanya watu watende mabaya. Je, wakati mwingine wewe hushindwa kufanya mema?— Hali hiyo hutupata sisi sote. Shetani anafanya iwe vigumu kutenda mema. Lakini kuna sababu nyingine inayofanya isiwe rahisi kufanya mema siku zote. Je, unaijua?— Ni kwa sababu tumerithi dhambi.

Dhambi hiyo ndiyo inafanya iwe rahisi kutenda mabaya kuliko kutenda mema. Basi, tunahitaji kufanya nini?— Ni lazima tujitahidi sana kufanya yaliyo mema. Tukijitahidi, tunakuwa na uhakika kwamba Yesu anayetupenda, atatusaidia.

Yesu alipokuwa duniani, alionyesha anawapenda watu ambao waliacha kufanya mabaya. Alielewa jinsi walivyojitahidi sana kubadilika. Kwa mfano, kuna wanawake ambao walikuwa wamefanya ngono na wanaume wengi. Bila shaka hilo ni kosa. Biblia huwaita wanawake hao makahaba.

Kwa nini Yesu alimsamehe mwanamke huyu aliyekuwa amefanya mambo mabaya?

Wakati mmoja mwanamke mmoja kahaba alisikia kuhusu Yesu, akaja mahali alipokuwa Yesu katika nyumba ya Farisayo. Akammwagia Yesu mafuta miguuni na kupangusa machozi yake kwenye miguu ya Yesu kwa nywele zake. Alisikitikia sana dhambi zake, basi Yesu akamsamehe. Lakini yule Farisayo aliona kwamba mwanamke huyo hafai kusamehewa.—Luka 7:36-50.

Unajua Yesu aliwaambia nini baadhi ya Mafarisayo?— Aliwaambia: “Makahaba wanawatangulia ninyi kuingia katika ufalme wa Mungu.” (Mathayo 21:31) Yesu alisema hivyo kwa sababu makahaba walimwamini na kuacha njia zao mbaya. Lakini Mafarisayo waliendelea kuwatendea wanafunzi wa Yesu mambo mabaya.

Kwa hiyo Biblia inaposema kwamba jambo tunalofanya ni baya, tunapaswa kuliacha. Na tunapojifunza yale Yehova anataka tufanye, tunapaswa kufurahia kuyafanya. Kisha tutamfurahisha Yehova naye atatupatia uzima wa milele.

Ili tuepuke kutenda mabaya, tusome pamoja Zaburi 119:9-11 (118:9-11, “Dy”); Mithali 3:5-7; na 12:15.