Ona video zinazopatikana

Ona habari zilizo ndani

SURA YA SABA

Tumaini la Kweli juu ya Watu Tuliowapenda Waliokufa

Tumaini la Kweli juu ya Watu Tuliowapenda Waliokufa
  • Namna gani tunajua kama ufufuo ni jambo litakalofanyika kweli?

  • Nini inayoonyesha kama Yehova anatamani kweli kuwafufua watu waliokufa?

  • Ni nani watakaofufuliwa?

1-3. Ni adui gani anayetufuata sisi wote, na sababu gani kujifunza mambo Biblia inayofundisha kunatuliza moyo?

WAZIA unamukimbia adui fulani anayetaka kukuua. Anakushinda sana nguvu na mbio. Unajua kama hana huruma kwa kuwa umekwisha kuona namna aliua marafiki wako fulani. Unakimbia kadiri uwezavyo, lakini yeye anaendelea kukukaribia. Inaonekana hauna tena tumaini. Lakini, bila kutazamia, unaona mutu fulani anatokea ili kukuokoa. Mutu huyo ni mwenye nguvu sana kuliko adui yako, naye anakuambia kama atakusaidia. Utasikia moyo unatulia kabisa, sivyo?

2 Tunaweza kusema vilevile kama adui asiye na huruma kama huyo anakufuata. Anatufuata sisi wote. Kama tulivyojifunza katika Sura ya 6, Biblia inasema kama kifo ni adui. Hakuna mwanadamu anayeweza kuepuka ao kushindana na kifo. Wengi kati yetu tumekwisha kuona namna adui huyo alivyowaua watu tuliowapenda. Lakini, Yehova ana nguvu sana kuliko kifo. Yeye ndiye Mutu mwenye upendo anayetaka kutuokoa, na ameonyesha kama ana nguvu za kushinda adui huyo. Pia, anaahidi kumuharibu kabisa adui huyo milele. Biblia inafundisha hivi: “Adui wa mwisho atakayeangamizwa ni kifo.” (1 Wakorintho 15:26) Hiyo ni habari njema kabisa!

3 Acha tuzungumuzie kwanza namna tunavyojisikia wakati kifo kinapomuchukua mutu tunayemupenda. Kufanya hivyo kutatusaidia tuelewe ahadi fulani itakayotufurahisha sana. Ndiyo, Yehova anaahidi kama watu waliokufa wataishi tena. (Isaya 26:19) Atawarudisha kwenye uzima tena. Ahadi hiyo ndilo tumaini la ufufuo.

WAKATI MUTU UNAYEMUPENDA ANAPOKUFA

4. (a) Yesu alisikia uchungu wa kufiwa, jambo hilo linatufundisha nini juu ya namna Yehova anavyojisikia mutu anapokufa? (b) Ni nani waliokuwa marafiki wa pekee wa Yesu?

4 Je, umekwisha kufiwa? Mutu anapofiwa anaweza kuwa na uchungu sana, huzuni na kujisikia kuwa anaishiwa kabisa. Wakati kama huo, tuna lazima ya kufarijiwa; tunaweza kufarijiwa kupitia Neno la Mungu. (2 Wakorintho 1:3, 4) Biblia inatusaidia tuelewe namna Yehova na Yesu wanavyojisikia mutu anapokufa. Yesu alionyesha kabisa sifa za Baba yake, na kuna habari zinazoonyesha kama alielewa uchungu wa kufiwa. (Yohana 14:9) Yesu alipokuwa akienda Yerusalemu, alikuwa akitembelea sana Lazaro na dada zake, Maria na Martha; ambao waliishi Bethania, karibu na Yerusalemu. Kwa kweli, walikuwa marafiki sana. Biblia inasema: ‘Yesu alimupenda Martha na dada yake na pia Lazaro.’ (Yohana 11:5) Lakini, kama tulivyoona katika Sura ya 6, Lazaro alikufa.

5, 6. (a) Yesu alijisikia namna gani alipoona ndugu na rafiki za Lazaro wakimulilia Lazaro? (b) Kwa nini kujua kama Yesu alisikia uchungu na huzuni ya kufiwa kunatutia moyo?

5 Yesu alijisikia namna gani rafiki yake alipokufa? Biblia inasema kama Yesu alienda mahali ndugu na rafiki za Lazaro walipokuwa wakimulilia Lazaro. Yesu alipowaona, alisikia huzuni sana. Biblia inasema: “Akaugua rohoni na kutaabika . . . akatokwa na machozi.” (Yohana 11:33, 35) Je, kwa kuwa Yesu alisikia huzuni, hilo linamaanisha kama hakuwa na tumaini? Hapana. Yesu alijua vizuri kama jambo fulani la ajabu lilikuwa karibu kutokea. (Yohana 11:3, 4) Hata hivyo, alisikia uchungu na huzuni ya kufiwa.

6 Kujua kama Yesu alisikia uchungu na huzuni ya kufiwa kunatutia moyo. Hilo linatufundisha kama Yesu na Baba yake, Yehova, wanachukia kifo. Lakini, Yehova ana uwezo wa kumupiga adui huyo na kumushinda! Acha sasa tuone kile Yesu alitimiza kutokana na nguvu ambazo Mungu alimutolea.

‘LAZARO, KUJA HUKU INJE!’

7, 8. Kwa nini kwa mawazo ya watu waliokuwa hapo, hakukuwa tena tumaini lolote juu ya Lazaro, lakini Yesu alifanya nini?

7 Lazaro alikuwa amezikwa katika kaburi. Yesu akaomba waondoe jiwe walilokuwa wametia kwenye mulango wa kaburi. Martha alipinga, kwa sababu kisha siku ine mwili wa Lazaro ulipaswa kuwa umeanza kuoza. (Yohana 11:39) Kwa mawazo ya watu, hakukuwa tena tumaini lolote.

Ufufuo wa Lazaro ulifurahisha watu sana.​—Yohana 11:38-44

8 Waliliondoa lile jiwe, na Yesu akapaza sauti: ‘Lazaro, kuja huku inje!’ Ni jambo gani lililotokea? ‘Huyo mutu aliyekuwa mufu akatoka.’ (Yohana 11:43, 44) Watu waliokuwa hapo walisikia furaha sana, sivyo? Walijua vizuri kama Lazaro, mudogo yao, ndugu yao, rafiki yao, jirani yao, alikuwa amekufa. Lakini sasa, yule mutu waliyemupenda alikuwa hapo, akisimama kati yao. Labda waliona hilo kuwa ndoto tu. Hakika, wengi wao walimukumbatia Lazaro kwa furaha kabisa. Kwa kweli, Yehova alishinda kifo!

Eliya alifufua mutoto wa mujane.​—1 Wafalme 17:17-24

9, 10. (a) Namna gani Yesu alionyesha kama hakumufufua Lazaro kwa nguvu zake mwenyewe? (b) Ni faida gani tunazoweza kupata ikiwa tunasoma habari za ufufuo katika Biblia?

9 Yesu hakujivuna kwa kusema alifanya muujiza huo kwa nguvu zake mwenyewe. Katika sala aliyofanya mbele ya kumufufua Lazaro, Yesu alionyesha waziwazi kama ni Yehova ndiye aliyemupa nguvu ya kumufufua Lazaro. (Yohana 11:41, 42) Hiyo haikuwa mara ya kwanza kwa Yehova kutumia nguvu zake ili kufufua mutu. Ufufuo wa Lazaro ni moja kati ya miujiza kenda ya ufufuo inayozungumuziwa katika Neno la Mungu, Biblia. * Kusoma na kujifunza miujiza hiyo kunafurahisha sana. Inatufundisha kama Mungu hana ubaguzi; kwa sababu kati ya wale waliofufuliwa kulikuwa vijana na watu waliokomaa, wanaume na wanawake, Waisraeli na watu wasio Waisraeli. Habari hizo zinaonyesha furaha kubwa ambayo watu walisikia. Kwa mufano, Yesu alipomufufua kijana mwanamuke, wazazi wake ‘walikuwa na shangwe kubwa.’ (Marko 5:42) Kwa kweli, Yehova aliwafanyia jambo ambalo liliwafurahisha sana na ambalo hawangesahau katika maisha yao yote.

Mutume Petro alimufufua mwanamuke Mukristo aliyeitwa Dorkasi.​—Matendo 9:36-42

10 Ni kweli, wale watu waliofufuliwa na Yesu walikufa tena. Je, hilo linamaanisha kama haikuwa lazima kuwafufua? Hapana. Habari hizo za Biblia zinasadikisha mafundisho mengine ya kweli ya lazima na zinatupatia tumaini.

HABARI ZA UFUFUO ZINATUFUNDISHA NINI?

11. Namna gani habari ya ufufuo wa Lazaro inaonyesha ukweli wa Mhubiri 9:5?

11 Biblia inafundisha kama watu waliokufa “hawajui lolote kamwe.” Hawaendelei kuishi mahali fulani na hawajui jambo lolote. Habari ya Lazaro inahakikisha ukweli huo. Lazaro alipofufuliwa, je, aliwafurahisha watu kwa kuwaelezea kama aliona mambo fulani mbinguni? Ao je, aliwaogopesha kwa kuwaelezea mambo yenye kutisha ya moto wa mateso? Hapana. Biblia haisemi Lazaro alielezea watu mambo kama hayo. Muda wa siku ine alizokuwa amekufa ‘hakujua lolote.’ (Mhubiri 9:5) Lazaro alikuwa mwenye kulala usingizi kabisa katika kifo.​—Yohana 11:11.

12. Sababu gani tunaweza kuamini kama Lazaro alifufuliwa kweli?

12 Habari ya Lazaro inatufundisha pia kama ufufuo ni jambo la kweli, wala si hadisi tu. Yesu hakumufufua Lazaro kwa uficho; watu wengi walikuwa hapo na walijionea wenyewe jambo hilo. Hata viongozi wa dini waliomuchukia Yesu hawakupinga kama muujiza huo umefanyika. Kwanza walisema: ‘Tufanye nini, kwa sababu mutu huyu [Yesu] anafanya ishara nyingi?’ (Yohana 11:47) Watu wengi walienda kumuona Lazaro aliyefufuliwa. Kwa hiyo, wengi zaidi kati yao walimuamini Yesu. Waliona Lazaro kuwa ushuhuda ulio wazi ulioonyesha kama Yesu alikuwa ametumwa na Mungu. Ushuhuda huo ulikuwa wenye nguvu sana; kwa hiyo, viongozi fulani wa dini ya Kiyahudi wenye mioyo migumu walifanya mipango ya kumuua Yesu na Lazaro.​—Yohana 11:53; 12:9-11.

13. Kwa nini tuamini kama Yehova anaweza kuwafufua watu waliokufa?

13 Je, kuamini kama watu wanaweza kufufuliwa ni ndoto tu? Hapana. Yesu alifundisha kama siku fulani ‘wale wote walio ndani ya makaburi’ watafufuliwa. (Yohana 5:28) Yehova ndiye Muumbaji wa uzima wote. Basi, si vigumu kuamini kama anaweza kuumba uzima tena. Ili afanye hivyo, inaomba asiwasahau wale waliokufa. Je, anaweza kuwakumbuka watu tuliowapenda waliokufa? Angani kuna nyota nyingi zisizohesabika, lakini Mungu anaita kila nyota kwa jina! (Isaya 40:26) Kwa hiyo, Yehova Mungu anaweza kukumbuka kila jambo juu ya watu waliokufa, na ana uwezo wa kuwafufua.

14, 15. Ayubu alisema nini ili kuonyesha kama Yehova anatamani sana kuwafufua watu waliokufa?

14 Hata hivyo, ni nini inayoonyesha kama Yehova anatamani kweli kuwafufua watu waliokufa? Biblia inafundisha kama ana tamaa kabisa ya kufanya hivyo. Ayubu, aliyekuwa mwanaume mwaminifu, aliuliza hivi: ‘Mutu akifa, je, anaweza kuishi tena?’ Ayubu alikuwa akisema kama atangojea katika kaburi mupaka wakati Mungu atakapomukumbuka. Alimuambia Yehova: “Utaita, na mimi mwenyewe nitakujibu. Kwa kuwa utaitamani sana kazi ya mikono yako.”​—Ayubu 14:13-15.

15 Wazia jambo hilo! Yehova anatamani sana kuwafufua watu waliokufa. Kujua kama Yehova anatamani sana kufanya hivyo kunafurahisha moyo sana, sivyo? Sasa ufufuo wenyewe utakuwa namna gani? Ni nani watakaofufuliwa, na watafufuliwa ili waishi wapi?

‘WOTE WALIO NDANI YA MAKABURI YA UKUMBUSHO’

16. Watu watakaofufuliwa wataishi katika hali gani?

16 Habari za Biblia za watu waliofufuliwa zinatusaidia kujua mambo mengi juu ya ufufuo wa wakati ujao. Watu waliofufuliwa walikutana tena na ndugu na marafiki wao. Itakuwa hivyo pia wakati wa ufufuo ujao​—lakini hali itakuwa nzuri zaidi. Kama tulivyojifunza katika Sura ya 3, Mungu anakusudia dunia nzima iwe paradiso. Kwa hiyo, watu watafufuliwa na kuishi katika dunia isiyo na vita, mauaji, na magonjwa. Wataishi milele katika dunia hii; katika hali ya amani na furaha.

17. Ni nani watakaofufuliwa?

17 Ni nani watakaofufuliwa? Yesu alisema kama wale ‘wote walio ndani ya makaburi ya ukumbusho wataisikia sauti yake [Yesu] na watatoka.’ (Yohana 5:28, 29) Tena Ufunuo 20:13 inasema hivi: “Bahari ikawatoa wale wafu waliokuwa ndani yake, na kifo na Kaburi [“Hadesi,” maelezo ya chini] vikawatoa wale wafu waliokuwa ndani yake.” Hadesi ni kaburi. (Soma Nyongeza, ukurasa wa 212-213.) Kaburi hilo litabaki bila kitu. Mamilioni ya watu wanaopumuzika humo wataishi tena. Mutume Paulo alisema hivi: “Kutakuwa na ufufuo wa waadilifu na wasio waadilifu pia.” (Matendo 24:15) Maana yake nini?

Katika Paradiso, watu waliokufa watafufuliwa na watakutana tena na ndugu na marafiki zao

18. Watu “waadilifu” watakaofufuliwa ni nani, na tumaini hilo linaweza kukusaidia namna gani katika maisha yako?

18 Kati ya watu “waadilifu” muna watu wengi walioishi mbele ya Yesu kuja duniani, ambao Biblia inazungumuzia. Wazia Noa, Abrahamu, Sara, Musa, Ruthu, Esta, na wengine wengi. Kitabu cha Waebrania sura ya 11 kinazungumuzia wanaume na wanawake fulani wenye imani walio kati ya “waadilifu” hao. Lakini, watumishi wa Yehova wanaokufa leo, wao pia wamo kati ya “waadilifu” hao. Kwa sababu tuna tumaini la ufufuo sisi hatuogopi tena kufa.​—Waebrania 2:15.

19. Watu “wasio waadilifu” ni nani, na kwa wema wake, Yehova atawapatia nafasi ya kufanya nini?

19 Sasa itakuwa namna gani juu ya wale wote ambao hawakumutumikia Yehova wala kumutii kwa sababu hawakupata nafasi ya kumujua? Mungu hatasahau mamilioni ya watu hao “wasio waadilifu.” Wao pia watafufuliwa na kupewa nafasi ya kujifunza juu ya Mungu wa kweli na kumutumikia. Katika kipindi cha miaka elfu moja, watu waliokufa watafufuliwa na kupewa nafasi ya kumutumikia Yehova hapa duniani pamoja na wanadamu wengine waaminifu. Kitakuwa kipindi cha ajabu sana. Biblia inaita kipindi hicho Siku ya Hukumu. *

20. Gehena ni nini, na ni nani wanaoenda humo?

20 Je, hilo linamaanisha kama mwanadamu yeyote aliyekufa atafufuliwa? Hapana. Biblia inasema kuna watu fulani waliokufa ambao wamo katika “Gehena.” (Luka 12:5) Gehena lilikuwa bonde la takataka lililokuwa inje ya muji wa kale wa Yerusalemu. Katika bonde hilo walikuwa wakiunguza mizoga na takataka ya muji. Maiti za watu ambao Wayahudi waliona kuwa hawastahili kuzikwa wala kufufuliwa zilitupwa humo. Kwa hiyo, Gehena inaonyesha vizuri kabisa uharibifu wa milele. Hata ikiwa Yesu ndiye atahukumu watu walio wazima na watu waliokufa, Yehova ndiye Mwamuzi Mukubwa. (Matendo 10:42) Hatawafufua hata kidogo watu ambao ni wabaya na wasiotaka kufanya mabadiliko.

UFUFUO ILI KUISHI MBINGUNI

21, 22. (a) Kuna ufufuo wa aina gani nyingine? (b) Ni nani mutu wa kwanza kabisa kufufuliwa na mwili wa kiroho?

21 Biblia inazungumuzia pia ufufuo wa aina nyingine; ufufuo huo unamufanya mwanadamu awe kiumbe cha kiroho ili kuishi mbinguni. Biblia inazungumuzia mutu mumoja tu aliyefufuliwa hivyo, ni Yesu Kristo.

22 Yesu aliuawa na kuzikwa, lakini Yehova hakumuacha mwana Wake mwaminifu abaki katika kaburi milele. (Zaburi 16:10; Matendo 13:34, 35) Mungu alimufufua Yesu, lakini si katika mwili wa kibinadamu. Mutume Petro anaeleza kama Kristo “aliuawa katika mwili, lakini akafanywa kuwa hai katika roho.” (1 Petro 3:18) Huo ulikuwa muujiza wa ajabu. Yesu alikuwa tena muzima, alifanywa tena kiumbe cha kiroho mwenye nguvu! (1 Wakorintho 15:3-6) Yesu ndiye mutu wa kwanza kabisa kufufuliwa hivyo, huo ulikuwa ufufuo wenye utukufu. (Yohana 3:13) Lakini, kulipaswa kuwa na watu wengine.

23, 24. Ni nani walio ‘kundi ndogo’ la Yesu, na ni wangapi?

23 Kwa kuwa Yesu alijua kama kisha muda mufupi atarudi mbinguni, aliwaambia wanafunzi wake waaminifu kama ataenda ‘kuwatayarishia mahali’ huko. (Yohana 14:2) Hao watakaoenda mbinguni, Yesu aliwaita ‘kundi ndogo.’ (Luka 12:32) Ni Wakristo wangapi waaminifu walio katika kundi hilo ndogo? Katika Ufunuo 14:1, mutume Yohana anasema hivi: ‘Nami nikaona, na, tazama! Mwana-Kondoo [Yesu Kristo] amesimama juu ya Mulima Sayuni, na pamoja naye 144 000 wakiwa na jina lake na jina la Baba yake limeandikwa juu ya mapaji ya nyuso zao.’

24 Mitume waaminifu wa Yesu wako kati ya Wakristo hao 144 000 wanaofufuliwa ili kuishi mbinguni. Wanaanza kufufuliwa wakati gani? Mutume Paulo aliandika kama wangeanza kufufuliwa wakati wa kuwapo kwa Kristo. (1 Wakorintho 15:23) Tutakapojifunza Sura ya 9, utaona kama tunaishi katika kipindi hicho cha wakati. Kwa hiyo, wachache kati ya wale 144 000 ambao bado wapo hapa duniani, mumoja wao akifa, mara moja anafufuliwa na kwenda kuishi mbinguni. (1 Wakorintho 15:51-55) Hata hivyo, watu wengi wana tumaini la kufufuliwa na kuishi katika Paradiso hapa duniani.

25. Tutajifunza nini katika sura inayofuata?

25 Hakika, Yehova atamushinda adui yetu kifo; atakiondoa milele! (Isaya 25:8) Lakini, unaweza kujiuliza, ‘Wale wanaofufuliwa na kwenda mbinguni watafanya kazi gani huko?’ Watakuwa katika serikali nzuri ya Ufalme huko mbinguni. Katika sura inayofuata, tutajifunza mengi juu ya serikali hiyo.

^ fu. 19 Juu ya Siku ya Hukumu na mambo ambayo Mungu atafuatilia ili kuhukumu watu, soma mafasirio zaidi katika Nyongeza, ukurasa wa 213-215.