Hamia kwenye habari

Hamia kwenye yaliyomo

SURA YA NANE

Ufalme wa Mungu Ni Nini?

Ufalme wa Mungu Ni Nini?
  • Biblia inatufundisha nini kuhusu Ufalme wa Mungu?

  • Ufalme wa Mungu utafanya nini?

  • Ufalme huo utatimiza mapenzi ya Mungu duniani wakati gani?

1. Tutazungumzia sala gani inayojulikana sana?

MAMILIONI ya watu ulimwenguni wanajua sala ambayo wengi huiita Sala ya Baba Yetu, au Sala ya Bwana. Majina hayo mawili yanarejelea ile sala inayojulikana sana ambayo Yesu Kristo mwenyewe aliitoa kama kielelezo. Ni sala yenye maana sana, na kuchunguza mambo matatu ya kwanza katika sala hiyo kutakusaidia kujua mambo mengi ambayo Biblia inafundisha.

2. Ni mambo gani matatu ambayo Yesu aliwafundisha wanafunzi wake waombe?

2 Mwanzoni mwa sala hiyo ya kielelezo, Yesu aliwafundisha wasikilizaji wake hivi: “Basi, ninyi msali hivi: ‘Baba yetu uliye mbinguni, jina lako na litakaswe. Ufalme wako na uje. Mapenzi yako na yatendeke duniani kama ilivyo mbinguni.’” (Mathayo 6:9-13) Mambo hayo matatu yanayoombwa yanamaanisha nini?

3. Tunahitaji kujua nini kuhusu Ufalme wa Mungu?

3 Tayari tumejifunza mengi kuhusu jina la Mungu, Yehova. Na kwa kadiri fulani tumezungumzia mapenzi ya Mungu, yaani, mambo ambayo amefanya na yale atakayowafanyia wanadamu. Hata hivyo, Yesu alimaanisha nini alipotuambia tusali: “Ufalme wako uje”? Ufalme wa Mungu ni nini? Ufalme huo utakapokuja, utalitakasaje jina la Mungu au kulifanya liwe takatifu? Na kuja kwa Ufalme huo kunahusianaje na kutendeka kwa mapenzi ya Mungu?

UFALME WA MUNGU NI NINI?

4. Ufalme wa Mungu ni nini, na Mfalme wake ni nani?

4 Ufalme wa Mungu ni serikali iliyosimamishwa na Yehova Mungu ikiwa na Mfalme ambaye amechaguliwa na Mungu. Mfalme wa Ufalme wa Mungu ni nani? Ni Yesu Kristo. Yesu akiwa Mfalme, ni mkuu kuliko watawala wa kibinadamu na anaitwa “Mfalme wa wale wanaotawala wakiwa wafalme na Bwana wa wale wanaotawala wakiwa mabwana.” (1 Timotheo 6:15) Ana nguvu za kufanya mambo mengi mazuri kuliko mtawala yeyote wa kibinadamu, hata yule aliye bora zaidi.

5. Ufalme wa Mungu unatawala kutoka wapi, nao utatawala nini?

5 Ufalme wa Mungu utatawala kutoka wapi? Kwani, Yesu yuko wapi? Unakumbuka, tulijifunza kwamba aliuawa kwenye mti wa mateso, na baadaye akafufuliwa. Muda mfupi baadaye, alirudi mbinguni. (Matendo 2:33) Kwa hiyo, huko ndiko Ufalme wa Mungu uliko, yaani, mbinguni. Ndiyo sababu Biblia huuita ‘ufalme wa mbinguni.’ (2 Timotheo 4:18) Ingawa Ufalme wa Mungu uko mbinguni, utatawala dunia.—Ufunuo 11:15.

6, 7. Kwa nini Yesu ni Mfalme wa pekee?

6 Kwa nini Yesu ni Mfalme wa pekee? Sababu moja ni kwamba, hatakufa kamwe. Ikimlinganisha na wafalme wa kibinadamu, Biblia inamwita Yesu “yeye peke yake asiyeweza kufa, anayekaa katika nuru isiyoweza kufikiwa.” (1 Timotheo 6:16) Hilo linamaanisha kwamba mambo yote mazuri ambayo Yesu atafanya yatadumu. Naye kwa kweli atafanya mambo mengi mazuri.

7 Hebu fikiria unabii huu wa Biblia kumhusu Yesu: “Roho ya Yehova itatua juu yake, roho ya hekima na ya uelewaji, roho ya shauri na ya nguvu, roho ya ujuzi na ya kumwogopa Yehova; naye atakuwa na shangwe katika kumwogopa Yehova. Na hatahukumu kulingana na sura inayoonekana kwa macho yake tu, wala kukaripia kulingana tu na jambo lililosikiwa na masikio yake. Naye atawahukumu kwa uadilifu watu wa hali ya chini, atakaripia kwa unyoofu kwa ajili ya watu wapole wa dunia.” (Isaya 11:2-4) Maneno hayo yanaonyesha kwamba Yesu atakuwa Mfalme mwadilifu na mwenye huruma atakayetawala watu wa dunia. Je, ungependa kuwa na mtawala kama huyo?

8. Ni nani watakaotawala pamoja na Yesu?

8 Jambo lingine kuhusu Ufalme wa Mungu ni kwamba Yesu hatatawala akiwa peke yake. Atatawala pamoja na wengine. Kwa mfano, mtume Paulo alimwambia Timotheo hivi: “Tukiendelea kuvumilia, tutatawala pamoja pia tukiwa wafalme.” (2 Timotheo 2:12) Naam, Paulo, Timotheo, na waaminifu wengine ambao wamechaguliwa na Mungu watatawala pamoja na Yesu katika Ufalme wa mbinguni. Ni wangapi watakaokuwa na pendeleo hilo?

9. Ni watu wangapi watakaotawala pamoja na Yesu, na Mungu alianza kuwachagua lini?

9 Kama tulivyoona katika Sura ya 7 ya kitabu hiki, mtume Yohana aliona katika maono “Mwana-Kondoo [Yesu Kristo] amesimama juu ya Mlima Sayuni [akiwa mfalme mbinguni], na pamoja naye 144,000 wakiwa na jina lake na jina la Baba yake limeandikwa juu ya mapaji ya nyuso zao.” Hao 144,000 ni nani? Yohana mwenyewe anatuambia hivi: “Hao ndio wale wanaoendelea kumfuata Mwana-Kondoo popote anapoenda. Hao walinunuliwa kutoka kati ya wanadamu wakiwa matunda ya kwanza kwa Mungu na kwa Mwana-Kondoo.” (Ufunuo 14:1, 4) Ndiyo, ni wafuasi waaminifu wa Yesu Kristo waliochaguliwa hasa kutawala mbinguni pamoja naye. Baada ya kufufuliwa na kuenda mbinguni, “watatawala wakiwa wafalme juu ya dunia,” pamoja na Yesu. (Ufunuo 5:10) Tangu siku za mitume, Mungu amekuwa akiwachagua Wakristo waaminifu ili kukamilisha idadi hiyo ya 144,000.

10. Kwa nini ni mpango wa upendo kwa Yesu na wale 144,000 waliofufuliwa kuwatawala wanadamu?

10 Mungu alionyesha upendo kwa kufanya mpango ili Yesu na wale 144,000 wawatawale wanadamu. Kwanza, Yesu amewahi kuwa mwanadamu na kuteseka. Paulo alisema kwamba Yesu “si mtu ambaye hawezi kuusikitikia udhaifu wetu, bali yeye ambaye amejaribiwa katika mambo yote kama sisi wenyewe, lakini bila kuwa na dhambi.” (Waebrania 4:15; 5:8) Watawala wenzake pia wameteseka na kuvumilia wakiwa wanadamu. Isitoshe, wamepambana na kutokamilika na kukabiliana na magonjwa ya aina mbalimbali. Bila shaka, wataelewa matatizo yanayowakabili wanadamu!

UFALME WA MUNGU UTAFANYA NINI?

11. Kwa nini Yesu aliwaambia wanafunzi wake waombe mapenzi ya Mungu yatendeke mbinguni?

11 Yesu alipowaambia wanafunzi wake waombe Ufalme wa Mungu uje, aliwaambia pia waombe mapenzi ya Mungu yatendeke “duniani kama ilivyo mbinguni.” Mungu yuko mbinguni, na sikuzote malaika waaminifu wamekuwa wakitenda mapenzi yake huko. Hata hivyo, katika Sura ya 3 ya kitabu hiki, tulijifunza kwamba malaika mwovu aliacha kutenda mapenzi ya Mungu na kuwafanya Adamu na Hawa watende dhambi. Katika Sura ya 10, tutajifunza mengi zaidi kuhusu yale ambayo Biblia inafundisha kumhusu malaika huyo mwovu, anayeitwa Shetani Ibilisi. Shetani na malaika walioamua kumfuata, wanaoitwa roho waovu, waliruhusiwa kuishi mbinguni kwa muda. Kwa hiyo, si wote waliokuwa mbinguni walikuwa wakitenda mapenzi ya Mungu. Mambo yangebadilika wakati Ufalme wa Mungu ungeanza kutawala. Mfalme mpya aliyetawazwa, Yesu Kristo, angepigana vita na Shetani.—Ufunuo 12:7-9.

12. Ni mambo gani mawili muhimu yanayotajwa katika Ufunuo 12:10?

12 Maneno yafuatayo ya kinabii yanaeleza jambo ambalo lingetukia: “Nikaisikia sauti kubwa mbinguni ikisema: ‘Sasa kumekuwa na wokovu na nguvu na ufalme wa Mungu wetu na mamlaka ya Kristo wake, kwa sababu [Shetani] mshtaki wa ndugu zetu ametupwa chini, anayewashtaki mchana na usiku mbele za Mungu wetu!’” (Ufunuo 12:10) Je, unaona mambo mawili muhimu yanayotajwa katika mstari huo wa Biblia? Kwanza, Ufalme wa Mungu unaanza kutawala Yesu Kristo akiwa Mfalme. Pili, Shetani anatupwa duniani kutoka mbinguni.

13. Hali imekuwaje baada ya Shetani kutupwa kutoka mbinguni?

13 Mambo hayo mawili yamekuwa na matokeo gani? Kuhusu mambo yaliyotokea mbinguni tunasoma hivi: “Kwa sababu hiyo furahini, enyi mbingu nanyi mnaokaa ndani yake!” (Ufunuo 12:12) Ndiyo, malaika waaminifu walio mbinguni wanafurahi kwa sababu baada ya Shetani na malaika zake kuondolewa, wote walio mbinguni ni waaminifu kwa Yehova Mungu. Kuna amani na upatano kamili wenye kudumu. Mapenzi ya Mungu yanatendeka mbinguni.

Kutupwa kwa Shetani na roho wake waovu kutoka mbinguni kulileta ole duniani. Matatizo hayo yatakwisha karibuni

14. Hali imekuwaje tangu Shetani alipotupwa duniani?

14 Hata hivyo, namna gani duniani? Biblia inasema: “Ole wa dunia na wa bahari, kwa sababu Ibilisi ameshuka kwenu, akiwa na hasira kali, akijua kwamba ana kipindi kifupi cha wakati.” (Ufunuo 12:12) Shetani ana hasira kwa sababu ametupwa kutoka mbinguni na ana kipindi kifupi tu cha wakati. Kwa hasira anasababisha dhiki, au “ole” duniani. Tutajifunza mengi zaidi kuhusu “ole” hiyo katika sura inayofuata. Hata hivyo, kwa kuwa Shetani ametupwa duniani na anasababisha dhiki, tunaweza kuuliza, Ufalme huo utafanyaje mapenzi ya Mungu yatendeke duniani?

15. Mapenzi ya Mungu kwa dunia ni nini?

15 Kumbuka mapenzi ya Mungu kwa dunia. Ulijifunza kuyahusu katika Sura ya 3. Katika Edeni, Mungu alionyesha kwamba mapenzi yake ni kwamba dunia iwe paradiso iliyojaa jamii ya wanadamu waadilifu na wasiokufa. Shetani aliwafanya Adamu na Hawa watende dhambi, na hilo likachelewesha kutimia kwa mapenzi ya Mungu duniani, lakini kusudi lake halikubadilika. Bado Yehova anakusudia kwamba “waadilifu wenyewe wataimiliki dunia, nao watakaa milele juu yake.” (Zaburi 37:29) Na Ufalme wa Mungu utatimiza hayo. Jinsi gani?

16, 17. Andiko la Danieli 2:44 linasema nini kuhusu Ufalme wa Mungu?

16 Hebu fikiria unabii ulio kwenye Danieli 2:44. Tunasoma: “Katika siku za wafalme hao, Mungu wa mbinguni atausimamisha ufalme ambao hautaharibiwa kamwe. Na ufalme huo hautapewa watu wengine wowote. Utazivunja na kuzikomesha falme hizi zote, nao utasimama mpaka wakati usio na kipimo.” Hilo linatuambia nini kuhusu Ufalme wa Mungu?

17 Kwanza, Ufalme wa Mungu ungesimamishwa “katika siku za wafalme hao,” au wakati falme nyingine zingekuwa zikitawala bado. Pili, Ufalme huo utadumu milele. Hautashindwa wala serikali nyingine haitachukua mahali pake. Tatu, tunaona kwamba kutakuwa na vita kati ya Ufalme wa Mungu na falme za ulimwengu huu. Ufalme wa Mungu utashinda. Hatimaye, Ufalme wa Mungu ndio utakaokuwa serikali pekee inayowatawala wanadamu. Kisha wanadamu watafurahia utawala bora zaidi.

18. Vita vya mwisho kati ya Ufalme wa Mungu na serikali za wanadamu vinaitwaje?

18 Biblia inasema mengi kuhusu vita vya mwisho kati ya Ufalme wa Mungu na serikali za ulimwengu huu. Kwa mfano, inafundisha kwamba mwisho unapokaribia, roho waovu wataeneza uwongo ili kuwadanganya “wafalme wa dunia nzima inayokaliwa.” Kwa kusudi gani? “Ili kuwakusanya [wafalme hao] pamoja kwa vita vya ile siku kuu ya Mungu Mweza-Yote.” Wafalme wa dunia watakusanywa pamoja “mahali panapoitwa katika Kiebrania Har–Magedoni.” (Ufunuo 16:14, 16) Kwa sababu ya mambo yanayotajwa katika mistari hiyo miwili, vita vya mwisho kati ya serikali za wanadamu na Ufalme wa Mungu vinaitwa vita vya Har–Magedoni.

19, 20. Kwa nini mapenzi ya Mungu hayatendeki duniani sasa?

19 Ufalme wa Mungu utatimiza nini kupitia Har–Magedoni? Fikiria tena mapenzi ya Mungu kwa dunia. Yehova Mungu alikusudia dunia ijae jamii ya wanadamu waadilifu na wakamilifu wakimtumikia katika Paradiso. Kwa nini hilo halitendeki sasa? Kwanza, sisi ni watenda dhambi na tunakuwa wagonjwa na kufa. Hata hivyo, tulijifunza katika Sura ya 5 kwamba Yesu alikufa kwa ajili yetu ili tuweze kuishi milele. Huenda unakumbuka maneno haya yaliyo katika Injili ya Yohana: “Mungu aliupenda ulimwengu sana hivi kwamba akamtoa Mwana wake mzaliwa-pekee, ili kila mtu anayemwamini asiangamizwe bali awe na uzima wa milele.”—Yohana 3:16.

20 Tatizo lingine ni kwamba watu wengi hutenda maovu. Wanasema uwongo, wanaiba, na kujihusisha katika ukosefu wa maadili. Hawataki kutenda mapenzi ya Mungu. Watu wanaotenda maovu wataharibiwa katika vita vya Mungu vya Har–Magedoni. (Zaburi 37:10) Sababu nyingine pia inayofanya mapenzi ya Mungu yasitendeke duniani ni kwamba serikali haziwatii moyo watu wafanye hivyo. Serikali nyingi hazina uwezo, ni katili, au ni zenye ufisadi. Biblia husema hivi waziwazi: “Mwanadamu amemtawala mwanadamu kwa kumuumiza.”—Mhubiri 8:9.

21. Ufalme utatendaje mapenzi ya Mungu duniani?

21 Baada ya Har–Magedoni, wanadamu watakuwa chini ya serikali moja tu, Ufalme wa Mungu. Ufalme huo utatenda mapenzi ya Mungu na kuleta baraka nzuri ajabu. Kwa mfano, utamwondoa Shetani na roho wake waovu. (Ufunuo 20:1-3) Nguvu za dhabihu ya Yesu zitatumiwa ili kuwaondolea wanadamu waaminifu magonjwa na kifo. Nao wataishi milele chini ya utawala wa Ufalme. (Ufunuo 22:1-3) Dunia itafanywa kuwa paradiso. Hivyo, Ufalme huo utafanya mpenzi ya Mungu yatendeke duniani na utalitakasa jina la Mungu. Hilo linamaanisha nini? Hilo linamaanisha kwamba hatimaye chini ya Ufalme wa Mungu kila mtu aliye hai atalitukuza jina la Yehova.

UFALME WA MUNGU UTACHUKUA HATUA WAKATI GANI?

22. Tunajuaje kwamba Ufalme wa Mungu haukuja Yesu alipokuwa duniani au baada tu ya yeye kufufuliwa?

22 Yesu alipowaambia wanafunzi wake wasali, “Acha Ufalme wako uje,” ilikuwa wazi kwamba Ufalme huo haukuwa umekuja. Je, ulikuja Yesu alipopaa kuenda mbinguni? Hapana, kwa kuwa Petro na Paulo walisema kwamba baada ya Yesu kufufuliwa, unabii huu katika Zaburi 110:1 ulitimizwa: “Neno la Yehova kwa Bwana wangu ni: ‘Keti kwenye mkono wangu wa kuume mpaka niwaweke adui zako kuwa kiti cha miguu yako.’” (Matendo 2:32-34; Waebrania 10:12, 13) Kulikuwa na kipindi cha kungoja.

Chini ya utawala wa Ufalme, mapenzi ya Mungu yatatendeka duniani kama ilivyo mbinguni

23. (a) Ufalme wa Mungu ulianza kutawala lini? (b) Sura ifuatayo itazungumzia nini?

23 Kipindi hicho cha kungoja kingeendelea kwa muda gani? Katika karne ya 19, wanafunzi wanyoofu wa Biblia walikadiria kwamba kipindi hicho kingefikia mwisho mwaka wa 1914. (Kuhusu tarehe hiyo, ona nyongeza “1914—Mwaka Muhimu Katika Unabii wa Biblia.”) Matukio ya ulimwengu yaliyoanza mwaka wa 1914 yanathibitisha kwamba kadirio hilo la wanafunzi wanyoofu wa Biblia lilikuwa sahihi. Utimizo wa unabii wa Biblia unaonyesha kwamba katika mwaka wa 1914, Kristo alitawazwa kuwa Mfalme, kisha Ufalme wa mbinguni wa Mungu ukaanza kutawala. Hivyo, tunaishi katika kile “kipindi kifupi cha wakati” kinachobaki cha Shetani. (Ufunuo 12:12; Zaburi 110:2) Tunaweza pia kusema kwa hakika kwamba hivi karibuni Ufalme wa Mungu utachukua hatua ili mapenzi ya Mungu yatendeke duniani. Je, hiyo ni habari njema kwako? Je, unaamini kwamba inawezekana? Sura ifuatayo itakusaidia kuona kwamba Biblia inafundisha mambo haya.