Hamia kwenye habari

Hamia kwenye yaliyomo

SURA YA 45

Ufalme wa Mungu Ni Nini? Na Tunaonyeshaje Kwamba Tunautaka?

Ufalme wa Mungu Ni Nini? Na Tunaonyeshaje Kwamba Tunautaka?

UNAJUA sala ambayo Yesu alifundisha wafuasi wake?— Iwapo huijui, tunaweza kuisoma pamoja kwenye Mathayo 6:9-13. Sala hii iitwayo pia Sala ya Bwana, inatia ndani maneno haya: “Ufalme wako na uje.” Unajua Ufalme wa Mungu ni nini?—

Hebu nikueleze, mfalme ni mtawala wa nchi au eneo. Na serikali yake huitwa ufalme. Katika nchi nyingine mtawala anaitwa rais. Mtawala wa serikali ya Mungu anaitwaje?— Ni Mfalme. Hivyo, serikali ya Mungu inaitwa Ufalme.

Unajua Yehova Mungu amemchagua nani awe Mfalme wa serikali Yake?— Mwana wake, Yesu Kristo. Kwa nini Yesu ni bora kuliko mtawala yeyote ambaye wanadamu wanaweza kuchagua?— Ni kwa sababu Yesu anampenda sana Baba yake, Yehova. Kwa hiyo anatenda mema wakati wote.

Zamani kabla ya Yesu kuzaliwa huko Bethlehemu, Biblia ilitaja kuzaliwa kwake na kwamba angekuwa Mtawala aliyechaguliwa na Mungu. Tusome habari hii kwenye Isaya 9:6, 7. Mistari hiyo inasema: ‘Mtoto amezaliwa kwetu, tumepewa mwana: na utawala utakuwa juu ya bega lake: naye ataitwa Mkuu wa Amani. Hakutakuwa na mwisho wa utawala wake wa kifalme na kwa amani.’

Hapo Yesu ameitwa “Mkuu” kwa kuwa yeye ni Mtawala wa Ufalme wa Mungu. Pia Yesu ni Mwana wa Mfalme Mkuu, Yehova. Lakini Yehova pia amemchagua Yesu kuwa Mfalme wa serikali Yake itakayotawala dunia kwa miaka elfu. (Ufunuo 20:6) Baada ya Yesu kubatizwa, alianza “kuhubiri na kusema: ‘Tubuni, kwa maana ufalme wa mbinguni umekaribia.’”—Mathayo 4:17.

Unafikiri ni kwa nini Yesu alisema Ufalme ulikuwa umekaribia?— Kwa sababu Mfalme ambaye baadaye angetawala mbinguni alikuwa pamoja nao! Ndiyo sababu Yesu aliwaambia watu hivi: “Ufalme wa Mungu umo katikati yenu.” (Luka 17:21) Je, hungefurahi kuwa karibu sana na hata kuweza kumgusa Mfalme wa Yehova?—

Basi niambie, Yesu alikuja duniani kufanya kazi gani muhimu?— Yesu alijibu swali hilo hivi: “Ni lazima nitangaze habari njema ya ufalme wa Mungu kwenye majiji mengine pia, kwa sababu nilitumwa kufanya hivyo.” (Luka 4:43) Yesu alijua kwamba hangefanya kazi yote ya kuhubiri peke yake. Unafikiri alifanya nini?—

Yesu alikuja duniani kufanya kazi gani?

Yesu aliwachukua wengine na kuwafundisha jinsi ya kuhubiri. Kwanza aliwafundisha wale 12 aliowachagua kuwa mitume wake. (Mathayo 10:5, 7) Lakini, je, Yesu aliwafundisha mitume wake tu kufanya kazi hiyo? La, Biblia inasema kwamba Yesu aliwafundisha wengine wengi kuhubiri. Kisha akawatuma wanafunzi wengine 70 wakiwa wawili-wawili wamtangulie. Nao walifundisha nini?— Yesu alisema: ‘Endeleeni kuwaambia, “Ufalme wa Mungu umekuja karibu nanyi.”’ (Luka 10:9) Kwa njia hiyo watu wakajifunza kuhusu serikali ya Mungu.

Katika Israeli la kale, wafalme wapya waliingia jijini wakiwa wamebebwa na mwana-punda ili watu wawaone. Yesu anafanya hivyo anapoenda Yerusalemu kwa mara ya mwisho. Yesu atakuwa Mtawala wa Ufalme wa Mungu. Je, watu wanataka awe Mfalme wao?—

Anapopita akiwa juu ya mwana-punda, umati unatandaza mavazi yao ya nje barabarani. Wengine wanakata matawi ya miti na kuyatandaza barabarani. Kwa kufanya hivyo wanaonyesha kwamba wanataka Yesu awe Mfalme wao. Wanasema: “Aliyebarikiwa ni Yule anayekuja akiwa ndiye Mfalme katika jina la Yehova!” Lakini si kila mtu anafurahi. Hata viongozi wa kidini wengine wanamwambia Yesu, ‘Waambie wanafunzi wako wanyamaze.’—Luka 19:28-40.

Kwa nini watu walibadili maoni na kumkataa Yesu asiwe Mfalme wao?

Siku tano baadaye Yesu anakamatwa na kupelekwa kwenye makao ya gavana, Pontio Pilato. Maadui wa Yesu wanasema kwamba Yesu anadai kuwa mfalme na kwamba anapinga serikali ya Roma. Basi Pilato anamwuliza Yesu maoni yake kuhusu mashtaka hayo. Yesu anamwambia kwamba hataki kuipindua serikali. Anamwambia Pilato: “Ufalme wangu si sehemu ya ulimwengu huu.”—Yohana 18:36.

Kisha Pilato anawaambia watu kwamba Yesu hana hatia yoyote. Lakini sasa watu hawataki Yesu awe Mfalme wao. Hawataki aachiliwe. (Yohana 18:37-40) Baada ya kuongea na Yesu tena, Pilato ana hakika kwamba Yesu hana kosa lolote. Hatimaye, baada ya kumtoa Yesu nje kwa mara ya mwisho, Pilato anasema: “Oneni! Mfalme wenu!” Lakini watu wakapiga kelele wakisema: “Mwondolee mbali! Mwondolee mbali! Mtundike mtini!”

Pilato anawauliza: “Je, nimtundike mtini mfalme wenu?” Wakuu wa makuhani wanajibu: “Sisi hatuna mfalme ila Kaisari.” Uovu ulioje! Makuhani hao waovu wamefaulu kuwachochea watu wampinge Yesu!—Yohana 19:1-16.

Leo mambo ni sawa na yalivyokuwa siku za Yesu. Kwa kweli watu wengi hawataki Yesu awe Mfalme wao. Wanaweza kusema wanamwamini Mungu, lakini hawataki Mungu au Kristo awaamulie la kufanya. Wanataka serikali yao wenyewe papa hapa duniani.

Namna gani sisi? Tunakuwa na maoni gani kumhusu Mungu tunapojifunza kuhusu Ufalme Wake na mambo yote mazuri utakayofanya?— Tunampenda, sivyo?— Basi, tunaweza kumwonyeshaje Mungu kwamba tunampenda na tunataka kuwa chini ya Ufalme wake?—

Kwa nini Yesu alibatizwa, na Mungu alionyeshaje kwamba alipendezwa na jambo hilo?

Tunaweza kumwonyesha Mungu kwamba tunampenda kwa kufuata mfano wa Yesu. Na Yesu alifanya nini kuonyesha kwamba anampenda Yehova?— Yeye alisema, “Sikuzote mimi hufanya mambo yanayompendeza.” (Yohana 8:29) Naam, Yesu alikuja duniani ‘kufanya mapenzi ya Mungu’ na “kuimaliza kazi yake.” (Waebrania 10:7; Yohana 4:34) Ona kile ambacho Yesu alifanya kabla ya kuanza kuhubiri.

Yesu alimwendea Yohana Mbatizaji katika Mto Yordani. Baada ya wao kuingia majini, Yohana alimzamisha kabisa Yesu ndani ya maji kisha akamwinua. Unajua ni kwa nini Yohana alimbatiza Yesu?—

Tunaweza kuwaambia wengine kuhusu Ufalme wa Mungu tukiwa wapi?

Yesu alimwambia Yohana ambatize. Lakini tunajuaje kwamba Mungu alitaka Yesu abatizwe?— Tunajua hivyo kwa sababu Yesu alipoinuka kutoka majini, alisikia sauti ya Mungu kutoka mbinguni ikisema: “Wewe ni Mwanangu, mpendwa; nimekukubali wewe.” Mungu hata alituma roho yake takatifu ikiwa kama njiwa ije juu ya Yesu. Hivyo, kwa kubatizwa Yesu alionyesha kwamba alitaka kumtumikia Yehova katika maisha yake yote, naam, milele.—Marko 1:9-11.

Kwa sasa bado wewe unakua. Lakini utafanya nini baadaye utakapokuwa mtu mzima?— Je, utafuata mfano wa Yesu na ubatizwe?— Unapaswa kumwiga, kwa sababu Biblia inasema kwamba alikuachia ‘kielelezo ufuate hatua zake kwa ukaribu.’ (1 Petro 2:21) Ukibatizwa, utaonyesha kwamba kwa kweli unataka kuwa chini ya Ufalme wa Mungu. Lakini ubatizo peke yake hautoshi.

Tunahitaji kutii mafundisho yote ya Yesu. Yeye alisema kwamba hatupaswi kuwa “sehemu ya ulimwengu.” Je, kweli kujiingiza katika mambo ya ulimwengu ni kumtii? Yesu na mitume wake hawakujihusisha na mambo kama hayo. (Yohana 17:14) Badala yake walifanya nini?— Waliwaambia wengine kuhusu Ufalme wa Mungu. Hiyo ilikuwa kazi muhimu maishani mwao. Je, sisi pia tunaweza kufanya hivyo?—Ndiyo, ikiwa tunaamini yale tunayosema tunaposali Ufalme wa Mungu uje.

Tafadhali soma maandiko haya mengine yanayotuambia mambo tunayoweza kufanya ili kuonyesha kwamba tunataka Ufalme wa Mungu uje: Mathayo 6:24-33; 24:14; 1 Yohana 2:15-17; na 5:3.