Hamia kwenye habari

Hamia kwenye yaliyomo

SURA YA 31

Mahali pa Kupata Faraja

Unafikiri huyu mwana-kondoo aliyepotea anahisije?

Mahali pa Kupata Faraja

JE, KUNA nyakati ambazo unahuzunika na kujihisi mpweke?— Je, kuna wakati unahisi kwamba hakuna mtu anayekupenda?— Watoto wengine hupatwa na hali hiyo. Lakini Mungu anaahidi: “Mimi mwenyewe sitakusahau.” (Isaya 49:15) Je, hilo si jambo la kupendeza?— Ndiyo, kwa kweli Yehova Mungu anatupenda sana!

Mwandikaji mmoja wa Biblia alisema: ‘Hata baba yangu na mama yangu waniache, Yehova mwenyewe angenichukua.’ (Zaburi 27:10) Kujua hivyo kunatupa faraja ya kweli, sivyo?— Ndiyo, Yehova anatuambia: “Usiogope, kwa maana mimi nipo pamoja nawe. . . . Nitakusaidia kwelikweli.”Isaya 41:10.

Hata hivyo, wakati mwingine Yehova humruhusu Shetani atuletee magumu. Yehova hata humruhusu Shetani awajaribu watumishi Wake. Wakati mmoja Ibilisi alimfanya Yesu ateseke sana mpaka akalia kwa sauti kubwa hivi kwa Yehova: “Mungu wangu, Mungu wangu, kwa nini umeniacha?” (Mathayo 27:46) Ijapokuwa Yesu aliteseka, bado alijua kwamba Yehova anampenda. (Yohana 10:17) Lakini Yesu alijua pia kwamba Mungu humruhusu Shetani awajaribu watumishi Wake na kuwatesa. Katika sura nyingine tutaeleza sababu ya Mungu kumruhusu Shetani afanye hivyo.

Tunapokuwa wachanga, inakuwa rahisi kuogopa wakati mwingine. Kwa mfano, umewahi kupotea?— Je, uliogopa?— Watoto wengi huogopa. Wakati mmoja Mwalimu Mkuu alizungumza kuhusu kupotea. Lakini aliyepotea hakuwa mtoto. Alikuwa kondoo.

Katika njia fulani wewe ni kama kondoo. Inawezekanaje hivyo? Kondoo ni wadogo na hawana nguvu sana. Nao wanahitaji mtu wa kuwatunza na kuwalinda. Mtu anayechunga kondoo anaitwa mchungaji.

Katika hadithi yake, Yesu alizungumzia mchungaji aliyekuwa na kondoo mia moja. Lakini mmoja wao akapotea. Labda kondoo huyo alitaka kuona ni nini kilichokuwa upande ule mwingine wa mlima. Baada ya muda mfupi tu, kondoo huyo akaenda mbali sana na wengine. Unaweza kuwazia jinsi kondoo huyo alivyohisi alipoangalia huku na huku na kushtuka kwamba yuko peke yake?—

Mchungaji angefanya nini akigundua kwamba kondoo huyo amepotea? Je, angesema potelea mbali na asihangaike kumtafuta? Au angewaacha wale kondoo 99 mahali salama na kwenda kumtafuta yule mmoja tu? Je, kondoo mmoja tu anastahili kutafutwa kwa bidii hivyo?— Kama ungalikuwa huyo kondoo aliyepotea, je, hungalipenda mchungaji akutafute?—

Ni nani aliye kama mchungaji anayeokoa kondoo wake?

Mchungaji aliwapenda kondoo wake wote, hata yule aliyepotea. Basi akaenda kumtafuta. Hebu fikiria jinsi kondoo huyo alivyofurahi alipomwona mchungaji akija! Na Yesu alisema kwamba mchungaji alifurahi kumpata kondoo wake. Alimfurahia sana kuliko wale 99 ambao hawakuwa wamepotea. Basi, ni nani aliye kama yule mchungaji katika hadithi ya Yesu? Ni nani anayetujali sana kama vile yule mchungaji alivyomjali kondoo wake?— Yesu alisema kwamba ni Baba yake wa mbinguni. Na Baba yake ni Yehova.

Yehova Mungu ndiye Mchungaji Mkuu wa watu wake. Anawapenda wote wanaomtumikia, kutia ndani wachanga kama wewe. Yeye hataki yeyote kati yetu aumie. Kwa hakika inafariji kujua kwamba Mungu anatujali sana hivyo!—Mathayo 18:12-14.

Je, unamwona Yehova akiwa halisi kama unavyomwona baba yako au mtu mwingine?

Je, kweli wewe unamwamini Yehova Mungu?— Je, unamwona kama mtu halisi?— Ni kweli kwamba hatuwezi kumwona Yehova. Hii ni kwa sababu yeye ni Roho. Ana mwili ambao hatuwezi kuuona kwa macho yetu. Lakini yeye ni halisi, na anaweza kutuona. Anajua wakati tunapohitaji msaada. Na tunaweza kuzungumza naye katika sala, kama vile tu tunavyoweza kuzungumza na mtu mwingine duniani. Yehova anataka tuzungumze naye katika sala.

Kwa hiyo ukihisi huzuni au upweke, unapaswa kufanya nini?— Zungumza na Yehova. Mkaribie, naye atakufariji na kukusaidia. Kumbuka kwamba Yehova anakupenda, hata wakati unapohisi upweke. Hebu tuchukue Biblia yetu. Tunaambiwa hivi katika Zaburi 23 kuanzia mstari wa 1: “Yehova ni Mchungaji wangu. Sitakosa chochote. Ananilaza katika malisho yenye majani mengi; ananiongoza kando ya mahali pa kupumzika palipo na maji ya kutosha.”

Ona kile mwandikaji anaongezea kutaja katika mstari wa 4: “Hata ingawa ninatembea katika bonde lenye kivuli kizito, siogopi chochote kibaya, kwa maana wewe uko pamoja nami; fimbo yako na gongo lako ndivyo vitu vinavyonifariji.” Hivyo ndivyo watu wanavyohisi iwapo Mungu wao ni Yehova. Wanapata faraja wakati wa taabu. Je, hivyo ndivyo unavyohisi?—

Kama vile mchungaji mwenye upendo anavyowatunza kondoo wake, ndivyo Yehova anavyowatunza watu wake sana. Anawaonyesha njia iliyo bora, nao wanafurahi kuifuata. Hata wanapokuwa na matatizo mengi, hawahitaji kuogopa. Mchungaji hutumia fimbo kuwalinda kondoo kutokana na wanyama ambao wanaweza kuwaumiza. Biblia inasimulia jinsi kijana mchungaji Daudi alivyowalinda kondoo wake dhidi ya simba na dubu. (1 Samweli 17:34-36) Na watu wa Mungu wanajua kwamba Yehova atawalinda pia. Wanaweza kujihisi wakiwa salama kwa sababu Mungu yuko pamoja nao.

Tunapokuwa na matatizo, ni nani anayeweza kutusaidia kama mchungaji anayelinda kondoo wake?

Kwa kweli Yehova anawapenda kondoo wake, naye anawatunza kwa fadhili. Biblia inasema: ‘Atawachunga kondoo wake mwenyewe kama mchungaji. Atawakusanya pamoja wana-kondoo kwa mkono wake.’—Isaya 40:11.

Je, hufurahi kujua kwamba hivyo ndivyo Yehova alivyo?— Ungependa kuwa kondoo wake?— Kondoo wanasikiliza sauti ya mchungaji wao. Wanakaa karibu naye. Je, wewe unamsikiliza Yehova?— Je, unakaa karibu naye?— Basi huhitaji kuogopa kamwe. Yehova atakuwa pamoja nawe.

Kwa upendo Yehova anawatunza wale wanaomtumikia. Tusome pamoja yale ambayo Biblia inasema kuhusu jambo hili katika Zaburi 37:25 (36:25, “Dy”); 55:2255:22 (54:23, “Dy”); na Luka 12:29-31.