Hamia kwenye habari

Hamia kwenye yaliyomo

SURA YA 38

Kwa Nini Tumpende Yesu?

Kwa Nini Tumpende Yesu?

WAZIA umo ndani ya mashua inayozama. Je, ungefurahi kuokolewa?— Vipi ikiwa mtu fulani anatoa uhai wake ili akuokoe?— Hivyo ndivyo Yesu Kristo alivyofanya. Kama tulivyojifunza katika Sura ya 37, alitoa uhai wake kuwa fidia ili tuokolewe.

Hatumaanishi kwamba Yesu anatuokoa tusizame. Basi, anatuokoa kutokana na nini? Je unakumbuka?— Anatuokoa kutokana na dhambi na kifo ambazo sisi sote tulirithi kutoka kwa Adamu. Hata kama watu wengine wamefanya mambo mabaya sana, Yesu alikufa kwa ajili yao pia. Je, unaweza kuhatarisha uhai wako ili kuokoa watu kama hao?—

Biblia inasema: “Kwa maana ni vigumu kwa yeyote kufa kwa ajili ya mtu mwadilifu; kwa kweli, labda, mtu anaweza kuthubutu kufa kwa ajili ya mtu mwema.” Hata hivyo Biblia inaeleza kwamba Yesu ‘alikufa kwa ajili ya watu wasiomwogopa Mungu.’ Hao wanatia ndani watu ambao hata hawamtumikii Mungu! Biblia inaendelea kusema: “Tulipokuwa tungali watenda-dhambi [tukiwa bado tunafanya mabaya], Kristo alikufa kwa ajili yetu.”—Waroma 5:6-8.

Je, unajua mtume yeyote ambaye hapo awali alifanya mambo mabaya sana?— Mtume huyo aliandika: “Kristo Yesu alikuja ulimwenguni ili kuwaokoa watenda-dhambi. Kati ya hao mimi ni wa kwanza kabisa.” Mtume aliyesema mambo hayo ni Paulo. Alisema kwamba wakati mmoja alikuwa ‘asiye na akili’ na kwamba alikuwa ameishi “katika ubaya.”—1 Timotheo 1:15; Tito 3:3.

Hebu wazia upendo wa Mungu wa kumtuma Mwana wake kuja kufa kwa ajili ya watu kama hao! Hebu chukua Biblia yako na usome habari hii kwenye Yohana sura ya 3, mstari wa 16. Mstari huo unasema: “Mungu aliupenda ulimwengu [yaani, watu wanaoishi duniani] sana hivi kwamba akamtoa Mwana wake mzaliwa-pekee, ili kila mtu anayemwamini asiangamizwe bali awe na uzima wa milele.”

Yesu alipata mateso gani alipotoa uhai wake kwa ajili yetu?

Yesu alithibitisha kwamba anatupenda kama vile Baba yake anavyotupenda. Labda unakumbuka tulisoma katika Sura ya 30 ya kitabu hiki baadhi ya mateso yaliyompata Yesu usiku ule aliokamatwa. Alipelekwa nyumbani kwa Kayafa, Kuhani Mkuu ili afanyiwe kesi. Mashahidi bandia waliletwa wakasema uwongo kumhusu Yesu, na watu wakampiga ngumi. Huo ndio wakati Petro alimkana Yesu. Hebu tuwazie tuko huko sasa na tunaona mambo mengine yanayotendeka.

Ni asubuhi sasa. Yesu amekesha usiku wote. Kwa sababu mashtaka ya usiku hayakuwa halali kisheria, makuhani wanaita haraka Sanhedrini, au mahakama kuu ya Kiyahudi, ili wafanye kesi nyingine. Tena wanamshtaki Yesu kwamba ametenda uhalifu dhidi ya Mungu.

Kisha makuhani wanamfunga Yesu na kumpeleka kwa Pilato, gavana Mroma. Wanamwambia Pilato: ‘Yesu anapinga serikali. Anapaswa kuuawa.’ Lakini Pilato anaelewa kwamba makuhani wanamdanganya. Basi Pilato anawaambia: ‘Sioni ubaya wowote kwa mtu huyu. Nitamwachilia.’ Lakini makuhani na watu wengine wanapaaza sauti: ‘La! Auawe!’

Baadaye, Pilato anajaribu tena kuwaambia kwamba atamweka Yesu huru. Lakini makuhani wanachochea umati kupiga kelele na kusema hivi: ‘Ukimwachilia, wewe pia unapinga serikali! Auawe!’ Umati unapiga makelele sana. Unajua Pilato anafanya nini?—

Anakubali kufanya kama wanavyotaka. Kwanza anaruhusu Yesu apigwe mijeledi. Kisha anampeleka kwa askari auawe. Wanaweka taji la miiba kwenye kichwa chake na kumwinamia kwa mzaha. Kisha wanampa Yesu mti mkubwa abebe, na wanampeleka nje ya jiji mpaka mahali paitwapo Fuvu la Kichwa. Wakiwa huko wanamtundika Yesu mtini kwa kumpigilia misumari mikononi na miguuni. Kisha wanausimamisha mti huo na kumfanya Yesu aning’inie juu yake. Anatoka damu, na maumivu ni makali wee!

Yesu hafi wakati uo huo. Ananing’inia tu mtini. Wakuu wa makuhani wanamfanyia mzaha. Nao wapita-njia wanasema: “Ikiwa wewe ni mwana wa Mungu, shuka kutoka kwenye mti wa mateso!” Lakini Yesu anajua kile ambacho Baba yake alimtuma kufanya. Anajua kwamba ni lazima atoe uhai wake mkamilifu ili tuweze kupata uzima wa milele. Hatimaye, karibu saa tisa alasiri hiyo, Yesu anamlilia Baba yake kisha anakufa. —Mathayo 26:36–27:50; Marko 15:1; Luka 22:39–23:46; Yohana 18:1–19:30.

Yesu alikuwa tofauti sana na Adamu! Adamu hakumpenda Mungu. Hakumtii Mungu. Wala Adamu hakutupenda sisi. Kwa sababu alifanya dhambi, sisi sote tumezaliwa katika dhambi. Lakini Yesu alionyesha kwamba anampenda Mungu na anatupenda sisi pia. Yeye alimtii Mungu wakati wote. Naye alitoa uhai wake ili atuondolee matatizo ambayo Adamu alituletea.

Tunaweza kufanya nini kuonyesha kwamba tunampenda Yesu?

Je, unathamini tendo hilo la Yesu la ajabu?— Unaposali kwa Mungu, je, wewe humshukuru kwa kutupatia Mwana wake?— Mtume Paulo alithamini kile ambacho Kristo alimfanyia. Paulo aliandika kwamba Mwana wa Mungu ‘alinipenda mimi akajitoa mwenyewe kwa ajili yangu.’ (Wagalatia 2:20) Yesu alikufa kwa ajili yangu na kwa ajili yako pia. Alitoa uhai wake mkamilifu ili tuweze kuishi milele! Kwa hakika, hiyo ni sababu kubwa inayopasa kutufanya tumpende Yesu.

Mtume Paulo aliwaandikia Wakristo katika jiji la Korintho: “Upendo alio nao Kristo hutushurutisha.” Upendo huo wapasa kutushurutisha tufanye nini? Unaonaje?— Ona jibu la Paulo: “Kristo alikufa kwa ajili ya wote ili kwamba waishi kwa ajili yake. Hawapaswi kuishi ili kujifurahisha wenyewe.”—Italiki ni zetu; 2 Wakorintho 5:14, 15, New Life Version.

Ni katika njia gani unaweza kuonyesha kwamba unaishi ili umpendeze Kristo?— Njia moja ni kwa kuwaambia wengine yale ambayo umejifunza kumhusu. Au fikiria hili: Uko peke yako, mama au baba hawawezi kuona kile unachofanya wala hakuna mtu yeyote anayeweza kukuona. Je, utatazama vipindi vya televisheni au kufanya mambo mengine ambayo unajua hayatamfurahisha Yesu?— Kumbuka kwamba sasa Yesu yuko hai, na anaona yote tufanyayo!

Ni nani anayeweza kuona kila kitu tunachofanya?

Sababu nyingine ya kumpenda Yesu ni kwamba tunataka kumwiga Yehova. Yesu alisema, “Baba ananipenda.” Unajua ni kwa nini Mungu anampenda Yesu na kwa nini sisi pia tunapaswa kumpenda?— Kwa sababu Yesu alikuwa tayari kufa ili mapenzi ya Mungu yatendeke. (Yohana 10:17) Kwa hiyo na tufanye yale Biblia inayosema: “Iweni waigaji wa Mungu, kama watoto wapendwa, na endeleeni kutembea katika upendo, kama vile Kristo pia alivyowapenda ninyi na kujitoa mwenyewe kwa ajili yenu.”—Waefeso 5:1, 2.

TIli tumthamini Yesu na yale aliyotufanyia, tafadhali soma Yohana 3:35; 15:9, 10; na 1 Yohana 5:11, 12.