Hamia kwenye habari

Hamia kwenye yaliyomo

SURA YA 36

Ni Nani Watakaofufuliwa? Nao Wataishi Wapi?

Ni Nani Watakaofufuliwa? Nao Wataishi Wapi?

KATIKA sura mbili zilizotangulia, tulisoma kuhusu watu wangapi waliofufuliwa?— Watano. Ni wangapi waliokuwa watoto?— Watatu. Na wa nne anaitwa kijana. Unafikiri hiyo inamaanisha nini?—

Inamaanisha kwamba Mungu anawapenda watoto na vijana. Lakini atawafufua watu wengine pia. Je, Mungu atawafufua watu waliofanya mema tu?— Tunaweza kufikiria hivyo. Lakini, watu wengi hawakujifunza ukweli kumhusu Yehova Mungu na Mwana wake. Kwa hiyo walifanya mabaya kwa sababu walifundishwa mambo yasiyo ya kweli. Unafikiri Yehova atawafufua watu kama hao?—

Biblia inasema: “Kutakuwa na ufufuo wa waadilifu na wasio waadilifu pia.” (Matendo 24:15) Kwa nini wale ambao hawakuwa waadilifu, au wale ambao hawakufanya mema, wafufuliwe?— Wao watafufuliwa kwa sababu hawakupata nafasi kamwe ya kujifunza kumhusu Yehova na yale anayotaka watu wafanye.

Kwa nini Mungu atafufua watu wengine ambao hawakufanya mema?

Unafikiri watu watafufuliwa lini?— Fikiria wakati Lazaro alipokufa na ahadi ambayo Yesu alimpa Martha dada yake: “Ndugu yako atafufuka.” Martha akajibu: “Ninajua atafufuka katika ufufuo siku ya mwisho.” (Yohana 11:23, 24) Martha alimaanisha nini aliposema Lazaro atafufuka katika “siku ya mwisho”?—

Paradiso ambayo Yesu anamwambia mtu huyu iko wapi?

Martha alikuwa amesikia ahadi hii ya Yesu: ‘Wale wote waliomo ndani ya makaburi ya ukumbusho watatoka.’ (Yohana 5:28, 29) Kwa hiyo “siku ya mwisho” ni wakati wale wote walio katika kumbukumbu la Mungu watakapofufuliwa. Siku hiyo ya mwisho si siku yenye muda wa saa 24. Itakuwa kipindi cha miaka elfu moja. Biblia inasema kwamba katika siku hiyo ‘Mungu atawahukumu watu wa dunia.’ Watakaohukumiwa watatia ndani wale watakaofufuliwa.—Matendo 17:31; 2 Petro 3:8.

Hebu wazia jinsi itakavyokuwa siku yenye furaha ajabu! Wakati wa kipindi cha hiyo siku ya miaka elfu moja, mamilioni ya watu waliokufa watafufuliwa. Yesu anapaita mahali ambapo watu hao wataishi kuwa Paradiso. Na tuone Paradiso itakuwa wapi na jinsi hali itakavyokuwa.

Karibu saa tatu kabla ya Yesu kufa katika mti wa mateso, anamwambia mtu aliye kwenye mti wa mateso karibu naye kuhusu Paradiso. Mtu huyo anauawa kwa sababu ya uhalifu aliofanya. Lakini mhalifu huyu anapomwona Yesu na kusikia yanayosemwa juu Yake, anaanza kumwamini Yesu. Basi mhalifu huyo anasema: “Unikumbuke utakapoingia katika ufalme wako.” Yesu anamjibu: “Kwa kweli mimi nakuambia leo, Utakuwa pamoja nami katika Paradiso.”—Luka 23:42, 43.

Tunaposoma kuhusu Paradiso, tunapaswa kuona nini akilini?

Yesu anamaanisha nini anaposema hivyo? Paradiso iko wapi?— Hebu fikiria. Kwanza kabisa hii Paradiso ilikuwa wapi?— Kumbuka kwamba Mungu aliwapa watu wa kwanza, Adamu na mke wake, paradiso papa hapa duniani ili waishi ndani yake. Iliitwa bustani ya Edeni. Kulikuwa na wanyama katika bustani hiyo, lakini hawakuwa hatari. Kulikuwa na miti yenye matunda mengi matamu, na vilevile mto mkubwa. Palikuwa mahali pazuri ajabu pa kuishi!—Mwanzo 2:8-10.

Tunaposoma kwamba mhalifu huyo atakuwa katika Paradiso, tunapaswa kuona akilini dunia hii ikiwa mahali maridadi pa kuishi. Je, Yesu atakuwa katika Paradiso hapa duniani pamoja na huyo mtu ambaye zamani alikuwa mhalifu?— La. Je, unajua ni kwa nini hatakuwa duniani?—

Ni kwa sababu Yesu atakuwa mbinguni akitawala akiwa Mfalme juu ya dunia Paradiso. Kwa hiyo, Yesu atakuwa pamoja na mtu huyo katika maana ya kwamba Yesu atamfufua na kumtimizia mahitaji yake. Lakini kwa nini Yesu atamruhusu mtu aliyekuwa mhalifu aishi katika Paradiso?— Hebu tuone jibu.

Kabla ya mhalifu huyo kuzungumza na Yesu, je, alijua makusudi ya Mungu?— La. Alifanya mabaya kwa sababu hakujua kweli kumhusu Mungu. Akiwa katika Paradiso atafundishwa makusudi ya Mungu. Kisha atapata nafasi ya kuthibitisha kwamba kwa kweli anampenda Mungu kwa kufanya mapenzi Yake.

Je, kila mtu atakayefufuliwa ataishi katika dunia Paradiso?— La. Unajua ni kwa nini?— Kwa sababu wengine watafufuliwa wakaishi na Yesu mbinguni. Watatawala na yeye juu ya dunia Paradiso wakiwa wafalme. Tunajuaje jambo hilo? Hebu tuone.

Usiku kabla ya kifo chake, Yesu aliwaambia mitume wake hivi: ‘Katika nyumba ya Baba yangu mbinguni, mna makao mengi, nami naenda kuwatayarishia ninyi mahali.’ Kisha Yesu anawaahidi: “Nitakuja tena nami nitawapokea ninyi nyumbani kwangu mwenyewe, ili mahali nilipo mimi, ninyi pia muwe hapo.”—Yohana 14:2, 3.

Yesu anaenda wapi baada ya kufufuliwa?— Anarudi mbinguni kuwa na Baba yake. (Yohana 17:4, 5) Kwa hiyo Yesu anawaahidi mitume wake na wanafunzi wengine kwamba atawafufua ili wawe pamoja naye mbinguni. Watafanya nini pamoja na Yesu huko?— Biblia inasema kwamba wanafunzi wake ambao watafufuliwa katika “ufufuo wa kwanza” wataishi mbinguni na watatawala juu ya dunia “wakiwa wafalme pamoja naye ile miaka elfu.”—Ufunuo 5:10; 20:6; 2 Timotheo 2:12.

Ni wangapi watakaofufuliwa katika “ufufuo wa kwanza” na watawale pamoja na Yesu wakiwa wafalme?— Yesu aliwaambia wanafunzi wake: “Msiogope, kundi dogo, kwa sababu Baba yenu amekubali kuwapa ninyi ufalme.” (Luka 12:32) Kuna idadi hususa ya “kundi dogo” wanaofufuliwa ili kuwa na Yesu katika Ufalme wa mbinguni. Biblia inaonyesha kwamba watu “144,000” wanafufuliwa kutoka duniani.—Ufunuo 14:1, 3.

Watakaofufuliwa wataishi wapi, nao watafanya nini?

Ni wangapi watakaoishi katika dunia Paradiso?— Biblia haisemi. Lakini Mungu aliwaambia Adamu na Hawa walipokuwa katika bustani ya Edeni wazae watoto na kuijaza dunia. Wakakosa kufanya hivyo. Lakini Mungu atahakikisha kwamba kusudi lake la kuijaza dunia watu waadilifu linatimizwa.—Mwanzo 1:28; Isaya 45:18; 55:11.

Hebu wazia tu jinsi itakavyopendeza kuishi katika Paradiso! Dunia yote itakuwa kama bustani. Itakuwa na ndege na wanyama na miti na maua maridadi ya kila aina. Hakuna mtu atakayekuwa na maumivu kwa sababu ya ugonjwa wala hakuna mtu atakayekufa. Watu wote watakuwa marafiki. Ikiwa tunataka kuishi milele katika Paradiso, basi tujitayarishe wakati huu.

Soma habari zaidi kuhusu kusudi la Mungu kwa dunia katika Mithali 2:21, 22; Mhubiri 1:4; Isaya 2:4; 11:6-9; 35:5, 6; na 65:21-24.