Hamia kwenye habari

Hamia kwenye yaliyomo

SURA YA 27

Mungu Wako Ni Nani?

Mungu Wako Ni Nani?

MUNGU wako ni nani? Kwa nini swali hilo ni muhimu?— Ni muhimu kwa sababu watu wanaabudu miungu mingi. (1 Wakorintho 8:5) Mtume Paulo alipopewa nguvu na Yehova ili amponye mtu ambaye hakuwa amewahi kutembea, watu walipaaza sauti hivi: “Miungu imekuwa kama binadamu nayo imeshuka kwetu!” Watu walitaka kuwaabudu Paulo na rafiki yake Barnaba. Wakamwita Paulo Herme na Barnaba wakamwita Zeu, ambayo yalikuwa majina ya miungu isiyo ya kweli.

Lakini Paulo na Barnaba hawakukubali kuabudiwa. Wakaruka ndani ya umati na kusema: ‘Acheni mambo haya ya bure mmjie Mungu aliye hai.’ (Matendo 14:8-15) “Mungu aliye hai,” ambaye aliumba vitu vyote ni nani?— Bila shaka, ni Yehova, ‘Aliye juu Zaidi, juu ya dunia yote.’ Yesu alimwita Yehova “Mungu wa pekee wa kweli.” Basi, ni nani pekee anayestahili kuabudiwa?— Ni Yehova peke yake!—Zaburi 83:18; Yohana 17:3; Ufunuo 4:11.

Kwa nini Paulo na Barnaba hawakuruhusu watu wawainamie?

Watu wengi wanaabudu miungu mingine badala ya “Mungu wa pekee wa kweli.” Mara nyingi wanaabudu vitu ambavyo wametengeneza kutoka kwa miti, mawe, au chuma. (Kutoka 32:4-7; Mambo ya Walawi 26:1; Isaya 44:14-17) Hata wanaume na wanawake mashuhuri hutukuzwa au kuabudiwa. Je, ni sawa kuwatukuza?—

Baada ya Sauli kuwa mtume Paulo, aliandika hivi: “Mungu wa mfumo huu wa mambo amezipofusha akili za wasioamini.” (2 Wakorintho 4:4) Huyu mungu ni nani?— Ni Shetani Ibilisi! Shetani amefanya watu waabudu watu wengine na vitu vingi.

Shetani alipojaribu kumfanya Yesu amsujudu na kumwabudu, Yesu alimwambia nini Shetani?— “Yehova Mungu wako ndiye unayepaswa kumwabudu, na yeye peke yake ndiye unayepaswa kumtolea utumishi mtakatifu.” (Mathayo 4:10) Kwa hiyo Yesu alionyesha wazi kwamba ni Yehova peke yake anayepaswa kuabudiwa. Hebu tusome kuhusu vijana fulani waliojua hivyo. Waliitwa Shadraki, Meshaki, na Abednego.

Vijana hao Waebrania walikuwa wa taifa la Mungu la Israeli ambao walipelekwa utekwani kule Babiloni. Wakiwa huko mfalme anayeitwa Nebukadneza alitengeneza sanamu kubwa ya dhahabu. Siku moja alitoa amri kwamba muziki uliposikika, kila mtu alipaswa kuiinamia sanamu hiyo. Na akaonya kwamba ‘kila mtu asiyeanguka chini na kuabudu angetupwa ndani ya tanuru inayowaka moto.’ Wewe ungefanya nini?—

Kwa nini watu hawa hawaisujudii sanamu?

Kwa kawaida, Shadraki, Meshaki, na Abednego walifanya kila kitu ambacho mfalme aliamuru. Lakini walikataa kuiinamia sanamu. Unajua ni kwa nini?— Kwa sababu sheria ya Mungu ilisema: ‘Usiwe na miungu mingine ila mimi. Usijifanyie sanamu ya kuchongwa wala kuiinamia.’ (Kutoka 20:3-5) Kwa hiyo, Shadraki, Meshaki, na Abednego walitii sheria ya Yehova badala ya kutii amri ya mfalme.

Mfalme akakasirika sana, na mara moja akaamuru vijana hao watatu Waebrania waletwe mbele yake. Naye akawauliza: ‘Je, ni kweli kwamba hamwitumikii miungu yangu? Nitawapa nafasi nyingine. Sasa mtakapoisikia sauti ya muziki angukeni chini na kuiabudu sanamu ambayo nimeitengeneza. Lakini msipoabudu mtatupwa ndani ya tanuru inayowaka moto. Na ni mungu gani anayaweza kuwaokoa kutoka mikononi mwangu?’

Vijana hao wangefanya nini sasa? Wewe ungefanya nini?— Wao wakamwambia mfalme: ‘Mungu ambaye tunamtumikia anaweza kutuokoa. Lakini kama sivyo, sisi hatuitumikii miungu yako, na sanamu yako ya dhahabu hatutaiabudu.’

Mfalme akakasirika sana. Naye akaamuru: ‘Itieni moto ile tanuru mara saba kuliko ilivyo kawaida!’ Kisha akawaamuru wanaume wenye nguvu wawafunge Shadraki, Meshaki, na Abednego na kuwatupa ndani ya tanuru! Hiyo tanuru ikawa na moto mkali sana hivi kwamba wanaume hao wa mfalme wakafa kwa miale ya moto! Namna gani hao Waebrania watatu?

Shadraki, Meshaki, na Abednego walianguka katikati ya moto. Hata hivyo wakasimama bila hata kuumia. Na sasa hawakuwa wamefungwa. Hiyo iliwezekanaje?— Mfalme akatazama ndani ya tanuru na mambo aliyoona yakamwogopesha sana. “Je, hatukutupa wanaume watatu ndani ya moto?” akauliza. Watumishi wake wakamjibu: “Ndiyo, Ee mfalme.”

Yehova aliwaokoaje watumishi wake kutoka kwenye tanuru yenye moto?

Mfalme akasema: ‘Tazama! Naona wanaume wanne wakitembea humo, na moto hauwadhuru.’ Huyo mtu wa nne alikuwa nani?— Ni malaika wa Yehova. Aliwalinda hao Waebrania watatu wasiumie.

Alipoona mambo hayo, mfalme akaenda mlangoni mwa tanuru na kuita kwa sauti: “Shadraki, Meshaki na Abednego, enyi watumishi wa Mungu Aliye Juu Zaidi, tokeni nje, mje hapa!” Walipotoka nje, kila mtu aliona kwamba hawajaungua. Hata hawakuwa na harufu ya moto. Kisha mfalme akasema: ‘Abarikiwe Mungu wa Shadraki, Meshaki na Abednego aliyemtuma malaika wake na kuwaokoa watumishi wake kwa sababu walikataa kuabudu mungu yeyote mwingine ila Mungu wao wenyewe.’—Danieli, sura ya 3.

Ni sanamu zipi zinazotukuzwa na watu leo?

Tunaweza kujifunza kutokana na mambo hayo yaliyotokea hapo zamani. Hata siku hizi watu hutengeneza sanamu ili ziabudiwe. Kitabu kinachoitwa The Encyclopedia Americana kinasema: “Bendera ni takatifu kama vile msalaba ulivyo mtakatifu.” Sanamu zinaweza kutengenezwa kutokana na miti, mawe, chuma au kitambaa. Wanafunzi wa Yesu wa mapema hawangemfanyia mfalme wa Roma tendo la ibada, jambo ambalo Daniel P. Mannix alisema ni sawa na “kukataa kusalimu bendera au kuimba wimbo wa taifa.”

Unafikiri Mungu anaonaje sanamu ya kidini ambayo imetengenezwa kutokana na kitambaa, mbao, mawe, au chuma?— Je, ingekuwa sawa mtumishi wa Yehova kuifanyia sanamu kama hiyo tendo la ibada?— Shadraki, Meshaki, na Abednego hawakufanya hivyo, Yehova akafurahi sana. Unawezaje kuiga mfano wao?

Wale wanaomtumikia Yehova hawawezi kuabudu mtu yeyote au kitu chochote. Soma yanayosemwa kuhusu mambo hayo katika Yoshua 24:14, 15, 19-22; Isaya 42:8; 1 Yohana 5:21; na Ufunuo 19:10.