Hamia kwenye habari

Hamia kwenye yaliyomo

SURA YA KWANZA

Ukweli Kumhusu Mungu

Ukweli Kumhusu Mungu
  • Je, kweli Mungu anakujali?

  • Mungu ana utu wa aina gani? Je, ana jina?

  • Je, tunaweza kuwa na uhusiano wa karibu pamoja na Mungu?

1, 2. Kwa nini ni vizuri kuuliza maswali?

JE, UMEWAHI kuona jinsi ambavyo watoto huuliza maswali? Wengi wao huanza kuuliza maswali mara tu wanapojua kuongea. Wanakutazama wakiwa wamekodoa macho kwa hamu na kuuliza maswali kama vile: Kwa nini anga ni bluu? Kwa nini nyota zinametameta? Ni nani aliyewafundisha ndege kuimba? Huenda ukajaribu sana kujibu, lakini mara nyingi si rahisi. Hata baada ya kuwapa jibu bora, huenda bado wakauliza: Kwa nini?

2 Si watoto peke yao wanaouliza maswali. Tunapoendelea kukua, sisi huuliza maswali. Tunauliza maswali ili tupate mwongozo, tujue hatari tunazohitaji kuepuka, au kwa sababu tu tunataka kujua. Hata hivyo, inaonekana kwamba watu wengi huacha kuuliza maswali, hasa yaliyo muhimu zaidi. Wao huacha kutafuta majibu.

3. Kwa nini watu wengi hawajitahidi kupata majibu ya maswali muhimu zaidi?

3 Fikiria swali lililo katika jalada la kitabu hiki, maswali yaliyo katika utangulizi wa kitabu hiki, au yale yaliyo mwanzoni mwa sura hii. Hayo ni baadhi ya maswali muhimu zaidi unayoweza kuuliza. Hata hivyo, watu wengi hawajitahidi kupata majibu ya maswali hayo. Kwa nini? Je, Biblia ina majibu? Watu fulani hufikiri kwamba Biblia haieleweki. Wengine huogopa kuuliza maswali ili wasiaibishwe au kudharauliwa. Hali wengine huamua kwamba maswali hayo yanaweza kujibiwa tu na viongozi na walimu wa dini. Wewe unaonaje?

4, 5. Ni maswali gani muhimu zaidi tunayoweza kuuliza maishani, na kwa nini tutafute majibu?

4 Bila shaka ungependa kupata majibu ya maswali muhimu zaidi maishani. Haikosi, nyakati nyingine wewe hujiuliza: ‘Maisha yana kusudi gani? Je, kusudi pekee la maisha ni kuzaliwa, kuzeeka, na kufa? Kwa kweli Mungu ana utu gani?’ Ni vizuri kuuliza maswali kama hayo, na ni muhimu kutafuta majibu yenye kuridhisha na yenye kutegemeka bila kukata tamaa. Yule mwalimu mashuhuri, Yesu Kristo, alisema hivi: “Endeleeni kuomba, nanyi mtapewa; endeleeni kutafuta, nanyi mtapata; endeleeni kupiga hodi, nanyi mtafunguliwa.”—Mathayo 7:7.

5 ‘Ukiendelea kutafuta’ majibu ya maswali hayo muhimu, utafaidika sana. (Methali 2:1-5) Hata uwe umeambiwa nini na watu wengine, kuna majibu, na unaweza kuyapata katika Biblia. Majibu hayo si magumu, yasiyoeleweka. Isitoshe, yatakupa tumaini na shangwe. Na yanaweza kukusaidia kuishi maisha yenye kuridhisha sasa. Kwanza, na tufikirie swali moja ambalo limewahangaisha watu wengi.

JE, MUNGU ANA HURUMA NA JE, ANAJALI?

6. Kwa nini watu wengi wanafikiri kwamba Mungu hajali wanadamu wanapoteseka?

6 Watu wengi hujibu hapana. Wanasema, ‘Ikiwa Mungu anajali, ulimwengu ungekuwa tofauti sana.’ Leo, ulimwengu umejaa vita, chuki, na mateso. Isitoshe, kila mmoja wetu huwa mgonjwa, huteseka, na kufiwa na wapendwa wake. Ndiyo sababu watu wengi husema, ‘Ikiwa Mungu anatujali na kuhangaikia matatizo yetu, kwa nini hazuii mambo hayo yasitupate?’

7. (a) Walimu wa dini wamewafanyaje watu wengi wafikiri kwamba Mungu hana huruma? (b) Biblia inafundisha nini hasa kuhusu majaribu ambayo huenda yakatupata?

7 Isitoshe, nyakati nyingine walimu wa dini huwafanya watu wafikiri kwamba Mungu hana huruma. Jinsi gani? Msiba unapotokea, wanasema ni mapenzi ya Mungu. Kwa kweli, walimu hao wanamlaumu Mungu kwa sababu ya mambo mabaya yanayotukia. Je, huo ndio ukweli kumhusu Mungu? Biblia inafundisha nini hasa? Andiko la Yakobo 1:13 linajibu: “Mtu akiwa chini ya jaribu, yeye asiseme: ‘Mungu ananijaribu.’ Kwa maana Mungu hawezi kujaribiwa na mambo maovu wala yeye mwenyewe hamjaribu yeyote.” Kwa hiyo, Mungu hasababishi kamwe uovu ambao unaona ulimwenguni. (Ayubu 34:10-12) Ni kweli kwamba anaacha mambo mabaya yatukie. Hata hivyo, kuna tofauti kubwa kati ya kuacha jambo litukie na kulisababisha.

8, 9. (a) Unaweza kutumia mfano gani kuonyesha tofauti iliyopo kati ya kuacha uovu uwepo na kuusababisha? (b) Kwa nini si haki kumlaumu Mungu kwa kuwaacha wanadamu wafuate njia isiyofaa?

8 Kwa mfano, wazia baba mwenye hekima na busara aliye na mwana ambaye tayari ni mtu mzima na bado anaishi nyumbani kwa wazazi wake. Mwana huyo akiasi na kuamua kuondoka nyumbani, baba yake hamzuii. Mwana huyo anaishi maisha mapotovu na kupata matatizo. Je, baba ndiye aliyesababisha matatizo ya mwanaye? Hapana. (Luka 15:11-13) Vivyo hivyo, Mungu hawazuii wanadamu wakishaamua kufuata njia isiyofaa, hata hivyo hasababishi matatizo yanayowapata. Kwa hiyo, basi, si haki kumlaumu Mungu kwa sababu ya matatizo yote yanayowapata wanadamu.

9 Mungu ana sababu nzuri za kuwaacha wanadamu wafuate njia isiyofaa. Akiwa Muumba wetu mwenye hekima na nguvu, hahitaji kutueleza sababu hizo. Hata hivyo, Mungu hutueleza kwa sababu ya upendo. Utajifunza kuhusu sababu hizo katika Sura ya 11. Lakini uwe na hakika kwamba Mungu hasababishi matatizo yanayotupata. Badala yake, anatupa tumaini pekee la utatuzi!—Isaya 33:2.

10. Kwa nini tunaweza kuwa na hakika kwamba Mungu ataondoa madhara yote yanayotokana na uovu?

10 Isitoshe, Mungu ni mtakatifu. (Isaya 6:3) Hilo linamaanisha kwamba yeye ni safi wala hana uovu hata kidogo. Kwa hiyo, tunaweza kumtumaini kabisa. Hatuwezi kuwatumaini wanadamu ambao nyakati nyingine wanakuwa wafisadi. Hata wanadamu wenye mamlaka ambao ni wanyoofu zaidi mara nyingi hawana uwezo wa kuondoa madhara yanayosababishwa na watu wabaya. Lakini Mungu ana nguvu zote. Anaweza na ataondoa madhara yote yanayowapata wanadamu kwa sababu ya uovu. Mungu atakapochukua hatua, atakomesha uovu milele!—Zaburi 37:9-11.

MUNGU ANAHISIJE KUHUSU UKOSEFU WA HAKI?

11. (a) Mungu anahisije kuhusu ukosefu wa haki? (b) Mungu anahisije kuhusu kuteseka kwako?

11 Mungu anahisije kuhusu mambo yanayoendelea ulimwenguni na maishani mwako? Kwanza kabisa, Biblia inafundisha kwamba Mungu ni “mpenda-haki.” (Zaburi 37:28) Kwa hiyo anapendezwa sana na mambo yanayofaa na kuchukizwa na mambo yasiyofaa. Anachukia ukosefu wa haki wa kila namna. Biblia inasema kwamba Mungu ‘aliumia moyoni mwake’ uovu ulipokuwa mwingi duniani wakati uliopita. (Mwanzo 6:5, 6) Mungu hajabadilika. (Malaki 3:6) Bado anachukia kuona mateso yanayoendelea ulimwenguni pote. Pia, Mungu anachukia kuona watu wakiteseka. Biblia inasema, “yeye anawajali ninyi.”—1 Petro 5:7.

Biblia inafundisha kwamba Yehova ni Muumba wa ulimwengu mwenye upendo

12, 13. (a) Kwa nini tuna sifa nzuri kama vile upendo, nao upendo unatufanya tuwe na maoni gani kuhusu ulimwengu? (b) Kwa nini unaweza kuwa na hakika kwamba Mungu atachukua hatua kuhusiana na matatizo ya ulimwengu?

12 Tunawezaje kuwa na hakika kwamba Mungu anachukia kuona watu wakiteseka? Uthibitisho mwingine ndio huu. Biblia inafundisha kwamba Mungu alimuumba mtu kwa mfano wake. (Mwanzo 1:26) Kwa hiyo, tuna sifa nzuri kwa sababu Mungu ana sifa nzuri. Kwa mfano, je, wewe husumbuka unapowaona watu wasio na hatia wakiteseka? Ikiwa unasumbuka kwa sababu ya ukosefu huo wa haki, uwe na hakika kwamba Mungu husumbuka hata zaidi.

13 Jambo moja la pekee kuhusu wanadamu ni kwamba tuna uwezo wa kuonyesha upendo. Mungu pia ana sifa hiyo. Biblia inafundisha kwamba “Mungu ni upendo.” (1 Yohana 4:8) Tuna upendo kwa sababu Mungu ana upendo. Je, upendo ungekuchochea kukomesha mateso na ukosefu wa haki unaoona ulimwenguni? Kama ungekuwa na uwezo wa kufanya hivyo, je, ungeyakomesha? Bila shaka ungeyakomesha! Uwe na hakika kwamba Mungu atakomesha mateso na ukosefu wa haki. Ahadi zinazotajwa katika utangulizi wa kitabu hiki si ndoto tu au matumaini yasiyo na msingi. Bila shaka ahadi za Mungu zitatimia! Hata hivyo, ili kuamini ahadi hizo, unahitaji kujua mengi zaidi kumhusu Mungu anayezitoa.

MUNGU ANATAKA UMJUE

Unapotaka mtu akujue, unamwambia jina lako, sivyo? Mungu anatujulisha jina lake katika Biblia

14. Mungu anaitwa nani, na kwa nini tunapaswa kulitumia jina lake?

14 Ukitaka mtu akujue, unaweza kufanya nini? Utamwambia jina lako, sivyo? Je, Mungu ana jina? Dini nyingi hujibu kwamba jina lake ni “Mungu” au “Bwana,” lakini hayo si majina yake binafsi. Hayo ni majina ya heshima kama vile “mfalme” na “rais.” Biblia inafundisha kwamba Mungu ana majina mengi ya heshima. Baadhi ya majina hayo ni “Mungu” na “Bwana.” Hata hivyo, Biblia inafundisha pia kwamba Mungu ana jina lake binafsi, yaani, Yehova. Andiko la Zaburi 83:18 linasema hivi: “Wewe, ambaye jina lako ni Yehova, wewe peke yako ndiye Uliye Juu Zaidi, juu ya dunia yote.” Ikiwa Biblia yako haina jina hilo, unaweza kutazama nyongeza “Jina la Mungu—Maana na Matumizi” ili ujue ni kwa nini. Ukweli ni kwamba jina la Mungu linapatikana mara elfu kadhaa katika hati za zamani za Biblia. Kwa hiyo, Yehova anataka ulijue jina lake na kulitumia. Tunaweza kusema kwamba anatumia Biblia kujitambulisha kwako.

15. Jina Yehova linamaanisha nini?

15 Mungu alijipa jina lenye maana. Jina lake, Yehova, linamaanisha kwamba anaweza kutimiza ahadi yoyote anayotoa na kufanya jambo lolote analokusudia. * Jina la Mungu ni la pekee, halina kifani. Ni lake peke yake. Yehova ni wa pekee katika njia mbalimbali. Jinsi gani?

16, 17. Tunaweza kujifunza nini kumhusu Yehova kutokana na majina haya ya heshima: (a) “Mweza-Yote”? (b) “Mfalme wa umilele”? (c) “Muumba”?

16 Tuliona kwamba andiko la Zaburi 83:18 linasema hivi kumhusu Yehova: “Wewe peke yako ndiye Uliye Juu Zaidi.” Vivyo hivyo, Yehova peke yake ndiye anayeitwa “Mweza-Yote.” Andiko la Ufunuo 15:3 linasema: “Matendo yako ni makuu na ya ajabu, Yehova Mungu, Mweza-Yote. Njia zako ni za uadilifu na za kweli, Mfalme wa umilele.” Jina “Mweza-Yote” linatufundisha kwamba Yehova ndiye mwenye nguvu zaidi kuliko wote. Nguvu zake hazina kifani; ni nyingi sana. Nalo jina “Mfalme wa umilele” linatukumbusha kwamba Yehova ni wa pekee katika njia nyingine. Yeye peke yake ndiye amekuwapo nyakati zote. Andiko la Zaburi 90:2 linasema: “Tangu wakati usio na kipimo mpaka wakati usio na kipimo [au, milele] wewe ni Mungu.” Maneno hayo yanatuchochea tumheshimu, sivyo?

17 Pia, Yehova ni wa pekee kwa sababu yeye peke yake ndiye Muumba. Andiko la Ufunuo 4:11 linasema: “Unastahili, Ee Yehova, naam, Mungu wetu, kupokea utukufu na heshima na nguvu, kwa sababu uliumba vitu vyote, na kwa sababu ya mapenzi yako vilikuwako navyo vikaumbwa.” Kila kitu unachoweza kuwazia, iwe viumbe wa roho mbinguni ambao hawaonekani, nyota zinazotapakaa katika anga la usiku, matunda yanayokua mitini, au samaki walio baharini na kwenye mito, vyote vipo kwa sababu Yehova ndiye Muumba!

JE, UNAWEZA KUMKARIBIA YEHOVA?

18. Kwa nini watu fulani wanahisi kwamba hawawezi kamwe kumkaribia Mungu, lakini Biblia inafundisha nini?

18 Kusoma kuhusu sifa za Yehova za ajabu, huwafanya watu fulani wamwogope. Wanahisi kwamba Mungu yuko juu sana wasiweze kumkaribia, nao ni duni machoni pake. Lakini je, hayo ni maoni yanayofaa? Biblia haifundishi hivyo. Inasema hivi kumhusu Yehova: “Hayuko mbali sana na kila mmoja wetu.” (Matendo 17:27) Hata Biblia inatuhimiza hivi: “Mkaribieni Mungu, naye atawakaribia ninyi.”—Yakobo 4:8.

19. (a) Tunawezaje kuanza kumkaribia Mungu, nasi tutapata faida gani? (b) Ni sifa gani za Mungu zinazokuvutia zaidi?

19 Unawezaje kumkaribia Mungu? Kwanza kabisa, endelea kujifunza kumhusu kama unavyofanya sasa. Yesu alisema: “Uzima wa milele ndio huu, waendelee kupata ujuzi juu yako wewe, Mungu wa pekee wa kweli, na juu ya yule uliyemtuma, Yesu Kristo.” (Yohana 17:3) Naam, Biblia inafundisha kwamba kujifunza kumhusu Yehova na Yesu huongoza kwenye “uzima wa milele”! Kama tulivyoona, “Mungu ni upendo.” (1 Yohana 4:16) Pia, Yehova ana sifa nyingine nyingi nzuri zenye kuvutia. Kwa mfano, Biblia inasema kwamba Yehova ni “Mungu mwenye rehema na neema, si mwepesi wa hasira naye ni mwingi wa fadhili zenye upendo na kweli.” (Kutoka 34:6) Yeye ni ‘mwema na yuko tayari kusamehe.’ (Zaburi 86:5) Mungu ana subira. (2 Petro 3:9) Yeye ni mshikamanifu. (Ufunuo 15:4) Kadiri unavyozidi kujifunza mengi katika Biblia, ndivyo utakavyozidi kujua jinsi Yehova ameonyesha sifa hizo na nyingine nyingi zenye kuvutia.

20-22. (a) Kwa kuwa hatuwezi kumwona Mungu, je, inamaanisha kwamba hatuwezi kumkaribia? Eleza. (b) Huenda watu fulani wasio na nia mbaya wakakusihi ufanye nini, lakini unapaswa kufanya nini?

20 Ni kweli kwamba huwezi kumwona Mungu kwa sababu yeye ni roho asiyeonekana. (Yohana 1:18; 4:24; 1 Timotheo 1:17) Hata hivyo, ukijifunza kumhusu katika Biblia, utaujua utu wake. Kama mtunga-zaburi alivyosema, unaweza “kuuona uzuri wa Yehova.” (Zaburi 27:4; Waroma 1:20) Unapozidi kujifunza kumhusu Yehova, atakuwa halisi zaidi kwako nawe utampenda na kumkaribia zaidi.

Upendo wa baba kwa watoto wake unaonyesha upendo mkubwa zaidi ambao Baba yetu wa mbinguni anatuonyesha

21 Utaelewa hatua kwa hatua ni kwa nini Biblia inatufundisha kumwona Yehova kuwa Baba yetu. (Mathayo 6:9) Mbali na kwamba ametupa uhai, anataka tuwe na maisha bora iwezekanavyo, kama vile baba yeyote mwenye upendo angewatakia watoto wake. (Zaburi 36:9) Pia, Biblia inafundisha kwamba wanadamu wanaweza kuwa rafiki za Yehova. (Yakobo 2:23) Hebu wazia—wewe unaweza kuwa rafiki ya Muumba wa ulimwengu!

22 Unapoendelea kujifunza mengi zaidi katika Biblia, huenda watu fulani wasio na nia mbaya wakakusihi uache kujifunza. Huenda wakaogopa kwamba utabadili dini yako. Lakini usimruhusu mtu yeyote akuzuie kufanya urafiki pamoja na Mungu.

23, 24. (a) Kwa nini unapaswa kuendelea kuuliza maswali kuhusu mambo unayojifunza? (b) Ni habari gani itakayozungumziwa katika sura inayofuata?

23 Ni kweli kwamba kuna mambo ambayo hutaelewa mwanzoni. Unyenyekevu unahitajiwa ili kuomba msaada, lakini usisite kuuliza kwa sababu ya aibu. Yesu alisema kwamba ni vizuri kuwa mnyenyekevu kama mtoto mchanga. (Mathayo 18:2-4) Kama tujuavyo, watoto huuliza maswali mengi. Mungu anataka upate majibu. Biblia inawasifu watu waliokuwa na hamu ya kujifunza kumhusu Mungu. Waliyachunguza Maandiko kwa uangalifu ili kuhakikisha kwamba mambo waliyokuwa wakijifunza ni ya kweli.—Matendo 17:11.

24 Njia bora zaidi ya kujifunza kumhusu Yehova ni kuichunguza Biblia. Biblia ni tofauti na vitabu vingine vyote. Jinsi gani? Sura inayofuata itazungumzia habari hiyo.

^ fu. 15 Unaweza kupata habari zaidi kuhusu maana ya jina la Mungu na jinsi linavyotamkwa katika nyongeza “Jina la Mungu—Maana na Matumizi.”