Hamia kwenye habari

Hamia kwenye yaliyomo

SURA YA 43

Ndugu Zetu na Dada Zetu Ni Akina Nani?

Ndugu Zetu na Dada Zetu Ni Akina Nani?

WAKATI mmoja Mwalimu Mkuu aliuliza swali la kushangaza. “Mama yangu ni nani, na ndugu zangu ni nani?” (Mathayo 12:48) Unaweza kujibu swali hilo?— Labda unajua kwamba mama ya Yesu alikuwa Maria. Unajua majina ya ndugu zake?— Je, alikuwa na dada pia?—

Biblia inasema kwamba ndugu za Yesu walikuwa “Yakobo na Yosefu na Simoni na Yuda.” Yesu alikuwa na dada pia alipohubiri duniani. Kwa kuwa Yesu alikuwa mzaliwa wa kwanza, hao wote walikuwa wadogo wake.—Mathayo 13:55, 56; Luka 1:34, 35.

Je, ndugu za Yesu walikuwa wanafunzi wake pia?— Biblia inasema kwamba mwanzoni ‘hawakumwamini.’ (Yohana 7:5) Hata hivyo, baadaye Yakobo na Yuda wakawa wanafunzi wake, na hata wakaandika vitabu vya Biblia. Unavijua vitabu ambavyo waliandika?— Ndiyo, ni barua ya Yakobo na ya Yuda.

Tunajua kwamba Yesu alikuwa angalau na dada wawili ijapokuwa hawatajwi katika Biblia. Lakini huenda walikuwa zaidi. Je, dada zake walikuwa wafuasi wake?— Biblia haisemi, kwa hiyo hatujui. Lakini unajua ni kwa nini Yesu aliuliza, “Mama yangu ni nani, na ndugu zangu ni nani?”— Hebu tuone.

Yesu alikuwa anawafundisha wanafunzi wake wakati mtu mmoja alipomkatiza na kumwambia: “Mama yako na ndugu zako wamesimama nje, wakitaka kusema nawe.” Yesu akatumia pindi hiyo kufundisha somo muhimu kwa kuuliza swali hili la kushangaza: “Mama yangu ni nani, na ndugu zangu ni nani?” Akinyosha mkono wake kuelekea wanafunzi wake, akasema: “Tazama! Mama yangu na ndugu zangu!”

Kisha Yesu akafafanua: “Yeyote yule anayefanya mapenzi ya Baba yangu aliye mbinguni, huyo ndiye ndugu yangu, na dada yangu, na mama yangu.” (Mathayo 12:47-50) Hiyo inaonyesha jinsi Yesu alivyokuwa na uhusiano wa karibu na wanafunzi wake. Anatufundisha kwamba aliwaona wanafunzi wake kama ndugu, dada, na mama wa kweli.

Yesu alisema kwamba ndugu na dada zake ni akina nani?

Wakati huo ndugu za Yesu mwenyewe—Yakobo, Yosefu, Simoni, na Yuda—hawakuamini kwamba Yesu ni Mwana wa Mungu. Inaelekea hawakuamini yale ambayo malaika Gabrieli alimwambia mama yao. (Luka 1:30-33) Hivyo, huenda hawakumtendea Yesu kwa fadhili. Yeyote anayefanya hivyo si ndugu au dada wa kweli. Unajua yeyote ambaye hamtendei ndugu yake au dada yake kwa fadhili?—

Biblia inasimulia kuhusu Esau na Yakobo na jinsi Esau alivyokasirika sana na kusema: “Nitamuua Yakobo ndugu yangu.” Mama yao, Rebeka, aliogopa sana hivi kwamba akamwagiza Yakobo aende mahali pengine ili asiuawe na Esau. (Mwanzo 27:41-46) Lakini, miaka mingi baadaye Esau alibadilika, akamkumbatia na kumbusu Yakobo.—Mwanzo 33:4.

Baadaye, Yakobo akawa na wana 12. Lakini wana wakubwa wa Yakobo hawakumpenda Yosefu ndugu yao mdogo. Walimwonea wivu kwa sababu alipendwa sana na baba yao. Basi wakamwuza kwa watu waliofanya biashara ya watumwa waliokuwa wakielekea Misri. Kisha wakamwambia baba yao kwamba Yosefu ameuawa na mnyama wa mwitu. (Mwanzo 37:23-36) Hilo lilikuwa jambo baya sana, sivyo?—

Baadaye, ndugu zake Yosefu waliomba msamaha. Yosefu akawasamehe. Umeona jinsi Yosefu alivyokuwa kama Yesu?— Mitume wa Yesu mwenyewe walimtoroka alipopata shida, na hata Petro akamkana. Hata hivyo, kama Yosefu alivyofanya, Yesu aliwasamehe wote.

Tunapaswa kujifunza somo gani kutokana na yale Kaini alimtendea Abeli?

Kisha kuna wale ndugu wawili Kaini na Abeli. Tunaweza kujifunza kutoka kwao pia. Mungu aliona kwamba Kaini hampendi ndugu yake kikweli. Basi Mungu akamwambia Kaini abadili maoni yake. Kama Kaini angalimpenda Mungu kikweli, angalimtii. Lakini hakumpenda Mungu. Siku moja Kaini alimwambia Abeli: “Twende shambani.” Abeli akakubali kwenda na Kaini. Wakiwa peke yao kule nje, Kaini alimpiga ndugu yake kwa nguvu na kumwua.—Mwanzo 4:2-8.

Biblia inatuambia kwamba tunapaswa kujifunza somo la pekee kutokana na habari hiyo. Somo gani?— “Huu ndio ujumbe ambao mmesikia tangu mwanzo, kwamba tunapaswa kupendana; si kama Kaini, aliyetokana na yule mwovu.” Kwa hiyo ndugu na dada wanapaswa kupendana. Hawapaswi kuwa kama Kaini.—1 Yohana 3:11, 12.

Kwa nini tusiwe kama Kaini?— Kwa sababu Biblia inasema kwamba ‘alitokana na yule mwovu,’ Shetani Ibilisi. Kwa sababu Kaini alitenda kama Ibilisi, ni kama tu Ibilisi alikuwa baba yake.

Unaona faida ya kuwapenda ndugu na dada zako?— Usipowapenda, unaiga watoto wa nani?— Watoto wa Ibilisi. Hungependa kuwa mtoto wa Ibilisi, sivyo?— Basi utaonyeshaje kwamba unataka kuwa mtoto wa Mungu?— Ni kwa kuwapenda ndugu na dada zako kikweli.

Lakini upendo ni nini?— Upendo ni hisia ya moyoni inayotusukuma tutake kuwatendea watu wengine mema. Tunaonyesha kwamba tunawapenda wengine tunapokuwa na shauku nao na tunapowatendea mema. Ni nani walio ndugu na dada zetu tunaopaswa kuwapenda?— Kumbuka, Yesu alisema kwamba ni wale walio katika familia yetu kubwa ya Kikristo.

Unaweza kuonyeshaje kwamba unampenda ndugu yako?

Kuna faida gani kuwapenda ndugu na dada hao Wakristo?— Biblia inasema: “Yeye ambaye hampendi ndugu yake [au dada yake], ambaye amemwona, hawezi kuwa anampenda Mungu, ambaye hajamwona.” (1 Yohana 4:20) Kwa hiyo hatuwezi kuwapenda wachache tu miongoni mwa ndugu zetu na dada zetu wa Kikristo. Ni lazima tuwapende wote. Yesu alisema: “Kwa jambo hili wote watajua kwamba ninyi ni wanafunzi wangu, mkiwa na upendo kati yenu wenyewe.” (Yohana 13:35) Je, unawapenda ndugu na dada wote?— Kumbuka kwamba kama huwapendi, kwa hakika humpendi Mungu.

Tunaweza kuonyeshaje kwamba kwa kweli tunawapenda ndugu na dada zetu?— Iwapo tunawapenda, hatutajaribu kuwaepuka eti kwa sababu hatutaki kuzungumza nao. Tunapaswa kuwa wenye urafiki kwa wote. Kila wakati tutawatendea mema na kuwa tayari kuwasaidia. Na wakipata matatizo, tutawasaidia kwani sisi kwa hakika ni familia moja kubwa.

Tunapowapenda ndugu na dada zetu wote kabisa, hiyo inathibitisha nini?— Kwamba sisi ni wanafunzi wa Yesu, Mwalimu Mkuu. Hivyo ndivyo tunavyotaka, sivyo?—

Maandiko mengine yanayozungumzia kuwapenda ndugu na dada zetu ni Wagalatia 6:10 na 1 Yohana 4:8, 21. Hebu fungua Biblia yako na uyasome.