Hamia kwenye habari

Hamia kwenye yaliyomo

SURA YA SITA

Wafu Wako Wapi?

Wafu Wako Wapi?
  • Inakuwaje tunapokufa?

  • Kwa nini tunakufa?

  • Je, ingefariji kujua ukweli kuhusu kifo?

1-3. Watu huuliza maswali gani kuhusu kifo, na dini mbalimbali huyajibuje?

WATU wameuliza maswali haya kwa maelfu ya miaka. Ni maswali muhimu. Hata tuwe nani au tunaishi wapi, tungependa kupata majibu ya maswali hayo.

2 Katika Sura ya 5, tulizungumzia jinsi dhabihu ya fidia ya Yesu Kristo ilivyofungua njia ya kupata uzima wa milele. Pia tulijifunza kwamba Biblia inatabiri kuhusu wakati ambapo “kifo hakitakuwapo tena.” (Ufunuo 21:4) Kwa sasa, sisi sote tunakufa. Mfalme Sulemani mwenye hekima alisema: “Walio hai wanajua kwamba watakufa.” (Mhubiri 9:5) Sisi hujitahidi kuishi muda mrefu iwezekanavyo. Hata hivyo, tungependa kujua ni nini hutupata tunapokufa.

3 Sisi huomboleza wapendwa wetu wanapokufa. Huenda tukauliza: ‘Wameenda wapi? Je, wanateseka? Je, wanaweza kutusaidia? Je, tunaweza kuwasaidia? Je, tutawaona tena?’ Dini za ulimwengu hujibu maswali haya kwa njia tofauti-tofauti. Baadhi ya dini hizo hufundisha kwamba ukiishi maisha ya uadilifu, utaenda mbinguni lakini ikiwa unaishi maisha mabaya, utateketezwa motoni. Dini nyingine hufundisha kwamba watu wanapokufa huenda kuishi katika makao ya roho pamoja na mababu zao. Na nyingine hufundisha kwamba wafu huenda ahera wakahukumiwe kisha huzaliwa upya katika mwili mwingine.

4. Dini nyingi hufundisha jambo gani la msingi kuhusu kifo?

4 Dini zote hizo zinafundisha jambo moja la msingi, kwamba sehemu fulani ya mwanadamu huendelea kuishi baada ya mwili kufa. Karibu kila dini, za zamani na za sasa, husema kwamba sisi huendelea kuishi milele tukiwa na uwezo wa kuona, kusikia, na kufikiri. Hata hivyo, hilo linawezekanaje? Hisia zetu, pamoja na mawazo yetu, zinahusiana na jinsi ubongo wetu unavyofanya kazi. Ubongo huacha kufanya kazi mtu anapokufa. Kumbukumbu letu na hisia zetu haziendelei kufanya kazi baada ya ubongo kufa.

INAKUWAJE MTU ANAPOKUFA?

5, 6. Biblia hufundisha nini kuhusu hali ya wafu?

5 Yehova, Muumba wa ubongo anajua kinachotukia tunapokufa. Anajua ukweli na katika Neno lake, Biblia, anaeleza hali ya wafu. Biblia inafundisha hivi waziwazi: Mtu anapokufa, hayupo tena. Kifo ni kinyume cha uhai. Wafu hawaoni, hawasikii wala kufikiri. Hakuna sehemu yoyote ya mwili wetu inayoendelea kuishi baada ya mwili kufa. Hatuna nafsi au roho isiyoweza kufa. *

Moto huenda wapi unapozimika?

6 Baada ya Sulemani kutaja kwamba walio hai wanajua kwamba watakufa, aliandika hivi: “Lakini wafu, hawajui lolote kamwe.” Kisha akafafanua kweli hiyo ya msingi kwa kusema kwamba wafu hawawezi kupenda wala kuchukia na kwamba “hakuna kazi, wala utungaji wala ujuzi wala hekima katika Kaburi.” (Mhubiri 9:5, 6, 10) Vivyo hivyo, andiko la Zaburi 146:4 linasema kwamba mtu anapokufa, “mawazo yake hupotea.” Sisi hufa wala hatuendelei kuishi baada ya mwili kufa. Maisha yetu ni kama moto. Unapozimika, hauendi popote. Haupo tena.

MAMBO AMBAYO YESU ALIFUNDISHA KUHUSU KIFO

7. Yesu alifafanuaje kifo?

7 Yesu Kristo alizungumzia hali ya wafu rafiki yake Lazaro alipokufa. Yesu aliwaambia wanafunzi wake: “Lazaro rafiki yetu anapumzika.” Wanafunzi walifikiri Yesu anamaanisha kwamba Lazaro anapumzika katika usingizi kwa sababu ni mgonjwa. Walikosea. Yesu akawaambia: “Lazaro amekufa.” (Yohana 11:11-14) Ona kwamba Yesu alifananisha kifo na pumziko au usingizi. Lazaro hakuwa mbinguni wala motoni. Hakuwa akikutana na malaika wala mababu. Wala hakuwa akibadilika ili azaliwe tena akiwa mwanadamu mwingine. Alikuwa akipumzika katika kifo kana kwamba analala usingizi mzito usio na ndoto. Maandiko mengine pia hulinganisha kifo na usingizi. Kwa mfano, mwanafunzi Stefano alipouawa kwa kupigwa mawe, Biblia inasema kwamba ‘alilala usingizi.’ (Matendo 7:60) Hali kadhalika, mtume Paulo aliwataja watu fulani katika siku zake ambao walikuwa “wamelala usingizi” katika kifo.—1 Wakorintho 15:6.

Yehova aliwaumba wanadamu waishi milele duniani

8. Tunajuaje kwamba Mungu hakukusudia watu wafe?

8 Je, Mungu alikusudia watu wafe? Hapana! Yehova alimuumba mwanadamu aishi milele duniani. Kama tulivyojifunza mwanzoni mwa kitabu hiki, Mungu aliwaweka wanadamu wawili wa kwanza katika paradiso yenye kupendeza. Aliwapa afya kamilifu. Yehova aliwatakia mema. Je, kuna mzazi yeyote mwenye upendo anayetaka watoto wake wateseke kwa sababu ya uzee na kifo? Bila shaka hakuna! Yehova aliwapenda watoto wake na alitaka waishi milele kwa furaha duniani. Biblia inasema hivi kuwahusu wanadamu: “Wakati usio na kipimo [Yehova] ameuweka ndani ya moyo wao.” (Mhubiri 3:11) Mungu alituumba tukiwa na tamaa ya kuishi milele. Naye amepanga jinsi tamaa hiyo itakavyotimizwa.

KWA NINI WANADAMU HUFA?

9. Yehova alimkataza Adamu kufanya nini, na kwa nini haikuwa vigumu kutii amri hiyo?

9 Kwa nini basi wanadamu hufa? Ili kupata jibu, lazima tuzingatie kilichotukia kulipokuwa na mwanamume na mwanamke mmoja tu duniani. Biblia inaeleza: “Yehova Mungu akachipusha katika nchi kila mti wenye kutamanika kwa macho ya mtu na ulio mwema kwa ajili ya chakula.” (Mwanzo 2:9) Hata hivyo, alikatazwa kufanya jambo moja. Yehova alimwambia Adamu hivi: “Matunda ya kila mti wa bustani unaweza kula mpaka ushibe. Lakini kuhusu matunda ya mti wa ujuzi wa mema na mabaya usile, kwa maana siku utakapokula, utakufa hakika.” (Mwanzo 2:16, 17) Haikuwa vigumu kutii amri hiyo. Kulikuwa na miti mingine mingi ambayo Adamu na Hawa wangekula matunda yake. Lakini amri hiyo iliwapa nafasi ya pekee ya kuonyesha shukrani kwa Yule aliyewapa kila kitu, kutia ndani uhai mkamilifu. Utii wao ungeonyesha pia kwamba waliheshimu mamlaka ya Baba yao wa mbinguni na kwamba walitaka mwongozo wake wenye upendo.

10, 11. (a) Wenzi wa kwanza wa kibinadamu walikosaje kumtii Mungu? (b) Kwa nini kutotii kwa Adamu na Hawa kulikuwa jambo zito?

10 Inasikitisha kwamba wenzi hao wa kwanza wa kibinadamu waliamua kutomtii Yehova. Akiongea kupitia nyoka, Shetani alimuuliza Hawa hivi: “Je, ni kweli kwamba Mungu alisema msile matunda ya kila mti wa bustani?” Hawa akamjibu: “Tunaweza kula matunda ya miti ya bustani. Lakini kuhusu kula matunda ya mti ulio katikati ya bustani, Mungu amesema, ‘Msiyale, wala msiyaguse ili msife.’”—Mwanzo 3:1-3.

11 Shetani akamwambia: “Hakika hamtakufa. Mungu anajua kwamba siku ileile mtakapokula matunda yake macho yenu yatafunguliwa, nanyi mtakuwa kama Mungu, mkijua mema na mabaya.” (Mwanzo 3:4, 5) Shetani alitaka Hawa aamini kwamba angefaidika kwa kula tunda lililokatazwa. Kulingana na Shetani, Hawa angeweza kujiamulia lililo sawa na lililo kosa; angefanya atakalo. Shetani pia alidai kwamba Yehova alikuwa amesema uwongo kuhusu matokeo ya kula tunda. Hawa alimwamini Shetani. Kwa hiyo alichukua tunda hilo akala. Kisha akampa mumewe, naye pia akala. Hawakufanya hivyo kwa kutojua. Walijua kwamba walikuwa wakifanya kile ambacho Mungu aliwaambia wasifanye. Kwa kula tunda hilo, walikosa kutii kimakusudi amri rahisi na isiyodai mengi. Walimdharau Baba yao wa mbinguni na mamlaka yake. Hawakuwa na sababu ya kutomheshimu Muumba wao mwenye upendo!

12. Ni nini kinachoweza kutusaidia kuelewa jinsi Yehova alivyohisi wakati Adamu na Hawa walipomwasi?

12 Kwa mfano: Ungehisije kama ungemlea na kumtunza mwana au binti ambaye angekataa kukutii na hivyo kuonyesha kwamba hakuheshimu wala hakupendi? Ungehisi uchungu moyoni. Wazia uchungu ambao Yehova alihisi wakati Adamu na Hawa walipomwasi.

Adamu alitoka mavumbini, naye alirudi mavumbini

13. Yehova alisema ingekuwaje kwa Adamu wakati wa kifo, na hilo linamaanisha nini?

13 Yehova hakuwa na sababu ya kuwaacha Adamu na Hawa wasiomtii waendelee kuishi milele. Walikufa kama Yehova alivyokuwa amesema. Adamu na Hawa wakakoma kuwapo. Hawakuendelea kuishi mahali pengine wakiwa viumbe wa roho. Tunajua hivyo kwa sababu ya yale ambayo Yehova alimwambia Adamu baada ya kuzungumza naye kuhusu uasi wake. Mungu alisema: ‘Utarudi katika udongo, kwa kuwa ulitolewa katika huo. Kwa maana wewe ni mavumbi nawe utarudi mavumbini.’ (Mwanzo 3:19) Mungu alimuumba Adamu kutokana na mavumbi ya nchi. (Mwanzo 2:7) Kabla ya kuumbwa, Adamu hakuwapo. Kwa hiyo, Yehova aliposema kwamba Adamu angerudi mavumbini, alimaanisha kwamba Adamu hangekuwapo tena. Adamu hangekuwa na uhai kama vile mavumbi yaliyotumiwa kumuumba yasivyo na uhai.

14. Kwa nini tunakufa?

14 Adamu na Hawa wangekuwa hai leo, lakini walikufa kwa sababu waliamua kutomtii Mungu na hivyo wakafanya dhambi. Tunakufa kwa sababu wazao wote wa Adamu wamerithi dhambi na kifo kutoka kwake. (Waroma 5:12) Dhambi hiyo ni kama ugonjwa mbaya sana uliorithiwa, ambao hakuna anayeweza kuuepuka. Kifo kinachosababishwa na dhambi ni laana. Kifo ni adui wala si rafiki. (1 Wakorintho 15:26) Tunapaswa kumshukuru Yehova sana kwa sababu ameandaa fidia ili kutuokoa kutokana na adui huyu mwenye kutisha!

KUNA FAIDA KUJUA UKWELI KUHUSU KIFO

15. Kwa nini inafariji kujua ukweli kuhusu hali ya wafu?

15 Mambo ambayo Biblia inafundisha kuhusu hali ya wafu yanafariji. Kama ambavyo tumeona, wafu hawahisi maumivu wala uchungu. Hatuna sababu ya kuwaogopa wafu kwani hawawezi kutuumiza. Hawahitaji msaada wetu wala hawawezi kutusaidia. Hatuwezi kuzungumza nao. Viongozi wengi wa kidini hudai kwamba wanaweza kuwasaidia wafu, na watu wanaowaamini huwapa pesa. Lakini kujua ukweli kuhusu hali ya wafu hutulinda tusidanganywe na wale wanaofundisha uwongo.

16. Ni nani anayeongoza mafundisho ya dini nyingi, na kwa njia gani?

16 Je, dini nyingi hukubali mafundisho ya Biblia kuhusu hali ya wafu? Nyingi hazikubali. Kwa nini? Kwa sababu mafundisho yao yanaongozwa na Shetani. Anatumia dini ya uwongo ili kuwafanya watu waamini kwamba baada ya miili yao kufa, wataendelea kuishi katika makao ya roho. Huo ni uwongo ambao Shetani anatumia pamoja na mambo mengine ya uwongo ili kuwafanya watu wamwache Yehova Mungu. Anafanyaje hivyo?

17. Kwa nini fundisho la mateso ya milele halimletei Yehova heshima?

17 Kama tulivyoona, dini fulani hufundisha kwamba mtu akiishi maisha mabaya, baada ya kifo ataenda motoni ili ateseke milele. Fundisho hilo halimletei Mungu heshima. Yehova ni Mungu mwenye upendo na hawezi kamwe kuwatesa watu hivyo. (1 Yohana 4:8) Wewe ungeonaje ikiwa mtu angemtia nidhamu mtoto asiyetii kwa kuishikilia mikono yake motoni ili aungue? Je, unaweza kumheshimu mtu huyo? Je, kweli hata ungetaka kumjua? Hapana hata kidogo! Inaelekea utamwona kuwa mkatili sana. Shetani anataka tuamini kwamba Yehova huwatesa watu motoni milele—kwa mabilioni ya miaka!

18. Kuwaabudu wafu kunategemea uwongo gani wa dini?

18 Pia Shetani hutumia dini fulani kufundisha kwamba baada ya watu kufa wao wanakuwa viumbe wa roho ambao wanapaswa kuheshimiwa na walio hai. Kulingana na fundisho hilo, roho za wafu zinaweza kuwa rafiki wazuri au adui wenye kuogopesha. Watu wengi wanaamini uwongo huo. Wanawaogopa wafu, wanawaheshimu, na kuwaabudu. Kinyume cha hilo, Biblia inafundisha kwamba wafu wanalala na kwamba tunapaswa kumwabudu tu Mungu wa kweli, Yehova, Mpaji na Muumba wetu.—Ufunuo 4:11.

19. Kujua ukweli kuhusu kifo hukusaidia kuelewa fundisho gani lingine la Biblia?

19 Kujua ukweli kuhusu wafu hukulinda usidanganywe na uwongo wa dini. Pia hukusaidia kuelewa mafundisho mengine ya Biblia. Kwa mfano, unapojua kwamba watu wanapokufa hawaendi katika makao ya roho, ahadi ya uzima wa milele katika paradiso duniani inakuwa na maana zaidi kwako.

20. Tutazungumzia swali gani katika sura inayofuata?

20 Zamani, mwanamume mwadilifu Ayubu, aliuliza swali hili: “Mtu akifa, je, anaweza kuishi tena?” (Ayubu 14:14) Je, mtu asiye na uhai anayelala usingizi katika kifo anaweza kufufuliwa? Biblia inafundisha jambo lenye kufariji sana kama tutakavyoona katika sura inayofuata.

^ fu. 5 Unaweza kupata habari zaidi kuhusu “nafsi” na “roho” katika nyongeza “Maneno “Nafsi“ na “Roho“ Yanamaanisha Nini?