Hamia kwenye habari

Hamia kwenye yaliyomo

SURA YA 35

Tunaweza Kufufuliwa!

Tunaweza Kufufuliwa!

TUKIFA, je, Mungu angependa kutufufua, yaani, kuturudisha hai tena?— Ayubu yule mtu mwema aliamini kwamba Mungu angependa kutufufua. Kwa hiyo, Ayubu alipoona anakaribia kufa, alimwambia Mungu hivi: ‘Utaita, na mimi mwenyewe nitakujibu.’ Ayubu alisema kwamba Yehova Mungu angetamani sana kumfufua.—Ayubu 14:14, 15.

Yesu ni kama Baba yake, Yehova Mungu. Yesu anataka kutusaidia. Mtu mwenye ukoma alipomwambia, “Ikiwa tu unataka, unaweza kunitakasa,” Yesu alijibu: “Ninataka.” Naye akamponya mtu huyo ukoma wake.—Marko 1:40-42.

Yehova alionyeshaje kwamba anapenda watoto wadogo?

Yesu alijifunza kutoka kwa Baba yake kuwapenda watoto. Mara mbili hapo zamani, Yehova aliwatumia watumishi wake kuwafufua watoto wadogo. Eliya alimsihi Yehova amfufue mwana wa mwanamke mmoja aliyekuwa amemkaribisha Eliya. Naye Yehova akamfufua. Yehova pia alimtumia mtumishi wake Elisha kumfufua mvulana mdogo.—1 Wafalme 17:17-24; 2 Wafalme 4:32-37.

Je, haifurahishi kujua kwamba Yehova anatupenda sana?— Yeye hatufikirii tu tunapokuwa hai. Iwapo tutakufa atatukumbuka. Yesu alisema kwamba Baba yake hata anawaona watu anaowapenda kuwa hai hata kama tayari wamekufa! (Luka 20:38) Biblia inasema kwamba ‘wala kifo wala uzima wala mambo yaliyo hapa sasa wala mambo yatakayokuja hayataweza kututenga na upendo wa Mungu.’—Waroma 8:38, 39.

Yesu alipokuwa duniani, alionyesha kwamba Yehova anawajali watoto wadogo. Kumbuka kwamba Yesu alitumia wakati kuzungumza na watoto kumhusu Mungu. Lakini, je, unajua kwamba Mungu alimpa Yesu nguvu za kufufua watoto?— Na tuzungumze kuhusu wakati Yesu alipomfufua binti mwenye umri wa miaka 12 wa mtu aitwaye Yairo.

Yairo aliishi na mke wake na binti yao mmoja tu karibu na Bahari ya Galilaya. Siku moja huyo binti mdogo akawa mgonjwa sana, na Yairo akatambua kwamba atakufa. Akaanza kumfikiria Yesu, yule mtu mzuri sana ambaye Yairo alisikia habari zake kwamba ana uwezo wa kuwaponya watu. Basi Yairo akaenda kumtafuta. Akampata Yesu akiwafundisha watu wengi ufuoni mwa Bahari ya Galilaya.

Yairo anapita katikati ya umati na kumpigia Yesu magoti. Anamwambia Yesu hivi: ‘Binti yangu mdogo ni mgonjwa sana. Njoo tafadhali umsaidie? Nakusihi uje.’ Mara moja Yesu akaenda na Yairo. Umati uliokuja kumwona Mwalimu Mkuu unamfuata pia. Lakini baada ya kwenda umbali fulani, watu fulani kutoka kwa Yairo wanakuja na kumwambia: ‘Binti yako amekufa! Usimsumbue mwalimu.’

Yesu akawasikia watu hao wakisema hivyo. Anajua jinsi Yairo anavyohuzunika kuhusu kifo cha mtoto wake wa pekee. Basi Yesu anamwambia: ‘Usiogope. Uwe tu na imani katika Mungu, na binti yako atakuwa mzima.’ Wanaendelea kwenda mpaka kwa Yairo. Rafiki zao wanalia. Wanahuzunika kwa sababu rafiki yao mchanga amekufa. Lakini Yesu anawaambia: ‘Acheni kulia. Mtoto huyu hakufa, bali amelala usingizi.’

Yesu anaposema maneno hayo, watu wanaanza kucheka, kwani wanajua kwamba msichana huyo amekufa. Basi, unafikiri ni kwa nini Yesu anasema kwamba amelala usingizi?— Unafikiri anataka kuwafunza watu somo gani?— Anataka wajue kwamba kifo kinaweza kuwa kama usingizi mzito. Anataka kuwafundisha kwamba kupitia nguvu za Mungu, anaweza kumfufua mtu aliyekufa kwa njia rahisi sana kama vile tunavyoweza kumwamsha mtu kutoka usingizini.

Hatua ya Yesu ya kumfufua binti ya Yairo inatufundisha nini?

Yesu anawaambia watu wote watoke nje ila mitume wake Petro, Yakobo, na Yohana na baba na mama ya msichana huyo. Kisha anaingia ndani alimo huyo mtoto. Anamshika kwa mkono wake na kusema: “Msichana, inuka!” Na mara moja akainuka na kuanza kutembea! Baba yake na mama yake wanajawa na shangwe wee!—Marko 5:21-24, 35-43; Luka 8:40-42, 49-56.

Hebu fikiria jambo hili. Ikiwa Yesu aliweza kumfufua msichana huyo mdogo, je, anaweza kuwafufua wengine pia?— Unafikiri kweli atafanya hivyo?— Ndiyo, atawafufua. Yesu mwenyewe alisema: “Saa inakuja ambayo wale wote waliomo ndani ya makaburi ya ukumbusho wataisikia sauti [yangu] na kutoka.”—Yohana 5:28, 29.

Unafikiri Yesu anataka kuwafufua watu?— Mfano mwingine katika Biblia unasaidia kujibu swali hilo. Jambo fulani lililotokea siku moja karibu na jiji la Naini linaonyesha jinsi Yesu anavyohisi kuhusu watu wanaoomboleza wakati wa mazishi.

Mwanamke mmoja yuko katika msafara wa mazishi ya mwana wake katika umati unaoondoka Naini. Mume wake alikuwa tayari amekufa, na sasa mwana wake wa pekee amekufa. Amehuzunika sana! Watu wengi wa Naini wanaambatana naye mwili wa mwana wake unapopelekwa nje ya jiji. Mwanamke huyo anaomboleza na hakuna mtu anayeweza kumtuliza.

Ikatukia kwamba siku hiyo Yesu na wanafunzi wake nao walikuwa wakielekea jiji la Naini. Wakiwa karibu na lango la jiji, wanakutana na umati ukienda kumzika mwana wa yule mwanamke. Yesu anapomwona huyo mwanamke anayeomboleza, anamhurumia. Moyo wake unaguswa anapoona huzuni kubwa aliyo nayo mwanamke huyo. Anataka kumsaidia.

Yesu akamwambia hivi kwa huruma na kwa uthabiti ili mwanamke huyo amsikilize: “Acha kulia.” Namna alivyozungumza na kutenda kunafanya watu wote wamtazame kwa shauku. Yesu anapoukaribia mwili huo, ni lazima watu wote wanashangaa kuhusu kile atakachofanya. Yesu anaamuru hivi: “Kijana, ninakuambia, Inuka!” Mara moja anaketi! Anaanza kuzungumza.—Luka 7:11-17.

Hebu wazia jinsi mwanamke huyo alivyohisi! Unaweza kuhisije kumpokea tena mpendwa aliyekufa?— Je, hiyo haionyeshi kwamba Yesu kwa kweli anawapenda watu na anataka kuwasaidia?— Hebu wazia jinsi itakavyopendeza katika ulimwengu mpya wa Mungu kuwakaribisha watakaofufuliwa!—2 Petro 3:13; Ufunuo 21:3, 4.

Ufufuo wa mtoto wa pekee wa mwanamke huyu unaonyesha nini?

Wakati huo baadhi ya watu watakaofufuliwa watakuwa watu tuliowajua hapo awali, kutia ndani watoto. Tutawajua kama vile tu Yairo alivyomjua binti yake alipofufuliwa na Yesu. Wengine watakuwa watu waliokufa mamia au maelfu ya miaka iliyopita. Lakini Mungu hatawasahau hata kama waliishi zamani sana.

Je, haipendezi kujua kwamba Yehova Mungu na Mwana wake Yesu wanatupenda sana?— Wanataka tuishi, si kwa miaka michache tu, bali milele!

Kuhusu tumaini ajabu la Biblia kuhusu wafu, tafadhali soma Isaya 25:8; Matendo 24:15; na 1 Wakorintho 15:20-22.