Ona video zinazopatikana

Ona habari zilizo ndani

SURA YA KENDA

Tunaishi Kweli Katika “Siku za Mwisho”?

Tunaishi Kweli Katika “Siku za Mwisho”?
  • Ni mambo gani Biblia ilisema zamani yanayotokea leo?

  • Biblia ilisema watu watakuwa na tabia gani katika “siku za mwisho”?

  • Ni mambo gani mazuri ambayo Biblia ilisema zamani juu ya “siku za mwisho”?

1. Ni nini inayoweza kutujulisha mambo yatakayotokea wakati ujao?

LABDA siku fulani uliangalia televizyo ao kusikia habari kwenye radio na kujiuliza ikiwa dunia hii inaenda wapi. Misiba inatokea kwa kushitukia na bila kutazamiwa, ni vigumu kujua ya kesho. (Yakobo 4:14) Lakini, Yehova yeye anajua mambo yatakayotokea kesho. (Isaya 46:10) Tangu zamani, Biblia, Neno lake, ilijulisha mambo mabaya yanayotokea siku zetu, lakini ilijulisha pia mambo mazuri yatakayotokea hivi karibuni.

2, 3. Wanafunzi wa Yesu walimuuliza ulizo gani, naye aliwapa jibu gani?

2 Yesu Kristo alifundisha kuwa Ufalme wa Mungu ndio utamaliza mambo yote mabaya na kufanya dunia iwe paradiso. (Luka 4:43) Watu walipenda kujua ni wakati gani Ufalme huo utakuja. Hata wanafunzi wake walimuuliza: ‘Ni nini itakayokuwa ishara ya kuwapo kwako na ya umalizio wa mufumo wa mambo?’ (Mathayo 24:3) Yesu aliwajibu kama ni Yehova Mungu peke yake ndiye anayejua kabisa ni wakati gani mwisho wa ulimwengu huu muovu utakuja. (Mathayo 24:36) Hata hivyo, Yesu alitabiri mambo ambayo yangetokea kwanza duniani mbele ya Ufalme wa Mungu kuwaletea wanadamu amani ya kweli na usalama wa kweli. Mambo ambayo Yesu alitabiri yanatokea siku za leo!

3 Mbele ya kuzungumuzia mambo yanayoonyesha kama tunaishi ‘umalizio wa mufumo wa mambo,’ acha tuzungumuzie kwanza kwa kifupi vita fulani iliyotokea mbinguni, na namna tunavyosumbuliwa na matokeo ya vita hiyo.

VITA INATOKEA MBINGUNI

4, 5. (a) Ni jambo gani lililofanyika mbinguni muda kidogo tu kisha Yesu kuwekwa kuwa Mufalme? (b) Kupatana na Ufunuo 12:12, vita hiyo ingekuwa na matokeo gani?

4 Katika Sura ya 8 tulijifunza kama Yesu Kristo aliwekwa kuwa Mufalme mbinguni katika mwaka wa 1914. (Danieli 7:13, 14) Kisha kupewa mamlaka ya Ufalme, muda kidogo baada ya hapo Yesu akaanza vita. Biblia inasema hivi: ‘Vita ikatokea gafula mbinguni. Mikaeli [jina lingine la Yesu] na malaika zake wakapigana na yule joka mukubwa [Shetani Ibilisi], naye joka mukubwa na malaika zake wakapigana.’ * Shetani na malaika zake, yaani mashetani, walishindwa katika vita hiyo, wakafukuzwa mbinguni na kutupwa duniani. Malaika waaminifu wa Mungu walifurahi kuona Shetani na mashetani wake wamefukuzwa mbinguni. Lakini wanadamu duniani hawangekuwa na furaha hiyo. Sababu gani? Biblia ilitabiri hivi: “Ole wa dunia . . . kwa sababu Ibilisi ameshuka kwenu, akiwa na hasira kali, akijua kwamba ana kipindi kifupi cha wakati.”​—Ufunuo 12:7, 9, 12.

5 Tafazali, acha tuzungumuzie matokeo ya vita hiyo iliyotokea mbinguni. Kwa sababu Shetani ana hasira kali, angeleta ole ao taabu duniani. Kama tutakavyoona, sasa tunaishi katika kipindi hicho cha taabu. Lakini kipindi hicho hakitakawia, ni “kipindi kifupi cha wakati.” Hata Shetani mwenyewe anajua hivyo. Biblia inaita kipindi hicho “siku za mwisho.” (2 Timotheo 3:1) Tunafurahi sana kujua kama karibuni Mungu ataondoa matatizo yote ambayo Ibilisi ameleta duniani, sivyo? Acha sasa tuchunguze mambo fulani ambayo Biblia ilisema tangu zamani na ambayo yanatendeka leo. Mambo hayo yanaonyesha kama tunaishi kweli katika siku za mwisho na karibuni Ufalme wa Mungu utawaletea wale wanaomupenda Yehova baraka za milele. Acha tuzungumuzie kwanza mambo ine ya alama ambayo Yesu alisema ingeonyesha kama tunaishi katika siku za mwisho.

MATUKIO MAKUBWA YA SIKU ZA MWISHO

6, 7. Namna gani maneno ya Yesu juu ya vita na upungufu wa chakula yanatimia leo?

6 “Taifa litasimama kupigana na taifa na ufalme kupigana na ufalme.” (Mathayo 24:7) Katika miaka 100 iliyopita, mamilioni ya watu wameuawa katika vita mbalimbali. Mwanahistoria mumoja Mwingereza aliandika hivi: ‘Watu wengi zaidi waliuawa katika miaka ya 1900 kuliko wakati mwingine wowote katika historia ya wanadamu. . . . Kilikuwa kipindi cha mufululizo wa vita. Kulikuwa na vipindi vifupi vya amani duniani, lakini vipindi hivyo vilikuwa vichache.’ Shirika la uchunguzi linaloitwa Worldwatch limeripoti hivi: “Hesabu ya watu waliokufa katika vita vya miaka ya 1901-2000 ilizidi mara tatu ile ya watu waliokufa katika vita vyote vilivyopiganwa tangu wakati wa Yesu Kristo mupaka mwaka wa 1899.” Tangu mwaka wa 1914 watu kupita milioni 100 wamekufa katika vita mbalimbali. Mamilioni ya watu wana uchungu na taabu sana kwa sababu wamepoteza ndugu ao rafiki katika vita. Labda wewe pia umekwisha kufikiwa na jambo hilo; kwa hiyo unaweza kuelewa namna watu hao wanavyojisikia.

7 “Kutakuwa na upungufu wa chakula.” (Mathayo 24:7) Watu wanaofanya uchunguzi wanasema kama miaka 30 iliyopita, chakula kimeongezeka sana. Hata hivyo, watu wanaendelea kukosa chakula kwa sababu wengi hawana feza za kutosha ili kununua chakula ao wanakosa mahali pa kulima mashamba. Katika inchi masikini, watu zaidi ya miliare moja ni masikini kabisa. Wengi wanateseka sana kwa sababu ya njaa. Shirika la Afya Ulimwenguni (OMS) linasema kama zaidi ya watoto milioni tano wanakufa kila mwaka kwa sababu ya kutokula vizuri.

8, 9. Ni nini inayoonyesha kama unabii wa Yesu juu ya matetemeko ya inchi na magonjwa ya kuambukiza unatimia?

8 ‘Kutakuwa na matetemeko makubwa ya inchi.’ (Luka 21:11) Shirika moja (The U.S. Geological Survey) limesema kama, kumekuwa na matetemeko ya inchi 19 hivi kila mwaka, ambayo yana nguvu za kutosha kubomoa kabisa majengo mengi na kupasua udongo. Na karibu kila mwaka kumekuwa na matetemeko ya inchi yenye nguvu za kutosha ili kuharibu kabisa majengo mbalimbali. Ripoti zenye kuaminika zinaonyesha kama tangu mwaka wa 1900 matetemeko ya inchi yamewaua watu zaidi ya milioni 2. Kitabu kimoja kinasema hivi: “Hata ikiwa kuna maendeleo ya kitekinolojia bado matetemeko ya inchi yanawaua watu wengi sana.”

9 ‘Kutakuwa na magonjwa ya kuambukiza.’ (Luka 21:11Habari Njema kwa Watu Wote) Ijapokuwa kuna maendeleo katika mambo ya kiganga, magonjwa ya zamani na mapya yanawashambulia wanadamu. Ripoti moja inasema kama magonjwa 20 yanayojulikana sana, kutia ndani kifua kikuu (tuberculose), malaria na kipindupindu (choléra), yameanza tena kuonekana katika miaka ya hivi karibuni, na dawa iliyopo haina nguvu tena ya kutunza aina fulani za magonjwa hayo. Tena, karibu magonjwa 30 mapya yametokea. Mengine kati ya magonjwa hayo hayana dawa na ni ya hatari kabisa.

TABIA ZA WATU KATIKA SIKU ZA MWISHO

10. Ni mambo gani yaliyotabiriwa katika 2 Timotheo 3:1-5 unayoona katika tabia za watu leo?

10 Biblia haisemi tu juu ya matukio makubwa yanayotokea duniani, lakini inasema pia kama watu hawatakuwa tena na tabia nzuri katika siku za mwisho. Mutume Paulo alieleza namna tabia za watu zingekuwa kwa ujumla. Katika 2 Timotheo 3:1-5, tunasoma hivi: ‘Katika siku za mwisho kutakuwa na nyakati za hatari zilizo ngumu kushugulika nazo.’ Kati ya mambo hayo, Paulo anasema watu watakuwa

  • wenye kujipenda wenyewe

  • wenye kupenda feza

  • wasiotii wazazi

  • wasio waaminifu

  • wasio na upendo wa asili

  • wasiojizuiza

  • wakali

  • wanaopenda raha kuliko Mungu

  • wenye namna ya kushikamana na Mungu lakini wanazikana nguvu zake

11. Kupatana na Zaburi 92:7, ni jambo gani litawapata watu wabaya?

11 Mahali unapoishi, watu wana tabia hizo? Hakika, wako hivyo. Watu walio na tabia hizo wako kila mahali. Hilo linaonyesha kama karibuni Mungu ataharibu watu hao wabaya, kwa kuwa Biblia inasema hivi: “Wakati waovu wanapochipuka kama majani na wote wanaotenda mambo yenye kuumiza wanapochanuka, ni ili wao wapate kuangamizwa milele.”​—Zaburi 92:7.

MAMBO MAZURI PIA YAMETOKEA!

12, 13. Je, “ujuzi wa kweli” umekuwa mwingi katika ‘wakati huu wa mwisho’ kama Biblia ilivyosema?

12 Ni wazi, siku za mwisho zimejaa taabu kama vile Biblia ilivyosema tangu zamani. Hata hivyo, katika dunia hii yenye matatizo, kuna mambo mazuri yanayotokea kati ya waabudu wa Yehova.

13 Nabii Danieli alitabiri hivi: “Ujuzi wa kweli utakuwa mwingi.” Hilo lingetimia wakati gani? “Wakati wa mwisho.” (Danieli 12:4) Hasa tangu mwaka wa 1914, Yehova amewasaidia wale wanaopenda kabisa kumutumikia wapate ujuzi zaidi wa Biblia. Wameelewa vizuri mafundisho ya kweli ya Biblia juu ya jina la Mungu na kusudi lake, zabihu ya ukombozi ambayo Yesu Kristo alitoa, hali ya watu waliokufa, na pia ufufuo. Zaidi ya hilo, waabudu wa Yehova wamejifunza namna ya kuwa na maisha yenye kuwaletea faida na kumuletea Mungu sifa. Wameelewa pia vizuri daraka la Ufalme wa Mungu na namna utakavyofanya mambo yawe mazuri duniani. Namna gani wanatumia ujuzi huo? Ulizo hilo linatukumbusha unabii mwingine ambao unatimia katika siku hizi za mwisho.

“Habari njema ya Ufalme itahubiriwa katika dunia yote inayokaliwa.”​—Mathayo 24:14

14. Leo, habari njema inahubiriwa katika inchi ngapi na luga ngapi, na ni nani wanaoihubiri?

14 Yesu alipozungumuzia ‘umalizio wa mufumo wa mambo,’ alitabiri hivi: “Habari njema ya ufalme itahubiriwa katika dunia yote inayokaliwa.” (Mathayo 24:3, 14) Duniani pote habari njema ya Ufalme inahubiriwa katika inchi zaidi ya 235 na katika luga zaidi ya 500. Watu wanajulishwa Ufalme huo ni nini, utafanya nini na yale tunapaswa kufanya ili kupata baraka zake. Mamilioni ya Mashahidi wa Yehova wanahubiri kwa bidii habari njema ya ufalme. Wanatoka katika ‘mataifa yote na makabila na vikundi vya watu na luga.’ (Ufunuo 7:9) Mashahidi wanajifunza Biblia na mamilioni ya watu kwa bure; watu wanaotaka kujua yale Biblia inafundisha kabisa. Namna unabii huo unavyotimia ni jambo la kushangaza kabisa; kwa kuwa Yesu alitabiri kama Wakristo wa kweli ‘wangechukiwa na watu wote’!​—Luka 21:17.

UTAFANYA NINI?

15. (a) Je, unakubali kama tunaishi kweli katika siku za mwisho, na sababu gani unakubali? (b) “Mwisho” utamaanisha nini kwa wale wote wanaokataa kumutii Yehova na itakuwa namna gani kwa wale wanaokubali utawala wa Ufalme wa Mungu?

15 Kwa kuwa mambo mengi ambayo Biblia ilisema yanatimia leo, je, haukubali kama tunaishi kweli katika siku za mwisho? Wakati Yehova ataona habari njema imehubiriwa kama anavyopenda, bila shaka “mwisho” utakuja. (Mathayo 24:14) “Mwisho” unamaanisha kuondolewa kwa ubaya wote duniani. Unamaanisha kuharibiwa kwa watu wote wanaokataa kumutii Mungu kwa makusudi. Yehova atatumia Yesu na malaika wenye nguvu ili kutimiza jambo hilo. (2 Wathesalonike 1:6-9) Shetani na mashetani wake hawatadanganya tena mataifa. Kisha Ufalme wa Mungu utawamwangia baraka nyingi wale wote wanaokubali utawala wake wa haki.​—Ufunuo 20:1-3; 21:3-5.

16. Ni jambo gani la hekima unalopaswa kufanya?

16 Kwa kuwa mwisho wa ulimwengu huu wa Shetani unakaribia, ni vizuri kila mumoja ajiulize, ‘Ninapaswa kufanya nini?’ Ni jambo la hekima uendelee kujifunza mengi juu ya Yehova na mambo anayotaka tufanye. (Yohana 17:3) Jifunze Biblia kwa bidii. Uwe na zoezi ya kukusanyika kwa kawaida na wengine wanaojikaza kufanya mapenzi ya Yehova. (Waebrania 10:24, 25) Fanya nguvu ujue mambo mengi ambayo Yehova Mungu anafundisha watu duniani pote, na ufanye mabadiliko katika maisha yako ili uweze kumupendeza Mungu.​—Yakobo 4:8.

17. Sababu gani uharibifu wa watu wabaya utashitua watu wengi?

17 Yesu alitabiri kama watu wengi watapuuza alama zinazoonyesha kama tunaishi kweli katika siku za mwisho. Uharibifu wa watu waovu utakuja kwa kushitukia na bila kutazamia. Siku hiyo itakuja kama mwizi usiku na watu wengi watashituka. (1 Wathesalonike 5:2) Yesu alitoa onyo hili: ‘Kwa maana kama vile siku za Noa zilivyokuwa, ndivyo kuwapo kwa Mwana wa binadamu kutakavyokuwa. Kwa maana kama vile walivyokuwa katika siku hizo kabla ya garika, wakila na kunywa, wanaume wakioa na wanawake wakiolewa, mupaka siku ambayo Noa aliingia ndani ya safina; nao hawakujali mupaka garika ikaja na kuwafagilia mbali wote, ndivyo kuwapo kwa Mwana wa binadamu kutakavyokuwa.’​—Mathayo 24:37-39.

18. Yesu alitoa onyo gani ambalo hatupaswi kuchukua kwa muchezo?

18 Kwa hiyo, Yesu aliwaambia watu waliokuwa wakimusikiliza: ‘Jiangalieni ninyi wenyewe kwamba mioyo yenu isilemewe kamwe na kula kupita kiasi na kunywa sana na mahangaiko ya maisha, na kwa gafula siku hiyo iwe juu yenu mara moja kama mutego. Kwa maana itakuja juu ya wale wote wanaokaa juu ya uso wa dunia yote. Basi, endeleeni kukesha wakati wote mukiomba dua ili mupate kufanikiwa kuponyoka mambo yote hayo yaliyokusudiwa kutukia, na kusimama mbele ya Mwana wa binadamu.’ (Luka 21:34-36) Hatupaswi kuchukua maneno hayo ya Yesu kwa muchezo. Kwa sababu gani? Kwa sababu ni wale tu wanaokubaliwa na Yehova Mungu na “Mwana wa binadamu,” Yesu Kristo, ndio walio na tumaini la kuokoka mwisho wa ulimwengu huu muovu wa Shetani na kuingia katika dunia mupya iliyo karibu sana ambamo wataishi milele!​—Yohana 3:16; 2 Petro 3:13.

^ fu. 4 Ili kupata maelezo yanayoonyesha kweli kama Mikaeli ni jina lingine la Yesu Kristo, soma Nyongeza, ukurasa wa 218-219.