Hamia kwenye habari

Hamia kwenye yaliyomo

SURA YA 44

Rafiki Zetu Wanapaswa Kuwa Watu Wanaompenda Mungu

Rafiki Zetu Wanapaswa Kuwa Watu Wanaompenda Mungu

RAFIKI ni watu tunaopenda kuzungumza nao na kushirikiana nao. Lakini ni muhimu kuwa na rafiki wanaofaa. Unafikiri ni nani aliye rafiki yetu mkubwa zaidi?— Ndiyo, ni Yehova Mungu.

Kweli tunaweza kuwa rafiki za Mungu?— Biblia inasema kwamba Abrahamu ambaye aliishi zamani alikuwa “rafiki ya Yehova.” (Yakobo 2:23) Unajua ni kwa nini alikuwa rafiki ya Yehova?— Biblia inasema kwamba Abrahamu alimtii Mungu. Alitii hata alipoambiwa afanye jambo gumu. Kwa hiyo ili tuwe rafiki za Yehova ni lazima tufanye mambo yanayompendeza, kama Abrahamu alivyofanya na kama vile Mwalimu Mkuu amekuwa akifanya wakati wote.—Mwanzo 22:1-14; Yohana 8:28, 29; Waebrania 11:8, 17-19.

Kwa nini Abrahamu alikuwa “rafiki ya Yehova”?

Yesu aliwaambia mitume wake: “Ninyi ni rafiki zangu ikiwa mnafanya ninalowaamuru.” (Yohana 15:14) Kwa kuwa mambo yote ambayo Yesu aliwaambia watu yalitoka kwa Yehova, Yesu alimaanisha kwamba rafiki zake ni watu wanaofanya yale ambayo Mungu anataka. Kwa kweli watu wote waliokuwa rafiki za Yesu walimpenda Mungu.

Baadhi ya rafiki wa karibu sana wa Mwalimu Mkuu walikuwa mitume wake, na unaweza kuona picha yao kwenye ukurasa wa 75 wa kitabu hiki. Walisafiri naye na wakamsaidia kuhubiri. Yesu alitumia muda mwingi na mitume wake. Walikuwa wakila pamoja, wakizungumza pamoja kumhusu Mungu, na kufanya mambo mengine pamoja. Lakini Yesu alikuwa na rafiki wengine wengi. Mara nyingi alifurahia kuwa pamoja nao.

Yesu alipenda sana kukaa na familia moja iliyoishi katika mji mdogo wa Bethania, nje ya jiji kubwa la Yerusalemu. Unawakumbuka?— Walikuwa Maria, Martha, na Lazaro ndugu yao. Yesu alimwita Lazaro rafiki yake. (Yohana 11:1, 5, 11) Yesu alipenda familia hiyo kwa sababu walimpenda na kumtumikia Yehova.

Kwa nini mara nyingi Yesu alipotembelea Yerusalemu aliishi na familia hii? Unajua majina yao?

Hii haimaanishi kwamba Yesu hakuwa mwenye fadhili kwa watu ambao hawakumtumikia Mungu. Aliwatendea kwa fadhili. Aliwatembelea nyumbani na hata akala pamoja nao. Kwa sababu hiyo wengine hata walisema kwamba Yesu ni “rafiki ya wakusanya-kodi na watenda-dhambi.” (Mathayo 11:19) Ukweli ni kwamba Yesu hakuwatembelea watu hao nyumbani mwao kwa sababu alipenda jinsi walivyojiendesha. Aliwatembelea ili kuwafundisha kumhusu Yehova. Alijaribu kuwasaidia waache njia zao mbaya na wamtumikie Mungu.

Kwa nini Zakayo amepanda juu ya mti huu?

Ilitokea hivyo siku moja katika jiji la Yeriko. Yesu alikuwa akipita akielekea Yerusalemu. Kulikuwa na umati wa watu na miongoni mwao alikuwemo mtu aitwaye Zakayo. Alitaka kumwona Yesu vizuri. Lakini Zakayo alikuwa mfupi na hangeweza kumwona Yesu kwa sababu umati ulimzuia. Basi alikimbia mbele yao na kupanda mti ili amwone Yesu vizuri.

Yesu alipofika kwenye mti huo, alitazama juu na kusema: ‘Shuka haraka, kwa maana leo nakutembelea kwako.’ Lakini Zakayo alikuwa tajiri aliyekuwa amefanya mambo mabaya. Kwa nini Yesu alitaka kumtembelea mtu kama huyo?—

Si kwamba Yesu alipenda jinsi Zakayo alivyoishi. Alienda huko kumfundisha juu ya Mungu. Alitambua namna mtu huyo alivyojitahidi kumwona. Kwa hiyo alijua kwamba huenda Zakayo angemsikiliza. Huo ulikuwa wakati mzuri kumwambia kuhusu namna Mungu anavyotaka watu waishi.

Kwa nini Yesu anamtembelea Zakayo, na Zakayo anaahidi kufanya nini?

Basi ikawaje?— Zakayo anafurahia mafundisho ya Yesu. Anasikitika sana kwamba aliwanyang’anya watu pesa zao, na anaahidi kuwarudishia. Kisha anakuwa mfuasi wa Yesu. Hapo ndipo Zakayo na Yesu wanakuwa rafiki.—Luka 19:1-10.

Tukifuata mfano wa Mwalimu Mkuu, je tunaweza kuwatembelea watu ambao si rafiki zetu?— Ndiyo. Lakini hatutawatembelea kwa sababu tunapenda jinsi wanavyojiendesha. Wala hatutafanya mabaya pamoja nao. Tutawatembelea ili tuwafundishe juu ya Mungu.

Lakini rafiki zetu wa karibu ni wale tunaoshirikiana nao. Ili wawe rafiki wazuri, ni lazima wawe wale wanaopendwa na Mungu. Huenda wengine hata wasimjue Yehova. Lakini iwapo wanataka kujifunza juu yake, tunaweza kuwasaidia. Na wanapompenda Yehova kama sisi, wanaweza kuwa rafiki zetu wa karibu.

Kuna njia nyingine ya kujua kama mtu anaweza kuwa rafiki mzuri. Chunguza mambo anayofanya. Je, anafurahia kuwafanyia watu wengine mambo mabaya na kuwacheka? Haifai kufanya hivyo, sivyo?— Je, yeye hujiingiza kwenye matatizo kila wakati? Hatungependa kujiingiza katika matata pamoja naye, sivyo?— Au je, yeye hupenda kufanya mambo mabaya kimakusudi huku akifikiria kwamba yeye ni mwerevu sana kwa sababu hakuna aliyemwona? Hata kama mtu huyo hakuonekana, Mungu alimwona, sivyo? Je, unafikiri watu wanaofanya mambo kama hayo wanaweza kuwa rafiki zetu?—

Tafadhali chukua Biblia yako. Tuone yale inayosema kuhusu namna rafiki wanavyoweza kuathiri maisha yetu. Fungua 1 Wakorintho sura ya 15, mstari wa 33. Je, umepata andiko hilo?— Mstari huo unasema: “Msipotoshwe. Mashirika mabaya huharibu tabia nzuri.” Hii inamaanisha tukiwa na rafiki wabaya, tunaweza kuwa wabaya. Na ni kweli pia kwamba rafiki wazuri hutusaidia kuwa na mazoea mazuri.

Tusisahau kwamba Yehova ndiye Mtu wa maana sana maishani mwetu. Hatutaki kuharibu uhusiano wetu pamoja naye, sivyo?— Basi, lazima tuhakikishe kwamba tunafanya urafiki na wale tu wanaompenda Mungu.

Umuhimu wa kuwa na rafiki wazuri umeonyeshwa kwenye Zaburi 119:115 (118:115, “Dy”c); Mithali 13:20; 2 Timotheo 2:22; na 1 Yohana 2:15.