Hamia kwenye habari

Hamia kwenye yaliyomo

SURA YA 46

Je, Mungu Atauharibu Ulimwengu Tena Kwa Maji

Je, Mungu Atauharibu Ulimwengu Tena Kwa Maji

UMEWAHI kusikia mtu yeyote akitaja mwisho wa ulimwengu?— Watu wengi leo huzungumzia mwisho huo. Wengine wanafikiri kwamba wanadamu watauharibu ulimwengu katika vita ya mabomu ya nyukilia. Je, unafikiri Mungu ataruhusu wanadamu waiharibu dunia yetu maridadi?—

Kama tulivyojifunza, Biblia hutaja mwisho wa ulimwengu. Biblia inasema: “Ulimwengu unapitilia mbali.” (1 Yohana 2:17) Unafikiri mwisho wa ulimwengu unamaanisha mwisho wa dunia?— La, Biblia inasema kwamba Mungu aliiumba dunia ili “ikaliwe” na watu. Ndiyo, ili watu wafurahie kuishi ndani yake. (Isaya 45:18) Zaburi 37:29 inasema: “Waadilifu wenyewe wataimiliki dunia, nao watakaa milele juu yake.” Hiyo ndiyo sababu Biblia inasema kwamba dunia itadumu milele.—Zaburi 104:5; Mhubiri 1:4.

Ikiwa mwisho wa ulimwengu haumaanishi mwisho wa dunia, unamaanisha nini basi?— Tunaweza kupata jibu tukichunguza kwa makini yaliyotendeka katika siku za Noa. Biblia inasema: “Ulimwengu wa wakati huo uliangamia kwa gharika ya maji.”—2 Petro 3:6.

Je, kuna mtu yeyote aliyeokoka mwisho wa ulimwengu huo wakati wa Gharika ya siku za Noa?— Biblia inasema kwamba Mungu “alimlinda Noa, mhubiri wa uadilifu, akiwa salama pamoja na wengine saba alipoleta gharika juu ya ulimwengu wa watu wasiomwogopa Mungu.”—2 Petro 2:5.

Ni ulimwengu gani ulioharibiwa katika siku za Noa?

Basi ni ulimwengu gani ulioharibiwa? Je, ni dunia au ni watu wabaya?— Biblia inasema kwamba ulikuwa “ulimwengu wa watu wasiomwogopa Mungu.” Ona kwamba Noa anaitwa “mhubiri.” Unafikiri alihubiri nini?— Noa alitoa onyo kuhusu mwisho wa ‘ulimwengu wa wakati huo.’

Yesu alipozungumzia Gharika kubwa, aliwaambia wanafunzi wake mambo ambayo watu watakuwa wakifanya kabla tu ya mwisho kuja. Hivi ndivyo alivyowaambia: “Katika siku hizo kabla ya gharika, [watu walikuwa] wakila na kunywa, wanaume wakioa na wanawake wakiolewa, mpaka siku ambayo Noa aliingia ndani ya safina, nao hawakujali mpaka gharika ikaja na kuwafagilia mbali wote.” Kisha Yesu akasema kwamba watu watafanya mambo kama hayo kabla ya mwisho wa ulimwengu huu.—Mathayo 24:37-39.

Maneno ya Yesu yanaonyesha kwamba tunaweza kujifunza kupitia mambo ambayo watu walifanya kabla ya Gharika. Kupitia yale uliyosoma katika Sura ya 10 ya kitabu hiki, je, unakumbuka mambo ambayo watu hao walifanya?— Watu wengine walikuwa wakatili na walifanya jeuri. Yesu akasema kwamba wengi wao hawakusikiliza Mungu alipomtuma Noa awahubirie.

Basi siku ikafika ambayo Yehova alikuwa amemwambia Noa kwamba angewaharibu waovu kwa gharika. Dunia yote na hata milima ingefunikwa na maji. Yehova akamwambia Noa ajenge safina kubwa. Ilifanana na sanduku kubwa kama inavyoonyeshwa kwenye picha katika ukurasa wa 238.

Mungu alimwambia Noa ajenge safina kubwa ili yeye na familia yake pamoja na wanyama waokolewe. Noa na familia yake walifanya kazi kwa bidii. Walikata miti mikubwa, wakatumia mbao zake kujenga safina. Kazi hiyo ilichukua miaka mingi kwa sababu safina ilikuwa kubwa sana.

Mbali na kujenga safina, unakumbuka Noa alifanya kazi gani nyingine kwa miaka hiyo yote?— Alihubiri, akiwaonya watu kuhusu Gharika iliyokuwa inakaribia. Je, kuna mtu yeyote aliyemsikiliza? Hakuna mtu aliyemsikiliza ila familia yake. Wengine walijishughulisha na mambo mengine tu. Unakumbuka Yesu alisema walikuwa wakifanya nini?— Walijishughulisha na kula, kunywa, kuoa, na kuolewa. Hawakufikiri kwamba wao ni wabaya, wala hawakumsikiliza Noa. Hebu tuone yaliyowapata.

Yehova alifunga mlango wa safina baada ya Noa na familia yake kuingia ndani. Watu waliokuwa nje ya safina bado hawakuamini kutakuwa na Gharika. Lakini kwa ghafula, maji yakaanza kumwagika kutoka mbinguni! Haikuwa mvua ya kawaida. Ilikuwa mvua kubwa sana! Punde maji yakawa mito mikubwa yenye makelele. Maji hayo yakaangusha miti mikubwa na kubiringisha miamba kana kwamba ni mawe madogo tu. Namna gani watu waliokuwa nje ya safina?— Yesu alisema: ‘Gharika ilikuja na kuwafagilia mbali wote.’ Wote waliokuwa nje ya safina wakafa. Kwa nini?— Kama Yesu alivyosema, “hawakujali.” Hawakusikiliza! —Mathayo 24:39; Mwanzo 6:5-7.

Kwa nini tusifikirie kujifurahisha tu?

Kumbuka Yesu alisema kwamba yaliyowapata watu hao ni onyo kwetu leo. Onyo gani?— Kwamba watu waliharibiwa si kwa sababu tu walikuwa wabaya lakini pia kwa sababu waliruhusu shughuli zao ziwazuie kujifunza kumhusu Mungu na kuhusu yale aliyokusudia kufanya. Tujihadhari tusiwe kama wao, sivyo?—

Unafikiri Mungu atatumia gharika kuharibu ulimwengu tena?— La, Mungu aliahidi kwamba hatafanya hivyo. Alisema: “Nawapa upinde wangu wa mvua katika wingu, nao utakuwa ishara.” Yehova alisema kwamba upinde utakuwa ishara kwamba “maji hayatakuwa gharika tena ili kuuharibu mwili wote.”—Mwanzo 9:11-17.

Hivyo tuna hakika kwamba Mungu hataharibu ulimwengu tena kwa gharika. Hata hivyo, Biblia inataja mwisho wa ulimwengu. Ni nani watakaookoka Mungu atakapoharibu ulimwengu huu?— Je, ni wale waliokuwa wakifuatia mambo yao wenyewe bila kujali kujifunza kumhusu Mungu? Je, ni wale ambao walikuwa na shughuli nyingi sana hivi kwamba hawakuwa na nafasi ya kujifunza Biblia? Unaonaje?—

Tungependa kuwa miongoni mwa wale watakaookolewa na Mungu, sivyo?— Je, halitakuwa jambo la kupendeza familia yetu ikiwa kama ya Noa ili sote tupate kuokolewa na Mungu?— Ili tuokoke mwisho wa ulimwengu, tunapaswa kuelewa jinsi Mungu atakavyoharibu ulimwengu huu na kuleta mwingine mpya wenye uadilifu. Hebu tuone jinsi atakavyofanya.

Biblia inatujibu kwenye Danieli sura ya 2, mstari wa 44. Andiko hili linasema hivi linapozungumzia wakati huu: “Katika siku za wafalme hao, Mungu wa mbinguni atausimamisha ufalme [au, serikali] ambao hautaharibiwa kamwe, na ufalme huo hautapewa watu wengine wowote. Utazivunja na kuzikomesha falme hizi zote, nao utasimama mpaka wakati usio na kipimo.”

Je, unaelewa hilo?— Biblia inasema kwamba serikali ya Mungu itaharibu serikali zote za wanadamu. Kwa nini?— Kwa sababu hawamtii yule ambaye Mungu amemchagua awe Mfalme. Na ni nani huyo?— Naam, ni Yesu Kristo!

Yesu Kristo, Mfalme aliyechaguliwa na Mungu, ataharibu ulimwengu huu kwenye Har-Magedoni

Yehova Mungu ana haki ya kuamua ni serikali gani inayopaswa kutawala, naye amemchagua Mwana wake Yesu kuwa Mfalme. Karibuni, Yesu Kristo Mtawala aliyechaguliwa na Mungu, ataziharibu serikali zote za ulimwengu huu. Kwenye Ufunuo sura ya 19, mstari wa 11 hadi 16, Biblia inasema kwamba Yesu ataharibu serikali zote, kama picha hii inavyoonyesha. Katika Biblia, vita ya Mungu ya kuharibu serikali zote za ulimwengu inaitwa Har-Magedoni.

Mungu anasema kwamba Ufalme wake utaharibu serikali za wanadamu. Lakini je, Mungu anatuambia tuziharibu?— La, katika Biblia, Har-Magedoni inaitwa “vita ya ile siku kuu ya Mungu Mweza-Yote.” (Ufunuo 16:14, 16) Ndiyo, Har-Magedoni ni vita ya Mungu, naye anatumia Yesu Kristo kuongoza majeshi ya mbinguni katika pigano hilo. Je, vita ya Har-Magedoni ni karibu? Hebu tuone jinsi tunavyoweza kujua.

Tusome pamoja kuhusu wakati Mungu atakapoondoa waovu wote na kuwaokoa wale wanaomtumikia, kwenye Mithali 2:21, 22; Isaya 26:20, 21; Yeremia 25:31-33; na Mathayo 24:21, 22.