Hamia kwenye habari

Hamia kwenye yaliyomo

SURA YA 41

Watoto Wanaomfurahisha Mungu

Watoto Wanaomfurahisha Mungu

UNAFIKIRI ni mtoto gani duniani aliyemfurahisha Yehova zaidi?— Ni Mwana wake, Yesu. Tuzungumzie mambo ambayo Yesu alifanya ili kumfurahisha Baba yake wa mbinguni.

Yesu na familia yao waliishi umbali wa safari ya siku tatu hivi kutoka Yerusalemu, kulipokuwa lile hekalu maridadi la Yehova. Yesu aliliita hekalu “nyumba ya Baba yangu.” Yeye na familia yao walienda huko kila mwaka kuhudhuria Pasaka.

Mwaka fulani, Yesu alipokuwa na umri wa miaka 12, familia yao ilianza safari ya kurudi nyumbani baada ya sherehe za Pasaka. Hawakutambua kwamba Yesu hayuko miongoni mwa watu wao wa ukoo na rafiki zao hadi waliposimama mahali ambapo wangelala usiku. Bila kupoteza wakati Maria na Yosefu wakarudi Yerusalemu kumtafuta. Unafikiri Yesu alikuwa wapi?—

Walimpata Yesu hekaluni. Alikuwa akiwasikiliza walimu na kuwauliza maswali. Nao walipomwuliza swali, alijibu. Walishangazwa na majibu yake mazuri. Unaelewa ni kwa nini Mungu alipendezwa na Mwana wake?—

Hatimaye Maria na Yosefu walitulia walipompata Yesu. Lakini Yesu hakuwa na wasiwasi. Alijua kwamba hekaluni ni mahali salama na panapofaa kuwa. Akawauliza: “Je! hamkujua kwamba ni lazima niwe katika nyumba ya Baba yangu?” Alijua kwamba hekalu ni nyumba ya Mungu, naye alipenda kuwa huko.

Baada ya hayo, Maria na Yosefu wakarudi nyumbani Nazareti wakiwa na Yesu mwenye umri wa miaka 12. Unafikiri Yesu aliwatendeaje wazazi wake?— Biblia inasema kwamba aliendelea “kujitiisha kwao.” Unafikiri hiyo inamaanisha nini?— Inamaanisha kwamba aliwatii. Ndiyo, alifanya kile wazazi wake walimwambia afanye, hata kama ilimaanisha kuteka maji kisimani.—Luka 2:41-52.

Yesu akiwa mtoto alimfurahishaje Mungu?

Basi fikiria hili: Ijapokuwa Yesu alikuwa mkamilifu, aliwatii wazazi wake wasio wakamilifu. Je, hilo lilimfurahisha Mungu?— Bila shaka, kwani Neno la Mungu linawaambia watoto: “Watiini wazazi wenu.” (Waefeso 6:1) Wewe pia utamfurahisha Mungu ukiwatii wazazi wako kama Yesu.

Njia nyingine ya kumfurahisha Mungu ni kwa kuwaambia wengine juu yake. Huenda watu wengine wakasema kwamba haifai vijana kufanya hivyo. Lakini watu walipojaribu kuwanyamazisha wavulana kufanya hivyo, Yesu alisema: ‘Hamkusoma katika Maandiko, “Kutoka katika kinywa cha watoto Mungu atatoa sifa”?’ (Mathayo 21:16) Kwa hiyo sote tunaweza kuwaambia wengine juu ya Yehova na jinsi alivyo Mungu mzuri, iwapo kwa kweli tunataka. Na kama tutafanya hivyo, tutamfurahisha Mungu.

Tunajifunza wapi mambo kumhusu Mungu ili tuwaambie wengine?— Tunapojifunza Biblia nyumbani. Lakini tunajifunza mengi mahali watu wa Mungu wanapokutana ili kujifunza. Lakini tutawajuaje watu wa Mungu?—

Watu hufanya nini katika mikutano yao? Je, kweli wao hufundisha yaliyo katika Biblia? Wao huisoma na kuizungumzia? Hivyo ndivyo tunavyomsikiliza Mungu, sivyo?— Tukiwa kwenye mikutano ya Kikristo tunatazamia kusikia yale ambayo Mungu anasema, sivyo?— Lakini vipi watu wakisema kwamba si lazima uishi kulingana na yale ambayo Biblia inasema? Je, utasema kwamba hao ni watu wa Mungu?—

Tufikirie jambo hili. Biblia inasema kwamba watu wa Mungu wangekuwa “watu kwa ajili ya jina lake.” (Matendo 15:14) Kwa sababu jina la Mungu ni Yehova, tunaweza kuwauliza watu kama Yehova ndiye Mungu wao. Wakisema la, basi tutajua kwamba wao si watu wake. Watu wa Mungu huwaambia wengine kuhusu Ufalme wa Mungu pia. Nao wanaonyesha upendo wao kwa Mungu kwa kutii amri zake.—1 Yohana 5:3.

Iwapo unawajua watu wanaofanya mambo yote hayo, jiunge nao ili kumwabudu Mungu. Usikilize kwa makini kwenye mikutano hiyo kisha utoe majibu maswali yanapoulizwa. Ndivyo Yesu alivyofanya alipokuwa katika nyumba ya Mungu. Nawe ukifanya mambo hayo, utamfurahisha Mungu kama vile Yesu alivyomfurahisha.

Unaweza kuwafikiria watoto wengine wanaotajwa katika Biblia ambao walimfurahisha Mungu?— Timotheo ni mfano bora. Baba yake hakuwa mwabudu wa Yehova. Lakini mama yake Eunike, na nyanya yake Loisi walimwamini Yehova. Timotheo aliwasikiliza na akajifunza kumhusu Yehova.

Timotheo alitaka kufanya nini ijapokuwa baba yake hakuwa mwabudu wa Yehova?

Timotheo alipokuwa mtu mzima, mtume Paulo alitembelea mji wao. Akatambua kwamba Timotheo anataka sana kumtumikia Yehova. Basi akamwalika Timotheo aambatane naye ili afanye zaidi katika utumishi wake kwa Mungu. Kila walikokwenda waliwaambia watu kuhusu Ufalme wa Mungu na kuhusu Yesu.—Matendo 16:1-5; 2 Timotheo 1:5; 3:14, 15.

Lakini, je, ni mifano tu ya wavulana wadogo waliomfurahisha Mungu tunayopata katika Biblia?— La. Mfikirie msichana mdogo Mwisraeli aliyemfurahisha Mungu. Alipokuwa hai, mataifa ya Siria na Israeli yalikuwa maadui. Siku moja Wasiria walipigana na Israeli wakamchukua msichana huyo mateka. Wakampeleka nyumbani kwa jemadari fulani aliyeitwa Naamani. Akawa kijakazi wa mke wa Naamani.

Naamani alikuwa na ugonjwa unaoitwa ukoma. Hakuna daktari aliyeweza kumponya. Lakini msichana huyo mdogo aliamini kwamba nabii fulani, mtumishi wa pekee wa Mungu, angeweza kumsaidia Naamani. Naamani na mke wake hawakuwa kamwe waabudu wa Yehova. Je, msichana huyo awaambie alichojua? Wewe ungalifanya nini?—

Msichana Mwisraeli alimfurahishaje Mungu?

Basi, msichana mdogo akasema: ‘Kama tu Naamani angeenda kwa nabii wa Yehova huko Israeli, angeponywa ukoma wake.’ Naamani akamsikiliza msichana huyo, akaenda kwa nabii wa Yehova. Alipofanya alivyoambiwa na nabii, alipona. Hiyo ikamfanya Naamani kuwa mwabudu wa Mungu wa kweli.—2 Wafalme 5:1-15.

Je, ungependa kumsaidia mtu kujifunza kumhusu Yehova na kuhusu yale awezayo kufanya, kama alivyofanya msichana yule mdogo?— Unaweza kumsaidia nani?— Labda mwanzoni hawatakubali kwamba wanahitaji msaada. Lakini unaweza kuwaambia mambo mazuri ambayo Yehova hufanya. Na huenda wakasikiliza. Kwa hakika hilo litamfurahisha Mungu.

Mambo yenye kutia moyo vijana wafurahie zaidi utumishi wa Mungu yanaweza kupatikana katika Zaburi 122:1 (121:1, “Dy”); 148:12, 13; Mhubiri 12:1; 1 Timotheo 4:12; na Waebrania 10:23-25.