Ona video zinazopatikana

Ona habari zilizo ndani

SURA YA KWANZA

Biblia Inafundisha Nini juu ya Mungu?

Biblia Inafundisha Nini juu ya Mungu?
  •  Mungu anakuhangaikia?

  • Mungu iko namna gani? Je, yeye ana jina?

  • Inawezekana kumukaribia Mungu?

1, 2. Sababu gani ni vizuri kuuliza maulizo?

JE, UMEKWISHA kuona namna watoto wanavyouliza maulizo? Watoto wengi wanaanza kuuliza maulizo wanapoanza tu kusema kama unavyoona kwenye picha hii. Wanapenda sana kujua mambo, ndio sababu utaona mutoto anafungua macho, anakutazama na kuuliza maulizo kama haya: Ni nani aliyeumba ndege? Maji ya mvua yanatoka wapi? Unaweza kujaribu namna yako yote ili kumujibia, lakini hatatosheka. Hata ukiisha kumupatia jibu nzuri anaweza kuuliza tena: Juu ya nini?

2 Si watoto tu ndio wanaouliza maulizo. Sisi pia kadiri tunavyoendelea kukomaa, tunauliza maulizo. Tunauliza watu wengine maulizo ili watuonyeshe njia fulani. Tunauliza pia maulizo ili kujua ikiwa kuna hatari fulani ya kuepuka, ao kwa sababu tunataka tu kujua jambo fulani. Lakini leo, watu wengi hawapendi tena kuuliza maulizo, hasa maulizo ya lazima sana. Ao tuseme wameacha kutafuta majibu ya maulizo hayo ya lazima.

3. Sababu gani watu wengine hawapendi tena kutafuta majibu ya maulizo ya lazima sana ambayo watu wanajiuliza?

3 Wazia kwanza juu ya ulizo linalopatikana kwenye jalada la kitabu hiki, wazia pia juu ya maulizo yanayoulizwa kwenye ukurasa wa 3, ao  yale yanayoulizwa hapa juu, mwanzo wa sura hii ya 1. Maulizo hayo ni kati ya maulizo ya lazima sana unayoweza kuuliza. Hata hivyo, watu wengi hawapendi tena kutafuta majibu ya maulizo hayo. Sababu gani? Watu fulani wanawaza mutu hawezi kuelewa majibu ya Biblia kwa sababu ni magumu sana. Wengine wanaogopa kuuliza maulizo kwa sababu ya haya ao wanawaza kama watawazarau. Na wengine wanawaza ni viongozi na walimu wa dini ndio wanaoweza kujibu maulizo hayo. Wewe pia unawaza hivyo? Je, Biblia ina majibu ya maulizo hayo?

4, 5. Ni maulizo gani fulani ya lazima sana tunayoweza kujiuliza juu ya maisha, na sababu gani tunapaswa kutafuta majibu ya maulizo hayo?

4 Hakika, wewe ungependa kupata majibu ya maulizo ya lazima sana ambayo watu wanajiuliza juu ya maisha. Labda wewe pia unajiuliza hivi: ‘Sababu gani tunaishi? Je, kusudi la maisha ni kuzaliwa, kuzeeka, na kufa, na basi? Mungu iko namna gani?’ Ni vizuri kabisa kujiuliza maulizo kama hayo, na ni jambo la lazima uendelee kutafuta majibu yanayosadikisha na ya kweli, mupaka utakapoyapata. Yesu Kristo, mwalimu anayejulikana sana, alisema hivi: ‘Endeleeni kuomba, nanyi mutapewa; endeleeni kutafuta, nanyi mutapata; endeleeni kupiga hodi, nanyi mutafunguliwa.’​—Mathayo 7:7.

5 ‘Ukiendelea kutafuta’ majibu ya maulizo hayo ya lazima, utapata faida sana. (Methali 2:1-5) Hata ikiwa watu wengine wamekwisha kukuambia nini juu ya maulizo hayo, jua kama majibu yanaweza kupatikana katika Biblia. Majibu hayo si magumu kabisa, unaweza kuyaelewa. Jambo nzuri zaidi, majibu hayo yatakufurahisha na kukupatia tumaini. Na yanaweza kukusaidia uwe mwenye kutosheka katika maisha yako. Kwanza, acha tujibie ulizo moja ambalo mara nyingi linawasumbua watu wengi.

JE, MUNGU ANA MOYO WA HURUMA NA JE, ANATUHANGAIKIA?

6. Sababu gani watu wengi wanawaza Mungu hawahangaikii watu wanaoteseka?

6 Watu wengi wanawaza Mungu hana moyo wa huruma na hatuhangaikii. Wanasema, ‘Ikiwa Mungu anatuhangaikia, maisha yetu hayangekuwa namna yalivyo leo.’ Leo, mambo tunayoona mahali pote ni vita, kuchukiana, na taabu. Tena, tunapatwa na magonjwa, tunateseka, tunafiwa na watu tunaowapenda. Kwa sababu hiyo, watu wengi wanajiuliza hivi: ‘Ikiwa Mungu anatuhangaikia na kuona magumu yetu, sababu gani hazuii mambo hayo yasitupate?’

7. (a) Namna gani mafundisho ambayo watu wengi wamefundishwa yamewafanya wawaze Mungu hana moyo wa huruma? (b) Biblia inafundisha kabisa nini juu ya mateso tunayopata?

7 Tena, mafundisho ambayo watu wanafundishwa ndio yanayowafanya wakati mwingine wawaze kama Mungu hana moyo wa huruma. Labda utajiuliza, namna gani? Kwa mufano, watu wanapopatwa na shida ao musiba, viongozi wao wa dini wanawaambia hayo ni mapenzi ya Mungu. Kwa kweli, wanaposema hivyo wanaonyesha kama ikiwa watu wanapatwa na mambo mabaya ni kosa la Mungu. Unawaza wanasema ukweli juu ya Mungu? Biblia inafundisha kabisa nini? Yakobo 1:13 inajibu hivi: ‘Mutu akiwa chini ya jaribu, yeye asiseme: Mungu ananijaribu. Kwa maana Mungu hawezi kujaribiwa na mambo maovu wala yeye mwenyewe hamujaribu yeyote.’ Kwa hiyo mambo mabaya unayoona katika dunia si mapenzi ya Mungu hata kidogo. (Ayubu 34:10-12) Hata hivyo, yeye anaacha mambo hayo mabaya yatupate. Lakini, jua hili: kuacha jambo fulani litokee ni tofauti sana na kufanya jambo hilo.

8, 9. (a) Ni mufano gani unaoweza kutumia ili kuonyesha kama kuacha jambo fulani litokee ni tofauti sana na kufanya jambo hilo? (b) Sababu gani si haki kusema kosa ni la Mungu kwa kuwa aliamua kuwaacha wanadamu wafuate njia mbaya?

8 Tuchukue mufano wa baba fulani mwenye hekima na upendo aliye na kijana mwenye kukomaa. Tuseme kijana huyo angali anaishi nyumbani pamoja na wazazi, lakini anaasi na anaamua kuondoka nyumbani. Baba yake anamuacha aende. Kijana huyo anaenda kufuata njia mbaya na kisha anapatwa na magumu. Je, tutasema ni baba yake ndiye aliyemuingiza katika magumu hayo? Hapana. (Luka 15:11-13) Vilevile, wakati wanadamu walichagua kufuata njia isiyofaa, Mungu aliwaacha wafanye hivyo; lakini hatuwezi kusema kama Mungu ndiye anayetokeza magumu ambayo wanadamu wanapata. Basi, si haki kusema kosa ni la Mungu ikiwa watu wanapatwa na magumu.

9 Ikiwa Mungu anawaacha wanadamu wafuate njia mbaya kuna sababu za maana zinazomusukuma kufanya hivyo. Kwa kuwa yeye ni Muumbaji wetu mwenye hekima na mwenye nguvu, halazimishwi kutuelezea sababu hizo. Lakini, kwa kuwa Mungu anatupenda, anatuelezea sababu hizo. Katika Sura ya 11 utajifunza mengi juu ya sababu hizo. Lakini jua kabisa kama si Mungu anayetuletea mateso. Ndiyo sababu yeye anatuahidi kama atamaliza mateso yetu!​—Isaya 33:2.

10. Sababu gani tunaweza kutumainia kama Mungu ataondoa mambo yote mabaya yanayowapata wanadamu kwa sababu ya uovu?

10 Tena, Mungu ni mutakatifu. (Isaya 6:3) Hilo linamaanisha kuwa yeye ni musafi na mwenye kutakata. Hana ubaya hata kidogo. Kwa hiyo, tunaweza kumutumainia kwa moyo wote. Lakini hatuwezi kuwatumainia wanadamu hivyo, kwa sababu wakati fulani wanaambukizwa na ubaya. Mara nyingi, hata kiongozi muzuri zaidi anaweza kushindwa kuondoa ubaya ambao umeletwa na watu waovu. Lakini Mungu yeye ni mwenye nguvu zote. Ana uwezo wa kuondoa mambo yote mabaya yanayowapata wanadamu kwa sababu ya uovu, na atauondoa kabisa. Wakati Mungu atauondoa uovu, atauondoa milele!​—Zaburi 37:9-11.

MUNGU ANAJISIKIA NAMNA GANI ANAPOONA MAMBO YA UKOSEFU WA HAKI?

11. Mungu anajisikia namna gani anapoona (a) ukosefu wa haki? (b) namna tunavyoteseka?

11 Namna gani Mungu anajisikia leo anapoona mambo ya ukosefu wa haki yanayotendeka katika dunia na yanayokupata? Jambo la kwanza, jua kama Biblia inafundisha kuwa Mungu ni ‘mupenda-haki.’ (Zaburi 37:28) Ndiyo sababu ameweka sheria juu ya mambo mazuri na mambo mabaya. Anachukia ukosefu wa haki wa kila namna. Hapo zamani, dunia ilipojaa na mambo mabaya, Biblia inasema Mungu ‘aliumia moyoni mwake.’ (Mwanzo 6:5, 6) Mungu hakubadilika. (Malaki 3:6) Hata leo anachukia kuona namna ulimwengu muzima unavyoteseka. Tena Mungu anachukia kuona namna watu wanavyoteseka. Biblia inasema “yeye [anawahangaikia] ninyi.”​—1 Petro 5:7.

Biblia inafundisha kama upendo ndio uliomusukuma Yehova aumbe ulimwengu

12, 13. (a) Sababu gani sisi wanadamu tuna sifa nzuri kama vile upendo, nao upendo unatufanya tujisikie namna gani tunapoona mambo ya ukosefu wa haki? (b) Sababu gani unapaswa kuwa hakika kama Mungu ataondoa kabisa mateso yanayowapata wanadamu?

12 Ni nini kinachotuhakikishia kama Mungu anachukia kuona namna watu wanavyoteseka? Tazama ushuhuda mwingine. Biblia inafundisha kama Mungu aliumba mutu kwa mufano wake. (Mwanzo 1:26) Kwa hiyo, sisi tuna sifa nzuri kwa sababu Mungu vilevile ana sifa nzuri. Kwa mufano, unapoona watu wasio na kosa wakiteseka, unajisikia vibaya, sivyo? Basi, ikiwa wewe unachukizwa na mambo hayo ya ukosefu wa haki, jua kama Mungu anachukizwa hata zaidi kuliko wewe.

13 Sisi wanadamu tuna uwezo wa kuonyesha upendo, na jambo hilo linatufanya tuwe tofauti na viumbe vingine hapa duniani. Sifa hiyo inaonyesha namna Mungu alivyo. Biblia inafundisha kuwa “Mungu ni upendo.” (1 Yohana 4:8) Sisi tuna upendo kwa sababu Mungu ana upendo. Kwa hiyo, upendo unaweza kukuchochea uondoe kabisa mateso na mambo ya ukosefu wa haki unayoona duniani, sivyo? Ikiwa ungekuwa na uwezo wa kuondoa mambo hayo yanayowatesa watu, ungeyaondoa, sivyo? Basi, ujue kama Mungu ataondoa kabisa mateso na mambo ya ukosefu wa haki. Ahadi zinazotajwa kwenye ukurasa wa 4 na wa 5 wa kitabu hiki si ndoto, wala si matumaini yasiyo na musingi. Hakika, ahadi za Mungu zitatimia! Hata hivyo, ili uamini ahadi hizo, unapaswa kwanza kumujua Mungu vizuri; yule Mungu aliyetoa ahadi hizo.

MUNGU ANAPENDA UMUJUE

Ikiwa ungependa mutu fulani akujue, ungependa kwanza ajue jina lako, sivyo? Mungu anatujulisha jina lake kupitia Biblia

14. Jina la Mungu ni nani, na sababu gani unapaswa kulitumia jina hilo?

14 Ikiwa ungependa mutu fulani akujue, ni jambo gani la kwanza ungependa ajue juu yako? Ungependa kwanza ajue jina lako, sivyo? Sasa wewe unajua jina la Mungu? Dini nyingi zinafundisha kama jina la Mungu ni “Mungu” ao “Bwana.” Lakini kati ya majina hayo hakuna jina lake la pekee. Majina hayo ni majina ya cheo tu ao ya heshima, kama vile jina “mufalme” na “raisi.” Biblia inafundisha kama Mungu ana majina mengi ya cheo. Lakini, inafundisha tena kama ana jina lake la pekee. Jina hilo ni Yehova. Andiko la Zaburi 83:18 linasema hivi: “Wewe, ambaye jina lako ni Yehova, wewe peke yako ndiye Uliye Juu Zaidi, juu ya dunia yote.” Ikiwa jina hilo halipatikani katika Biblia yako, unaweza kusoma Nyongeza kwenye ukurasa wa 195-197 wa kitabu hiki ili ujue sababu. Jambo unalopaswa kujua ni hili: katika maandishi ya kwanza-kwanza ya Biblia, jina hilo la Mungu linapatikana karibu mara 7 000. Hilo linaonyesha kama Yehova anapenda wewe ulijue jina lake na ulitumie. Tunaweza kusema Mungu anatumia Biblia ili kukujulisha jina lake.

15. Jina Yehova linamaanisha nini?

15 Mungu alijipatia jina lenye kuwa na maana sana. Jina Yehova linamaanisha Mungu anaweza kutimiza neno lote analoahidi na anaweza kutimiza kila jambo analopenda kufanya. * Hakuna jina lingine linalolingana na jina hilo, ni yeye tu anayestahili kuwa na jina hilo. Katika mambo mengi, Yehova hawezi kulinganishwa na mutu yeyote. Hilo linamaanisha nini?

16, 17. Majina ya cheo yafuatayo yanatufundisha nini juu ya Yehova? (a) “Mweza-Yote,” (b) ‘Mufalme wa umilele,’ (c) “Muumbaji.”

16 Tuliona kuwa andiko la Zaburi 83:18 linasema juu ya Yehova hivi: “Wewe peke yako ndiye Uliye Juu Zaidi.” Vilevile, ni Yehova peke yake anayeitwa “Mweza-Yote.” Andiko la Ufunuo 15:3 linasema hivi: ‘Matendo yako ni makubwa na ya ajabu, Yehova Mungu, Mweza-Yote. Njia zako ni za uadilifu na za kweli, Mufalme wa umilele.’ Jina la cheo “Mweza-Yote” linatufundisha kama Yehova ndiye mutu mwenye nguvu zaidi kuliko viumbe vyote. Nguvu zake ni nyingi sana, haziwezi kulinganishwa na nguvu za kiumbe chochote. Jina lake lingine la cheo ‘Mufalme wa umilele’ linatukumbusha jambo lingine linalomutofautisha kabisa Yehova na mutu yeyote. Ni yeye peke yake ndiye hana mwanzo. Andiko la Zaburi 90:2 linasema hivi: ‘Tangu wakati usio na kipimo mupaka wakati usio na kipimo [ao, milele] wewe ni Mungu.’ Maneno hayo yanatuchochea tumuheshimu sana, sivyo?

17 Pia, Yehova halinganishwi na mutu yeyote kwa sababu yeye tu ndiye Muumbaji. Andiko la Ufunuo 4:11 linasema hivi: “Unastahili, Ee Yehova, naam, Mungu wetu, kupokea utukufu na heshima na nguvu, kwa sababu uliumba vitu vyote, na kwa sababu ya mapenzi yako vilikuwako navyo vikaumbwa.” Kila kitu unachoweza kuwazia ao kuona​—iwe malaika walio mbinguni, iwe nyota zinazoonekana angani usiku, matunda juu ya miti, ao samaki walio katika bahari na katika mito, vyote hivyo vipo kwa sababu Yehova ndiye aliyeviumba!

UNAWEZA KUMUKARIBIA YEHOVA?

18. Sababu gani watu fulani wanawaza kama hawawezi kumukaribia Mungu, lakini Biblia inafundisha nini juu ya wazo hilo?

18 Watu fulani wanaposoma kama Yehova ana sifa za ajabu, wanaogopa sana. Wanawaza kama hawawezi kumukaribia Mungu kwa sababu yeye ni mukubwa sana, na wanawaza wao si kitu machoni pake. Unafikiri mawazo hayo ni sawa? Biblia haifundishi hivyo. Biblia inapozungumuza juu ya Yehova, inasema hivi: ‘Kweli, hayuko mbali sana na kila mumoja wetu.’ (Matendo 17:27) Kwanza Biblia yenyewe inatutia moyo kwa maneno haya: ‘Mukaribieni Mungu, naye atawakaribia ninyi.’​—Yakobo 4:8.

19. (a) Tunaweza kufanya nini ili tuanze kumukaribia Mungu, na tutapata faida gani? (b) Ni sifa gani za Mungu ambazo zinakuvutia sana?

19 Unaweza kufanya nini ili umukaribie Mungu? Jambo la kwanza, endelea kujifunza juu ya Mungu kama unavyofanya sasa. Yesu alisema hivi: ‘Uzima wa milele ndio huu, waendelee kupata ujuzi juu yako wewe, Mungu wa pekee wa kweli, na juu ya yule uliyemutuma, Yesu Kristo.’ (Yohana 17:3) Ni wazi, Biblia inafundisha kuwa kujifunza juu ya Yehova na Yesu kunaongoza kwenye “uzima wa milele”! Tumekwisha kuona kama “Mungu ni upendo.” (1 Yohana 4:16) Lakini Yehova ana sifa zingine nyingi nzuri zenye kuvutia. Kwa mufano, Biblia inasema kama Yehova ni ‘Mungu mwenye rehema na neema, si mwepesi wa hasira naye ni mwingi wa fazili zenye upendo na kweli.’ (Kutoka 34:6) Yeye ni ‘mwema na yuko tayari kusamehe.’ (Zaburi 86:5) Yeye ni Mungu muvumilivu. (2 Petro 3:9) Yeye ni mushikamanifu. (Ufunuo 15:4) Ukiendelea kusoma Biblia zaidi, utaona namna Yehova ameonyesha sifa hizo na sifa zingine nyingi zenye kuvutia.

20-22. (a) Kwa kuwa hatuwezi kumuona Mungu, je, hilo linamaanisha kuwa hatuwezi kumukaribia? Fasiria. (b) Watu fulani wanaweza kukuambia nini, lakini unapaswa kufanya nini?

20 Ni kweli, hauwezi kumuona Mungu kwa sababu yeye ni roho, na roho haiwezi kuonekana. (Yohana 1:18; 4:24; 1 Timotheo 1:17) Hata hivyo, kwa kujifunza Biblia, unaweza kujua namna Mungu alivyo na sifa zake. Kama mutunga-zaburi alivyosema, unaweza “kuuona uzuri wa Yehova.” (Zaburi 27:4; Waroma 1:20) Unapoendelea kujifunza juu ya Yehova, utaona kama yeye ni mutu kabisa anayeishi, na hilo litakufanya umupende zaidi na ujisikie kuwa unamukaribia zaidi.

Namna baba mwenye upendo anavyowapenda watoto wake ndivyo Baba yetu wa mbinguni anavyotupenda sana

21 Na hatua kwa hatua utajua sababu gani Biblia inatufundisha kama Yehova ni Baba yetu kweli. (Mathayo 6:9) Yeye ni Baba yetu kwa sababu alitupatia uzima na kwa sababu anataka tuwe na maisha mazuri zaidi, kama vile baba fulani mwenye upendo anavyotaka watoto wake wawe na maisha mazuri kila siku. (Zaburi 36:9) Tena, Biblia inatufundisha kama wanadamu wanaweza kuwa marafiki wa Yehova. (Yakobo 2:23) Wewe vilevile unaweza kuwa rafiki ya Muumbaji wa ulimwengu, ni jambo la ajabu, sivyo?

22 Unapoendelea kujifunza mambo mengi katika Biblia, labda watu fulani watakuambia uache kujifunza Biblia. Labda watu hao wanawaza kama wanafanya hivyo kwa faida yako. Labda wanaogopa kuwa unataka kubadilisha dini yako. Lakini, usiache mutu yeyote akuzuie kufanya urafiki na Mungu.

23, 24. (a) Sababu gani inakuomba kuendelea kuuliza maulizo juu ya mambo unayojifunza? (b) Sura ya 2 itazungumuzia habari gani?

23 Hakika, unapoanza kujifunza, kuna mambo ambayo hautaelewa vizuri. Lakini usiache haya ikuzuie kuuliza; inaomba kuwa na unyenyekevu ili kuuliza maulizo. Yesu alisema ni vizuri kuwa munyenyekevu kama mutoto mudogo. (Mathayo 18:2-4) Na kama tunavyojua, watoto wanauliza maulizo mengi. Mungu anapenda upate majibu ya maulizo yako. Biblia inazungumuza juu ya watu fulani ambao walikuwa na hamu sana ya kujifunza mambo ya Mungu, nayo inawasifu sana watu hao. Waliyachunguza Maandiko vizuri kabisa ili kuhakikisha kama mambo waliyokuwa wakijifunza ni ya kweli.​—Matendo 17:11.

24 Kuichunguza Biblia ndiyo njia nzuri zaidi ya kumujua Yehova. Biblia ni tofauti na vitabu vingine vyote. Namna gani? Sura ya 2itazungumuzia habari hiyo.

^ fu. 15 Katika Nyongeza kwenye ukurasa wa 195-197, utapata habari nyingi zinazoonyesha maana ya jina la Mungu na namna ya kulitamuka.