Ona video zinazopatikana

Ona habari zilizo ndani

SURA YA PILI

Biblia Ni Kitabu Kilichotoka kwa Mungu

Biblia Ni Kitabu Kilichotoka kwa Mungu
  • Ni mambo gani yanayotofautisha Biblia na vitabu vingine vyote?

  • Namna gani Biblia inaweza kukusaidia ujue namna ya kushindana na magumu yako?

  • Sababu gani unaweza kuaminia unabii mbalimbali ulio katika Biblia?

1, 2. Sababu gani Biblia ni zawadi yenye kufurahisha kabisa ambayo Mungu ametupatia?

JE, UNAKUMBUKA namna ulivyojisikia siku ile rafiki yako fulani alikupatia ao kukutumia zawadi nzuri? Hakika, ulichangamuka na kufurahi sana. Kwa kweli, rafiki anapokupatia ao kukutumia zawadi, inaonyesha kama anakuhangaikia na anafurahia urafiki wenu. Hakika, wewe pia ulimushukuru rafiki yako.

2 Biblia ni zawadi ya Mungu, na tunapaswa kumushukuru sana kwa zawadi hiyo. Biblia ni kitabu kilicho tofauti na vitabu vingine. Inatujulisha mambo ambayo hatungejua. Kwa mufano, inatuelezea namna dunia na mbingu zenye kujaa nyota viliumbwa, na namna mwanaume na mwanamuke wa kwanza waliumbwa. Kanuni za Biblia ni za kweli na zinaweza kumusaidia mutu ajue namna ya kushindana na magumu na mahangaiko ya maisha. Inatufasiria namna Mungu atatimiza kusudi lake na kufanya maisha yawe mazuri sana duniani. Kweli, Biblia ni zawadi yenye kufurahisha kabisa!

3. Kwa kuwa Yehova ametupatia Biblia, hilo linaonyesha nini, na sababu gani hilo ni jambo lenye kufurahisha sana?

3 Tena, Biblia ni zawadi yenye kufurahisha sana kwa sababu inatufundisha mambo fulani juu ya Mutoaji wa zawadi hiyo, yaani, Yehova Mungu. Kwa kuwa Yehova ametupatia Biblia, anapenda tumujue vizuri. Biblia inaweza kabisa kukusaidia umukaribie Yehova.

4. Sababu gani namna Biblia zinavyogawanywa ni jambo lenye kushangaza?

4 Ikiwa una Biblia, jua kama watu wengine pia wana kitabu hicho. Biblia inapatikana katika luga zaidi ya 2 500, yote nzima ao kwa sehemu; kwa hiyo watu wengi duniani wanaweza kuipata (zaidi ya 90%). Biblia zaidi ya milioni moja zinagawanywa kila juma! Mamilioni na mamilioni ya Biblia zimekwisha kuchapishwa, iwe yote nzima ao kwa sehemu. Kwa kweli, hakuna kitabu kingine kinacholingana na Biblia.

“Biblia Takatifu​—Tafsiri ya Ulimwengu Mpya” inapatikana katika luga nyingi

5. Ni katika maana gani Biblia ‘iliongozwa na roho ya Mungu’?

5 Jambo lingine ni hili: Biblia ‘imeongozwa na roho ya Mungu.’ (2 Timotheo 3:16) Maana yake nini? Biblia yenyewe inajibu hivi: “Wanadamu walisema yaliyotoka kwa Mungu kama walivyoongozwa na roho takatifu.” (2 Petro 1:21) Kwa mufano: Baba fulani anaweza kumuomba mutoto wake amuandikie barua. Mutoto huyo ataandika mawazo ya baba yake. Kwa hiyo, barua hiyo ni ya baba huyo wala si ya mutoto wake. Vilevile, habari iliyo katika Biblia ni ya Mungu, si ya watu walioiandika. Kwa hiyo, Biblia yote nzima ni “neno la Mungu.”​—1 Wathesalonike 2:13.

BIBLIA HAIDANGANYIKI, NA HAIJIPINGI

6, 7. Sababu gani namna Biblia nzima inavyopatana si jambo lenye kushangaza kabisa?

6 Biblia iliandikwa kwa muda wa miaka zaidi ya 1 600. Wale walioandika Biblia hawakuishi wote wakati mumoja wala hawakuwa wakifanya kazi moja. Kulikuwa walimaji wa mashamba, wavuaji wa samaki na wachungaji wa kondoo. Wamoja walikuwa manabii, wengine waamuzi na wengine wafalme. Luka, mumoja wa wale walioandika injili alikuwa muganga. Waandikaji hao walikuwa na maisha tofauti, lakini, mambo yote waliyoandika hayapingani. *

7 Kitabu cha kwanza cha Biblia kinatuelezea namna magumu ya wanadamu yalivyoanza. Na kitabu cha mwisho kinatuonyesha namna gani dunia nzima itakuwa paradiso. Sehemu zote za Biblia zinazungumuzia mambo yaliyotokea kwa maelfu ya miaka, na kila sehemu inatusaidia katika njia fulani kujua kusudi la Mungu ni nini na namna litakavyotimia. Namna Biblia nzima inavyopatana si jambo lenye kushangaza kabisa, inapatana hivyo kwa sababu ni kitabu kilichotoka kwa Mungu.

8. Ni nini inayoonyesha kama Biblia haidanganyiki inapozungumuzia mambo ya sayansi.

8 Inapozungumuzia mambo ya sayansi, Biblia haidanganyiki. Inazungumuzia hata mambo ambayo watu wamekuja kuvumbua kisha miaka mingi. Kwa mufano, kitabu cha Walawi kina sheria ambazo Waisraeli walipewa juu ya usafi na kuwatenga watu wenye magonjwa ya kuambukiza; lakini, wakati huo mataifa jirani hayakujua mambo hayo. Huko zamani Biblia ilikuwa imekwisha kusema kama dunia ina umbo la muviringo; lakini wakati huo watu walikuwa na mawazo tofauti. (Isaya 40:22) Tena, Biblia ilisema kama dunia ‘imetundikwa pasipo na kitu.’ (Ayubu 26:7) Kwa kweli, Biblia si kitabu cha sayansi. Lakini, inapozungumuzia mambo ya sayansi, haidanganyiki; kwa sababu ni kitabu kilichotoka kwa Mungu, sivyo?

9. (a) Namna gani Biblia yenyewe inaonyesha kama haidanganyiki juu ya mambo ya historia, na kama ina habari zilizo kweli? (b) Waandikaji wa Biblia waliandika hata makosa yao, jambo hilo linatufundisha nini juu ya Biblia?

9 Vilevile Biblia inapozungumuzia mambo ya historia haidanganyiki, ina habari za kweli; si mambo ya kuwazia-wazia tu. Kwa mufano, inapotaja majina ya watu inaonyesha pia kizazi chao. * Mara nyingi wanahistoria hawaandiki kushindwa kwa mataifa yao; lakini waandikaji wa Biblia hawakuwa wakificha ukweli, waliandika hata makosa yao wenyewe na makosa ya taifa lao. Tuchukue mufano wa Musa, aliyeandika kitabu cha Hesabu. Yeye mwenyewe aliandika kosa kubwa alilofanya na azabu kali aliyopata kwa sababu ya kosa lake. (Hesabu 20:2-12) Katika vitabu vingine, ni vigumu mutu kusema makosa yake hivyo. Lakini habari kama hiyo inapatikana katika Biblia kwa sababu ni kitabu kilichotoka kwa Mungu.

NI KITABU CHENYE MASHAURI YA HEKIMA

10. Biblia ni kitabu chenye mashauri ya hekima, sababu gani jambo hilo halipaswi kutushangaza?

10 Kwa sababu Biblia iliongozwa na roho ya Mungu, ina ‘faida ili kufundisha, kukaripia, kunyoosha mambo.’ (2 Timotheo 3:16) Kwa kweli, Biblia ni kitabu chenye mashauri ya hekima. Inazungumuzia hali na tabia zetu. Hilo si jambo la kushangaza, kwa kuwa Yehova Mungu, aliyeandikisha Biblia, ndiye pia Muumbaji! Yeye anatujua kupita namna tunavyojijua, anajua sana mawazo yetu na namna tunavyojisikia. Tena anajua ni nini inayoweza kutuletea furaha, na mambo tunayopaswa kuepuka.

11, 12. (a) Ni mambo gani Yesu alifundisha katika Mahubiri yake ya Mulimani? (b) Biblia inazungumuzia pia mambo gani ya lazima, na sababu gani mashauri yake ni yenye faida sikuzote?

11 Tuchukue mufano wa mafundisho ya Yesu yanayoitwa Mahubiri ya Mulimani yanayopatikana katika Mathayo sura ya 5 mupaka ya 7. Katika mafundisho hayo ya ajabu, Yesu alifundisha mambo mengi; kama vile namna ya kupata furaha ya kweli, namna ya kusikilizana na wengine matatizo yanapotokea, namna ya kusali, na namna ya kuwa na maoni mazuri juu ya vitu vya kimwili. Maneno ya Yesu yaliwachochea watu waliomusikiliza na yaliwasaidia; leo pia yanafanya hivyo.

12 Katika Biblia muna kanuni juu ya maisha ya familia, mazoea ya kazi, na namna ya kuishi pamoja na wengine. Kanuni za Biblia ni kwa ajili ya kila mutu, na mashauri yake ni yenye faida sikuzote. Maneno ambayo Mungu alisema kupitia nabii wake Isaya, yanaonyesha kwa kifupi hekima ya Biblia, alisema hivi: “Mimi, Yehova, ni Mungu wako, Yeye anayekufundisha ili ujifaidi mwenyewe.”​—Isaya 48:17.

NI KITABU CHA UNABII

Isaya, mumoja kati ya waandikaji wa Biblia, alitabiri kuanguka kwa Babiloni

13. Yehova alimutuma nabii Isaya aandike habari gani juu ya uharibifu wa Babiloni?

13 Biblia ina unabii mbalimbali, unabii mwingine umekwisha kutimia. Kwa mufano: Miaka zaidi ya 700 mbele ya kuja kwa Yesu, Yehova alimutuma nabii Isaya kutabiri uharibifu wa Babiloni. (Isaya 13:19; 14:22, 23) Alitoa maelezo mengi ili kuonyesha namna uharibifu huo ungetokea. Alitabiri kama majeshi ya askari yatakausha maji ya muto wa Babiloni na kuingia bila hata kupigana. Si hayo tu. Unabii ulitaja hata jina la mufalme atakayechukua muji wa Babiloni, yaani, Sirise [ao Koreshi].​—Isaya 44:27–45:2.

14, 15. Namna gani mambo mengine ambayo nabii Isaya alitabiri ao kusema mbele ya wakati yalitimia?

14 Kisha miaka 200 hivi, mwezi wa kumi, usiku wa tarehe 5/6, 539 mbele ya kuzaliwa kwa Yesu, jeshi la askari lilitia kambi karibu na Babiloni. Ni nani aliyeongoza jeshi hilo? Ni Sirise, mufalme wa Perse ao Uajemi. Kwa hiyo, mambo yote yalikuwa tayari ili unabii huo wa ajabu utimie. Lakini unabii ulisema mbele ya wakati kama jeshi la Sirise litachukua muji wa Babiloni bila kupigana, je, jambo hilo lilifanyika hivyo?

15 Usiku huo, watu wa Babiloni walikuwa na karamu ya sikukuu; waliwaza hakuna jambo lolote linaloweza kuwapata kwa kuwa muji wa Babiloni ulizungukwa na kuta kubwa. Wakati huo, Sirise alifanya muto wa maji uliokuwa ukipita kati ya muji uchukue njia nyingine. Maji yalipunguka sana na maaskari wake walivuka na kukaribia kuta za muji. Sasa, namna gani maaskari hao wangeingia katika muji huo wenye kuta kubwa? Usiku huo, kwa sababu isiyojulikana, walinzi walisahau kufunga milango ya muji!

16. (a) Nabii Isaya alitabiri kama mwisho wa Babiloni utakuwa namna gani? (b) Je, jambo hilo lilitimia?

16 Nabii Isaya alitabiri tena juu ya Babiloni hivi: ‘Hatakaliwa kamwe, wala hatakuwa na makao kwa kizazi baada ya kizazi. Na hapo Muarabu hatapiga hema lake, na hakuna wachungaji watakaoruhusu makundi yao kulala hapo.’ (Isaya 13:20) Unabii huo ulisema mbele ya wakati mambo ambayo yangetokea kisha kuanguka kwa muji wa Babiloni. Ulisema hakuna mutu atakayekaa katika muji wa Babiloni, milele na milele. Unaweza kujionea utimizo wa maneno hayo. Katika inchi ya Irak, mahali ambapo muji wa Babiloni ulipatikana zamani, kilometa 80 hivi kusini mwa Baghdad, hakuna mutu anayeishi huko. Hilo linaonyesha wazi kama yale Yehova alisema yalitimia, Yeye alisema hivi: ‘Nami nitamufagia kwa ufagio wa maangamizi.’​—Isaya 14:22, 23. *

Magofu ya Babiloni

17. Namna gani kutimia kwa unabii wa Biblia kunafanya imani yetu iwe na nguvu?

17 Kujua kama Biblia ni kitabu cha unabii unaotimia kabisa kunafanya imani yetu iwe na nguvu, sivyo? Kwa kuwa wakati wa zamani Yehova Mungu alitimiza ahadi zake, tunaamini kabisa kama atatimiza tena ahadi yake ya kuifanya dunia iwe paradiso. (Hesabu 23:19) Kwa kweli, tuna ‘tumaini la uzima wa milele ambao Mungu, asiyeweza kusema uongo, aliahidi nyakati za zamani za kale.’​—Tito 1:2. *

“NENO LA MUNGU LIKO HAI”

18. Mutume Paulo anasema maneno gani ya lazima sana juu ya “neno la Mungu”?

18 Mambo ambayo tumejifunza katika sura hii yanaonyesha kweli kabisa kama Biblia ni kitabu kilicho tofauti na vitabu vingine. Lakini si mambo hayo tu yanayofanya Biblia iwe ya lazima sana. Mutume Paulo alionyesha jambo lingine linalofanya Biblia iwe kitabu cha pekee; alisema hivi: “Neno la Mungu liko hai nalo lina nguvu na ni lenye makali zaidi kuliko upanga wowote wenye makali kuwili nalo huchoma hata kufikia kugawanya nafsi na roho, na viungo na urojorojo wake, nalo linaweza kutambua fikira na makusudio ya moyo.”​—Waebrania 4:12.

19, 20. (a) Unapaswa kufanya nini ili Biblia ikusaidie kujichunguza vizuri? (b) Namna gani unaweza kuonyesha kama unapendezwa na zawadi hiyo ya Mungu, yaani, Biblia?

19 Kusoma “neno” la Mungu kunaweza kubadilisha maisha yetu. Kunaweza kutusaidia tujichunguze tena vizuri. Tunaweza kusema kama tunamupenda Mungu, lakini namna tutatenda kisha kusikia yale ambayo Biblia inafundisha, ndio itaonyesha ni nini iliyo katika mawazo yetu na moyo wetu.

20 Kwa kweli, Biblia ni kitabu kilichotoka kwa Mungu. Kwa hiyo, tunapaswa kusoma, kujifunza, na kupenda Biblia. Onyesha kama unapendezwa na zawadi hiyo ya Mungu kwa kuendelea kujifunza habari zilizo ndani. Kwa kufanya hivyo, utajua vizuri zaidi kusudi la Mungu juu ya wanadamu. Katika sura inayofuata tutazungumuzia kusudi hilo na namna litakavyotimia.

^ fu. 6 Watu wengine wanasema kama sehemu fulani za Biblia zinapingana, lakini hawana ushuhuda wowote ili kuhakikisha mawazo yao. Soma kitabu Biblia​Neno la Mungu au la Binadamu? sura ya 7, kilichochapishwa na Mashahidi wa Yehova.

^ fu. 9 Soma pia Luka 3:23-38, inaonyesha wazi kizazi cha Yesu.

^ fu. 16 Unaweza kupata habari zaidi juu ya unabii wa Biblia katika broshua Kitabu kwa Ajili ya Watu Wote, ukurasa wa 27-29, iliyochapishwa na Mashahidi wa Yehova.

^ fu. 17 Kuharibiwa kwa Babiloni ni mufano mumoja tu kati ya unabii mbalimbali wa Biblia uliotimia. Mufano mwingine ni ule uharibifu wa muji wa Tiro na Ninawi. (Ezekieli 26:1-5; Sefania 2:13-15) Nabii Danieli alitabiri pia namna serikali kubwa zenye kutawala dunia zingefuatana kisha serikali ya Babiloni kuanguka. Alitaja pia serikali ya muungano wa Wamedi na Waperesi na Ugiriki. (Danieli 8:5-7, 20-22) Ili kupata habari zaidi juu ya unabii mbalimbali unaozungumuzia Masiya Yesu Kristo, soma Nyongeza iliyo kwenye ukurasa wa 199-201.